Tengenezo na Kazi Yao ya Ulimwenguni Pote
Kuna viunganishi kadhaa vinavyotumiwa kuelekeza kazi ya kutoa ushahidi katika nchi zaidi ya 200 ambako inafanywa. Mwelekezo wa jumla unatoka kwa Baraza Linaloongoza katika makao makuu Brooklyn, New York. Baraza Linaloongoza hutuma wajumbe kila mwaka kwenye “maeneo ya dunia” 15 au zaidi ulimwenguni pote ili kushauriana na wajumbe wa matawi katika kila eneo la dunia. Katika maofisi ya tawi, kuna Halmashauri za Tawi zenye washiriki kuanzia watatu kufika saba wanaosimamia kazi katika mabara yaliyo chini ya mamlaka yao. Mengi ya matawi hayo yana vifaa vya kuchapia, mengine yakiwa yanaendesha matbaa za rotary zenye mwendo wa kasi sana. Nchi au eneo linalotumikiwa na kila tawi hugawanywa kuwa wilaya, na wilaya nazo hugawanywa kuwa mizunguko. Kila mzunguko una makundi kama 20. Mwangalizi wa wilaya hutembelea mizunguko ya wilaya yake kwa kuzunguka kwa zamu. Makusanyiko mawili yanafanywa kila mwaka kwa kila mzunguko. Pia kuna mwangalizi wa mzunguko, naye kwa kawaida hutembelea kila kundi katika mzunguko wake mara mbili kwa mwaka, akisaidia Mashahidi watengeneze na kuifanya kazi ya kuhubiri katika eneo ambalo kundi hilo limegawiwa.
Kundi la mahali penu na Jumba la Ufalme ndilo kitovu kinachotumiwa kuwaambia watu habari njema katika jumuiya yenu. Sehemu zilizo chini ya kila kundi hugawanywa kuwa maeneo madogo katika ramani. Hayo hugawiwa mashahidi mmoja mmoja ambao hujitahidi kutembelea kila nyumba na kusema na watu waliomo. Kila kundi, likiwa lenye Mashahidi wachache kufikia 200 hivi, lina wazee waliopewa mgawo wa kusimamia kazi mbalimbali. Kila mtangazaji mmoja mmoja wa habari njema ni wa muhimu sana katika tengenezo la Mashahidi wa Yehova. Kila mmoja wa Mashahidi, awe anatumikia katika makao makuu ya ulimwengu, katika matawi, au katika makundi, hufanya kazi hiyo ya shambani kwa yeye binafsi kuwaambia wengine juu ya Ufalme wa Mungu.
Mwishowe, ripoti za utendaji huo hufikia makao makuu ya ulimwengu, na Kitabu-Mwaka huandikwa na kutangazwa kila mwaka. Vilevile, chati hutangazwa kila mwaka katika toleo la Januari 1 la Mnara wa Mlinzi. Vichapo hivyo viwili hutoa ripoti zenye kueleza habari nyingi juu ya mambo yaliyotimizwa kila mwaka katika kutoa ushahidi kwa Yehova na Ufalme wake mikononi mwa Kristo Yesu. Kitabu-Mwaka cha 1991 charipoti kwamba katika 1990 Mashahidi na watu wenye kupendezwa 9,950,058 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Katika mwaka wa utumishi wa 1990, Mashahidi wa Yehova walitumia zaidi ya saa 895,229,424 wakitangaza habari njema na wapya 301,518 walibatizwa. Vitabu vilivyoangushwa vilijumlika vikawa mamia ya mamilioni ya nakala.