Kufaidika Kutokana na “Mpatanishi Mmoja kati ya Mungu na Wanadamu”
1. (a) Sababu gani Wayahudi wa leo hawapendezwi na agano jipya? (b) Ni nani peke yake ambaye angeweza kukusudia hilo agano jipya na mpatanishi walo?
LEO hakuna lo lote la yale mataifa 152 yaliyo washiriki wa Umoja wa Mataifa linalopendezwa kufanya agano pamoja na Yehova, Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Hasha, wala hata wale Wayahudi 15,000,000 ambao kwa sasa wametawanyika kuizunguka dunia. Ujapokuwako unabii wa Yeremia 31:31-34, wao wanapendelea kuamini kwamba wangali chini ya agano la Torati la kale lililopatanishwa na Musa. “Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe [kwa kujitahidi kufuata agano la Torati], hawakujitia chini ya haki ya Mungu,” inayopatikana kwao kupitia kwa agano jipya. (Rum. 10:1-3) Yehova, Mungu wa haki ya kweli, alikusudia agano jipya hilo. Yeye peke yake ndiye angeweza kulisimamisha na kuchagua mpatanishi walo mwenye kufaa.
2. Yehova alisema kwamba angefanya agano jipya na nani, naye angefanya nini kupitia kwalo kwa habari ya uovu na dhambi yao na maarifa yao juu yake?
2 “Angalia, siku zinakuja, asema [Yehova], nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. . . . Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema [Yehova]; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue [Yehova]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema [Yehova]; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.”—Yer. 31:31-34.
3. Wakati uliowekwa wa agano jipya ulitegemea kutokea kwa nani, na je! jambo hilo lilimpasa Musa?
3 Yehova alilifanya agano jipya hilo “na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda” wakati gani? Wakati wa jambo hilo ulitegemea mpatanishi ambaye Yehova alichagua kwa ajili ya agano hilo. Musa asingefufuliwa kutoka kwa wafu ili awe mpatanishi wa hilo agano jipya. Yeye asingekuwa mwenye kusaidia zaidi wale walio katika agano jipya kuliko alivyosaidia Israeli.
4. Kulingana na mwanafunzi Mwebrania wa mwalimu Farisayo Gamalieli, mpatanishi wa Mungu wa agano jipya ni nani?
4 Hatuachwi na shaka lo lote juu ya yule aliyekuwa mpatanishi mwenye kuhitajiwa. Hapa twaiendea barua iliyoongozwa kwa roho waliyoandikiwa Waebrania na yule mwanafunzi Mwebrania aliyekuwa akiketi miguuni pa mwalimu Farisayo mwenye kujulikana wa karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, yaani, Gamalieli. Akionyesha tofauti kati ya Musa na huyo mpatanishi mpya, yeye anaendelea kusema hivi: “Ndiyo pia ilivyokuwa kwa Musa. Wakati alipokuwa karibu kuitengeneza ile hema, Mungu alimwambia: “Tengeneza kila kitu kufuatana na ule mfano ulioonyeshwa kule mlimani [Sinai].” Lakini sasa Yesu amepewa huduma ya kikuhani iliyo bora zaidi kuliko yao, kama vile agano alilothibitisha kati ya watu na Mungu ni bora zaidi, kwani lina msingi wake katika ahadi za mambo yaliyo bora zaidi.” (Ebr, 8:5, 6, HNWW) “Na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili,”—Ebr. 12:24.
5. Kabla ya kifo chake, Yesu alionyeshaje kwamba alitambua wakati ulikuwa umefika kwa mahali pa agano la kale la Torati kuchukuliwa na agano jipya?
5 Yesu alitambua kwamba wakati ulikuwa umefika kwa Yehova kuweka lile agano jipya mahali pa lile agano la kale la Torati ya Musa. Hivyo, katika usiku wa Sikukuu ya Kupitwa kabla ya kifo chake Ijumaa, Nisani 14, mwaka 33 W.K., alianzisha ukumbusho wa kifo chake cha dhabihu. Alipochukua kikombe cha divai ya Ukumbusho, yeye alisema kwa mitume wake kumi na mmoja waaminifu: “Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.” (Mt. 26:27, 28) Au, kama ambavyo mtume Paulo anavyoyaweka maneno ya Yesu: “Hiki ni kikombe cha Agano jipya linalothibitishwa kwa damu yangu. Fanyeni hivi, kila mnapokunywa, kwa kunikumbuka.” (1 Kor. 11:25, HNWW) Kwa sehemu za siku tatu alikuwa mfu katika kaburi na asingeweza kuanza kutenda kama mpatanishi wa hilo agano jipya.
6. Ili kuyatimiza maneno ya Mungu katika agano jipya juu ya kusamehe dhambi na kutokumbuka dhambi tena, ni jambo gani lililokuwa la lazima?
6 Ingawa Yeremia 31:31-34 haikutaja, kungali kulihitajiwa dhabihu ili agano jipya lianze kutenda kazi. Dhabihu ilihitajiwa kwa sababu, katika usemi wa agano jipya, Mungu alisema hivi: “Nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yer. 31:34) Damu ya wanyama ilitumiwa katika kufanyiza agano la kale la Torati ya Musa, na kwa makusudi ya kutakasa. Kwa kupatana na jambo hilo, mpatanishi Musa “aliinyunyizia damu ile hema na vyombo vya ibada. “Naam, kadiri ya Sheria karibu kila kitu chaweza kutakaswa kwa damu, na dhambi nazo zaondolewa tu ikiwa damu imemwagwa.” (Ebr. 9:21, 22, HNWW) Yesu alikuwa angali ana thamani ya damu ya uhai wake alipofufuliwa kutoka kwa wafu Jumapili, Nisani 16, 33 W.K. Hilo ndilo jambo ambalo Waebrania 13:20 linaonyesha wakati linaposema hivi: “Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu Mchungaji Mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu Yesu.”—Yohana 10:11.
7. Kwa sababu Kristo alitoa dhabihu bora zaidi kwa ajili ya agano jipya, damu yake inafanya nini kwa habari ya dhamiri na vilevile kwa ajili ya “wateule”?
7 Kwa sababu agano jipya lilianza kutendeshwa kazi kwa dhabihu bora zaidi, Waebrania waliofanywa Wakristo waliulizwa hivi: “Basi si zaidi damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa [roho ya] milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu, mpate [kumtolea utumishi mtakatifu] Mungu aliye hai? Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walio [na Mungu] waipokee ahadi ya urithi wa milele.” (Ebr. 9:14, 15) Walakini ni wakati gani damu ya Kristo ilipoanza kusafisha dhamiri za Waebrania wale waliofanywa Wakristo ambao walikuwa wamekuwa chini ya agano la kwanza,” agano la Torati ambalo lilikuwa limepatanishwa na Musa katika Mlima Sinai?
8. Damu ya Kristo ilianza kusafisha wakati gani dhamiri za Waebrania waliofanywa Wakristo ambao walikuwa chini ya agano la Torati la kwanza?
8 Si wakati wa kufufuliwa kwa Kristo kutoka kwa wafu, bali katika siku ya 50 tangu wakati huo. Yaani, katika siku ya Pentekoste baada ya yeye kupaa mbinguni na kuingia mahali alipo Mungu “mbinguni kwenyewe ambako sasa anasimama mbele za Mungu kwa ajili yetu.”—Ebr. 9:24, HNWW.
9. Katika siku ya Pentekoste wakati Petro alipowaambia Wayahudi waliochomwa dhamiri kwamba msamaha wa dhambi zao ungetokana na kubatizwa kwao katika jina la Yesu Kristo, jambo hilo lilithibitisha nini kwa habari ya maagano?
9 Katika siku hiyo ya Pentekoste mtume Petro alitoa hotuba kwa Wayahudi na waongofu Wayahudi waliotahiriwa ambayo ilichoma dhamiri zao. “Tufanye nini?” wakauliza. Petro akajibu hivi: “Tubuni na kila mmoja wenu abatizwe kwa jina la Yesu Kristo ili mpate kuondolewa dhambi zenu na kupokea ile zawadi ya [roho takatifu].” (Matendo 2:37, 38, HNWW) Ahadi hii ya msamaha wa dhambi zao ambazo walitubia ilithibitisha jambo fulani. Jambo gani? Kwamba agano jipya la Mungu pamoja na msaada walo wa msamaha wa dhambi lilikuwa limeanza kutenda kazi siku iyo hiyo, kwa kuwa agano la kale la Torati ya Musa lilikuwa limegongomelewa (limetundikwa) kwenye mti wa kifo wa Yesu Kristo!—Efe. 2:15, 16; Kol. 2:14; Ebr. 8:8-13; Yer. 31:34.
10. Petro alikaziaje uhakika huo juu ya maagano siku chache baadaye wakati wa kuzungumza na Wayahudi wenye hatia ya damu katika hekalu la Yerusalemu?
10 Uhakika uu huu ulikaziwa siku chache baadaye. Wakati huo Petro aliambia mkusanyiko wa Wayahudi wenye hatia ya damu kwenye hekalu hivi: “Kwa hiyo, tubuni, na kugeuka ili mfutishe dhambi zenu, kwamba majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa Yehova mwenyewe na kwamba apate kumtuma Kristo mliyewekewa ninyi, Yesu, ambaye mbingu, kweli, lazima imweke ndani yake yenyewe mpaka nyakati za kurudishwa kwa vitu vyote ambavyo Mungu alisema kupitia kwa kinywa cha manabii wake watakatifu wa wakati wa kale.” Mwishowe Petro alimalizia hotuba yake kwa kusema hivi: “Mungu, akiisha kumfufua mtumishi wake Yesu, alimtuma kwenu ninyi kwanza, ili kuwabarikia kwa kumwepusha kila mmoja wenu na maovu yake.”—Matendo 3:19-21, 26, NW.
‘MPATANISHI’ WA WANGAPI?
11. Mambo ya hakika yanaonyeshaje kama Mungu alifanya hilo agano jipya na, nyumba ya Israeli wa mwili na nyumba ya Yuda wa mwili wa asili?
11 Hata hivyo, je! Mungu alikuwa akilifanya agano jipya na “nyumba ya Israeli” wa mwili, wa asili, na “nyumba ya Yuda” wa mwili, wa asili? Jambo hilo lingewezekanaje, kwa kuwa Wayahudi wa asili wa hizo nyumba mbili walikuwa wamemkataa kijeuri Mpatanishi mtarajiwa wa hilo agano jipya na, kama taifa, walikuwa wakiadhimisha sikukuu ya Pentekoste katika wakati uliowekwa kwenye hekalu katika Yerusalemu? Mungu asingeweza kufanya hivyo. Yeye alikuwa na wazo la kufanya hilo agano jipya na taifa la Israeli wa Kikristo lililozaliwa karibuni, taifa la Israeli wa kiroho, ambalo lilizaliwa katika siku iyo hiyo ya Pentekoste wakati ‘roho takatifu iliposhuka juu’ ya wanafunzi waliobatizwa wa Yesu Kristo, wapata 120 wao. (Matendo 11:15) Hawa walikuwa wamengojea, si hekaluni, bali katika chumba cha orofani katika Yerusalemu. Hapo wanafunzi hao, ambao tayari walikuwa wamezamishwa majini, walizaliwa kwa roho ya Mungu wawe watoto wake wa kiroho, “Israeli wa Mungu.” Wakiwa hivyo waliingizwa kwenye agano jipya hilo kupitia kwa Mpatanishi wa kimbinguni, Yesu Kristo, Nabii aliye mkubwa zaidi kuliko Musa.—Matendo 2:1-36; Yoeli 2:28, 29; Yohana 3:3, 5; Gal. 6:16.
12. Kwa kupatana na utaratibu wa Mungu wa kutenda, upatanishi wa Yesu Kristo ulipanuliwaje katika mwaka uliofuata Pentekoste hiyo?
12 Kwa hiyo Yesu Kristo mbinguni ndiye Mpatanishi kati ya Mungu na Waisraeli wa kiroho, wakati hao wanapokuwa wangali wanaume na wanawake katika mwili. Hata ndani ya mipaka ya ushirika wa hili “taifa takatifu” dogo upatanishi wa Yesu Kristo umepanuka, kwa kuwa Mungu amefuata utaratibu fulani katika kuruhusu jamii za watu kwenye hilo agano jipya. Kwa hiyo, kwa muda wa mwaka mmoja hivi tangu Pentekoste ya mwaka 33 W.K., Yesu alikuwa Mpatanishi wa hao Waisraeli wa kiroho ambao walikuwa Wayahudi wa mwili au waongofu Wayahudi waliotahiriwa peke yao. Wapata 3,000 wa hawa waliongezwa katika Israeli wa kiroho katika siku hiyo ya Pentekoste, 33 W.K. (Matendo 2:10, 37-41) Kisha, inaelekea kwamba katika mwaka uliofuata (34 W.K.) kama matokeo ya mateso ya Sauli wa Tarso, “habari njema” juu ya Kristo zilihubiriwa katika Samaria na roho takatifu ‘ikashuka juu’ ya waamini waliobatizwa huko. (Matendo 8:15-17) Kuanzia wakati huo na kuendelea upatanishi wa Yesu ulipanuliwa ili uwafaidi Waisraeli wa kiroho ambao walikuwa wanaume na wanawake Wasamaria.
13. Miaka miwili baada ya Wasamaria kukubaliwa, Yesu alikuwaje mpatanishi wa jamii ya tatu ya Waisraeli wa kiroho, nao Wayahudi waliofanywa Wakristo katika Yerusalemu walilikubalije jambo hilo?
13 Miaka miwili yapita sasa. Mwishowe, katika vuli ya mwaka 36 W.K., au miaka mitatu na nusu baada ya kifo na kufufuliwa kwa Yesu, yeye aanza kuwa mpatanishi kwa jamii ya tatu ya Waisraeli wa kiroho, wale waliochukuliwa kutoka Mataifa wasiotahiriwa, kuanzia na akida Mwitalia, Komelio. Baada ya mtume Petro kuripoti juu ya badiliko hili la matukio lenye kustaajabisha kwa Wayahudi waliofanywa Wakristo katika Yerusalemu, walisema hivi: “Mungu amewapa watu [wasiotahiriwa] wa mataifa mengine nafasi ya kutubu na kuwa na uzima!”—Matendo 8:1 mpaka 11:18, HNWW.
14. Paulo aliwaambia nini wazee wa Efeso juu ya kuhubiri kwake juu ya kumtubia Mungu, naye alikuwa sasa akitumikia kama mhudumu kwa faida ya agano gani?
14 Zaidi ya miaka 20 baada ya jambo hilo, Paulo alikuwa angali anatenda kama mtume kwa mataifa naye alikuwa akimaliza safari yake ya tatu ya umisionari. Akiwa njiani kurudi Yerusalemu alisimama Mileto na kuzungumza na wazee wa kundi katika Efeso, Asia Ndogo. Aliwaambia namna alivyofanya kazi, akisema hivi: “Nikawashuhudia [kikamilifu] Wayahudi na [Wagiriki] wamtumbie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo. Basi sasa, angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni.” (Matendo 20:21, 22) Yeye hakuwa tena akitumikia kama Farisayo kwa faida ya lile agano la kale la Torati ya Musa. Mahali pake, kama ambavyo anaandika katika 2 Wakorintho 3:5, 6, “utoshelevu wetu watoka kwa Mungu. Naye ndiye aliyetutosheleza [sisi] kuwa wahudumu wa agano jipya; si wa andiko, bali wa roho; kwa maana andiko huua, bali roho huhuisha.”
15. Wakati wa kuzungumza juu ya “wahudumu wa agano jipya,” Paulo alitia nani ndani ya neno ‘sisi,’ na je! hao walikuwa sehemu ya Baraza ya Upatanishi kati ya Mungu na wanadamu?
15 Mtume huyo anamaanisha nani hapa anaposema ‘sisi’? Katika utangulizi wa barua yake yeye anatufahamisha wale wanaotiwa ndani katika ‘sisi,’ kwa kusema hivi: “Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu, na Timotheo ndugu yetu; kwa [kundi] la Mungu lililoko Korintho.” (2 Kor. 1:1) Kwa hiyo, Paulo na Timotheo walikuwa “wahudumu wa agano jipya; . . . wa roho.” Kwa usemi huu Paulo hakumaanisha kwamba yeye na Timotheo walikuwa Baraza ya Upatanishi, wakishiriki upatanishi pamoja na Yesu. Hasha, kwa kuwa wao wenyewe walikuwa Waisraeli wa kiroho ambao kwa ajili yao Yesu alitumikia kama Mpatanishi wa Mungu. Yesu peke yake ndiye ‘mpatanishi wa agano jipya.’—Ebr. 12:24, NW.
16, 17. Katika 1 Timotheo 1:20 hadi 2:7, ni wazo gani linalomwongoza Paulo amtaje Kristo Yesu kuwa mpatanishi?
16 Katika kumwandikia Timotheo moja kwa moja, Paulo anaelekeza na kutaja upatanishi wa Yesu anapoendelea kusema hivi: “Himenayo na Iskanda, ambao nimempa Shetani watu hao, ili wafundishwe wasimtukane Mungu. Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote [ila si kutia ndani Himenayo na Iskanda wakufuru]; kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.
17 “Hili ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu; ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli. Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote [au, namna zote za watu; maneno ya pambizoni, NW]—; utakaoshuhudiwa kwa majira yake. Nami kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa [wasiotahiriwa] katika imani na kweli.”—1 Tim. 1:20 mpaka 2:7.
18. (a) Kwa hiyo je! Paulo alikuwa akimsihi Timotheo atende kama mpatanishi kati ya Mungu na wale watumishi wa serikali? (b) Ni nani ambao wangefaidika kutokana na maombi yaliyoelekezwa kwa Mungu juu ya hao watumishi wa serikali?
18 Hivyo Paulo alisihi kwamba “dua, na sala, na maombezi” yanapaswa kutolewa “kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka.” Lakini hakuwa akimsihi Timotheo atende kama mpatanishi kati ya Mungu na hao watumishi wa serikali. Kuwaongoa (kuwageuza) hao watumishi wa serikali kwenye Ukristo kusingekuwa kusudi la hizo “dua, na sala, na maombezi.” Kwa hakika, ni nani, wangefaidika kutokana na maombi hayo yaliyoelekezwa kwa Mungu? Kusudi la matoleo hayo kwa Mungu lilikuwa nini? Kwamba sisi Wakristo kama Paulo na Timotheo “tuishi’ maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.”—1 Tim. 2:2.
19. Kuishi maisha ya utawa kungetokeza nini, nalo jambo hilo ni “zuri, nalo lakubalika” kwa nani?
19 Kuishi maisha hayo ya utulivu, utauwa, na ustahivu kungetokeza wokovu wa Wakristo waliotoa maombi hayo kuhusiana na watawala wa kisiasa. Wokovu wa Wakristo waliotoa maombi hayo kuzuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu.” Sababu gani hivyo? Kwa Sababu ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.” Kwa kupatana na jambo hilo anayeitwa hapa “Mwokozi wetu” si, Yesu Kristo, bali “Mungu.”
20. Kulingana na 1 Timotheo 2:5, 6, ni nini sehemu ya Kristo Yesu katika mpango wa Mungu wa wokovu?
20 Basi, sehemu ya Kristo katika mpango huu wa wokovu, ni nini? Paulo anaendelea kusema hivi: “Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu [si, wanadamu wote] ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.”—1 Tim. 2:5, 6.
21. (a) Barua ya Paulo kwa Timotheo ilikuwa juu ya mhudumu gani akiandikia mhudumu gani mwingine? (b) Agano hilo linadumu kwa muda gani, nao “ukombozi” unafanya sehemu gani kwa habari ya jambo hilo?
21 Paulo alikuwa akiandika kulingana na mambo ya hakika ya karne ya kwanza ya Ukristo, wakati ambapo agano jipya lilianza kutendeshwa kazi. Ndani yalo “wanadamu” wa mataifa yote, Wayahudi, Wasamaria, Mataifa wasiotahiriwa, tayari walikuwa wamekwisha ingizwa baada ya kufanywa kuwa sehemu ya Israeli wa kiroho. Kristo Yesu alikuwa mpatanishi wa hilo agano jipya. Barua ya Paulo kwa Timotheo kwa habari hii ilikuwa juu ya ‘mhudumu mmoja wa agano jipya’ akiandikia ‘mhudumu mwingine wa agano jipya.’ Hilo agano jipya kati ya “Mungu Mwokozi wetu,” na Israeli wa kiroho linaendelea maadamu bado wapo Waisraeli wa kiroho katika mwili kama “wanadamu” hapa duniani. “Ukombozi” wa Yesu unatoa msingi kwa wanaume na wanawake wa namna zote kuwa Waisraeli wa kiroho na kuletwa katika hilo agano jipya ambalo Kristo Yesu ndiye ‘mpatanishi mmoja’ walo.
22. (a)Inaonekanaje wazi kwamba agano jipya linakaribia mwisho wake, nao upatanishi wa Kristo utakoma wakati gani? (b) Sababu gani Waisraeli wa kiroho waliotukuzwa hawatahitaji mpatanishi ye yote, nao watatenda katika vyeo gani wakati huo?
22 Kungali na zaidi ya 9,000 ambao wanadai kuwa Waisraeli wa kiroho katika agano jipya. Kama vile Paulo na Timotheo, hawa ni “wahudumu wa agano jipya.” (2 Kor. 3:6; 1:1) Kwa wazi agano jipya linakaribia mwisho wa kutenda kwalo kwa kusudi la kutokeza Waisraeli wa kiroho 144,000 wanaopata kibali ya Mungu kwa kushirikishwa na Yesu Kristo katika ufalme wa kimbinguni, serikali inayofaa kwa wanadamu. Wakati wale wa mwisho wa hawa Waisraeli wa kiroho waliokubaliwa watakapokoma kuwa “wanadamu” kwa sababu ya kifo cha kidunia na ufufuo wa kushiriki katika ufalme wa kimbinguni, ndipo upatanishi wa Yesu utakapokoma pia. Hali yao iliyorithiwa yenye dhambi katika mwili, ambayo ilihitaji mpatanishi atende kati yao na Mungu wa utakatifu, itaachwa nyuma. Kama vile malaika watakatifu wa mbinguni, Waisraeli hao wa kiroho waliotukuzwa hawatahitaji mpatanishi kati yao na Yehova Mungu. (Ufu. 22:3, 4) Chini ya Yesu Kristo watatumika kama wafalme, makuhani na mahakimu washirika juu ya ulimwengu wote wa wanadamu.—Ufu. 7:4-8; 14:1-3; 20:4, 6; Luka 22:28-30.
“MKUTANO MKUBWA” WA WAFAIDIKAJI WA KIDUNIA
23, 24. (a) Ni nani ambao wanatenda wakishirikiana na mabaki ya Waisraeli wa kiroho, na ni mwaliko gani uliotolewa kwao kwa habari ya Chakula cha Bwana cha jioni? (b) Wao wanajitambua wenyewe kutokuwa nini, na hata hivyo wanafaidikaje kutokana na utendaji wa agano jipya?
23 Leo, kulingana na maandishi ya kweli, kuna “mkutano mkubwa” wa Wakristo waliojiweka wakf na kubatizwa ambao wanatenda kazi kwa kushirikiana na mabaki wachache wa Israeli wa kiroho. Tangu masika ya mwaka 1938, wamekaribishwa wahudhurie sherehe ya ukumbusho wa kifo cha Kristo, si ili wale mkate na kunywa divai ya ukumbusho, mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu, bali kama watazamaji wenye heshima.a Wanamtambua Yesu Kristo kuwa Mfalme wao wa kimbinguni tangu Majira ya Mataifa yalipokoma katika mwaka 1914. Kwa juhudi wanajiunga na mabaki ya Waisraeli wa kiroho katika kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa “ushuhuda kwa mataifa yote” kabla ya taratibu hii ya mambo kumalizika katika “dhiki kuu” inayokuja. (Mt. 24:14, 21, NW) Wao wanatambua kuwa wao si Waisraeli wa kiroho katika agano jipya lililopatanishwa na Yesu Kristo, wala si sehemu ya ‘uzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu.’—1 Pet. 2:9.
24 Hata hivyo wanafaidika kutokana na utendaji wa hilo agano jipya. Wanafaidika nalo kama vile, katika Israeli ya kale, “mgeni” alivyofaidika kwa kuishi kati ya Waisraeli ambao walikuwa katika agano la Torati.—Kut. 20:10; Law. 19:10, 33, 34; Ufu. 7:9-15.
25. Ili kuendelea kuwa katika uhusiano na Yehova Mungu, “mkutano mkubwa” unapaswa kuendelea kuwa na umoja na nani, na sababu gani hivyo?
25 Ili kuendelea kuwa katika uhusiano pamoja na “Mungu Mwokozi wetu,” “mkutano mkubwa” unahitaji kuendelea kuwa na umoja pamoja na mabaki ya Israeli wa kiroho. Sababu gani? Kwa sababu Waisraeli hao wa kiroho ndio lile “taifa takatifu” ambalo twalisoma katika Yeremia 31:35, 36, mara tu baada ya Mungu kuahidi hivi juu ya agano jipya: “[Yehova] asema hivi, awapaye watu jua, ili kuwa nuru wakati wa mchana, na amri za mwezi na nyota, ili kuwa nuru wakati wa usiku, aichafuaye bahari, hata mawimbi yake yakavuma [juu ya Wamisri wenye kufuatia Waisraeli]; [Yehova] wa majeshi, ndilo jina lake; Amri hizi zikiondoka, zisiwe mbele zangu, asema [Yehova], ndipo wazao wa Israeli nao wataacha kuwa taifa mbele zangu milele.”
26. Kwa hiyo Israeli wa kiroho watakuwa wa kudumu katika tengenezo la Mungu la ulimwenguni pote wakiwa nini, naye Yesu Kristo atatawala juu ya wale watakaokuwa katika dunia iliyo paradiso akiwa wapi?
26 Yehova asingeweza kuachilia taifa la Israeli wa kiroho litoweke kutoka katika tengenezo lake la ulimwenguni pote kama vile asivyoweza kuachilia mianga ya kimbinguni ambayo inaamrisha nuru kwa dunia yetu ikome. Katika mbingu Israeli wa kiroho watakuwa Yerusalemu Mpya ambao katika huo Yesu Kristo atatawala kama Mfalme juu ya “mkutano mkubwa” wenye kuokoka na wanadamu wote wafu waliofufuliwa kwenye uzima katika dunia iliyo paradiso.—Ufu. 21:2-4.—Kutoka The Watchtower Nov. 15, 1979.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama tangazo “Ukumbusho,” uku. 50, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) toleo la Februari 15, 1938; pia uku. 75, mafungu 51, 52, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) toleo la Machi 1, 1938. Angalia tangazo “Ukumbusho” katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Februari 15, 1937 uku. 50.
[Picha katika ukurasa wa 17]
Agano la kale la Torati liligongomelewa juu ya mti wa mateso
Agano jipya lilianza kutenda kazi katika Pentekoste