Maisha na Huduma ya Yesu
Kutoitikadi kwa Mafarisayo kwa Sababu ya Ugumu wa Moyo
WAZAZI wa aliyekuwa mwombaji-maskini kipofu wanaogopa wanapoitwa mbele ya Mafarisayo. Wao wanajua kwamba moyo umepigwa konde kuondosha sinagogini mtu ye yote anayejisemea ana imani katika Yesu. Kukatiliwa nje kwa njia hiyo kutoka kwenye ushirika wa wengine mtaani kunaweza kufanyiza ugumu mkubwa sana, hasa juu ya jamaa maskini. Kwa hiyo wazazi hao wana nadhari.
“Je! huyu ndiye mwana wenu ambaye ninyi mnasema alizaliwa akiwa kipofu?” Mafarisayo wanauliza. “Ni jinsi gani, basi, yeye anaona kwa wakati uliopo?”
“Sisi tunajua kwamba huyu ni mwana wetu na kwamba yeye alizaliwa akiwa kipofu,” wazazi hao wanahakikisha. “Lakini jinsi ilivyo kwamba yeye sasa anaona sisi hatujui, au ni nani alifungua macho yake sisi hatujui.” Kwa uhakika mwana wao amewaambia yote yaliyotukia, lakini kwa uangalifu wazazi hao wanasema hivi: “Mwulizeni yeye. Yeye ana umri wa kutosha. Lazima yeye ajinenee mwenyewe.”
Basi, Mafarisayo wanamwita tena mwanamume yule. Wakati huu wanajaribu kumtisha-tisha kwa kumwonyesha kwamba wao wamekusanya ithibati ya kuonyesha uhalifu dhidi ya Yesu. “Mpe Mungu utukufu,” wao wanadai kinguvu. “Sisi tunajua kwamba mwanamume huyu ni mtenda dhambi.”
Mwanamume huyo aliyekuwa kipofu hakani shtaka lao, kwa kuonelea hivi: “Kama yeye ni mtenda dhambi mimi sijui.” Lakini yeye anaongezea hivi: “Jambo moja mimi najua, kwamba, ijapokuwa mimi nilikuwa kipofu, kwa wakati uliopo mimi naona.”
Wakijaribu kupata dosari katika ushuhuda wake, Mafarisayo wanauliza tena: “Ni nini ambalo yeye alikufanya wewe? Ni jinsi gani yeye alifungua macho yako?”
“Mimi tayari niliwaambia ninyi,” mwanamume yule analalamika, “na bado ninyi hamkusikiliza. Kwa nini ninyi mnataka kusikia hilo tena?” Kwa kukejeli yeye anauliza: “Ninyi hamtaki kuwa wanafunzi wake pia, mnataka?”
Jibu hili linawatia Mafarisayo hao hasira kali. “Wewe ni mwanafunzi wa mwanamume huyo,” wao wanatokeza shtaka, “lakini sisi ni wanafunzi wa Musa. Sisi tunajua kwamba Mungu amenena kwa Musa; lakini kwa habari ya mwanamume huyu, sisi hatujui yeye ni wa kutoka wapi.”
Akionyesha mshangao, mwombaji-maskini huyo mnyenyekevu anarudisha hivi: “Kwa uhakika hii ni ajabu, kwamba ninyi hamjui yeye ni wa kutoka wapi, na bado yeye alifungua macho yangu.” Ni shauri gani linalopasa kukatwa kutokana na jambo hili? Huyo mwombaji-maskini anaonyesha ule uhakika unaojulikana wazi: “Sisi tunajua kwamba Mungu hasikilizi watenda dhambi, lakini ikiwa mtu ye yote ni mwenye kuogopa Mungu na anafanya mapenzi yake, yeye anasikiliza mmoja huyu. Kutoka zamani imekuwa haijasikiwa kamwe kwamba mtu ye yote alifungua macho ya mmoja aliyezaliwa akiwa kipofu.” Hivyo, shauri la kukatwa linapasa kuwa wazi: “Kama mwanamume huyu hangekuwa wa kutoka kwa Mungu, yeye hangeweza kufanya jambo lo lote hata kidogo.”
Mafarisayo hawana jibu kwa fikira hiyo ya wazi. Wao hawawezi kuelekeana na ukweli, na kwa hiyo wanatukana mwanamume yule hivi: “Wewe kwa ujumla ulizaliwa katika dhambi, na bado wewe unatufundisha sisi?” Hapo, wao wanatupa nje mwanamume yule, inaonekana wakimwondosha nje asiwe wa sinagogi.
Wakati Yesu anapopata habari juu ya jambo ambalo wamefanya, yeye anatafuta mwanamume huyo na kusema: “Je! wewe unatia imani katika Mwana wa binadamu?”
“Yeye ni nani, bwana,” anajibu mtu huyo aliyekuwa mwombaji-maskini kipofu, “ili kwamba mimi nipate kutia imani katika yeye?”
“Yeye anayenena na wewe ndiye huyo,” Yesu anajibu.
Mara hiyo mwanamume huyo anainama mbele ya Yesu na kusema: “Mimi natia imani katika yeye, Bwana.”
Ndipo Yesu anapoeleza: “Kwa ajili ya hukumu hii mimi nilikuja ndani ya ulimwengu: kwamba wale wasioona waweze kuona na wale wanaoona waweze kuwa vipofu.”
Hapo, Mafarisayo ambao wanasikiliza wanauliza: “Sisi si vipofu pia, je! tu vipofu?” Kama wao wangekiri kwamba wao ni vipofu kiakili, kungekuwa na udhuru kwa ajili ya upinzani wao kwa Yesu. Kama vile Yesu anavyowaambia: “Kama ninyi mngalikuwa mu vipofu, ninyi mngalikuwa hamna dhambi.” Hata hivyo, wao wanasisitiza kwamba wao si vipofu na hawahitaji nuru ya mwelimisho wo wote wa kiroho. Kwa hiyo Yesu anaonelea hivi: “Sasa ninyi mnasema, ‘Sisi tunaona.’ Dhambi yenu inabaki.” Yohana 9:19-41.
◆ Kwa nini wazazi wa aliyekuwa mwombaji-maskini wanaogopa wakati wanapoitwa mbele ya Mafarisayo, na kwa hiyo ni jinsi gani wao wanajibu kwa nadhari?
◆ Ni jinsi gani Mafarisayo wanajaribu kutisha-tisha mwanamume huyo aliyekuwa kipofu?
◆ Ni hoja gani ya kiakili ya mwanamume huyo inayowatia kiruu Mafarisayo?
◆ Kwa nini Mafarisayo hawana udhuru kwa ajili ya upinzani wao kwa Yesu?