Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ip-1 sura 7 kur. 73-86
  • Ole kwa Shamba la Mizabibu Lisilo na Uaminifu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ole kwa Shamba la Mizabibu Lisilo na Uaminifu!
  • Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Utunzaji wa Shamba la Mizabibu
  • Shamba la Mizabibu na Mmilikaji Wake
  • Kutambua Shamba la Mizabibu la Mungu Leo
  • “Zabibu-Mwitu”
  • Matokeo ya Pupa
  • Mtego wa Vitumbuizo Vyenye Kutilika Shaka
  • Kuchukia Dhambi na Kupenda Kweli
  • Mfano wa Wafanyakazi Katika Shamba la Mizabibu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Mifano Miwili Kuhusu Mashamba ya Mizabibu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Kufichuliwa na Vielezi vya Shamba la Mizabibu
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Kafichuliwa na Vielezi vya Shamba la Mizabibu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
ip-1 sura 7 kur. 73-86

Sura ya 7

Ole kwa Shamba la Mizabibu Lisilo na Uaminifu!

Isaya 5:1-30

1, 2. “Mpenzi” apanda nini, lakini lathibitikaje kuwa lenye kukatisha tamaa?

“MFANO huu hauna kifani kuhusiana na uzuri wa lugha na ubora wa stadi katika mawasiliano yenye matokeo.” Ndivyo alivyosema mwelezaji mmoja wa Biblia akirejezea mistari ya kwanza ya Isaya sura ya 5. Mbali na kuwa sanaa, maneno ya Isaya yatoa wazo lenye kuchochea hisia juu ya utunzaji wenye upendo wa Yehova kwa watu wake. Wakati huohuo, maneno hayo yatuonya dhidi ya mambo yanayomchukiza.

2 Mfano wa Isaya waanza hivi: “Na nimwimbie mpenzi wangu wimbo wa mpenzi wangu katika habari za shamba lake la mizabibu. Mpenzi wangu alikuwa na shamba la mizabibu, kilimani penye kuzaa sana; akafanya handaki kulizunguka pande zote, akatoa mawe yake, akapanda ndani yake mzabibu ulio mzuri, akajenga mnara katikati yake, akachimba shinikizo ndani yake; akatumaini ya kuwa utazaa zabibu, nao ukazaa zabibu-mwitu.”—Isaya 5:1, 2; linganisha Marko 12:1.

Utunzaji wa Shamba la Mizabibu

3, 4. Shamba la mizabibu lapewa utunzaji gani wenye upendo?

3 Iwapo Isaya awaimbia kihalisi wasikilizaji wake mfano huo au la, huo kwa hakika wavuta fikira zao. Labda wengi wao wanafahamu kazi ya kupanda shamba la mizabibu, na ufafanuzi wa Isaya ni dhahiri na halisi. Sawa na wakuzao mizabibu leo, mmilikaji wa shamba la mizabibu apanda, si mbegu za zabibu, bali mzabibu “ulio mzuri [‘uliochaguliwa,’ BHN],” au “mzabibu mwekundu,” (NW) ulio bora—kitawi au mche kutoka kwa mzabibu mwingine. Kwa kufaa, yeye apanda mizabibu “kilimani penye kuzaa sana,” mahali ambapo shamba la mizabibu litasitawi.

4 Kazi ngumu yahitajika ili shamba la mizabibu lizae. Isaya aeleza kuwa mmilikaji ‘afanya handaki [“alililima vizuri,” BHN] shamba na kutoa mawe yake’—kazi ngumu, yenye kuchosha sana! Yaelekea atumia mawe yaliyo makubwa ‘kujenga mnara.’ Nyakati za kale, minara hiyo ilikuwa vituo vya walinzi walioilinda mimea dhidi ya wezi na wanyama.a Pia, ajenga ukuta wa mawe ili kuyazunguka matuta ya shamba hilo la mizabibu. (Isaya 5:5) Mara nyingi hilo lilifanywa ili kuzuia mmomonyoko wa udongo wa juu ulio muhimu.

5. Mmilikaji atarajia nini kwa kufaa kutoka kwa shamba lake la mizabibu, lakini yeye apata nini?

5 Baada ya kufanya kazi kwa bidii ili kulilinda shamba lake la mizabibu, mmilikaji ana haki ya kulitazamia lizae matunda. Kwa kutazamia hilo, yeye achimba shinikizo la divai. Lakini je, mavuno yanayotarajiwa yatokea? La, shamba hilo la mizabibu lazaa zabibu-mwitu.

Shamba la Mizabibu na Mmilikaji Wake

6, 7. (a) Ni nani aliye mmilikaji wa shamba la mizabibu, na shamba la mizabibu ni nini? (b) Mmilikaji aomba hukumu gani ifanywe?

6 Mmilikaji ni nani, nalo shamba la mizabibu ni nini? Mmilikaji wa shamba la mizabibu ajibu maswali hayo anaposema: “Sasa, enyi wenyeji wa Yerusalemu, nanyi watu wa Yuda, amueni, nawasihi, kati ya mimi na shamba langu la mizabibu. Je! ni kazi gani iliyoweza kutendeka ndani ya shamba langu la mizabibu nisiyoitenda? Basi, nilipotumaini ya kuwa litazaa zabibu, mbona lilizaa zabibu-mwitu? Haya basi, sasa nitawaambieni nitakalolitenda shamba langu la mizabibu; nitaondoa kitalu [“ua wa miti,” “NW”] chake, nalo litaliwa; nitabomoa ukuta wake, nalo litakanyagwa.”—Isaya 5:3-5.

7 Naam, Yehova ndiye mmilikaji wa shamba hilo la mizabibu, naye ni kama mtu anayeenda mahakamani, akitaka hukumu itolewe kati yake na shamba lake la mizabibu linalokatisha tamaa. Basi, shamba hilo la mizabibu ni nini? Mmilikaji aeleza: “Shamba la mizabibu la BWANA wa majeshi ndilo nyumba ya Israeli, na watu wa Yuda ni mche wake wa kupendeza.”—Isaya 5:7a.

8. Isaya amaanisha nini kwa kumwita Yehova “mpenzi wangu”?

8 Isaya amwita Yehova, aliye mmilikaji wa shamba la mizabibu, “mpenzi wangu.” (Isaya 5:1) Isaya aweza tu kumtaja Mungu kwa njia hiyo yenye urafiki kwa sababu ana uhusiano wa karibu pamoja Naye. (Linganisha Ayubu 29:4; Zaburi 25:14.) Hata hivyo, upendo wa nabii huyo kwa Mungu hauwezi kulingana na upendo ambao Mungu ameonyesha “shamba lake la mizabibu”—taifa ‘alilolipanda.’—Linganisha Kutoka 15:17; Zaburi 80:8, 9.

9. Yehova amelitunzaje taifa lake kama shamba la mizabibu lenye kuthaminiwa?

9 Yehova ‘alilipanda’ taifa lake katika nchi ya Kanaani na kuwapa sheria na kanuni zake, zilizokuwa kama ukuta wa kuwalinda ili mataifa mengine yasiwafisidi. (Kutoka 19:5, 6; Zaburi 147:19, 20; Waefeso 2:14) Pamoja na hayo, Yehova aliwapa waamuzi, makuhani, na manabii wa kuwafundisha. (2 Wafalme 17:13; Malaki 2:7; Matendo 13:20) Israeli ilipotishwa kwa uvamizi wa kijeshi, Yehova aliinua wakombozi. (Waebrania 11:32, 33) Kwa kufaa, Yehova auliza: “Je! ni kazi gani iliyoweza kutendeka ndani ya shamba langu la mizabibu nisiyoitenda?”

Kutambua Shamba la Mizabibu la Mungu Leo

10. Yesu alitoa mfano gani unaohusu shamba la mizabibu?

10 Huenda Yesu alikuwa akizingatia maneno ya Isaya alipotoa mfano wa walimaji wauaji: “Kulikuwa na mtu, mwenye nyumba, aliyepanda shamba la mizabibu na kuweka ua kulizunguka naye akachimba sindikio la divai katika hilo akasimamisha mnara, na kulikodisha kwa walimaji, na kusafiri nchi ya nje.” Kwa kuhuzunisha, walimaji hao walimsaliti mmilikaji wa shamba hilo la mizabibu, hata wakamwua mwanaye. Kisha Yesu akaonyesha kuwa mfano huo ulihusisha mengi kuliko tu Israeli halisi, aliposema hivi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu [Israeli la kimwili] na kupewa kwa taifa lenye kutokeza matunda yao.”—Mathayo 21:33-41, 43.

11. Ni shamba gani la mizabibu la kiroho lililokuwapo katika karne ya kwanza, lakini ni nini kilichotukia baada ya kifo cha mitume?

11 “Taifa” jipya hilo lilithibitika kuwa “Israeli wa Mungu”—taifa la kiroho la Wakristo watiwa-mafuta lenye idadi ya jumla ya 144,000. (Wagalatia 6:16; 1 Petro 2:9, 10; Ufunuo 7:3, 4) Yesu aliwafananisha wanafunzi hao na “matawi” katika “mzabibu wa kweli,” yaani, yeye mwenyewe. Kwa kawaida, matawi hayo hutarajiwa kuzaa matunda. (Yohana 15:1-5) Ni lazima wadhihirishe sifa kama za Kristo na kuishiriki kazi ya kuhubiri “habari njema hii ya ufalme.” (Mathayo 24:14; Wagalatia 5:22, 23) Lakini tangu kifo cha wale mitume kumi na wawili, wengi wa wale wanaodai kuwa matawi ya “mzabibu wa kweli” wamethibitika kuwa bandia—kwa kuzaa zabibu-mwitu badala ya matunda mema.—Mathayo 13:24-30, 38, 39.

12. Maneno ya Isaya yahukumuje Jumuiya ya Wakristo, nayo yana fundisho gani kwa Wakristo wa kweli?

12 Kwa hiyo, shutuma ya Isaya juu ya Yuda yahusu Jumuiya ya Wakristo leo. Uchunguzi wa historia yake—vita zake, krusedi zake, Mabaraza yake ya Kuhukumu Wazushi—wafunua kadiri ambayo matunda yake yamekuwa machungu! Hata hivyo, shamba la mizabibu la kweli la Wakristo watiwa-mafuta pamoja na waandamani wao wa “umati mkubwa” lazima watii maneno ya Isaya. (Ufunuo 7:9) Iwapo watampendeza mmilikaji wa shamba la mizabibu, ni lazima wao, mmoja-mmoja na pia wakiwa kikundi, wazae matunda yanayompendeza.

“Zabibu-Mwitu”

13. Yehova atalifanyaje shamba lake la mizabibu kwa kuwa lazaa matunda mabovu?

13 Baada ya kufanya kila jambo linalowezekana ili kulitunza na kulilima shamba lake la mizabibu, Yehova ana haki ya kutarajia liwe “shamba la mizabibu la mvinyo.” (Isaya 27:2) Hata hivyo, badala ya kuzaa matunda yawezayo kutumiwa, lazaa “zabibu-mwitu,” kihalisi “vitu vinavyovunda” au “matunda yanayovunda (yaliyooza).” (Isaya 5:2; NW, kielezi-chini; Yeremia 2:21) Kwa hiyo, Yehova atangaza kuwa ataondoa “ua [wake] wa miti” unaolizunguka na kulilinda taifa hilo. Taifa hilo ‘litaharibiwa’ nalo litaachwa na kupata ukame. (Soma Isaya 5:6.) Musa alikuwa ameonya kwamba wangepatwa na mambo hayo iwapo wangekataa kuitii Sheria ya Mungu.—Kumbukumbu la Torati 11:17; 28:63, 64; 29:22, 23.

14. Yehova atarajia matunda gani kutoka kwa taifa lake, lakini hilo lazaa nini badala yake?

14 Mungu atarajia taifa hilo lizae matunda mema. Mika, aliyeishi wakati wa Isaya, atangaza hivi: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” (Mika 6:8; Zekaria 7:9) Hata hivyo, taifa hilo lashindwa kutii himizo la Yehova. “[Mungu] akatumaini kuona hukumu ya haki, na kumbe! aliona dhuluma; alitumaini kuona haki, na kumbe! alisikia kilio.” (Isaya 5:7b) Musa alitabiri kuwa taifa hilo lisilo na uaminifu lingezaa zabibu zenye sumu kutoka kwa “mzabibu wa Sodoma.” (Kumbukumbu la Torati 32:32) Basi, yaelekea kwamba ukosefu wa adili katika ngono, pamoja na ugoni-jinsia-moja, ni sehemu ya mkengeuko wao kutoka kwa Sheria ya Mungu. (Mambo ya Walawi 18:22) Usemi “dhuluma [“uvunjaji wa sheria,” NW]” waweza pia kufasiriwa “umwagaji wa damu.” Hapana budi matendo hayo ya kinyama yamesababisha “kilio” kwa wale wanaotendwa vibaya—kilio ambacho kimeyafikia masikio ya Mpanzi wa shamba la mizabibu.—Linganisha Ayubu 34:28.

15, 16. Wakristo wa kweli waweza kuepukaje kuzaa matunda mabovu ambayo Israeli ilizaa?

15 Yehova Mungu “apenda uadilifu na haki.” (Zaburi 33:5, BHN) Aliwaamuru Wayahudi hivi: “Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki.” (Mambo ya Walawi 19:15) Kwa hiyo ni lazima tuepuke kuegemea upande mmoja tunaposhughulikiana, wala tusiruhusu kamwe mambo kama vile jamii, umri, mali, au umaskini yapotoe maoni yetu kuhusu watu. (Yakobo 2:1-4) Hasa ni muhimu kwa waangalizi ‘kutofanya jambo lolote kulingana na mwelekeo wenye kuegemea upande,’ sikuzote wajaribu kusikiliza pande zote za jambo kabla ya kukata hukumu.—1 Timotheo 5:21; Mithali 18:13.

16 Na zaidi, yaweza kuwa rahisi kwa Wakristo wanaoishi katika ulimwengu wenye kuasi sheria kusitawisha maoni mabaya au mwelekeo wa kuasi viwango vya Mungu. Ingawa hivyo, Wakristo wa kweli lazima wawe “tayari kutii” sheria za Mungu. (Yakobo 3:17) Kujapokuwa ukosefu wa adili katika ngono na jeuri ya “mfumo mwovu wa mambo uliopo,” wao wahitaji ‘kufuliza kuangalia sana kwamba jinsi wanavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima.’ (Wagalatia 1:4; Waefeso 5:15) Wao huazimia kuepuka maoni yenye uendekevu juu ya ngono, na hali za kutoelewana zitokeapo, wapaswa kuzitatua pasipo “hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi.” (Waefeso 4:31) Wakristo wa kweli humletea Mungu heshima nao hupata upendeleo wake kwa kusitawisha uadilifu.

Matokeo ya Pupa

17. Ni mwenendo gani mwovu unaoshutumiwa katika ole wa kwanza wa Isaya?

17 Katika mstari wa 8, Isaya haendelei kunukuu maneno ya Yehova. Huku akishutumu baadhi ya “zabibu-mwitu” zinazozaliwa katika Yuda, yeye binafsi atangaza ole wa kwanza kati ya ole sita: “Ole wao waongezao nyumba baada ya nyumba, na kuweka shamba karibu na shamba, hata hapana nafasi tena, nanyi hamna budi kukaa peke yenu kati ya nchi! BWANA wa majeshi asema katika masikio yangu, Hakika majumba mengi yatakuwa ukiwa, naam, majumba makubwa, mazuri, yatakuwa hayana watu. Kwa maana shamba la mizabibu la eka kumi litatoa bathi moja tu, na homeri ya mbegu itatoa efa tu.”—Isaya 5:8-10.

18, 19. Watu wa siku ya Isaya wanapuuzaje sheria za Yehova kuhusu mali, na matokeo yatakuwa nini kwao?

18 Katika Israeli ya kale, nchi yote ilikuwa mali ya Yehova. Kila familia ilipata urithi kutoka kwa Mungu, ambao wangeweza kuukodisha au kuukopesha, ila hawangeweza kuuuza “kabisa kabisa.” (Mambo ya Walawi 25:23) Sheria hiyo ilizuia utumiaji mbaya, kama vile kuhodhi mashamba. Hiyo pia ilizilinda familia zisiwe maskini hohehahe. Ijapokuwa hivyo, watu fulani katika Yuda walikuwa wakivunja kwa pupa sheria za Mungu juu ya mali. Mika aliandika hivi: “Nao hutamani mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na nyumba yake, naam, mtu na urithi wake.” (Mika 2:2) Lakini Mithali 20:21 yaonya hivi: “Urithi uliopatikana mwanzo kwa haraka, mwisho wake, lakini, hautabarikiwa.”

19 Yehova aahidi kuwanyang’anya watu hao wenye pupa mali waliyoipata kwa ufisadi. Nyumba wanazonyakua ‘hazitakuwa na watu.’ Mashamba wanayotamani yatazaa tu sehemu ndogo sana ya uwezo wake. Wakati na namna barabara ya kutimizwa kwa laana hiyo haukutaarifiwa. Yamkini yarejezea, angalau kwa sehemu, zile hali zinazosababishwa na uhamisho wa baadaye huko Babiloni.—Isaya 27:10.

20. Wakristo leo waweza kuepukaje kuiga mtazamo wenye pupa waliokuwa nao watu fulani huko Israeli?

20 Wakristo leo lazima wachukie kabisa pupa isiyoridhika kama ile waliyokuwa nayo Waisraeli wa kale. (Mithali 27:20) Vitu vya kimwili vinapopewa umuhimu kupita kiasi, ni rahisi kujitweza kwa kufuatia njia zisizo za adili ili kupata pesa. Huenda mtu akanaswa kwa urahisi katika biashara zisizofaa au miradi isiyofaa ya kutajirika haraka. “Afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.” (Mithali 28:20) Basi, ni muhimu kama nini turidhike na vitu tulivyo navyo!—1 Timotheo 6:8.

Mtego wa Vitumbuizo Vyenye Kutilika Shaka

21. Ni dhambi gani zinazoshutumiwa katika ole wa pili wa Isaya?

21 Kisha ole wa pili wa Isaya: “Ole wao waamkao asubuhi na mapema, wapate kufuata kileo; wakishinda sana hata usiku wa manane mpaka mvinyo imewaka kama moto ndani yao! Na kinubi, na zeze, na matari, na filimbi, na mvinyo, zote ziko katika karamu zao; lakini hawaiangalii kazi ya BWANA wala kuyafikiri matendo ya mikono yake.”—Isaya 5:11, 12.

22. Ni ukosefu gani wa kujidhibiti unaodhihirika katika Israeli, na kutakuwa na matokeo gani kwa taifa hilo?

22 Yehova ndiye “Mungu mwenye furaha” naye haudhiwi na tafrija yenye kiasi ya watumishi wake. (1 Timotheo 1:11) Hata hivyo, hao watafutaji wa raha wamezidi! “Wale walewao hulewa usiku,” Biblia yasema. (1 Wathesalonike 5:7) Lakini katika unabii huo, watu wanaofanya karamu zenye makelele huanza karamu zao za ulevi alfajiri nao huendelea hadi jioni! Wao hutenda kana kwamba Mungu hayuko, kana kwamba hatawahukumu kulingana na matendo yao. Isaya atabiri wakati ujao ulio mbaya kwa watu kama hao. “Watu wangu wamechukuliwa mateka, kwa kukosa kuwa na maarifa [“ujuzi,” “NW”]; na watu wao wenye cheo wana njaa, na wengi wao waona kiu sana.” (Isaya 5:13) Kwa sababu wamekataa kutenda kupatana na ujuzi wa kweli, watu wa Mungu wa agano—wakubwa kwa wadogo—wataingia Sheoli.—Soma Isaya 5:14-17.

23, 24. Wakristo hutakiwa wadhihirishe kujidhibiti na usawaziko wa aina gani?

23 “Sherehe zenye kelele za ulevi na ulafi” au “karamu zenye makelele” pia zilikuwa tatizo miongoni mwa Wakristo fulani katika karne ya kwanza. (Wagalatia 5:21; Byington; 2 Petro 2:13) Basi haishangazi kwamba Wakristo fulani leo waliojiweka wakfu wamekosa ufahamu kuhusiana na vikusanyiko vya kirafiki. Wengine wamepiga makelele na kufanya ugomvi kwa sababu ya kunywa kileo kupita kiasi. (Mithali 20:1) Hata wengine wamekosa adili kwa kuchochewa na kileo kingi mno, na vikusanyiko fulani vimeruhusiwa kuendelea karibu usiku kucha, na kuvuruga utendaji wa Kikristo siku inayofuata.

24 Hata hivyo, Wakristo wenye usawaziko huzaa matunda ya kimungu nao hujidhibiti na kusawazika wanapochagua tafrija. Wao hutii shauri la Paulo katika Waroma 13:13: “Kama katika wakati wa mchana acheni tujiendeshe kwa adabu, si katika sherehe zenye makelele ya ulevi na vipindi vya kulewa.”

Kuchukia Dhambi na Kupenda Kweli

25, 26. Isaya afunua hali gani mbovu ya kufikiri kwa Waisraeli katika ole wa tatu na wa nne?

25 Sasa sikiliza ole wa tatu na wa nne wa Isaya: “Ole wao wavutao uovu kwa kamba za ubatili, na dhambi kama kwa kamba za gari! Wasema, Na afanye haraka, aihimize kazi yake, tupate kuiona; na likaribie shauri lake aliye Mtakatifu wa Israeli, tupate kuliona. Ole wao wasemao kwamba uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu; watiao giza badala ya nuru, na nuru badala ya giza; watiao uchungu badala ya utamu, na utamu badala ya uchungu!”—Isaya 5:18-20.

26 Hiyo yawafafanua kinaganaga kama nini wale wanaozoea dhambi! Wameshikamana na dhambi kama vile wanyama wavutao mizigo wanavyofungwa kwenye magari. Watenda-dhambi hao hawaogopi siku yoyote ya hukumu inayokuja. Wao wasema kwa dhihaka: “[Mungu] na . . . aihimize kazi yake”! Badala ya kuitii Sheria ya Mungu, wao hupotoa mambo, wakitangaza kuwa “uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu.”—Linganisha Yeremia 6:15; 2 Petro 3:3-7.

27. Wakristo leo waweza kuepukaje mtazamo kama ule wa Waisraeli?

27 Ni lazima Wakristo leo waepuke kabisa-kabisa mtazamo kama huo. Kwa kielelezo, wao huyakataa maoni ya ulimwengu yanayosema kwamba uasherati na ugoni-jinsia-moja ni sawa. (Waefeso 4:18, 19) Ni kweli kwamba huenda Mkristo “a[ka]chukua hatua fulani isiyo ya kweli” ambayo ingeweza kusababisha kutenda dhambi nzito. (Wagalatia 6:1) Wazee kutanikoni wako tayari kuwasaidia wale ambao wameanguka na wanahitaji msaada. (Yakobo 5:14, 15) Kupitia sala na shauri linalotegemea Biblia, yawezekana kupata tena nafuu ya kiroho. La sivyo, kuna hatari ya kuwa “mtumwa wa dhambi.” (Yohana 8:34) Badala ya kumdhihaki Mungu na kupoteza ufahamu wa siku ya hukumu inayokuja, Wakristo hujitahidi kudumu “bila doa na bila waa” mbele za Yehova.—2 Petro 3:14; Wagalatia 6:7, 8.

28. Ni dhambi gani zinazoshutumiwa katika ole za mwisho za Isaya, na Wakristo leo waweza kuepukaje dhambi kama hizo?

28 Kwa kufaa basi, Isaya aongeza ole hizi za mwisho: “Ole wao walio wenye hekima katika macho yao wenyewe, na wenye busara katika fikira zao wenyewe! Ole wao walio hodari kunywa kileo chenye nguvu, watu waume wenye nguvu kuchanganya vileo; wampao haki mwenye uovu, ili wapewe ijara, na kumwondolea mwenye haki haki yake!” (Isaya 5:21-23) Yamkini waamuzi katika nchi hiyo ndio walioambiwa maneno hayo. Wazee wa kutaniko leo huepuka kuwa “wenye hekima katika macho yao wenyewe.” Wao hukubali kwa unyenyekevu shauri kutoka kwa wazee wenzao nao hushikamana kabisa na maagizo ya tengenezo. (Mithali 1:5; 1 Wakorintho 14:33) Wao wana usawaziko katika utumiaji wa vileo, nao hawatumii vileo kamwe kabla ya kushughulikia majukumu ya kutaniko. (Hosea 4:11) Wazee pia huepuka kabisa kuonekana kuwa wenye kupendelea. (Yakobo 2:9) Wazee hao ni tofauti kama nini na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo! Makasisi wengi huficha watenda-dhambi mashuhuri na wenye mali miongoni mwao, kinyume kabisa cha maonyo ya mtume Paulo katika Waroma 1:18, 26, 27; 1 Wakorintho 6:9, 10; na Waefeso 5:3-5.

29. Ni mwisho gani wenye msiba utakaolipata shamba la mizabibu la Yehova la Israeli?

29 Isaya amalizia ujumbe huo wa unabii kwa kusimulia mwisho wenye msiba kwa wale ambao “wameikataa sheria ya BWANA” na kushindwa kuzaa matunda ya uadilifu. (Isaya 5:24, 25; Hosea 9:16; Malaki 4:1) Atangaza hivi: “[Yehova] atawatwekea bendera mataifa toka mbali, naye atawapigia miunzi tokea mwisho wa nchi; na tazama, watakuja mbio mbio upesi sana.”—Isaya 5:26; Kumbukumbu la Torati 28:49; Yeremia 5:15.

30. Ni nani atakayekusanya “taifa kubwa” dhidi ya watu wa Yehova, na matokeo yatakuwaje?

30 Nyakati za kale, mhimili uliokuwa mahali palipoinuka ungalikuwa kama “bendera [“ishara,” NW],” au kama mahali pa kukusanyika, kwa watu au majeshi. (Linganisha Isaya 18:3; Yeremia 51:27.) Sasa Yehova mwenyewe atakusanya “mataifa [“taifa kubwa,” NW]” ili litekeleze hukumu yake.b ‘Atalipigia miunzi,’ yaani, atageuza fikira za taifa hilo kwa watu wake waliopotoka ambao ni kama chombo kinachostahili kutekwa. Kisha nabii huyo afafanua shambulio la kasi na lenye kutisha la washindi hao walio kama simba ambao ‘watakamata mateka,’ yaani, taifa la Mungu, na “kuyachukua na kwenda zao salama” utekwani. (Soma Isaya 5:27-30a.) Na tokeo kwa nchi ya watu wa Yehova lahuzunisha kama nini! “Mtu akiitazama nchi, ataona giza na dhiki nayo nuru imetiwa giza katika mawingu yake.”—Isaya 5:30b.

31. Wakristo wa kweli waweza kuepukaje adhabu iliyoletwa juu ya shamba la mizabibu la Yehova la Israeli?

31 Naam, shamba la mizabibu ambalo Mungu alipanda kwa upendo lajithibitisha kuwa lisilozaa—linalostahili tu kuharibiwa. Maneno ya Isaya kwa wote wanaotaka kumtumikia Yehova leo yanatoa fundisho lenye nguvu kama nini! Na wajitahidi kuzaa matunda ya uadilifu peke yake, yamletee Yehova sifa nayo yatokeze wokovu wao wenyewe!

[Maelezo ya Chini]

a Wasomi fulani huamini kuwa majengo ya bei rahisi na ya muda mfupi, kama vile mahema, au vibanda, yalitumiwa mara nyingi kuliko minara ya mawe. (Isaya 1:8) Kuwepo kwa mnara kungeonyesha kuwa mwenye-shamba amelifanyia “shamba lake la mizabibu” kazi kubwa zaidi.

b Katika unabii mwingine mbalimbali, Isaya atambulisha Babiloni kuwa taifa linalotekeleza hukumu ya Yehova yenye kuangamiza dhidi ya Yuda.

[Picha katika ukurasa wa 83]

Mtenda-dhambi ameshikamana na dhambi kama vile mnyama avutaye mizigo anavyofungwa kwenye gari

[Picha kaitika ukurasa wa 85]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki