Sura 28
Kupatana Katika Upendo
1. (a) Wewe unawezaje kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu? (b) Halafu ni lazima utii amri gani?
UNAPOENDELEA kuongeza maarifa na kumthamini Yehova Mungu na makusudi yake, utataka ushirikiane kikawaida na watu walio na imani na tumaini ilo hilo. Kwa kufanya hivyo, utakuwa sehemu ya tengenezo la Mungu linaloonekana, udugu wa kweli wa Kikristo. Halafu itakuwa lazima utii amri inayosema “mwupende ushirika mzima wa ndugu.”—1 Petro 2:17; 5:8, 9, NW.
2. (a) Ni amri gani mpya ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake? (b) Semi hizi “mmoja na mwenzake” na “miongoni mwenu wenyewe” zinaonyesha nini waziwazi? (c) Kuwa na upendo ni kwa maana namna gani?
2 Yesu Kristo alikazia umaana wa wafuasi wake kupendana wao kwa wao. Aliwaambia hivi: “Mimi ninawapa ninyi amri mpya, mwonyeshane upendo mmoja na mwenzake . . . Kwa hiyo wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, ikiwa mnao upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35, NW) Semi hizi “mmoja na mwenzake” na “miongoni mwenu wenyewe” zinaonyesha waziwazi kwamba Wakristo wote wa kweli wangekuwa pamoja katika kikundi kimoja au tengenezo moja. (Warumi 12:5; Waefeso 4:25) Na tengenezo hilo lingetambuliwa kwa kupendana kwa washiriki walo. Mtu asipokuwa na upendo, mambo mengineyo yanakuwa ya bure tu.—1 Wakorintho 13:1-3.
3. Biblia inakaziaje umaana wa kupenda na kuwaangalia Wakristo wenzetu?
3 Kwa hiyo, Wakristo wa kwanza walikumbushwa mara nyingi hivi: “Mwe na wepesi wa kuonyeshana shauku mmoja na mwenzake.” “Mkaribishane mmoja na mwenzake.” “Mwe watumwa wa mmoja na mwenzake.” “Mwe wenye kuonyeshana fadhili mmoja na mwenzake, wepesi kuhurumia.” “Endeleeni kuchukuliana mmoja na mwenzake na kusameheana kabisa mmoja na mwenzake ikiwa ye yote ana sababu ya kulalamika juu ya mwenzake.” “Endeleeni kufarijiana mmoja na mwenzake na kujengana mmoja na mwenzake.” “Mwe wenye kuamanikana mmoja na mwenzake.”—Warumi 12:10; 15:7; Wagalatia 5:13; Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13, 14; 1 Wathesalonike 5:11, 13; 1 Petro 4:8; 1 Yohana 3:23; 4:7, 11, NW.
4. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba lazima Wakristo wapende watu wengine, zaidi ya ‘kupendana wao kwa wao’? (b) Hasa Wakristo wanapaswa kupenda nani?
4 Walakini, hiyo haina maana ya kwamba Wakristo wa kweli wanapaswa kuwapenda washiriki wenzao tu wa tengenezo la Mungu. Inawapasa vilevile kuwapenda wengine. Kwa kweli, Biblia inawasihi waongezeke “katika kuonyeshana upendo mmoja na mwenzake na wote.” (1 Wathesalonike 3:12; 5:15, NW) Akitoa maoni yanayofaa na yenye kusawazika, mtume Paulo aliandika hivi: “Na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10) Hivyo ijapokuwa inawapasa Wakristo wawapende watu wote, kutia na adui zao, sana-sana inawapasa wapende washiriki wenzao wa tengenezo la Mungu, ndugu na dada zao wa Kikristo.—Mathayo 5:44.
5. Ni nini kinachoonyesha kwamba Wakristo wa kweli. katika nyakati za kwanza na leo, wamejulikana kwa upendo wao?
5 Wakristo wa kwanza walijulikana kwa upendo huo walioonyeshana mmoja na mwenzake. Kulingana na Tertuliano, mwandikaji wa karne ya pili, watu walikuwa wakisema hivi juu yao: ‘Tazama wanavyopendana mmoja na mwenzake, na namna walivyo tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake!’ Upendo kama huo vilevile unaonwa kati ya Wakristo wa kweli leo. Lakini, je! hiyo ina maana ya kwamba hakuna hata kidogo matatizo wala magumu kati ya Wakristo wa kweli?
MATOKEO YA KUTOKAMILIKA
6. Ni kwa sababu gani hata Wakristo wa kweli nyakati nyingine wanatendana dhambi?
6 Kwa kujifunza kwako Biblia unajua kwamba sote tumerithi kutokamilika kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Warumi 5:12) Hivyo tuna maelekeo ya kufanya mabaya. “Sisi sote tunafanya makosa mara nyingi,” Biblia inasema. (Yakobo 3:2, HNWW; Warumi 3:23) Na imekupasa ujue kwamba washiriki wa tengenezo la Mungu vilevile ni watu wasiokamilika na mara nyingine wanafanya mambo yasiyofaa. Hiyo inaweza kutokeza matatizo na magumu hata kati ya Wakristo wa kweli.
7. (a) Ni kwa sababu gani Euodia na Sintike walihitaji kuambiwa “wawe na nia moja”? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba kwa asili hao walikuwa wanawake Wakristo wema?
7 Ifikirie hali ya wanawake wawili, Euodia na Sintike, katika kundi la kwanza la Filipi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Namsihi Euodia, namsihi na Sintike, wawe na nia moja katika Bwana.” Ni kwa sababu gani Paulo aliwatia moyo wanawake hao wawili “wawe na nia moja”? Kwa wazi, kulikuwako matata kati yao. Biblia haielezi yalikuwa matata gani. Labda walioneana wivu kwa njia fulani. Hata hivyo, kwa asili hao walikuwa wanawake wema. Walikuwa wamekuwa Wakristo kwa muda fulani, miaka iliyotangulia wakiwa wameshiriki na Paulo katika kazi ya kuhubiri. Hivyo aliliandikia kundi hilo hivi: “Uwasaidie wanawake hao; kwa maana waliishindania Injili pamoja nami.”—Wafilipi 4:1-3.
8. (a) Ni matata gani yaliyotokea kati ya Paulo na Barnaba? (b) Kama ungalikuwapo ukaona matata hayo, ungalikata shauri gani?
8 Siku moja vilevile kulitokea matata kati ya mtume Paulo na msafiri mwenzake Barnaba. Walipokuwa karibu kuondoka katika safari yao ya pili ya umisionari, Barnaba alitaka achukue Marko binamu yake aende pamoja nao. Walakini, Paulo hakutaka Marko aandamane nao, kwa vile Marko alivyokuwa amewaacha akarudi nyumbani wakati wa safari yao ya kwanza ya umisionari. (Matendo 13:13) Biblia inasema: “Ndipo kukatokea mfoko mkali wa hasira, hivi kwamba wakatengana mmoja na mwenzake.” (Matendo 15:37-40, NW) Ebu wazia hilo! Kama ungalikuwapo na kuona huo “mfoko mkali wa hasira,” je! ungalikata shauri kwamba Paulo na Barnaba hawakuwa sehemu ya tengenezo la Mungu kwa sababu ya mwenendo waliouonyesha wakati huo?
9. (a) Ni dhambi gani ambayo Petro alifanya, na ni nini kilichomfanya atende hivyo? (b) Paulo alifanya nini alipoona lililokuwa likitendeka?
9 Pindi nyingine mtume Petro alifanya kosa. Aliacha kushirikiana sana na Wakristo wa Mataifa wasio Wayahudi kwa sababu ya kuogopa kuchukiwa na baadhi ya Wakristo Wayahudi ambao kwa makosa walikuwa wakiwadharau ndugu zao wa Mataifa. (Wagalatia 2:11-14) Mtume Paulo alipoona jambo ambalo Petro alikuwa akifanya, aliulaumu mwenendo wa Petro usiofaa mbele ya wote wale waliokuwapo. Kama wewe ungalikuwa ndiwe Petro ungalionaje?—Waebrania 12:11.
KUMALIZA MAGUMU KWA UPENDO
10. (a) Petro alionaje alipoonyeshwa makosa? (b) Tunaweza kujifunza nini kwa mfano wa Petro?
10 Petro angaliweza kumkasirikia Paulo. Angaliweza kukwazwa na njia ambayo Paulo alikuwa ametumia ili kumwonyesha makosa mbele ya wengine. Lakini hakufanya hivyo. (Mhubiri 7:9) Petro alikuwa mnyenyekevu. Alikubali kuonyeshwa kosa. Naye hakuliruhusu jambo hilo lifanye upendo wake kwa Paulo upoe. (1 Petro 3:8, 9) Angalia namna Petro baadaye alivyomtaja Paulo katika barua ya kuwatia moyo Wakristo wenzake: “Ifikirieni saburi ya Bwana yetu kuwa wokovu, kama vile ndugu yetu mpendwa Paulo kulingana na hekima aliyopewa alivyowaandikia ninyi pia.” (2 Petro 3:15, NW) Ndiyo, Petro aliruhusu upendo ufunike gumu hilo, ambalo katika kisa hiki lilikuwa limetokana na mwenendo wake mbaya.—Mithali 10:12.
11. (a) Ijapokuwa walifanya mfoko wa hasira, Paulo na Barnaba walionyeshaje kwamba walikuwa Wakristo wa kweli? (b) Tunaweza kufaidikaje na mfano wao?
11 Namna gani lile tatizo lililokuwa kati ya Paulo na Barnaba? Hilo pia lilimalizwa kwa upendo. Kwa maana baadaye, Paulo alipoliandikia kundi la Korintho, alimtaja Barnaba kuwa mfanya kazi mwenzake aliye mkubwa sana. (1 Wakorintho 9:5, 6) Ijapokuwa Paulo anaonekana kuwa alikuwa na sababu nzuri ya kutilia mashaka ubora wa Marko kama mwenzi wa kusafiri nao, baadaye kijana huyo alikomaa kwa kiasi cha kwamba Paulo aliweza kumwandikia Timotheo hivi: “Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi.” (2 Timotheo 4:11) Tunaweza kufaidika na mfano huo wa kumaliza tofauti kati ya mtu na mwenzake.
12. (a) Sababu gani tunaweza kudhania kwamba Euodia na Sintike walimaliza tofauti zao? (b) Kulingana na Wagalatia 5:13-15, ni kwa sababu gani ni jambo la maana sana Wakristo wamalize tofauti zao kwa upendo?
12 Basi, namna gani Euodia na Sintike? Je! walimaliza tofauti zao, wakiruhusu upendo ufunike dhambi zo zote ambazo huenda walitendana? Biblia haituambii ilivyokuwa kwao mwishowe. Lakini, kwa sababu walikuwa wanawake wema waliokuwa wamefanya kazi pamoja na Paulo katika huduma yake ya Kikristo, tunaweza kudhani kwa kufaa kwamba walilikubali kwa unyenyekevu shauri walilopewa. Barua ya Paulo ilipopokewa, tunaweza kuwawazia wakiendeana na kutatua tatizo lao kwa roho ya upendo.—Wagalatia 5:13-15.
13. Ni mfano gani wa kuonyesha upendo ambao Yehova Mungu anaweka?
13 Huenda wewe pia ukaona ni vigumu kupatana na mtu fulani, au watu fulani, katika kundi. Ijapokuwa huenda wakawa watahitaji muda mrefu kusitawisha sifa za kweli za Kikristo, ebu fikiria hili: Je! Yehova Mungu anangoja mpaka watu waondoe njia zao zote zilizo mbaya kabla ya kuwapenda? Hapana; Biblia inasema: “Mungu anapendekeza upendo wake mwenyewe kwetu sisi kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda dhambi Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Warumi 5:8, NW) Tunahitaji kufuata mfano huo wa Mungu na kuwaonyesha upendo wale wanaofanya mambo mabaya na ya upumbavu.—Waefeso 5:1, 2; 1 Yohana 4:9-11; Za-buri 103:10.
14. Ni shauri gani ambalo Yesu alitoa juu ya kutokulaumu wengine?
14 Kwa kuwa sote ni watu wasiokamilika, Yesu alifundisha kwamba haitupasi tuwe wenye kulaumu wengine. Ni kweli kwamba wengine wana makosa, lakini hata sisi tuna makosa. “Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii?” Ye-su akauliza. (Mathayo 7:1-5) Kwa kulikumbuka shauri hilo lenye hekima, tutasaidiwa tupatane na ndugu na dada zetu.
15. (a) Ni kwa sababu gani ni jambo la maana tusamehe wengine hata tunapokuwa na sababu ya kuwalalamikia? (b) Katika mfano wake ulio katika Mathayo sura ya 18, Yesu alifundishaje uhitaji wa kusamehe?
15 Ni lazima kabisa tuwe wenye rehema na wenye kusamehe. Ni kweli kwamba huenda ukawa na sababu ya kweli ya kumlalamikia ndugu au dada. Lakini likumbuke shauri hili la Biblia: “Endeleeni kuchukuliana mmoja na mwenzake na kusameheana kabisa mmoja na mwenzake ikiwa ye yote ana sababu ya kulalamika juu ya mwenzake.” Lakini ni kwa sababu gani uwasamehe wengine unapokuwa na sababu ya kweli ya kuwalalamikia? Ni kwa sababu ‘Yehova alikusamehe wewe kabisa,’ Bi-lia inajibu. (Wakolosai 3:13, NW) Na ikiwa tunataka kupokea msamaha wake, Yesu alisema ni lazima tuwasamehe wengine. (Mathayo 6:9-12, 14, 15) Kama vile yule mfalme anayetajwa katika mmoja wa mifano ya Yesu, Yehova ametusamehe sisi mara maelfu, hivyo, je! sisi hatuwezi kusamehe ndugu zetu mara chache?—Mathayo 18:21-35; Mithali 19:11.
16. (a) Kulingana na 1 Yohana 4:20, 21, kumpenda Mungu kunahusianaje na kuwapenda Wakristo wenzetu? (b) Ni hatua gani inayohitaji kuchukuliwa iwapo ndugu yako ana neno juu yako?
16 Hatuwezi kuizoea kweli na wakati uo huo tuwe tukiwatenda ndugu na dada zetu kwa njia isiyo ya upendo, isiyo ya kusamehe. (1 Yohana 4:20, 21; 3:14-16) Hivyo, basi, ukikosana wakati wo wote na Mkristo mwenzako, usiache kusema naye. Usiweke kinyongo moyoni, lakini ondoeni tatizo hilo kwa roho ya upendo. Ikiwa wewe umemkosea ndugu yako, uwe tayari kuomba radhi na msamaha.—Mathayo 5:23, 24.
17. Ni mwendo gani unaofaa uchukue ikiwa mtu fulani anakukosea?
17 Lakini namna gani kama mtu anakutukana, au anakukosea kwa njia fulani nyingine? Biblia inashauri hivi: “Usiseme, Nitamtenda kama alivyonitenda mimi.” (Mithali 24:29; Warumi 12:17, 18) Yesu Kristo alishauri hivi: “Mtu akikupiga kofi shavu la kulia, mgeuzie pia shavu la pili.” (Matayo 5:39, HNWW) Kofi halikusudiwi kuumiza mtu kimwili, bali kutusi au kuchokoza tu. Kwa njia hiyo Yesu alikuwa akifundisha wafuasi wake waepuke kuvutwa kuingia katika pigano au ugomvi. Badala ya ‘kulipa watu ovu kwa ovu, au tusi kwa tusi,’ imekupasa ‘utafute amani na kuizingatia.’—1 Petro 3:9, 11, HNWW; Warumi 12:14.
18. Imetupasa tujifunze nini kwa mfano wa Mungu wa kupenda mataifa yote?
18 Kumbuka kwamba ni lazima ‘tuupende ushirika mzima wa ndugu.’ (1 Petro 2:17, NW) Yehova Mungu anaweka mfano. Yeye hana ubaguzi. Jamii zote za watu ni sawa machoni pake. (Matendo 10:34, 35; 17:26) Wale watakaolindwa kuipita ‘ile dhiki kuu’ inayokuja wanachukuliwa kutoka “kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” (Ufunuo 7:9, 14-17) Hivyo, kwa kumwiga Mungu, haitupasi kuwapenda wengine kidogo kwa sababu ati ni wa jamii ya watu tofauti, taifa tofauti au cheo tofauti, au wana rangi tofauti ya ngozi.
19. (a) Imetupasa tuwaone na kuwatendeaje Wakristo wenzetu? (b) Sisi tunaweza kuwa na pendeleo gani kubwa?
19 Pata kuwajua sana wote wale walio katika kundi la Kikristo, nawe utawapenda na kuwathamini. Watendee walio wakubwa kwa umri kama baba zako na mama zako, vijana kama ndugu na dada zako. (1 Timotheo 5:1, 2) Ni pendeleo kweli kweli kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu linaloonekana ambalo ni kama jamaa, ambalo washiriki walo wanapatana sana katika upendo. Itakuwa vizuri kama nini kuishi milele katika paradiso duniani pamoja na jamaa hiyo yenye upendo!—1 Wakorintho 13:4-8.
[Picha katika ukurasa wa 233]
Tunaweza kujifunza nini kwa tukio lililohusu Euodia na Sintike?
[Picha katika ukurasa wa 235]
Je! mabishano yaliyokuwa kati ya Paulo na Barnaba yalikuwa na maana ya kwamba wao hawakuwa washiriki wa tengenezo la Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 236]
Wakristo wa kweli wanaacha upendo ufunike sababu zote za kulalamika
[Picha katika ukurasa wa 237]
Ndani ya tengenezo la Mungu, Wakristo wanaongozwa na upendo wapatane kama watu walio sawa