Sehemu ya 2
Dunia Isiyo Na Kuteseka
1, 2. Ni maoni gani tofauti waliyo nayo wengi?
HATA hivyo, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wana maoni yaliyo tofauti kabisa. Wao wanaona kimbele wakati ujao ulio mzuri ajabu kwa ajili ya ainabinadamu. Wao husema kwamba karibuni papa hapa duniani utakuwapo ulimwengu usio na uovu na kuteseka hata kidogo. Wao wana uhakika kwamba karibuni mambo mabaya yataondolewa kabisa na ulimwengu mpya kabisa usimamishwe. Wao hata husema kwamba msingi wa huo ulimwengu mpya unafanyizwa sasa hivi!
2 Watu hao wanasadiki kwamba ulimwengu huo mpya hautakuwa na vita, ukatili, uhalifu, ukosefu wa haki, na umaskini. Utakuwa ulimwengu usio na magonjwa, huzuni, machozi, na hata kifo. Wakati huo watu watakua wafikie ukamilifu na kuishi milele kwa furaha katika paradiso ya kidunia. Kwani, wale ambao wamekufa hata watafufuliwa na kuwa na fursa ya kuishi milele!
3, 4. Kwa nini watu hao wanahisi kuwa wenye hakika juu ya maoni yao?
3 Je! maoni hayo juu ya wakati ujao ni ndoto tu, tamanio tu la kiakili lisiloweza kutimia? Sivyo, hata kidogo. Msingi wayo ni imani yenye msingi imara kwamba Paradiso hiyo inayokuja itakuwapo bila shaka. (Waebrania 11:1) Kwa nini wana hakika sana hivyo? Kwa sababu mweza yote, Muumba wa ulimwengu wote mzima ameuahidi.
4 Kuhusu ahadi za Mungu, Biblia husema hivi: “Halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA [Yehova, New World Translation], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” “Mungu si mtu, aseme uongo . . . Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza?” “BWANA [Yehova, NW] wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile [n]ilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.”—Yoshua 23:14; Hesabu 23:19; Isaya 14:24.
5. Ni maswali gani yanayohitaji kujibiwa?
5 Hata hivyo, ikiwa kusudi la Mungu lilikuwa kusimamisha paradiso ya kidunia isiyo na kuteseka, kwanza kabisa, kwa nini ameruhusu mambo mabaya yatukie? Kwa nini alingoja miaka elfu sita mpaka sasa ili kusahihisha makosa? Je, karne hizo zote za kuteseka zaweza kudokeza kwamba kwa kweli Mungu hatujali sisi, au hata kwamba hayuko?