Maisha na Huduma ya Yesu
Kuponya Mwanamume Aliyezaliwa Akiwa Kipofu
WAYAHUDI wanapojaribu kumpiga Yesu kwa mawe akiwa hekaluni, yeye anajificha na kutoroka. Lakini haondoki Yerusalemu. Baadaye, siku ya Sabato, yeye na wanafunzi wake wanatembea jijini wanapomwona mwanamume mmoja ambaye amekuwa kipofu tangu alipozaliwa. “Rabi, nani aliyetenda dhambi,” wanafunzi wanamuuliza Yesu, “mwanamume huyo au wazazi wake, hivi kwamba yeye akazaliwa akiwa kipofu?”
Pengine wanafunzi wanaitikadi, kama wanavyoitikadi marabi fulani kwamba mtu anaweza kutenda dhambi akiwa tumboni mwa mamaye. Lakini Yesu anajibu hivi: “Wala mwanamume huyu hakutenda dhambi wala wazazi wake, lakini ilikuwa ili kazi za Mungu ziweze kudhihirishwa katika kisa hiki.” Upofu wa mwanamume huyo si tokeo la kosa fulani halisi au dhambi iliyotendwa na mwanamume huyo au wazazi wake. Dhambi ya mwanamume wa kwanza Adamu ilitokeza kutokamilika kwa wanadamu wote, na hivyo wanaelekea kupatwa na kasoro kama vile kuzaliwa kipofu. Kasoro hii katika mwanamume huyo sasa inatoa nafasi kwa Yesu kudhihirisha kazi za Mungu.
Yesu anakazia uharaka wa kufanya kazi hizi. “Lazima sisi tufanye kazi zake yeye aliyenipeleka mimi kungali mchana,” yeye anasema; “Usiku unakuja wakati ambapo hakuna mwanamume ataweza kufanya kazi. Mradi mimi nipo ulimwenguni mimi ndimi nuru ya ulimwengu.” Karibuni kifo cha Yesu kitamtumbukiza katika giza la kaburi ambamo hawezi kutenda lo lote. Kwa wakati huu, yeye ndiye chanzo cha mwangaza kwa ulimwengu.
Baada ya kusema mambo haya, Yesu anatema mate chini naye anatengeneza udongo kwa mate hayo. Anauweka machoni pa mwanamume mwenye upofu na kusema: “Nenda ukaoshe katika kidimbwi cha Siloamu.” Mwanamume huyo anatii. Naye anapofanya hivyo, anaweza kuona! Jinsi anavyofurahi anaporudi, kuweza kuona kwa mara ya kwanza maishani mwake!
Majirani na wengine wanaomfahamu wanashangaa. “Huyu ndiye yule mwanamume aliyezoelea kuketi na kuomba-omba, sivyo?” wao wanauliza. “Ndiye,” watu fulani wanajibu. Lakini wengine hawawezi kuitikadi hilo: “Sivyo, lakini yeye anafanana naye.” Hata hivyo, mwanamume huyo anasema: “Mimi ndiye.”
“Jinsi gani, basi, macho yako yalifunguliwa?” watu wanataka kujua
“Mwanamume anayeitwa Yesu alifanya udongo na akanipaka machoni kisha akasema kwangu mimi, ‘Nenda Siloamu na ukaoshe.’ Kwa hiyo mimi nikaenda na kuosha nami naona.”
“Mwanamume huyo yuko wapi?” wanauliza.
“Mimi sijui,” anajibu.
Sasa watu wanamwongoza mwanamume huyo ambaye alikuwa kipofu wakati mmoja kwa viongozi wao wa kidini, Mafarisayo. Hao pia wanamuuliza alipata kuona jinsi gani. “Yeye aliweka udongo kwenye macho yangu, na mimi nikaosha na ninaona.” mwanamume huyo anaeleza.
Kwa kweli, Mafarisayo wapaswa kufurahi pamoja na mwombaji huyo aliyeponywa! Lakini badala yake wao wanamlaumu Yesu waziwazi. “Mwanamume huyo hatoki kwa Mungu,” wao wanadai. Kwa nini wanasema hivyo? “Kwa sababu hashiki Sabato.” Na bado Mafarisayo wengine wanashangaa: “Inawezekanaje mwanamume mwenye dhambi atende ishara za namna hii?” Basi kuna mgawanyo kati yao.
Kwa sababu hii, wanamuuliza mwanamume yule: “Wewe wasemaje juu yake, kwa kuwa amefungua macho yako?”
“Yeye ni nabii,” anajibu.
Mafarisayo wanakataa kuitikadi hilo. Wao wanasadikishwa kwamba lazima kuna uafikiano fulani wa kisiri kati ya Yesu na mwanamume huyu ili kuwapumbaza watu. Basi ili wakate maneno wao wanawaita wazazi wa mwombaji huyo ili wawaswali. Yohana 8:59; 9:1-18, NW.
◆ Ni nini kilichosababisha upofu wa mwanamume yule na ni nini kisichousababisha?
◆ Ni usiku gani ambao hakuna mtu anaweza kufanya kazi?
◆ Mwanamume yule anapoponywa, wale wanaomjua wanajibiza kwa njia gani?
◆ Mafarisayo waligawanyika jinsi gani kuhusu ponyo la mwanamume huyo?