Maisha na Huduma ya Yesu
Yohana Aitayarisha Njia
MIAKA kumi na saba imepita tangu Yesu alipokuwa mtoto wa miaka 12 akiwauliza maulizo walimu hekaluni. Ni masika ya mwaka 29 W.K. na inaelekea kuwa kila mtu anasema habari za Yohana binamu wa Yesu, anayehubiri katika nchi yote karibu-karibu na Mto Yordani.
Yohana ni mwanamume wa kuvutia kweli kweli, katika sura na usemi pia. Mavazi yake yametengenezwa kwa manyoya ya ngamia, naye anavaa mshipi wa ngozi kuzunguka kiuno chake. Chakula chake ni nzige na asali ya mwituni. Na ujumbe wake ni nini? “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.”
Ujumbe huo unasisimua wasikilizaji wake. Wengi wanautambua uhitaji wa kutubu, yaani, kugeuza mwelekeo wao na kukataa mwendo wao wa zamani wa maisha kuwa usiotamanika. Kwa hiyo kutoka eneo lote la karibu na Yordani, na hata kutoka Yerusalemu, watu wanamjia Yohana kwa wingi, naye anawabatiza, akiwachovya chini ya maji ya Yordani. Kwa sababu gani?
Yohana anabatiza watu iwe mfano, au utambuzi, wa toba yao ya moyoni kwa sababu ya dhambi walizolitenda agano la Torati ya Mungu. Hivyo wakati Wafarisayo na Wasadukayo fulani wa kidini wanapokuja Yordani, Yohana anawalaani. “Enyi wazao wa nyoka,” anasema. “Zaeni matunda yapasayo toba.”
Kwa sababu ya watu kuelekeza sana fikira zao kwenye Yohana, Wafarisayo wanatuma makuhani na Walawi wamwendee. Wanamuuliza: “U nani? tuwape majibu wale waliotupeleka. Wanenaje juu ya nafsi yako?”
Yohana anaeleza: “Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, Inyosheni njia ya [Yehova]! kama vile alivyonena nabii Isaya.” Yohana anaitayarisha njia kwa kufanya watu wawe na hali ya moyoni inayofaa ili wamkubali Masihi, atakayekuwa Mfalme. Juu ya Huyo, Yohana anasema: “Yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake.”
Hivyo ujumbe wa Yohana, “ufalme wa mbinguni umekaribia,” unatumika kuwa ujulisho wa hadharani kwamba huduma ya Mfalme aliyewekwa na Yehova, Yesu Kristo, iko karibu kuanza. Yohana 1:6-8, 15-28; Mathayo 3:1-12; Luka 3:1-18; Matendo 19:4.
◆ Yohana ni mwanamume wa namna gani?
◆ Sababu gani Yohana anabatiza watu?
◆ Sababu gani Yohana angeweza kusema Ufalme umekaribia?