Kuwasiliana na Pepo
Maana: Imani ya kwamba sehemu ya roho ya wanadamu huendelea kuishi baada ya mwili kufa nayo inaweza kuwasiliana na watu walio hai, kwa kawaida inafanya hivyo kupitia mtu anayepitisha habari hizo. Watu fulani huamini kwamba kila kitu chenye mwili na matukio yote ya asili yana roho ndani yake. Ulozi ni kutumia nguvu ambazo inakubaliwa kwamba zinatoka kwa roho waovu. Namna zote za kuwasiliana na pepo zinashutumiwa katika Biblia.
Je, kweli mwanadamu anaweza kuwasiliana na “roho” ya mpendwa aliyekufa?
Mhu. 9:5, 6, 10: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe . . . Pia, upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea, na mpaka wakati usio na kipimo hawana fungu lolote tena katika chochote ambacho kitafanywa chini ya jua. Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.”
Eze. 18:4, 20: “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Kwa hiyo, nafsi si kitu fulani kinachoendelea kuishi baada ya mwili kufa na ambacho wanadamu walio hai wanaweza kuwasiliana nacho baada ya hapo.)
Zab. 146:4: “Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Roho inaposemwa kuwa ‘inatoka’ katika mwili, hiyo ni njia nyingine tu ya kusema kwamba nguvu za uhai zimeacha kutenda. Kwa hiyo, baada ya mtu kufa, roho yake haiendelei kuishi ikiwa kitu kisicho na mwili ambacho kinaweza kufikiri na kutimiza mambo kikiwa nje ya mwili. Roho hiyo si kitu ambacho walio hai wanaweza kuwasiliana nacho baada ya mtu kufa.)
Ona pia ukurasa wa 102-104, chini ya kichwa, “Kifo.”
Je, Biblia haisemi kwamba Mfalme Sauli aliwasiliana na nabii Samweli baada ya Samweli kufa?
Simulizi hilo linapatikana katika 1 Samweli 28:3-20. Mstari wa 13 na 14 huonyesha kwamba Sauli mwenyewe hakumwona Samweli bali alikisia tu kutokana na ufafanuzi aliopewa na yule mwanamke mwenye kuwasiliana na pepo akisema kwamba amemwona Samweli. Sauli alitaka sana kuamini kwamba alikuwa Samweli na kwa hiyo akakubali kudanganywa. Mstari wa 3 unasema kwamba Samweli alikuwa amekufa na kuzikwa. Maandiko yaliyonukuliwa chini ya kichwa kidogo kilichotangulia yanaonyesha wazi kwamba hakukuwa na sehemu yoyote ya Samweli iliyokuwa hai katika ulimwengu mwingine ambayo ingeweza kuwasiliana na Sauli. Sauti iliyojifanya kuwa sauti ya Samweli ilikuwa ya mjanja fulani aliyejifanya kuwa Samweli.
Wale wanaojaribu kusema na wafu wanawasiliana na nani hasa?
Ukweli kuhusu hali ya wafu unaelezwa waziwazi katika Biblia. Lakini ni nani aliyejaribu kuwadanganya wanadamu wawili wa kwanza kuhusu kifo? Shetani alipinga onyo la Mungu kwamba kutotii kungeleta kifo. (Mwa. 3:4; Ufu. 12:9) Baadaye, bila shaka, ikawa wazi kwamba wanadamu walikufa hakika kama Mungu alivyokuwa amesema. Basi, kupatana na akili, ni nani aliyetunga wazo la kwamba kwa kweli wanadamu hawafi bali kwamba sehemu fulani ya roho ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mwili kufa? Udanganyifu huo unamfaa Shetani Ibilisi, ambaye Yesu alimwita “baba ya uwongo.” (Yoh. 8:44; ona pia 2 Wathesalonike 2:9, 10.) Wanadamu hawajafaidika na ile imani kwamba kwa kweli wafu wako hai katika ulimwengu mwingine na kwamba tunaweza kuwasiliana nao. Kinyume cha hilo, andiko la Ufunuo 18:23 linasema kwamba, kupitia mazoea ya Babiloni Mkubwa ya kuwasiliana na pepo, “mataifa yote yalipotoshwa.” Zoea la kuwasiliana na pepo kwa ‘kuzungumza na wafu’ kwa kweli ni udanganyifu unaoweza kuwafanya watu wajihusishe na roho waovu (malaika wenye ubinafsi ambao walimwasi Mungu) na mara nyingi husababisha mtu asikie sauti ambazo hataki kusikia na kusumbuliwa na roho hao waovu.
Je, kuna madhara yoyote mtu akitafuta kuponywa au kupata ulinzi kupitia kuwasiliana na pepo?
Gal. 5:19-21: “Matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo . . . Kuhusu mambo hayo mimi ninawaonya ninyi kimbele, kama vile nilivyowaonya kimbele, kwamba wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Kutafuta msaada kwa kuwasiliana na pepo humaanisha kwamba mtu anauamini uwongo wa Shetani kuhusu kifo; anatafuta shauri kutoka kwa watu wanaojaribu kupata nguvu kutoka kwa Shetani na roho wake waovu. Mtu kama huyo anaonyesha kuwa yuko upande wa wale ambao ni adui za waziwazi za Yehova Mungu. Badala ya kupewa msaada wa kweli, yeyote anayeendelea katika mwenendo huo hupata madhara yenye kudumu.)
Luka 9:24: “Yeyote yule anayetaka kuiokoa nafsi [au, uhai] yake ataipoteza; lakini yeyote yule anayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu [kwa sababu yeye ni mfuasi wa Yesu Kristo] ndiye atakayeiokoa.” (Mtu akivunja kimakusudi amri za Neno la Mungu zilizoandikwa waziwazi kwa kujaribu kuulinda au kuuhifadhi uhai wake wa sasa, atapoteza tazamio la uzima wa milele. Huo ni upumbavu kama nini!)
2 Kor. 11:14, 15: “Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru. Kwa hiyo si jambo kubwa kama wahudumu wake wakiendelea pia kujigeuza wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu.” (Kwa hiyo hatupaswi kupotoshwa wakati baadhi ya mambo yanayofanywa kwa kuwasiliana na pepo yanapoonekana kuleta faida ya muda.)
Ona pia ukurasa wa 355-359, chini ya kichwa, “Uponyaji.”
Je, ni jambo la hekima kutumia njia za kuwasiliana na pepo ili kujua yatakayotokea wakati ujao au kuhakikisha umefanikiwa katika kazi fulani?
Isa. 8:19: “Nao wakiwaambia ninyi: ‘Toeni maombi kwa wenye kuwasiliana na pepo au kwa wale wenye roho ya kubashiri wanaonong’oneza na kusema maneno kwa sauti za chini,’ je, kundi lolote la watu halipaswi kutoa maombi kwa Mungu wake?”
Law. 19:31: “Msiwaendee wenye kuwasiliana na pepo, wala msitafute shauri la wajuzi wa kubashiri matukio, ili kutiwa unajisi nao. Mimi ni Yehova Mungu wenu.”
2 Fal. 21:6: “[Mfalme Manase] akafanya uchawi, akatafuta ishara za bahati na kufanyiza wenye kuwasiliana na pepo na wajuzi wa kubashiri matukio. Alifanya kwa kiasi kikubwa yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, na kumtia uchungu.” (Mazoea hayo ya kuwasiliana na pepo hasa yalihusisha kutafuta msaada wa Shetani na roho wake waovu. Si ajabu kwamba hayo yalikuwa “mabaya machoni pa Yehova,” na kwa sababu hiyo alimhukumu Manase vikali. Lakini alipotubu na kuacha mazoea hayo mabaya Yehova alimbariki.)
Mtu anaweza kupata madhara gani akishiriki katika michezo inayohusu namna ya uaguzi au akitafuta maana ya jambo fulani linaloonekana kuwa ishara ya bahati nzuri?
Kum. 18:10-12: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.” (Uaguzi ni kutaka kujua mambo yaliyofichika au kutabiri matukio, si kutokana na utafiti, bali kwa kufasiri ishara za bahati au kwa msaada wa nguvu zenye kupita uwezo wa wanadamu. Yehova alikataza mazoea hayo kati ya watumishi wake. Kwa nini? Mazoea hayo yote ni kuwaalika roho wachafu wawasiliane na mtu au wampagae. Kushiriki katika mambo hayo ni ukosefu mkubwa wa uaminifu kwa Yehova.)
Mdo. 16:16-18: “Kijakazi fulani mwenye roho, roho mwovu wa uaguzi, akakutana nasi. Yeye alikuwa akiwapatia mabwana zake faida nyingi kwa kufanya ufundi wa kubashiri.” (Kwa wazi, mtu yeyote anayependa uadilifu hawezi kutafuta habari kutoka katika chanzo hicho, kwa kusudi zito wala kwa mchezo tu. Paulo alichoshwa na kulia kwake, naye akamwamuru roho huyo amtoke.)
Je, roho waovu wanaweza kuvaa miili ya wanadamu?
Katika siku za Noa, malaika wasiotii walivaa miili ya wanadamu. Walioa, nao wakazaa watoto. (Mwa. 6:1-4) Hata hivyo, Gharika ilipokuja, malaika hao walilazimika kurudi katika makao ya roho. Andiko la Yuda 6 linasema hivi kuwahusu: “Na malaika ambao hawakubaki mahali pao pa kwanza bali wakayaacha makao yao wenyewe yanayofaa amewaweka akiba wakiwa na vifungo vya milele chini ya giza zito kwa ajili ya hukumu ya ile siku kuu.” Mungu hakuwashusha tu kutoka katika mapendeleo yao ya zamani mbinguni na kuwatupa katika giza zito kuhusu makusudi ya Yehova, bali pia kutajwa kwa vifungo kunaonyesha kwamba amewazuia. Wasifanye nini? Inaonekana amewazuia wasichukue miili yenye nyama wanayoweza kutumia kufanya ngono na wanawake, kama walivyokuwa wamefanya kabla ya Gharika. Biblia inasema kwamba malaika waaminifu, wakiwa wajumbe wa Mungu, walivaa miili ya wanadamu katika kufanya kazi zao hapa duniani mpaka karne ya kwanza W.K. Lakini baada ya Gharika, malaika hao waliokuwa wamezitumia vibaya zawadi zao walinyang’anywa uwezo wa kuvaa miili ya wanadamu.
Hata hivyo, ni jambo lenye kupendeza kwamba inaonekana roho waovu wanaweza kuwafanya wanadamu waone maono, na yale wanayoona huenda yakaonekana kuwa ya kweli. Ibilisi alipomshawishi Yesu, inaonekana alitumia njia hizo ili amwonyeshe Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.”—Mt. 4:8.
Mtu anawezaje kuepuka uvutano wa pepo?
Met. 18:10: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” (Hilo halimaanishi kwamba kutumia jina la Mungu ni hirizi ya kufukuza uovu. “Jina” la Yehova linamwakilisha yeye mwenyewe. Sisi tunapewa ulinzi tunapopata kumjua na kumtegemea kikamili, kujitiisha chini ya mamlaka yake na kutii amri zake. Tukifanya hivyo, na tukimwomba atupe msaada, na kutumia jina lake, atatupa ulinzi ambao ameahidi katika Neno lake.)
Mt. 6:9-13: “Basi, ninyi msali hivi: ‘ . . . Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.’” Unapaswa pia ‘kudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) (Mungu husikia sala hizo kutoka kwa wale wanaotamani kikweli kuijua kweli na kumwabudu yeye kwa njia inayompendeza.)
1 Kor. 10:21: “Hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.” (Wale wanaotaka urafiki na ulinzi wa Yehova lazima waache kabisa kushiriki katika mikutano ya kuwasiliana na pepo. Kupatana na mfano ulioandikwa katika Matendo 19:19, pia ni muhimu mtu kuviharibu au kuviondoa kwa njia inayofaa vitu vyote vinavyohusiana na kuwasiliana na pepo.)
Yak. 4:7: “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Ili kufanya hivyo, jifunze kwa bidii mapenzi ya Mungu na kuyafuata katika maisha yako. Huku upendo wa Mungu ukikuimarisha usiwaogope wanadamu, kataa kabisa kushiriki katika desturi zozote zinazohusiana na kuwasiliana na pepo au kutii sheria zozote za mtu mwenye kuwasiliana na pepo.)
Vaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu” ambayo yanafafanuliwa katika Waefeso 6:10-18 na uwe na bidii katika kuyadumisha yote katika hali nzuri.