Abudu Mungu kwa Masharti Yake
YESU alisema kwa Mungu hivi katika sala: “Hii ndiyo maana ya uhai wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Maarifa ya aina gani? “Mapenzi yake [Mungu] ni kwamba namna zote za watu waokolewe na kuja kwenye maarifa yaliyo sahihi ya ukweli.” (1 Timotheo 2:4, NW) The Amplified Bible hufasiri kifungu kile cha mwisho hivi: “Kuujua barabara na kwa usahihi Ukweli [wa kimungu].”
Kwa hiyo Mungu atutaka tumjue yeye na makusudi yake kwa usahihi, kwa kupatana na ukweli wa kimungu. Na Neno la Mungu, Biblia Takatifu, ndicho chanzo cha ukweli huo. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17) Watu wajifunzapo kwa usahihi mambo ambayo Biblia husema juu ya Mungu, hapo wataepuka kuwa kama wale ambao hutajwa kwenye Warumi 10:2, 3, NW, ambao walikuwa na “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na maarifa sahihi.” Au kama Wasamaria, ambao Yesu alisema hivi kwao: “Mnaabudu msichokijua.”—Yohana 4:22.
Kwa hiyo, ikiwa sisi twataka kibali cha Mungu, twahitaji kujiuliza hivi: Mungu husema nini juu yake mwenyewe? Yeye hutaka aabudiwe jinsi gani? Ni nini makusudi yake, nasi twapaswa kujipatanishaje nayo? Maarifa sahihi juu ya ukweli hutupa sisi majibu yafaayo kwa maswali hayo. Hapo ndipo twaweza kuabudu Mungu kwa masharti yake.
Kuvunjia Mungu Heshima
“WAO wanaoniheshimu nitawaheshimu,” asema Mungu. (1 Samweli 2:30) Je! ni kumheshimu Mungu kuwa sawa naye? Je! ni kumheshimu kumwita Mariamu “mama ya Mungu” na “Mpatanishi wa kike . . . kati ya Muumba na viumbe Wake,” kama ifanyavyo New Catholic Encyclopedia? Sivyo, mawazo hayo hufedhehesha Mungu. Hakuna mtu aliye sawa na yeye; wala yeye hakuwa na mama wa kimnofu, kwa kuwa Yesu hakuwa Mungu. Na hakuna “Mpatanishi wa kike,” kwa maana Mungu ameweka ‘mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu,’ Yesu.—1 Timotheo 2:5; 1 Yohana 2:1, 2.
Pasipo hata shaka moja, fundisho la Utatu limevuruga na kupunguza uelewevu wa watu juu ya cheo cha kweli cha Mungu. Huzuia watu wasimjue kwa usahihi Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima, Yehova Mungu, na wasimwabudu kwa masharti yake. Kama alivyosema mwanatheolojia Hans Küng: “Kwa nini mtu yeyote atake kuongezea upekee wa Mungu kitu chochote ambacho chaweza kuupunguzia uzito au kuutangua tu umoja na upekee huo?” Lakini hivyo ndivyo imani katika Utatu imefanya.
Wale wanaoamini katika Utatu ‘hawaamini Mungu kwa maarifa sahihi.’ (Warumi 1:28, NW) Mstari huo husema hivi pia: “Mungu aliwaachilia kwenye hali ya akilini isiyokubaliwa, ili kufanya mambo yasiyofaa.” Mistari 29 hadi 31 huorodhesha baadhi ya mambo hayo “yasiyofaa,” kama vile ‘uuaji wa kimakusudi, ugomvi, kuwa bandia kwa miafaka, kutokuwa na shauku ya kiasili, kukosa rehema.’ Mambo hayo hayo yamezoewa na dini ambazo hukubali Utatu.
Mathalani, mara nyingi Wanautatu wamenyanyasa na hata wakaua wale waliokataa fundisho la Utatu. Na hata wamezidi hapo. Wameua Wanautatu wenzao wakati wa vita. Ni jambo gani ambalo lingekuwa ‘lisilofaa’ kuliko Wakatoliki kuua Wakatoliki, Waorthodoksi kuua Waorthodoksi, Waprotestanti kuua Waprotestanti—yote hayo kwa jina la Mungu yule yule mmoja wa Utatu?
Hata hivyo, Yesu alisema wazi hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Neno la Mungu hupanua jambo hili, likisema: “Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki [uadilifu, NW] hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake.” Hufananisha wale ambao huua ndugu zao wa kiroho na “Kaini alivyokuwa wa yule mwovu [Shetani], akamwua ndugu yake.”—1 Yohana 3:10-12.
Hivyo, kufundisha mafundisho yenye mvurugo juu ya Mungu kumeongoza kwenye vitendo ambavyo huvunja sheria zake. Kwa kweli, lililotukia katika sehemu zote za Jumuiya ya Wakristo ni lile ambalo mwanatheolojia Mdenmarki S/oren Kierkegaard alifasili: “Jumuiya ya Wakristo imeondolea mbali Ukristo bila kuwa na habari kwamba inafanya hivyo.”
Hali ya kiroho ya Jumuiya ya Wakristo yafaana na aliloandika mtume Paulo: “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana; ni wenye machukizo, waasi, wala kwa kila tendo jema hawafai.”—Tito 1:16.
Karibuni, Mungu aletapo mwisho wa mfumo mbovu wa mambo uliopo, Jumuiya ya Wakristo yenye kuamini Utatu itatozwa hesabu. Nayo itahukumiwa vikali kwa vitendo na mafundisho yayo yenye kuvunjia Mungu heshima.—Mathayo 24:14, 34; 25:31-34, 41, 46; Ufunuo 17:1-6, 16; 18:1-8, 20, 24; 19:17-21.
Ukatae Utatu
MSIMAMO wa kweli za Mungu hauwezi kuachwa kwa kuridhiana na mambo mengine. Kwa hiyo, kuabudu Mungu kwa masharti yake kwamaanisha kukataa fundisho la Utatu. Fundisho hilo hupinganisha yale ambayo manabii, Yesu, mitume, na Wakristo wa mapema waliamini na kufundisha. Hupinganisha yale ambayo Mungu husema juu yake mwenyewe katika Neno lake mwenyewe lililovuviwa. Hivyo, yeye hushauri hivi: “Kirini kwamba mimi peke yangu ndimi Mungu na kwamba hakuna mwingine yeyote kama mimi.”—Isaya 46:9, TEV.
Masilahi ya Mungu hayatumikiwi kwa kuvuruga njia ya kumwelewa yeye na kuifanya ya kifumbo. Badala ya hivyo, kwa kadiri watu wazidivyo kuvurugika juu ya Mungu na makusudi yake, ndivyo jambo hilo limfaavyo zaidi Hasimu wa Mungu, Shetani Ibilisi, yule ‘mungu wa ulimwengu huu.’ Yeye ndiye huendeleza mafundisho hayo bandia ili ‘kupofusha akili za wasioamini.’ (2 Wakorintho 4:4) Na fundisho la Utatu pia hutimiza masilahi ya makasisi ambao hutaka kudumisha uvutano wao juu ya watu, kwa maana wao hufanya ionekane kana kwamba ni wanatheolojia peke yao wawezao kulielewa.—Ona Yohana 8:44.
Maarifa sahihi juu ya Mungu huleta kitulizo kikubwa. Hutuweka huru na mafundisho yenye kuhitilafiana na Neno la Mungu na pia na matengenezo ambayo yameasi imani. Kama Yesu alivyosema: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”—Yohana 8:32.
Kwa kuheshimu Mungu kuwa mkuu kupita wote na kumwabudu kwa masharti yake, sisi twaweza kuepuka hukumu atakayoleta karibuni juu ya Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani. Badala ya hiyo, twaweza kutazamia upendeleo wa Mungu wakati mfumo huu uishapo: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, bali yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anabaki milele.”—1 Yohana 2:17, NW.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Mchongo huu wa karne nyingi katika Ufaransa huonyesha “bikira” Mariamu akitawazwa na Utatu. Imani katika Utatu iliongoza kwenye kumpa Mariamu heshima ya kuwa “Mama ya Mungu”