Sura 70
Kuponya Mwanamume Aliyezaliwa Akiwa Kipofu
WAYAHUDI wanapojaribu kumpiga Yesu kwa mawe, yeye haondoki Yerusalemu. Baadaye, siku ya Sabato, yeye na wanafunzi wake wanatembea jijini wakati wanapomwona mwanamume mmoja ambaye amekuwa kipofu tangu alipozaliwa. Wanafunzi wamuuliza Yesu: “Rabi, nani aliyetenda dhambi, mwanamume huyu, au wazazi wake, hivi kwamba yeye akazaliwa akiwa kipofu?”
Pengine wanafunzi wanaamini, kama wanavyoamini marabi fulani kwamba, mtu anaweza kutenda dhambi akiwa tumboni mwa mamaye. Lakini Yesu anajibu hivi: “Wala mwanamume huyu hakutenda dhambi wala wazazi wake, lakini ilikuwa ili kazi za Mungu zipate kudhihirishwa katika kisa chake.” Upofu wa mwanamume huyo si tokeo la kosa fulani halisi au dhambi iliyotendwa na mwanamume huyo au wazazi wake. Dhambi ya mwanamume wa kwanza Adamu ilitokeza kutokamilika kwa wanadamu wote, na hivyo wanaelekea kupatwa na kasoro kama vile kuzaliwa wakiwa vipofu. Kasoro hii katika mwanamume yule sasa inamtolea Yesu fursa adhihirishe kazi za Mungu.
Yesu akazia uharaka wa kufanya kazi hizi. “Lazima sisi tufanye kazi zake yeye aliyenipeleka wakati kungali mchana,” yeye anasema. “Usiku waja wakati ambapo hakuna mtu anayeweza kufanya kazi. Maadamu mimi nipo ulimwenguni, mimi ndimi nuru ya ulimwengu.” Karibuni kifo cha Yesu kitamtumbukiza katika giza la kaburi ambamo hawezi kutenda lolote. Kwa wakati huu, yeye ndiye chanzo cha nuru ya elimu kwa ulimwengu.
Baada ya kusema mambo haya, Yesu anatema mate chini naye anatengeneza udongo kwa mate hayo. Anauweka machoni pa yule mwanamume kipofu na kusema: “Nenda ukaoshe katika kidimbwi cha Siloamu.” Mwanamume huyo anatii. Naye anapofanya hivyo, anaweza kuona! Jinsi anavyoona shangwe anaporudi, kuweza kuona kwa mara ya kwanza maishani mwake!
Majirani na wengine wanaomfahamu wanashangaa. “Huyu ndiye yule mwanamume aliyezoea kuketi na kuomba-omba, sivyo?” wao wanauliza. “Ndiye,” watu fulani wanajibu. Lakini wengine hawawezi kuamini hilo: “Sivyo, lakini yeye anafanana naye.” Hata hivyo, mwanamume huyo anasema: “Mimi ndiye.”
“Basi, macho yako yalifunguliwaje?” watu wanataka kujua.
“Mwanamume anayeitwa Yesu alifanya udongo na akanipaka machoni kisha akasema kwangu, ‘Nenda Siloamu ukaoshe.’ Kwa hiyo mimi nikaenda na kuosha nami ninaona.”
“Mwanamume huyo yuko wapi?” wanauliza.
“Mimi sijui,” anajibu.
Sasa watu wanamwongoza mwanamume huyo ambaye wakati mmoja alikuwa kipofu kwa viongozi wao wa kidini, wale Mafarisayo. Hao pia wanamuuliza alipataje kuona. “Yeye aliweka udongo kwenye macho yangu, na mimi nikaosha nami ninaona,” mwanamume huyo anaeleza.
Hakika, Mafarisayo wapaswa kushangilia pamoja na mwombaji huyo aliyeponywa! Lakini badala ya hivyo, wao wanalaumu Yesu waziwazi. “Mwanamume huyo hatoki kwa Mungu,” wao wanadai. Kwa nini wanasema hivyo? “Kwa sababu hashiki Sabato.” Na bado Mafarisayo wengine wanauliza kwa kushangaa: “Inawezekanaje mwenye dhambi atende ishara za namna hii?” Basi kuna mgawanyiko kati yao.
Kwa sababu hii, wanamuuliza mwanamume yule: “Wewe wasemaje juu yake, kwa kuwa amefungua macho yako?”
“Yeye ni nabii,” anajibu.
Mafarisayo wanakataa kuamini hilo. Wao wanasadiki kwamba lazima kuna uafikiano fulani wa kisiri kati ya Yesu na mwanamume huyu ili kuwapumbaza watu. Basi ili wakate maneno, wao wanawaita wazazi wa mwombaji huyo ili wawaulize maswali. Yohana 8:59; 9:1-18, NW.
▪ Ni nini kisababishi cha upofu wa mwanamume yule, na ni nini kisichousababisha?
▪ Ni nini ule usiku ambao hakuna mtu awezaye kufanya kazi?
▪ Mwanamume yule anapoponywa, wale wanaomjua wanatendaje kwa kuitikia?
▪ Mafarisayo wanagawanyikaje juu ya kuponywa kwa mwanamume huyo?