Sura 106
Kufichuliwa na Vielezi vya Shamba la Mizabibu
YESU yuko hekaluni. Sasa hivi tu ndipo amevuruga viongozi wa kidini waliodai kujua yeye anafanya mambo kwa mamlaka ya nani. Kabla wao hawajatulia kutoka kwenye vurugu yao, Yesu auliza hivi: “Nyinyi mwafikiri nini?” Halafu kwa njia ya kielezi, yeye awaonyesha wao ni watu wa aina gani hasa.
“Mtu mmoja alikuwa na watoto wawili,” Yesu asimulia. “Akiendea yule wa kwanza, akasema, ‘Mtoto, enda ukafanye kazi leo katika shamba la mizabibu.’ Kwa kujibu huyu akasema, ‘Nitaenda, bwana,’ lakini hakwenda. Akikaribia yule wa pili, akasema ivyo hivyo. Kwa kujibu huyu akasema, ‘Mimi sitaenda.’ Baadaye akahisi majuto na kwenda. Ni yupi wa wale wawili aliyefanya penzi la baba yake?” Yesu auliza.
“Ni yule wa mwisho,” wapinzani wake wakajibu.
Kwa hiyo Yesu aeleza hivi: “Kwa kweli mimi nasema kwenu nyinyi kwamba wakusanya kodi na makahaba wanaenda mbele yenu nyinyi kuingia katika ufalme wa Mungu.” Kwa kweli, wakusanya kodi na makahaba walikataa kutumikia Mungu hapo kwanza. Lakini ndipo, kama yule mtoto wa pili, wakatubu na kumtumikia. Kwa upande mwingine, viongozi wa kidini, kama yule mtoto wa kwanza, walijidai kuwa wamtumikia Mungu, hata hivyo, kama vile Yesu aarifuvyo: “Yohana [Mbatizaji] aliwajia nyinyi katika njia ya uadilifu, lakini nyinyi hamkumwamini. Hata hivyo, wakusanya kodi na makahaba walimwamini, na nyinyi, ingawa mliona jambo hili, hamkuhisi majuto baadaye ili mmwamini.”
Ndipo Yesu aonyesha kwamba jambo ambalo limewashinda viongozi hawa wa kidini si kutojali tu kutumikia Mungu. Sivyo, bali kwa kweli wao ni watu waovu. “Kulikuwa mtu mmoja, mwenye nyumba,” Yesu asimulia, “aliyepanda shamba la mizabibu na kuweka ugo kulizunguka na akachimba shinikizo la divai humo na kusimamisha mnara, na kulikodisha kwa walimaji, na kusafiri ng’ambo. Majira ya matunda yalipofika, yeye alipeleka watumwa wake kwa walimaji ili watwae matunda yake. Hata hivyo, walimaji walichukua wale watumwa wake, na mmoja wakampiga sana, mwingine wakaua, mwingine wakampiga kwa mawe. Tena yeye akapeleka watumwa wengine, wengi kuliko wale wa kwanza, lakini wakawafanya hawa ivyo hivyo.”
“Watumwa” hao ni manabii ambao “mwenye nyumba,” Yehova Mungu, aliwatuma kwa “walimaji” wa ‘shamba lake la mizabibu.’ Walimaji hawa ni wawakilishi wenye kuongoza wa taifa la Israeli, taifa ambalo Biblia yalitambulisha kuwa ‘shamba la Mungu la mizabibu.’
Kwa kuwa “walimaji” wawatenda vibaya na kuwaua “watumwa,” Yesu aeleza hivi: “Mwisho [mwenye shamba la mizabibu] aliwapelekea mwana wake, akisema, ‘Watastahi mwana wangu.’ Kwa kumwona mwana walimaji wakasema miongoni mwao wenyewe, ‘Huyu ndiye mrithi; njoni, acheni tumuue tupate urithi wake!’ Kwa hiyo wao wakamtwaa na kumtupa nje ya shamba la mizabibu na kumuua.”
Sasa, akiwaambia viongozi hao wa kidini, Yesu auliza hivi: “Wakati mwenye shamba la mizabibu ajapo, yeye atawafanya nini walimaji hao?”
“Kwa sababu ni waovu,” viongozi wa kidini wajibu “yeye ataleta uharibifu mwovu juu yao na atakodisha shamba la mizabibu kwa walimaji wengine, ambao watamtolea yeye matunda uwapo ni wakati wayo.”
Kwa njia hiyo bila kujua viongozi hao wa kidini wapiga mbiu ya kujihukumu wenyewe, kwa maana wao wamo miongoni mwa “walimaji” Waisraeli wa “shamba la mizabibu” la Yehova ambalo ni taifa la Israeli. Tunda ambalo Yehova atarajia kutoka kwa walimaji hao ni imani katika Mwana wake, yule Mesiya wa kweli. Kwa sababu ya wao kushindwa kuandaa tunda hilo, Yesu aonya hivi: “Je! nyinyi hamjasoma kamwe katika Maandiko [kwenye Zaburi 118:22, 23], ‘Jiwe ambalo wajenzi walikataa ndilo lile ambalo limekuwa jiwe kuu la pembeni. Jambo hili limetoka kwa Yehova, nalo ni zuri sana machoni petu’? Hii ndiyo sababu mimi nasema kwenu nyinyi, ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu nyinyi na kupewa taifa linalotokeza matunda yalo. Pia, mtu anayeanguka juu ya jiwe hili atavunjika-vunjika kabisa. Kwa habari ya yeyote ambaye hilo laanguka juu yake, litamsaga-saga kabisa.”
Sasa waandishi na wakuu wa makuhani watambua kwamba Yesu ananena kuwahusu, nao wataka kumuua, yule “mrithi” halali. Kwa hiyo pendeleo la kuwa watawala katika Ufalme wa Mungu litatwaliwa kutoka kwao wakiwa taifa, na taifa jipya la ‘walimaji wa shamba la mizabibu’ litafanyizwa, moja ambalo litatokeza matunda yafaayo.
Kwa sababu viongozi wa kidini wahofu umati wa watu, ambao wamwona Yesu kuwa nabii, hawajaribu kumuua katika pindi hii. Mathayo 21:28-46; Marko 12:1-12; Luka 20:9-19; Isaya 5:1-7, NW.
▪ Wale watoto wawili katika kielezi cha Yesu cha kwanza wawakilisha nani?
▪ Ni nani wanaowakilishwa na “mwenye nyumba,” “shamba la mizabibu,” “walimaji,” “watumwa,” na “mrithi” katika kielezi cha pili?
▪ Itakuwaje kwa ‘walimaji wa shamba la mizabibu,’ na ni nani watachukua mahali pao?