Sura 24
Sababu Iliyomfanya Yesu Aje Duniani
SIKU ya Yesu katika Kapernaumu akiwa na wanafunzi wake wanne imekuwa yenye shughuli nyingi, ikimalizia kwa kuletewa na watu wa Kapernaumu wagonjwa wao wote ili waponywe wakati wa jioni hiyo. Hapakupata kuwa na wakati wa faragha.
Sasa ni asubuhi na mapema kesho yake. Kunapokuwa kungali na giza, Yesu aamka na kwenda nje peke yake. Aenda mahali anapokuwa peke yake aweze kupelekea Babaye sala kwa faragha. Lakini faragha ya Yesu ni ya muda mfupi kwa sababu wakati Petro na wengine watambuapo kwamba yeye hayupo, waenda nje wakamtafute.
Wampatapo Yesu, Petro asema: “Watu wote wanakutafuta.” Watu wa Kapernaumu wataka Yesu akae pamoja nao. Wathamini kikweli mambo ambayo amewafanyia! Lakini je, Yesu alikuja duniani ili afanye hasa maponyo hayo ya kimuujiza? Yeye asema nini juu ya hilo?
Kulingana na usimulizi mmoja wa Biblia, Yesu awajibu wanafunzi wake hivi: “Twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea.” Ingawa watu wamhimiza Yesu akae nao, yeye awaambia: “Kwenye miji mingine pia ni lazima mimi nitangaze habari njema za ufalme, kwa sababu kwa ajili ya jambo hilo mimi nilitumwa.”
Ndiyo, Yesu alikuja duniani kwa kusudi hasa la kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu, ambao utaondoa malawama juu ya jina la Babaye kisha uondoe daima mabaya yote yanayopata aina ya kibinadamu. Lakini, ili atoe ushuhuda wa kwamba ametumwa na Mungu, Yesu afanya maponyo ya kimuujiza. Musa pia alitumia njia iyo hiyo ya kufanya miujiza karne nyingi zilizopita ili athibitishe haki zake za kuwa mtumishi wa Mungu.
Sasa, wakati Yesu aondokapo Kapernaumu akaihubiri miji mingine, wanafunzi wake wanne waenda pamoja naye. Hao wanne ni Petro na Andrea nduguye, na Yohana na Yakobo nduguye. Utakumbuka kwamba juma lililotangulia tu wao walikaribishwa wawe wafanya kazi wenzi wa kwanza wa Yesu wenye kusafiri naye.
Ziara ya Yesu ya kuhubiri katika Galilaya pamoja na wanafunzi wake wanne inapata mafanikio makubwa! Kwa kweli, ripoti juu ya utendaji wake yaenea hata katika Shamu yote. Umati mkubwa kutoka Galilaya, Yudea, na ng’ambo ya Yordani wafuata Yesu na wanafunzi wake. Marko 1:35-39; Luka 4:42, 43; Mathayo 4:23-25; Kutoka 4:1-9, 30, 31.
▪ Ni jambo gani latukia asubuhi inayoifuata siku ile yenye shughuli nyingi ya Yesu katika Kapernaumu?
▪ Kwa nini Yesu alitumwa duniani, na miujiza yake yatimiza kusudi gani?
▪ Ni nani waenda pamoja na Yesu katika ziara yake ya kuhubiri katika Galilaya, na utendaji wa Yesu waitikiwaje?