Misa
Maana: Kama inavyoelezwa na Kundi Takatifu la Ibada za Kanisa Katoliki, Misa ni “—Dhabihu ambayo katika hiyo Dhabihu ya Msalaba inadumishwa;—Ukumbusho wa kifo na ufufuo wa Bwana, aliyesema ‘fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu’ (Luka 22:19);—Karamu takatifu ambapo, kupitia ushirika wa Mwili na Damu ya Bwana, Watu wa Mungu hushiriki faida za Dhabihu ya Pasaka, hufanya upya Agano Jipya ambalo Mungu amefanya pamoja na wanadamu mara moja kwa wakati wote kupitia Damu ya Kristo, na katika imani na tumaini hutangulia kuonyesha na kutarajia karamu ya mwisho katika ufalme wa Baba, wakitangaza kifo cha Bwana ‘hata ajapo.’” (Eucharisticum Mysterium, Mei 25, 1967) Hiyo ndiyo njia ya Kanisa Katoliki ya kufanya kile wanachoelewa kwamba Yesu Kristo alifanya katika Mlo wa Jioni wa Bwana.
Je, mkate na divai vinabadilishwa hakika na kuwa mwili na damu ya Kristo?
Katika “Ungamo Zito la Imani” Juni 30, 1968, Papa Paulo wa Sita alitangaza hivi: “Tunaamini kwamba kama vile mkate na divai vilivyotakaswa na Bwana katika Mlo wa Jioni wa Bwana vilibadilishwa vikawa Mwili Wake na Damu Yake ambavyo vilipasa kutolewa kwa ajili yetu juu ya msalaba, vivyo hivyo mkate na divai vinavyotakaswa na padri vinabadilishwa na kuwa Mwili na Damu ya Kristo aliyetawazwa kwa utukufu mbinguni, na Sisi tunaamini kwamba kuwapo kwa kifumbo kwa Bwana, chini ya kuonekana kwa vitu hivyo vinavyoonekana kwa hisia zetu kuwa ni vilevile baadaye kama kabla ya Utakaso, ni kuwapo ambako ni kwa kweli na halisi. . . . Kwa kufaa, Kanisa linaliita badiliko hilo la kifumbo kuwa kubadilika kwa mkate na divai kuwa mwili na damu halisi ya Kristo.” (Official Catholic Teachings—Christ Our Lord, Wilmington, N.C.; 1978, Amanda G. Watlington, uku. 411) Je, Maandiko Matakatifu yanakubaliana na imani hiyo?
Yesu alimaanisha nini aliposema, “Huu ndio mwili wangu,” “Hii ndiyo damu yangu”?
Mt. 26:26-29, UV: “Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akisema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki, kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.”
Kuhusu maneno “huu ndio mwili wangu” na “hii ndiyo damu yangu,” kumbuka mambo haya yafuatayo: Mo husema hivi, “huu unamaanisha mwili wangu,” “hii inamaanisha damu yangu.” (Italiki zimeongezwa.) NW husema vivyo hivyo. LEF hutafsiri maneno hayo hivi, “huu unawakilisha mwili wangu,” “hii inawakilisha damu yangu.” (Italiki zimeongezwa.) Tafsiri hizo zinapatana na yale yanayosemwa katika muktadha, katika mstari wa 29, katika chapa mbalimbali za Kikatoliki. VB husema hivi: “Sitakunywa tena mazao haya ya mzabibu, mpaka siku ile nitakapokunywa yale mapya, pamoja nanyi, katika ufalme wa Babangu.” (Italiki zimeongezwa.) UV, ZSB, BHN pia huonyesha Yesu akielekeza kwenye kile kilichokuwa katika kikombe kama “uzao huu wa mzabibu,” “matunda ya mizabibu,” “divai ya zabibu,” na hiyo ilikuwa baada ya Yesu kusema, “Hii ndiyo damu yangu.”
Fikiria maneno “huu ndio mwili wangu” na “hii ndiyo damu yangu” kwa kukumbuka maneno mengine yaliyo wazi yanayotumiwa katika Maandiko. Yesu pia alisema, “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu,” “Mimi ndimi mlango wa kondoo,” “Mimi ndimi mzabibu wa kweli.” (Yoh. 8:12; 10:7; 15:1, UV) Je, lolote kati ya maneno hayo lilimaanisha kubadilika kimuujiza?
Katika andiko la 1 Wakorintho 11:25 (UV), mtume Paulo aliandika kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana na kutoa mawazo hayohayo kwa kutumia maneno tofauti kidogo. Badala ya kumnukuu Yesu akisema hivi kuhusu kikombe, “Nyweni nyote katika hiki . . . kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano,” alitumia maneno haya: “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu.” Hakika hilo halikumaanisha kwamba kikombe hicho kilibadilishwa kimuujiza na kuwa agano jipya. Je, si jambo linalopatana na akili zaidi kukata shauri kwamba kilichokuwa katika kikombe kiliwakilisha damu ya Yesu ambayo ilihalalisha agano jipya?
Yesu alimaanisha nini aliposema maneno yaliyo katika Yohana 6:53-57?
“Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi.”—Yoh. 6:53-57, UV.
Je, ieleweke kwamba hayo yanamaanisha walipaswa kula kihalisi mwili wa Yesu na kunywa damu yake? Ikiwa ingekuwa hivyo, Yesu angekuwa akiunga mkono kuvunjwa kwa Sheria ambayo Mungu alikuwa amewapa Waisraeli kupitia Musa. Sheria hiyo ilikataza kula aina yoyote ya damu. (Law. 17:10-12) Kinyume cha kuunga mkono jambo kama hilo, Yesu alipinga kabisa kuvunjwa kwa takwa lolote la Sheria hiyo. (Mt. 5:17-19) Kwa hiyo jambo ambalo Yesu alikuwa nalo akilini lazima lilikuwa kula na kunywa kwa maana ya mfano, yaani, kuwa na imani katika dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu.—Linganisha na Yohana 3:16; 4:14; 6:35, 40.
Je, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wafanye ukumbusho wa kifo chake tu, au pia wafanye kawaida ya ibada ambayo kwa hakika ingefanya upya dhabihu yake?
Kulingana na kichapo The Documents of Vatican II: “Katika Mlo wa Jioni wa Bwana, katika usiku ambao Yeye alisalitiwa, Mwokozi wetu alianzisha Dhabihu ya Ekaristi ya Mwili na Damu Yake. Yeye alifanya hivyo ili adumishe dhabihu ya Msalaba . . . ”—(New York, 1966), kilichohaririwa na W. M. Abbott, S.J., uku. 154; italiki zimeongezwa.
The Catholic Encyclopedia inasema hivi: “Kanisa linakusudia Misa ionwe kuwa ‘dhabihu ya kweli na halisi’ . . . Hata hivyo, chanzo kikuu cha fundisho letu ni mapokeo, ambayo tangu nyakati za zamani zaidi yanatangaza thamani ya uombezi ya Dhabihu ya Misa.”—(1913), Buku la 10, uku. 6, 17.
Yesu mwenyewe alisema: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” (Luka 22:19; 1 Kor. 11:24, UV) Katika Luka 22:19, BHN na ZSB husema hivi: “Fanyeni hivi kwa kunikumbuka.” Yesu hakusema kwamba jambo alilofanya katika Mlo wa Jioni wa Bwana lilikuwa dhabihu yake mwenyewe wala hakusema kwamba wanafunzi wake walipaswa kufanya upya dhabihu yake.
Ebr. 9:25-28, UV: “Wala si kwamba ajitoe mara nyingi, kama vile kuhani mkuu [Myahudi] aingiavyo katika patakatifu kila mwaka kwa damu isiyo yake; kama ni hivyo ingalimpasa kuteswa mara nyingi tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu; lakini sasa, mara moja tu, . . . amefunuliwa, azitangue dhambi kwa dhabihu ya nafsi yake. Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu; kadhalika Kristo naye, akiisha kutolewa sadaka mara moja.” (Italiki zimeongezwa.)
Je, yote hayo ni “fumbo lisiloweza kufahamika”?
Biblia inasema kuhusu mafumbo ya Mungu, au siri takatifu. Lakini hakuna moja la mafumbo hayo linalopingana na kweli za Kimaandiko zilizoandikwa waziwazi. Kuhusu wale waliotanguliza mapokeo yao badala ya Maandiko, Yesu alisema: “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”—Mt. 15:7-9, UV.
Je, Yesu alikusudia ukumbusho huo ufanywe labda kila siku au kila juma?
Kichapo Basic Catechism kinasema: “Kazi za Pekee za Wakristo Wakatoliki” hutia ndani “kushiriki Misa kila Jumapili na sikukuu ya amri.” (Boston, 1980, uku. 21) “Kwa hakika waamini wanatiwa moyo kushiriki Misa na kupokea Komunyo mara kwa mara, hata kila siku.”—The Teaching of Christ—A Catholic Catechism for Adults, Chapa Iliyofupishwa (Huntington, Ind.; 1979), uku. 281.
Je, marejeo yote katika Maandiko kuhusu “kuumega mkate” yanaonyesha kwamba kifo cha Kristo kilikuwa kikikumbukwa? (Mdo. 2:42, 46; 20:7, UV) Yesu ‘aliimega mikate’ walipokuwa wakila chakula hata kabla ya Mlo wa Jioni wa Bwana. (Marko 6:41; 8:6) Mkate uliotumiwa na Wayahudi wakati huo haukuwa ule ambao watu wengi wanaujua leo. Wakati wa kuula, mara nyingi waliumega au kukata kipande.
Yesu hakutaja waziwazi Ukumbusho wa kifo chake ulipaswa kufanywa mara ngapi. Hata hivyo, aliuanzisha kwenye tarehe ya Pasaka ya Wayahudi, sikukuu ambayo, kwa wanafunzi wake, mahali pake palichukuliwa na Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Pasaka ilikuwa sherehe ya kila mwaka, iliyofanywa Nisani 14. Vivyo hivyo, sherehe za Wayahudi, yaani, Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, Sherehe ya Majuma (Pentekoste), Sherehe ya Vibanda, au ya Kukusanya, na Siku ya Upatanisho zote zilifanywa mara moja kila mwaka.
Je, kutolewa kwa Misa kunazisaidia nafsi zilizo toharani (purgatori)?
Kichapo The Teaching of Christ—A Catholic Catechism for Adults kinasema: “Neno hili ‘toharani’ halimo katika Biblia, wala fundisho la toharani halifundishwi waziwazi katika Biblia. . . . Vitabu vya Mababa vina marejeo mengi si kuhusu kuwako kwa toharani tu, bali pia uhakika wa kwamba waamini waliokufa wanaweza kusaidiwa kwa sala za walio hai, hasa kwa Dhabihu ya Misa.”—Uku. 347, 348.
Kuhusu hali ya wafu, Maandiko Matakatifu yanasema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhu. 9:5, UV) “Nafsi [“roho,” UV; “yeyote,” BHN] inayofanya zambi, itakufa.” (Eze. 18:4, ZSB) (Ona pia ukurasa wa 102-104, chini ya kichwa “Kifo.”)