Sura 14
Baada ya Agano Jipya—Ufalme wa Mileani
1, 2. (a) Yale mamilioni ya wafaidikaji wa utendaji wa lile agano jipya yanaweza kulinganishwa na nani leo? (b) Yale masharti ya agano jipya yalisema nini?
MAMILIONI ya watu kuzunguka dunia yote wamepokea faida kubwa kutokana na agano jipya, ingawa hawamo ndani yalo. Wao ni kama wakazi wasio Waisraeli walioishi katika Israeli wakati wa siku zile agano la Torati ya Musa lilipokuwa likitenda. (Kutoka 20:10) Imekuwaje hivyo kwa mamilioni yanayoendelea kuongezeka ya wafaidikaji yanayoshirikiana na mabaki ya Waisraeli wa kiroho leo?
2 Katika unabii wa Yeremia 31:31-34, Yeye aliyeweka masharti ya agano jipya alisema hivi: “Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”
3. (a) Sheria ya agano la kale la Musa ilitolewa kwa Israeli kwa namna gani? (b) Kabla ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuanza kuandikwa, ni wapi Mungu alikoandikisha sheria za agano jipya?
3 Kwa habari ya agano la Torati, Yehova Mungu, kupitia nabii Musa akiwa mpatanishi, aliwapa Israeli wa asili “ile hati iliyoandikwa . . . , [iliyokuwa na] hukumu.” (Wakolosai 2:14) Namna gani, basi, juu ya sheria ya agano jipya? Mpatanishi walo hakupaswa kuiandika juu ya mawe, au kuiandika katika hati. Mpatanishi walo hakuacha maandishi yo yote yake mwenyewe. Tunahakikisha ni nini iliyo sheria ya agano jipya kutokana na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoongozwa na Mungu. (2 Timotheo 3:16) Lakini hata kabla ya hayo Maandiko ya Kigiriki kuanza kuandikwa, kuanzia karibu na mwaka wa 41 W.K., Yehova Mungu alianza kuandika sheria yake ya agano jipya. Wakati gani? Siku ya Pentekoste, 33 W.K. Wapi? Pale pale hasa ambapo muda mrefu uliotangulia yeye aliahidi kuiandika: “Nitatia sheria zangu katika akili zao, na katika mioyo yao nitaziandika.”—Waebrania 8:10, NW.
4. Mungu kuandika sheria zake juu ya moyo na kuzitia katika akili ya watumishi wake kungekuwa na matokeo gani mema?
4 Zikiwa zimeandikwa juu ya mioyo, kungekuwa na uwezekano kidogo sana wa sheria hizo kuachwa kupendwa na wale wanaozitii. Ikiwa sheria hizo zingetiwa “katika akili zao,” pangekuwa na uwezekano mdogo sana kwao kuzisahau. Hivyo, washikaji wa sheria hizo wanasema hivi, katika maneno ya Zaburi 119:97: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” Kutoka ndani sana yao wenyewe, wanaweka shauku zao juu ya sheria za Yehova kama zilivyotolewa kupitia Mpatanishi wake, Yesu Kristo. Hivyo, wakiwa na kusudi linalofaa, wanaazimia kushika sheria hizo zenye thamani kubwa. Hilo linawahusu wote “kundi dogo” lililo katika agano jipya na “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” ambao, hawamo katika agano jipya, bali wako chini yalo.—Linganisha 1 Yohana 5:3; Yohana 14:15.
Suala la Ufalme Lawekwa Mbele!
5. Mpatanishi wa lile agano jipya alitabiri nini kwenye Mathayo 24:12-14?
5 Washikaji wa sheria za lile agano jipya hawawezi kuruhusu hata kidogo washindwe na yale ambayo Mpatanishi, Yesu Kristo alitabiri kuwa sehemu ya ile “ishara . . . ya umalizio wa mfumo wa mambo”: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa idadi kubwa zaidi utapoa. Lakini yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa. Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:3, 12-14, NW.
6. (a) Je! Mathayo 24:14 ulikuwa ni unabii tu? (b) Ni nani ambao wameuchukua kuwa zaidi ya unabii tu, na ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya uvumilivu wao?
6 Huu usemi wa mwisho kuhusu ushuhuda wa duniani pote wa Ufalme haukuwa uwe utabiri tu. Ulikuwa uelekezi kwa wanafunzi wake wanaoishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” Ulikuwa ni mwongozo wa mwendo wao wa tendo unaofaa mpaka mwisho wenyewe wa mfumo wa mambo usio na upendo na unaojawa na kutokutii sheria kwa ujumla, si kutoheshimu tu sheria ya Mungu. Ni nani leo wanaothibitika kuwa Wakristo wa kweli, wakichukua maneno hayo ya Yesu Kristo kuwa uelekezi kwao? Mambo ya hakika ya kihistoria ambayo yameongezeka tangu 1919 yanajibu kikweli, ni “Mashahidi wa Yehova”! Shughuli yao ya elimu ya Biblia kuhusu Ufalme ndiyo kubwa zaidi iliyopata kuwekwa kwenye maandishi, nao wameonyesha uvumilivu ndani yayo katika wakati wa miaka 67 iliyopita. Kila mwaka sasa, inaongezeka kwa ukubwa na kwa nguvu.
7, 8. (a) Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Shetani alijaribu kufanya nini kwa wale waliomo katika lile agano jipya? (b) Katika kipindi cha baada ya vita, lile suala la Ufalme lilitokeaje mbele?
7 Shetani Ibilisi alijaribu kuzuia shughuli hii kubwa ya elimu ya Biblia kwa kulifanya baki dogo la Waisraeli wa kiroho lifutiliwe mbali wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. He, alishindwa! Upesi, baada ya kuhuishwa kwao kutoka hali kama ya kifo kiangazi cha mwaka wa 1919, walifanya mkusanyiko wao wa kwanza wa baada ya vita katika Seda Pointi, Ohaiyo, Septemba wa mwaka huo. Kwenye mkusanyiko wa pili wa Seda Pointi Septemba 1922, lile suala la Ufalme lilitokea mbele. Siku ya nne ya mkusanyiko huo, iliyoitwa “Ndiyo Siku,” msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi alileta hotuba yake yenye kusisimua kwenye upeo mzuri sana kwa kupaaza sauti hivi:
8 “Basi rudini shambani, Enyi wana wa Mungu Aliye Juu Zaidi Sana! Jivikeni viunoni silaha zenu! Iweni makini, kesheni, iweni watendaji, iweni mashujaa. Iweni Mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila kisehemu cha Babeli kiwe ukiwa. Utangazeni ujumbe kwa marefu na mapana. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Ninyi ni mawakili wake wa utangazaji. Kwa hiyo tangazeni, tangazeni, tangazeni, Mfalme na Ufalme wake.”
Kupata Kumjua Yehova kwa Ufahamu Zaidi
9. (a) Kwa sababu ya kuongezeka kwa ushuhuda kuhusiana na serikali ya uadilifu, lazima watu wachukue msimamo gani? (b) Wale wanaochukua msimamo unaofaa wanapewa maarifa gani?
9 Sasa imekuwa zaidi ya miaka 70 tangu Kristo alipotawazwa katika Ufalme akiwa na mamlaka ya Ufalme 1914. Tangu hapo, ushuhuda kuhusu serikali ya uadilifu ya Mungu umeongezeka sana. Watu wa ulimwengu wa wanadamu lazima wachukue msimamo wao kuhusu suala la Ufalme, ama wawe upande wa Ufalme ama waupinge. Na wale wanaochukua msimamo wao upande wa serikali ya kimungu wanatimiziwa maneno haya ya maana ya agano jipya: “Hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue [Yehova]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao.”—Yeremia 31:34.
10. (a) Kwa hiyo, ni chini ya jina gani yale mabaki ya Waisraeli wa kiroho yalianza kuwakaribisha wale “kondoo wengine”? (b) Hao “kondoo wengine” walipata maarifa gani?
10 Mwaka wa 1935 mabaki ya Waisraeli wa kiroho yalianza kuwakaribisha “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema katika ushirika wenye kutenda pamoja nao katika “kundi moja” chini ya Yesu Kristo, wote wakiwa Mashahidi wa Yehova. Ndipo hao “kondoo wengine” walioanza kuongezeka wakawe “mkutano mkubwa” usio na hesabu iliyotangulia kuwekwa, walianza pamoja na mabaki yaliyozaliwa kwa roho, ‘kuzishika amri za Mungu,’ na kufanya kazi ya kutoa “ushuhuda wa Yesu.” (Ufunuo 7:9-17; 12:17) Hivyo tangu mwanzo katika mwaka wa 1935, hao “kondoo wengine” vilevile walipata kumjua Yehova “tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao.”
11. Jinsi gani maarifa ya Kikristo ya kumjua Yehova ni tofauti na ni bora zaidi ya yale ya Wayahudi chini ya agano la Torati?
11 Hata hivyo, jinsi gani maarifa ya Kikristo ya kumjua Yehova ni tofauti na ni bora kuliko maarifa ambayo Wayahudi walikuwa nayo chini ya agano la kale la Torati ya Musa? Mfanyi wa kimbingu wa agano jipya anaendelea kutuambia: “Maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:34; Waebrania 8:12) Sababu ya hilo ni kwamba, agano jipya msingi wake ni dhabihu bora zaidi kupitia Mpatanishi aliye bora zaidi. (Waebrania 8:6; 9:11, 12, 22, 23) Dhabihu iliyo bora zaidi ya Mpatanishi aliye bora zaidi haihitaji kurudiwa, kama ilivyokuwa katika Siku ya Upatanisho ya kila mwaka chini ya lile agano la kale la Torati ya Musa. (Waebrania 10:15-18) Kwa sababu ya hayo yote, maarifa ya kumjua Yehova waliyo nayo wale walimo katika na chini ya agano jipya kweli kweli ni bora zaidi, yenye kutajirisha zaidi, yenye kufahamisha zaidi, yenye kukamilika zaidi ya maarifa ya kumjua Mungu ambayo Wayahudi walikuwa nayo chini ya agano la Torati.
12. Zaidi ya yote, ni cheo gani alicho nacho Yehova kuelekea wale wanaoingizwa katika agano jipya na wale walio chini yalo?
12 Zaidi ya yote, Yehova Mungu, Mfanyi-Agano, ndiye Mfalme juu ya wale anaoleta katika agano jipya na juu ya wale anaoweka chini yalo. (Mathayo 5:34, 35; Yeremia 10:7) Mtume Paulo, miaka 1,850 kabla ya Yesu kutawazwa akiwa Mfalme katika mbingu 1914, alielekeza kwenye umaliki wa Yehova juu ya wale wanaotii sheria za agano jipya akisema: “Sasa kwa Mfalme wa milele, asiyeweza kuona uharibifu, asiyeonekana, Mungu peke yake, na iwe heshima na utukufu milele na milele. Amina.”—1 Timotheo 1:17.
Ufalme wa Mileani Baada ya “Dhiki Kubwa”
13. (a) Ni wakati gani na chini ya hali gani ule “mkutano mkubwa” utaingia kabisa kwenye baraka zinazomiminika kutoka agano jipya? (b) Ni kusudi gani kuu ambalo agano jipya litakuwa limetimiza?
13 “Mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine,” ambao haumo katika agano jipya lakini uko chini yalo, unatazamia kutoka ukiwa hai katika “dhiki ile iliyo kuu.” Baada ya kuharibiwa kwa huu mfumo wa mambo uliopo uliohukumiwa maangamizi, utafurahia, kwa miaka elfu, utawala wa Yesu Kristo pamoja na warithi washirika wake juu ya dunia safi. (Ufunuo 7:9-14) Ndipo kusudi la agano jipya litakuwa limetimizwa, lile la kutokeza “watu wa milki ya Mungu” wawe warithi wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu. (1 Petro 2:9; Matendo 15:14) Kupitia Ufalme wa Mungu, baraka zitamiminika kwa wingi sana juu ya “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wenye kuokoka. Shetani Ibilisi pamoja na tengenezo lake la kishetani lisiloonekana watakuwa wamekwisha tiwa katika shimo refu nao hawataweza kuingilia mambo.—Ufunuo 21:1-4; 20:1-3.
14. “Mkutano mkubwa” utakuwa umekwisha pata matayarisho gani mazuri?
14 “Mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wenye kuokoka utakuwa umekwisha pata matayarisho mazuri ya kuanza maisha katika mfumo mpya wa mambo. Kama vile mabaki ya Waisraeli wa kiroho, utakuwa umekwisha pata kumjua Mungu “tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao.” (Yeremia 31:34) Katika sala kwa Mungu, yule Mfalme anayetawala wakati mmoja alisema hivi: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Kwa hiyo maarifa hayo ya ulimwengu mzima ya kumjua Yehova Mungu yataleta wokovu wa milele. Itakuwa hivyo si kwa “mwili” tu utakaookolewa ukiwa hai uipite ile “dhiki kubwa” bali pia kwa mabilioni ya wanadamu wafu yatakaosikia sauti ya Mfalme na kutoka makaburi yao ya ukumbusho. Wote hao watakaofufuliwa watapewa maarifa yote yanayohitajiwa ya kumjua Yehova.—Mathayo 24:21, 22, NW; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:11-15.
15. Kwa sababu gani kutimizwa kwa agano jipya hakutatokeza hasara yo yote kwa “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine”?
15 Kwa furaha, kutimizwa kwa agano jipya la Mungu mpaka lipate fanikio tukufu hakutatokeza hasara kwa “mkutano mkubwa” wa wenye mfano wa kondoo ambao wataokoka uharibifu wa huu mfumo wa mambo uliohukumiwa maangamizi. Badala yake, kutafungua njia ya kupata baraka zilizo nzuri hata zaidi apa hapa penye dunia safi ambayo watarithi iwe yao na ambayo watakuwa na sehemu ya kwanza kuigeuza iwe paradiso ya kuenea tufe lote. (Mathayo 25:34; Luka 23:43) Upesi sasa, wale wanaoiharibu dunia watakuwa wametoweka, “bali wamngojao [Yehova] ndio watakaoirithi [dunia]. . . . Wenye upole watairithi dunia, [nao] watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:9-11) Nyote ushangilieni Ufalme wa Mileani wa Yehova Mungu kupitia “Mwana-Mfalme wa Amani” utakaofuata kutimizwa kwa agano jipya!
[Picha katika ukurasa wa 119]
Habari njema za Ufalme wa Mungu zitahubiriwa duniani pote kabla ya huu mfumo kwisha