Sura 71
Mafarisayo Wakosa Kuamini kwa Kupenda
WAZAZI wa aliyekuwa mwombaji kipofu wanaogopa wanapoitwa mbele ya Mafarisayo. Wao wanajua kwamba imeazimiwa kwamba yeyote anayetumia imani katika Yesu atafukuzwa kutoka katika sinagogi. Kukatiliwa nje kwa njia hiyo kutoka kwenye ushirika wa wengine mtaani kunaweza kufanyiza magumu makubwa sana, hasa juu ya jamaa maskini. Kwa hiyo wazazi hao wana tahadhari.
“Je! huyu ndiye mwana wenu ambaye nyinyi mwasema alizaliwa akiwa kipofu?” Mafarisayo wanauliza. “Basi, inakuwaje anaona sasa?”
“Sisi tunajua kwamba huyu ni mwana wetu na kwamba yeye alizaliwa akiwa kipofu,” wazazi hao wanahakikisha. “Lakini jinsi ilivyo kwamba yeye sasa anaona sisi hatujui, au ni nani aliyefungua macho yake sisi hatujui.” Kwa uhakika mwana wao lazima awe amewaambia yote yaliyotukia, lakini kwa tahadhari wazazi hao wanasema hivi: “Muulizeni yeye. Yeye ana umri wa kutosha. Lazima yeye ajinenee mwenyewe.”
Basi, Mafarisayo wanamwita tena mwanamume yule. Wakati huu wanajaribu kumtisha-tisha kwa kumwonyesha kwamba wao wamekusanya uthibitisho wa kuonyesha uhalifu dhidi ya Yesu. “Mpe Mungu utukufu,” wao wanadai kinguvu. “Sisi tunajua kwamba mwanamume huyu mi mtenda dhambi.”
Mwanamume huyo aliyekuwa kipofu hakani shtaka lao, kwa kuonelea hivi: “Kama yeye ni mtenda dhambi mimi sijui.” Lakini yeye anaongeza hivi: “Jambo moja mimi ninajua, ni kwamba, ijapokuwa mimi nilikuwa kipofu, kwa wakati huu mimi naona.”
Wakijaribu kupata kosa katika ushahidi wake, Mafarisayo wanauliza tena: “Yeye alikufanya nini? Yeye alifunguaje macho yako?”
“Mimi tayari nimekwisha waambia,” mwanamume yule analalamika, “na bado nyinyi hamkusikiliza. Kwa nini nyinyi mnataka kusikia hilo tena?” Yeye anauliza kwa dharau hivi: “Nyinyi hamtaki kuwa wanafunzi wake pia, sivyo?”
Jibu hili linawatia Mafarisayo hao hasira kali. “Wewe ni mwanafunzi wa mwanamume huyo,” wao wanashtaki, “lakini sisi ni wanafunzi wa Musa. Sisi tunajua kwamba Mungu amenena na Musa; lakini kwa habari ya mwanamume huyu, sisi hatujui yeye ametoka wapi.”
Akionyesha mshangao, mwombaji huyo mnyenyekevu anajibu hivi: “Hakika hii ni ajabu, kwamba nyinyi hamjui yeye ametoka wapi, na bado yeye alifungua macho yangu.” Ni shauri gani linalopasa kukatwa kutokana na jambo hili? Huyo mwombaji anaonyesha ule uhakika unaojulikana wazi: “Sisi tunajua kwamba Mungu hasikilizi watenda dhambi, lakini ikiwa mtu yeyote ni mwenye kuhofu Mungu na anafanya mapenzi yake, yeye amsikiliza huyo. Tokea zamani haijasikiwa kamwe kwamba mtu yeyote alifungua macho ya mmoja aliyezaliwa akiwa kipofu.” Hivyo, shauri la kukatwa linapasa kuwa wazi: “Kama mwanamume huyo hangekuwa ametoka kwa Mungu, yeye hangeweza kufanya jambo lolote hata kidogo.”
Mafarisayo hawana jibu kwa kuwaza huko kuzuri kuliko wazi. Wao hawawezi kuelekeana na ukweli, na kwa hiyo wanatukana mwanamume yule hivi: “Wewe kwa ujumla ulizaliwa katika dhambi, na bado wewe unatufundisha sisi?” Hapo, wao wanamtupa nje mwanamume yule, inaonekana wakimfukuza katika sinagogi.
Wakati Yesu anapopata habari juu ya jambo ambalo wamefanya, yeye anatafuta mwanamume huyo na kusema: “Je! wewe unaweka imani katika Mwana wa binadamu?”
Katika kujibu, yule mwombaji ambaye wakati mmoja alikuwa kipofu anauliza, “Yeye ni nani, bwana, ili niweke imani katika yeye?”
“Yeye anayenena nawe ndiye huyo,” Yesu anajibu.
Mara hiyo, mwanamume huyo anainama mbele ya Yesu na kusema: “Mimi naweka imani katika yeye, Bwana.”
Ndipo Yesu anapoeleza: “Kwa ajili ya hukumu hii mimi nilikuja ulimwenguni: kwamba wale wasioona wapate kuona na wale wanaoona wapate kuwa vipofu.”
Basi, Mafarisayo ambao wanasikiliza wanauliza: “Sisi si vipofu pia, je! tu vipofu?” Kama wao wangekiri kwamba wao ni vipofu kiakili, kungekuwa na udhuru kwa ajili ya upinzani wao kwa Yesu. Kama vile Yesu anavyowaambia: “Kama nyinyi mngalikuwa mu vipofu, nyinyi mngalikuwa hamna dhambi.” Hata hivyo, wao wanasisitiza kwamba wao si vipofu na hawahitaji nuru ya elimu yoyote ya kiroho. Kwa hiyo Yesu anaonelea hivi: “Sasa nyinyi mnasema, ‘Sisi tunaona.’ Dhambi yenu inabaki.” Yohana 9:19-41, NW.
▪ Kwa nini wazazi wa aliyekuwa mwombaji wanaogopa wakati wanapoitwa mbele ya Mafarisayo, na kwa hiyo wao wanajibuje kwa tahadhari?
▪ Mafarisayo wanajaribuje kutisha-tisha mwanamume huyo aliyekuwa kipofu?
▪ Ni hoja gani ya mwanamume huyo inayopatana na akili ambayo inawatia Mafarisayo hasira kali?
▪ Kwa nini Mafarisayo hawana udhuru kwa ajili ya upinzani wao kwa Yesu?