Sura 11
Yohana Aitayarisha Njia
MIAKA 17 imepita tangu Yesu alipokuwa mtoto wa miaka 12 akiwauliza walimu maswali hekaluni. Ni masika ya mwaka 29 W.K., na yaonekana kila mtu, asema habari za Yohana, binamu ya Yesu, anayehubiri katika nchi yote ya kandokando ya Mto Yordani.
Yohana ni mwanamume wa kuvutia kweli kweli, katika sura na usemi pia. Mavazi yake yametengenezwa kwa manyoya ya ngamia, naye avaa mshipi wa ngozi kuzunguka kiuno chake. Chakula chake ni nzige mdudu na asali ya mwituni. Na ujumbe wake ni nini? “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.”
Ujumbe huo unasisimua wasikilizaji wake. Wengi wanautambua uhitaji wa kutubu, yaani, kugeuza mwelekeo wao na kukataa mwendo wao wa zamani wa maisha kuwa ni usiotamanika. Kwa hiyo, kutoka eneo lote la karibu na Yordani, na hata kutoka Yerusalemu, watu wanamjia Yohana kwa wingi, naye awabatiza, akiwazamisha ndani ya maji ya Yordani. Kwa sababu gani?
Yohana abatiza watu ili kufananisha, au kukiri kwao toba yao ya kutoka moyoni kwa sababu ya dhambi walizolitenda agano la Torati ya Mungu. Hivyo, wakati baadhi ya Mafarisayo na Masadukayo wa kidini wanapokuja Yordani, Yohana awashutumu vikali. “Enyi wazao wa nyoka,” asema. “Zaeni matunda yapasayo toba; wala msiwaze mioyoni mwenu kwamba, Tunaye baba ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba Mungu aweza katika mawe haya kumwinulia Ibrahimu watoto. Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni.”
Kwa sababu ya usikivu anaopokea Yohana, Wayahudi watuma kwake makuhani na Walawi. Hao wauliza: “U nani?”
“Mimi siye Kristo,” akiri Yohana.
“Ni nini basi?” wauliza. “U Eliya wewe?”
“Mimi siye,” ajibu.
“Wewe u nabii yule?”
“La.”
Hivyo wasisitiza: “U nani? tuwape majibu wale waliotupeleka. Wanenaje juu ya nafsi yako?”
Yohana aeleza: “Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, Inyosheni njia ya Bwana, [Yehova, NW] kama vile alivyonena nabii Isaya.”
“Mbona basi wabatiza,” wataka kujua, “ikiwa wewe si Kristo, wala Eliya, wala nabii yule?”
“Mimi nabatiza kwa maji,” ajibu. “Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi. Ndiye yule ajaye nyuma yangu.”
Yohana anaitayarisha njia kwa kufanya watu wawe na hali ya moyoni inayofaa ili wamkubali Mesiya, atakayekuwa Mfalme. Kuhusu Huyo, Yohana asema: “Yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake.” Kwa kweli, Yohana hata asema hivi: “Ajaye nyuma yangu amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu.”
Hivyo, ujumbe wa Yohana, “ufalme wa mbinguni umekaribia,” watumika kuwa ujulisho kwa watu wote kwamba huduma ya Mfalme aliyewekwa na Yehova, Yesu Kristo, iko karibu kuanza. Yohana 1:6-8, 15-28; Mathayo 3:1-12; Luka 3:1-18; Matendo 19:4.
▪ Yohana ni mwanamume wa namna gani?
▪ Ni kwa nini Yohana abatiza watu?
▪ Kwa nini Yohana aweza kusema kwamba Ufalme umekaribia?