Upendano Husitiri Wingi wa Dhambi
“Iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.”—1 Pet. 4:8.
1, 2. (a) Ni makosa gani ambayo sote tunafanya, na sababu gani huenda hata tukayafanya mara nyingi zaidi? (b) Ni nini kitakachotusaidia tushinde matatizo yanayotukia?
JE! WEWE umepata kusema vikali na mtu fulani, na mara hiyo ukaona ingekuwa heri kama hungesema hivyo? Au umepata kutenda bila huruma katika njia fulani, kisha ukasikitika? Bila shaka sote tumefanya hivyo. Wakati mikazo na shida juu yetu inapoongezeka wakati mwisho wa hii taratibu ya mambo unapokaribia karibu zaidi, huenda zitakuwa mara nyingi zaidi tutakapoumizana na kukasirikiana. Basi imetupasa tufanye nini wakati matatizo yanapotukia?
2 Katika kutafuta jibu ni jambo lenye msaada kuangalia kwa uangalifu yanayosemwa katika 1 Petro 4:7, 8. Hapo panatajwa kwamba, kwa kuwa mwisho wa mambo yote umekaribia, imetupasa ‘tuwe na akili, tukeshe katika sala,’ lakini hasa imetupasa tuwe na “juhudi nyingi katika kupendana.” Sasa angalia sababu inayotolewa juu ya upendo huu ulivyo wa maana sana. Habari yasema hivi: “Kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.” Hii ni sehemu ya maana sana kufikiria.
3. (a) Yatupasa sote tusemeje? (b) Ni maneno gani sahihi ambayo Biblia inasema juu yetu?
3 Ni lazima tuseme kwamba sisi sote tumerithi maelekeo ya kufanya makosa au dhambi kwa sababu ya kutokutii na kutokamilika kwa wazazi wetu wa kwanza Adamu na Hawa. (Rum. 5:12) Mara nyingi sote tunakosa kufuata yaliyo haki. Ndani yetu mna maelekeo ya kuwa wenye kuonea wivu, kukasirika, kujivuna, kuwa wasiosamehe, na mambo kama hayo. Je! sisi wenyewe hatukasiriki nyakati nyingine tunaposhindwa na maelekeo haya yenye dhambi? Hata hivyo maelekeo haya mabaya yako, na yatupasa tujue kwamba, pindi fulani, yataonekana katika maneno na matendo. Akiandika chini ya uongozi wa Mungu, mwanafunzi Yakobo alisema kwa usahihi hivi: “Twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu.” Lakini hakuna walio wakamilifu. “Hakuna mtu asiyetenda dhambi,” Biblia yasema.—Yak. 3:2; 1 Fal. 8:46.
4. (a) Maoni yetu yawe nini wakati dhambi zinapotokea, lakini yatupasa tufanye nini? (b) Ni nini kltakachotusaidia tuchunguze mambo kwa maoni yanayofaa wakati matatizo yanapotukia?
4 Hivyo ni jambo la lazima kuwa na maoni yanayofaa juu ya uhusiano wa sisi kwa sisi. Maelekeo yenye dhambi yataonekana katikati ya Wakristo, bila kujali kujitahidi kwetu kuzuia yasitokee. (Rum. 7:15-20) Haitupasi tushtuke na kuudhika mno, labda kukata shauri kwamba makosa haya ni ishara ya kwamba hatushirikiani na kundi la kweli la Kikristo. Sivyo; badala yake, imetupasa tutafute ushuhuda wa kuonyesha kwamba upendo umesitiri dhambi hizi. Kwa hiyo, ni jambo la lazima tujizoeze upendo tuonyeshe kwamba sisi ni sehemu ya kundi la kweli la Kikristo. Walakini, si vyepesi sikuzote kufanya jambo jema na lenye upendo. Biblia hutusaidia tufahamu hili. Inatufahamisha yaliyotokea katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza tuweze kusaidiwa kuchunguza mambo kwa maoni yanayofaa, ili tuwe na usawa ikiwa matatizo yanatokea.
WANAWAKE WAFILIPI WENYE TATIZO
5. (a) Ebu simulia machache juu ya mwanzo wa kundi la Filipi. (b) Mtume Paulo aliandikia kundi hilo barua ya namna gani?
5 Kwanza, na tufikirie hali iliyotokea katika kundi la Kikristo katika Filipi, mji mkuu wa wilaya ya Makedonia. Mtume Paulo alianzisha kundi hili katika mwaka wa 50 C.E. akiwa katika ziara yake wakati wa safari yake ya pili ya umisionari. (Matendo 16:11-40) Miaka michache baadaye, wakati wa safari yake ya tatu ya umisionari, kwa wazi Paulo aliweza kutembelea tena kundi la Filipi. (Matendo 20:1-6) Kisha, yapata miaka kumi baada ya kuanzisha kundi, Paulo alivutwa na matendo ya ajabu ya Wafilipi ya fadhili na bidii za Kikristo awaandikie barua yenye shauku ya upendo na kutia moyo. Aliwasifu sana katika barua yote, isipokuwa mtajo mfupi mmoja tu wa kutengeneza kosa mwishoni mwa barua yake.
6. Paulo aliandika nini juu ya Euodia na Sintike, na hili latokeza maulizo gani?
6 Paulo aliandika hivi: “Basi, ndugu zangu, wapendwa wangu, ninaowaonea shauku, furaha yangu, na taji yangu, hivyo simameni imara katika Bwana, wapenzi wangu.” Lakini ebu sasa angalia maneno yake yafuatayo: “Namsihi Euodia, namsihi Sintike, wawe na nia moja katika Bwana.” (Flp. 4:1, 2) Sababu gani Paulo alisema hivi? Sababu gani alilitia moyo kundi ‘lisimame imara katika Bwana,’ kisha akawachagua wanawake hawa wawili, Euodia na Sintike, na kuwasihi wawe na nia moja katika Bwana?
7. (a) Yaelekea ni sababu gani wanawake hawa wawili hawakuwa na nia moja katika Bwana? (b) Kujua kwa Paulo juu ya nia yao labda kunaonyesha nini?
7 Kwa wazi, lilikuwako tatizo fulani kati ya wanawake hawa wawili; kwa wazi hawakuungana katika nia moja. Sasa Biblia haituambii tatizo lao lilikuwa nini, au iliyokuwa sababu ya matata kati yao. Labda katika njia fulani walikuwa wakioneana wivu. Labda wote wawili hawakupatana tabia, na pengine waliudhiana hata wakaacha kusemezana. Bila kujali tatizo lilikuwa nini, kulikuwako mabishano fulani, kwa sababu hawakuwa na “nia moja katika Bwana.” Naye Paulo alijua hali hiyo mamia ya maili mbali katika Rumi, alikokuwa akiandika barua, kuonyesha kwamba labda tatizo hilo lilikuwa limekaa muda mrefu na kujulikana sana kati ya ndugu.
8. (a) Kwa asili, Euodia na Sintike walikuwa wanawake wa namna gani, na ni nini linaloonyesha hivi? (b) Twaweza kupata onyo gani kutokana na hayo yaliyotukia karne ya kwanza?
8 Hata hivyo, wakati uo huo, kwa asili hawa walikuwa wanawake wema wa Kikristo. Wote wawili walikuwa wakimtumikia Yehova Mungu pamoja na ndugu na dada zao. Kwa maana Paulo anaendelea kuliandikia kundi hivi: “Uwasaidie wanawake hao; kwa maana waliishindania Injili pamoja nami.” (Flp. 4:3) Hivyo Euodia na Sintike walikuwa wamekuwa Wakristo kwa muda fulani, wakiwa wamefanya kazi mwanzoni pamoja na Paulo katika kuendeshwa kwa kazi ya kuhubiri. Lakini sasa walikuwa na tatizo. Hivyo, basi, ikiwa matatizo kama haya yalikuwako katika kundi la karne ya kwanza, je! ituudhi mno ikiwa matatizo yanayofanana na hayo yanatukia leo? Lakini si wanawake peke yao waliokuwa na matatizo hayo.
MATATIZO KATI YA WAZEE WA KIKRISTO
9, 10. (a) Ni nini lililokuwa limempata Yohana Marko wakati wa safari ya kwanza ya umisionari ya Paulo na Barnaba? (b) Sababu gani Barnaba alitaka kumchukua Marko katika safari ya pili ya umisionari, ingawaje mawazo ya Paulo yalikuwa nini?
9 Wazee wa Kikristo, pia, walikuwa na matatizo, hata wazee wenye kujulikana sana. Ebu mfikirie mtume Paulo na msafiri mwenzake wa kwanza Barnaba, kwa mfano. Walikuwa wamemaliza safari ya kwanza ya umisionari, wakianzisha makundi fulani ya Kikristo, na sasa walikuwa wakifikiria safari ya pili, kama Biblia inavyoeleza: “Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! turejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la [Yehova], wa hali gani.” (Matendo 15:36) Yohana Marko alikuwa ameandamana nao katika safari hiyo ya kwanza, lakini kwa sababu fulani isiyofunuliwa, habari yasema hivi, “Yohana akawaacha akarejea Yerusalemu,” alikoishi Mariamu, mama yake.—Matendo 13:13.
10 Hivyo, wakati Paulo na Barnaba walipokuwa wakizungumza juu ya safari yao ya pili ya umisionari, Marko akatajwa. Biblia yatuambia yaliyotukia: “Barnaba akaazimu kumchukua Yohana aliyeitwa Marko pamoja nao. Bali Paulo hakuona vema kumchukua huyo aliyewaacha huko Pamfilia, asiende nao kazini.” (Matendo 15:37, 38) Hivyo hapa palikuwa na tofauti ya maoni. Labda Barnaba aliona kwamba Marko alikuwa na sababu nzuri ya kurudia Yerusalemu wakati wa safari ya kwanza; pengine mama yake alikuwa mgonjwa naye akarudi akawe pamoja naye. Hatujui. Lakini, kwa upande mwingine, ikiwa kuondoka kwa Marko kweli kulikuwa bila kufikiri, kusiko na sababu, kwa wazi Barnaba aliona kwamba Marko alikuwa ameonywa na wakati huu angeendelea na kazi. Lakini Paulo hakudhani hivyo. Yeye hakutaka Marko afuate. Sasa, je! wewe hungedhani kwamba wazee hawa wa Kikristo waliokomaa wangeweza kumaliza tatizo katika njia yenye amani? Lakini kukatukia nini?
11. (a) Ni nini yaliyokuwa matokeo ya kutopatana huku kwa Paulo na Barnaba juu ya Marko? (h) Je! tatizo hili kati ya wazee wa Kikristo laonyesha kwamba hawakuwa watumishi wa kweli wa Mungu?
11 Biblia yasema hivi: “Basi palitokea mashindano [makali] baina yao hata wakatengana. Barnaba akamchukua Marko akatweka kwenda Kipro. Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka.” (Matendo 15:39, 40) Waweza kuwazia hilo! Wazee hawa wawili wenye kujulikana sana hawakuwa na mabishano kidogo, bali “mashindano [makali]” kati yao, juu ya jambo dogo sana. Hivyo wakatengana, kwa wazi bila kuoneana vizuri. Kama ungalikuwako huko na kuona haya, je! ungalikata shauri kwamba bila shaka hili si tengenezo la Mungu, kwa sababu ya namna wazee hawa wenye kujulikana sana walivyokuwa wametenda?
12. Ni dhambi gani ambayo Petro alifanya wakati wa kutembelea Antiokia, na ni sababu gani iliyomfanya atende hivi?
12 Au ebu fikiria tukio jingine ambalo ni tofauti kidogo, lililotukia katika Antiokia. Wakati mtume Petro alipoutembelea mji huu katika Shamu, alishirikiana na kundi zima, akila na kuongea bila kuogopa na kwa uhuru katika nyumba za waamini wa Mataifa. Alijua kwamba ilifaa kufanya hivi, kwa kuwa, miaka iliyotangulia, alikuwa ameongozwa na Mungu kwenda kumhubiri Kornelio, aliyegeuka kuwa mwongofu wa Mataifa wa kwanza asiyetahiriwa kuwa Mkristo. Walakini, wakati Wakristo fulani wa Kiyahudi, waliotoka kwa Yakobo ndugu mzazi mmoja na Yesu katika Yerusalemu, walipotembelea Antiokia, kwa kuogopa asilaumiwe na “waliotahiriwa,” Petro alianza kutoka na kujitenga na Wakristo wa Mataifa. Vilevile Wakristo wa Kiyahudi huko wakaanza kufanya hivyo. Kwa wazi hivi havikuwa vizuri: Ilikuwa dhambi upande wa Petro kuleta mtengano huo katika kundi la Kikristo.
13. (a) Maoni ya Paulo yalikuwa nini wakati alipokuwa Antiokia akaona yaliyokuwa yakitukia? (b) Ni kwa sababu gani Petro alikuwa mnafiki katika matendo yake, hata hivyo ilikuwa kama nini kuonyeshwa makosa mbele ya kundi lote?
13 Wakati kama huu mtume Paulo pia alikuwa katika Antiokia, naye akakasirishwa na aliyoona yakitukia. Katika barua yake kwa Wagalatia, alieleza hivi: “Nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa [Petro] mbele ya wote, Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa kufuata desturi za Wayahudi?” (Gal. 2:11-14) Petro alijua kwamba ile torati ya Musa haikuwa ikitumika tena, na alikuwa ametangulia kuonyesha hivi kwa kushirikiana kwa uhuru pamoja na Mataifa. (Matendo 10:28, 29) Ingawa hivyo sasa, kwa sababu ya kuogopa, alikuwa akianzisha tena mitengano iliyotolewa chini ya torati ya Musa, lakini Torati aliyojua haiwahusu tena Wakristo wa Kiyahudi. (Efe. 2:13-18) Hivyo ‘kurudi kwake nyuma na kujitenga’ na Wakristo wa Mataifa kwa wazi kulikuwa tendo la kinafiki lililosababishwa na kuogopa ambavyo Wakristo fulani wa Kiyahudi, hasa wale wa Yerusalemu, wangemfikiria. Na hivyo, Paulo aliufunua unafiki wa Petro mbele ya kundi zima. Wewe ungalionaje ikiwa ungalikuwa Petro?—Ebr. 12:11.
KUACHA UPENDANO USITIRI DHAMBI
14. (a) Petro angaliweza kuonaje juu ya kupokea karipio hili kutoka kwa Paulo? (b) Walakini, ni maoni gani juu ya Paulo baadaye yanaonyesha kwamba Petro aliacha upendano usitiri dhambi yake hii?
14 Ebu fikiria namna Petro angaliweza kuona. Alikuwa mtu mwenye kujulikana sana kati ya mitume, akiwa amekwisha kutangulia kupewa mapendeleo ya pekee ya utumishi na Yesu Kristo mwenyewe. (Mt. 16:18, 19; Matendo 2:14-41; 10:34-48) Paulo alikuwa mpya zaidi katika tengenezo la Kikristo, na tazama sasa akimpinga Petro kinaganaga (macho kwa macho) mbele ya kundi lote. Kwa hasira kali Petro angaliweza kuona hivi, ‘Paulo anathubutuje kusema nami namna ile mbele ya kundi.’ Lakini sivyo, Petro alikuwa mnyenyekevu. Alikubali onyo, na hakuliruhusu limfanye aache kumpenda Paulo. Kwa maana angalia namna Petro alivyoelekeza kwa Paulo katika barua ya kuwatia moyo Wakristo wenzake: “Uhesabuni uvumilivu wa Bwana wetu kuwa ni wokovu, kama vile na ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa.” (2 Pet. 3:15) Ndiyo, Petro aliacha upendano usitiri hilo tatizo, lililokuwa limetokana na dhambi yake mwenyewe. Bila shaka Petro alionyesha sifa inayotofautisha kundi la kweli la Kikristo!
15. (a) Je! tatizo kati ya Paulo na Barnaba lilitatuliwa, na ni jambo gani linaloonyesha kwamba lilitatuliwa? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba labda Paulo alikubali makosa yo yote ya kumhukumu Marko?
15 Namna gani tatizo kati ya Paulo na Barnaba lililotokea katika habari ya kumchukua Marko katika safari pamoja nao? Je! tatizo hili, ambalo mwisho wake ukawa mashindano makali lilifunikwa pia baadaye na upendano? Ndiyo, yaonekana ilikuwa hivyo. Kwa maana baadaye Paulo alipoliandikia kundi la Korintho wakati alipokuwa akifanya kazi ya umisionari katika Efeso, alisema juu ya Barnaba, pamoja na Petro na mitume wengine, kama wafanya kazi wenzake wa karibu. (1 Kor. 9:5, 6) Kwa wazi Paulo alikubali makosa yake yo yote ya kumhukumu Marko, na labda alimwomba radhi Marko na pia Barnaba kwa unyenyekevu. Kwa maana baadaye Paulo anamsifu Marko. Hasa, katika mojawapo ya barua zake kwa Timotheo, aliandika hivi: “Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi.”—2 Tim. 4:11; Kol. 4:10.
16. (a) Je! ni jambo la busara kudhani kwamba Euodia na Sintike walitatua matatizo yao? (b) Hata hivyo, yaelekea wangaliweza kuonyesha maoni gani mabaya?
16 Basi, namna gani Euodia na Sintike? Je! walitatua matatizo yao, wakiacha upendano usitiri dhambi zo zote ambazo labda walitendeana? Biblia haituambii yaliyotukia kwao mwishowe. Lakini kwa vile walikuwa wanawake wema waliokuwa wamejitahidi kwa umoja pamoja na Paulo katika huduma yake ya Kikristo, twaweza kudhania kwa kufaa kwamba walipokea kwa unyenyekevu shauri lililotolewa. Wakati barua ya Paulo iliposomwa, twaweza kuwazia kwamba baada ya mkutano waliendeana na kutatua tatizo lao katika roho ya upendano. Kwa upande mwingine, wangaliweza kushupazwa na shauri lililotolewa. Wangaliweza kuwa na maoni haya: ‘Paulo ana haki gani kuandikia kundi lote juu ya tatizo letu?’ Na hivyo matatizo yao hayangaliweza kutatuliwa, hata kuwa mabaya zaidi. Namna gani kama ingetokea hivi?
17. (a) Kama Euodia na Sintike hawangetatua matatizo yao, yangalitokea mambo gani? (b) Je! leo twaweza kujifunza jambo fulani kutokana na mambo hayo yanayoelekea kutokea?
17 Basi, barua hii kwa Wafilipi iliandikwa wapata mwaka wa 60 C.E. Miaka michache baadaye, mwaka wa 64 C.E,, mtawala wa Kirumi Nero kama inavyosemekena aliuteketeza mji wa Rumi kisha akawalaumu Wakristo kwamba ndio waliofanya hivyo. Upesi baadaye kulitokea mateso makuu juu ya Wakristo. Namna gani kama mateso haya yangeenea Filipi pia, na Euodia na Sintike wakatiwa gerezani, kama walivyofanywa Paulo na Sila, miaka iliyotangulia? (Matendo 16:19-34) Namna gani kama wangewekwa katika gereza moja, na kuwa pamoja katika chumba kimoja cha gereza? Basi, kama hawakuwa wenye nia moja, na kama matatizo yao yangekuwa yamekuwa makubwa hata wakachukiana, jambo gani lingaliweza kutukia? Wangaliweza kuharibiana kiroho, labda wakiharibiana uhusiano na Yehova Mungu. Hilo lingalikuwa jambo la kusikitisha kama nini! Na litakuwa jambo la kusikitisha kama nini leo ikiwa hatuna upendano mwingi sana wakati “dhiki kubwa” itakapokuja juu ya taratibu hii ya mambo!—Mt. 24:21.
UPENDANO WA LAZIMA SANA MWISHO UKARIBIAPO
18. (a) Ni lazima tujifunze kufanya nini? (b) Mwisho unapokaribia, ni hali gani ya ulimwengu inayoelekea kuwa yakazia lazima ya kuwapenda ndugu na dada katika kundi letu wenyewe?
18 Hili ni jambo tunalopaswa tulifikirie sana. Mwisho wa mambo yote umekaribia, na ni lazima tusitawishe upendano mwingi ili ‘usitiri wingi wa dhambi’ tulizo nazo sote. (Yak. 3:2) Ni lazima tuwapende ndugu na dada zetu bila kujali makosa yao, tabia zao zenye kuudhi, au mambo mengine juu yao ambayo huenda ni yenye kuchukiza kwetu. Kwa maana ebu fikiri juu yake: Wakati taratibu hii inapokaribia kuanguka kabisa katika “dhiki kubwa,” na bila shaka njia za kupashana habari zinapoharibika na njia za kisasa za kusafiria zinapokuwa haziwezekani, utaweza kupata habari kutoka kwa akina nani uwape msaada na kupokea msaada kutoka kwao? Si ndugu zetu walio katika kundi la mbali maili elfu moja, maili mia moja, au labda hata maili ishirini au kumi. Sivyo, bali Yehova Mungu amewatoa Wakristo wenzetu katika kundi letu wenyewe watutie nguvu na kutusaidia. Ni watu hawa walio karibu nasi hasa, washiriki wetu wa Kikristo walio karibu sana, ndio lazima tupende nasi tupendwe nao. Lo! namna uhusiano huu wa karibu sana utakavyokuwa wenye maana katika nyakati zenye taabu zilizoko mbele!
19. Huenda matokeo yakawa nini tukishindwa kuwa na upendano mwingi sana?
19 Tusipokuwa na upendano mwingi sana kwa wale waliomo katika kundi letu wenyewe, matokeo yaweza kuwa mabaya sana. Mtume Paulo alionyesha hili alipokuwa akiwaandikia Wakristo katika Galatia, ambao kwa wazi walikuwa na tatizo fulani katika kupatana pamoja. Alisihi hivi: “Tumikianeni kwa upendo. Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako. Lakini mkiumana na kulana, angalieni msije mkaangamizana.” (Gal. 5:13-15) Ndiyo, kama hatuna upendano, huenda tukavunjana na hata kuharibiana uhusiano na Yehova. Jambo hili lingeweza kutokeza kukosa kwetu kuokoka “dhiki kubwa” iliyo karibu sana!
20. Biblia yaonyeshaje kwamba lazima kumpenda Mungu kufuatane na kuwapenda ndugu zetu?
20 Hivyo, basi, ni lazima kweli tujitahidi kusitawisha upendano. Hatuwezi kuwa tukizoea kweli na wakati uo huo tuwaonee ndugu zetu kinyongo, au katika njia nyingine tuwatendee katika njia isiyo ya upendo. Biblia ni wazi sana juu ya jambo hili, ikisema hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.” Hakuna shaka juu yake, tuna wajibu wa kupendana.—1 Yohana 4:20, 21; 3:14-16.
JIFUNZE KWA WAALIMU BORA
21. (a) Huenda wengine wakaonaje juu ya ndugu zao? (b) Hata hivyo Yehova Mungu anatoa mfano gani katika kuonyesha upendo?
21 Lakini huenda mtu fulani akasema hivi: “Wewe hufahamu. Wengine katika kundi letu hawatendi kama Wakristo wa kweli. Njia zao zinakasirisha sana na kuchukiza mno.” Inaweza kuwa kwamba inachukua watu wengine muda mrefu kusitawisha sifa za kweli za Kikristo. Hata hivyo Yehova Mungu, Muumba wetu mkamilifu, awapenda. Yeye hangojei mpaka tuwe karibu na kukamilika, au hata mpaka tuanze kubadili utu wetu kupatana na njia zake, kabla hajatupenda. Sivyo, bali Biblia yasema hivi: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Rum. 5:8) Ndiyo, tulipokuwa tungali twaendelea sana na mwendo wa kufanya makosa na kuwa na nia zenye kuchukiza mno, zenye choyo, Yehova alitupenda. Huu ndio mfano tunaokaribishwa tuufuate katika kuonyesha upendo.—Efe. 5:1, 2.
22, 23. (a) Ni tabia gani mbaya iliyojifunua katikati ya mitume wa Yesu karibu na Kapernaumu? (b) Tabia hii ilijifunuaje tena, na ni shauri gani ambalo Yesu alitoa?
22 Yesu Kristo, pia, alituwekea sisi mfano mzuri sana katika jambo hili. Alijikusanyia wanafunzi ambao kwa asili walikuwa watu wema. Ingawaje, walikuwa na tabia mbaya. Kwa mfano, wakiwa njiani kuelekea Kapernaumu, walianza kubishana. Habari ya Biblia yasema hivi: “Wakafika Kapernaumu; hata [Yesu] alipokuwamo nyumbani, akawauliza, Mlishindania nini njiani? Wakanyamaza; kwa maana njiani walikuwa wakibishana wao kwa wao, ni nani aliye mkubwa.” Basi Yesu akamleta mtoto mchanga katikati yao, akaweka mikono yake juu yake, akawaambia wanafunzi wake kwamba ni lazima wajinyenyekeze wenyewe kama watoto wachanga, wasitafute ukubwa.—Marko 9:33-37; Mt. 18:1-6.
23 Walakini, muda si muda, walipokuwa wakikaribia Yerusalemu, mitume Yakobo na Yohana wakamjia Yesu wakamwomba vyeo viwili vilivyo vikubwa kuliko vyote katika ufalme wake, mmoja akiwa mkono wake wa kuume na mwingine mkono wake wa kushoto. Biblia yasema hivi: “Hata wale kumi waliposikia wakaanza kuwakasirikia Yakobo na Yohana.” Hivyo Yesu akawakemea tena juu ya tabia hii iliyokuwa ndani yao wakati huo. Akawaambia hivi: “Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote.”—Marko 10:35-45.
24. (a) Ni mfano gani wa unyenyekevu ambao Yesu aliwekea mitume wake katika kula chakula cha mwisho cha Kupitwa pamoja, hata hivyo upesi baada ya hapo walikuwa wakibishania nini? (b) Yesu aliendeleaje kuwaonyesha mitume wake upendo, na kwa matokeo gani?
24 Labda kulipita kama juma baadaye Yesu alipokutana ale chakula chake cha mwisho cha Kupitwa pamoja na wanafunzi wake. Yeye alilijua tatizo lililokuwa kati yao; basi yaelekea karibu na mwanzo wa chakula hicho cha mwisho pamoja nao, Yesu alifanya nini? Alichukua bakuli, akalijaza maji, akamwendea mmoja mmoja wa mitume akawaosha miguu yao! (Yohana 13:4-17) Lo! ni mfano bora wa unyenyekevu kama nini kwao kufuata! Ingawaje kukatukia nini baadaye, wakati wa jioni ile ile? Biblia yatuambia hivi: “Yakatokea mashindano kati yao, kwamba ni nani anayehesabiwa kuwa mkubwa.” (Luka 22:24) Waweza kuwazia hilo! Hata hivyo Yesu hakukata tamaa na kwa kuchukia sana, kusema hivi, ‘Ninyi watu ni bure kabisa. Nachoka na ninyi. Hamtajifunza kamwe kuwa wanafunzi wangu wa kweli.’ Hapana, bali wakati walipokuwa wangali wakionyesha tabia hizo zenye dhambi, Yesu aliwapenda. Aliendelea kuwaonya kwa upole na kuwashauri. (Luka 22:25-27) Na mwishowe walijifunza, na baadaye wakafanya kazi katika umoja, bila hata mmoja kati yao kwa kutaka makuu akitafuta ukuu na sifa.
25. (a) Ni faida gani itakayotokana na kuuacha upendano usitiri dhambi? (b) Sababu gani ni lazima sana tuwe na upendano mwingi sana sasa?
25 Kweli kweli upendano ‘utasitiri wingi wa dhambi.’ Hasa, kwa kujizoeza upendano—kwa kuwa wenye kusamehe, na kwa kusaidiana na kuonyana kwa upole—tutazuia dhambi zisifanyize madhara au matatizo yenye kuchukua muda mrefu. Usisahau kamwe aliyoandika mtume Petro juu ya maana ya upendano katika wakati huu wenye hatari katika historia: “Mwisho wa mambo yote umekaribia,” akasema. “Basi, iweni na akili, mkeshe katika sala. Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.” Bila shaka ni lazima tujizoeze upendano mwingi sasa. Kuokoka kwetu kwenyewe kuingia katika taratibu mpya yenye haki ya Mungu kwategemea tufanye hivyo.—1 Pet. 4:7, 8.
—Kutoka The Watchtower, June 1, 1975.
[Picha katika ukurasa wa 545]
Ili kusaidia wanafunzi wake washinde tabia mbaya, Yesu alimleta mtoto katikati yao akawaambia ni lazima wajinyenyekeze wenyewe kama watoto wachanga