Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 31 kur. 704-709
  • Jinsi Huchaguliwa na Kuongozwa na Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Huchaguliwa na Kuongozwa na Mungu
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uchaguzi wa Mungu Katika Nyakati za Biblia
  • Namna Gani Kuhusu Kuchagua kwa Mungu Leo?
  • Jitihada ya Kutafuta Ile Kweli kwa Mafanikio
  • Jinsi Yehova Anavyowaongoza Watu Wake
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Namna Yehova Anavyoongoza Watu Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Jinsi ya Kutambua Dini ya Kweli
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 31 kur. 704-709

Sura ya 31

Jinsi Huchaguliwa na Kuongozwa na Mungu

“MAWAZO mazuri yanaonyesha kwamba kungekuwako dini moja tu ya kweli. Hiyo inapatana na uhakika wa kwamba yule Mungu wa kweli ‘si Mungu wa machafuko, bali wa amani.’ (1 Wakorintho 14:33) Biblia inasema kwamba hakika kuna ‘imani moja’ tu. (Waefeso 4:5) Basi, ni nani walio kikundi cha waabudu wa kweli leo? Tunasema wazi bila kusita kwamba ni Mashahidi wa Yehova,” chajulisha wazi kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.a

‘Mnawezaje kuwa na uhakika hivyo kwamba mna dini ya kweli?’ huenda wengine wakauliza. ‘Nyinyi hamna uthibitisho unaopita uwezo wa kibinadamu—kama vile vipawa vya kimuujiza. Na katika muda wa miaka je, hamjawajibika kufanya marekebisho katika maoni na mafundisho yenu? Basi mnawezaje kuwa na uhakika kabisa kwamba mnaongozwa na Mungu?’

Ili kujibu maswali hayo, ni jambo lenye msaada kufikiria kwanza jinsi Yehova alivyochagua na kuongoza watu wake katika nyakati za kale.

Uchaguzi wa Mungu Katika Nyakati za Biblia

Katika karne ya 16 K.W.K., Yehova aliwakusanya Waisraeli kwenye Mlima Sinai na kuwaalika wawe watu wake waliochaguliwa. Hata hivyo, kwanza aliwajulisha kwamba kulikuwa na matakwa hususa ambayo wangewajibika kutimiza. Yeye aliwaambia hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli . . . , hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu.” (Kut. 19:5, italiki ni zetu.) Kupitia Musa, Yehova alionyesha waziwazi matakwa hayo, na kisha watu wakaitikia kusema: “Hayo yote aliyoyanena BWANA tutayatenda.” Kisha Yehova akafanya agano na Israeli na kuwapa Sheria yake.—Kut. 24:3-8, 12.

Kuchaguliwa na Mungu—ni pendeleo kuu jinsi gani! Lakini pendeleo hilo lililetea Israeli daraka la kutii kikamili Sheria ya Mungu. Kushindwa kufanya hivyo kungewafanya wakataliwe wakiwa taifa. Ili atie ndani yao hofu ifaayo ili waweze kumtii yeye, Yehova alifanya ishara zenye kutazamisha, zipitazo uwezo wa kibinadamu—“palikuwa na ngurumo na umeme,” na “mlima wote ukatetemeka sana.” (Kut. 19:9, 16-18; 20:18, 20) Kwa miaka karibu 1,500 iliyofuata, Waisraeli walikuwa katika msimamo wa pekee—walikuwa watu waliochaguliwa na Mungu.

Hata hivyo, katika karne ya kwanza W.K., hali ilibadilika sana. Israeli ilipoteza cheo chayo chenye upendeleo, ikatupiliwa mbali na Yehova kwa sababu ya kumkataa Mwanae. (Mt. 21:43; 23:37, 38; Mdo. 4:24-28) Kisha Yehova akaanzisha kutaniko la Kikristo la mapema, msingi walo ukiwa Kristo. Kwenye Pentekoste 33 W.K., Yehova alimwaga roho yake takatifu juu ya wafuasi wa Yesu katika Yerusalemu, akiwafanya wawe “jamii iliyochaguliwa, . . . taifa takatifu, watu kwa ajili ya miliki ya pekee.” (1 Pet. 2:9, NW; Mdo. 2:1-4; Efe. 2:19, 20) Wakawa “wachaguliwa wa Mungu.”—Kol. 3:12, NW.

Kuwa mshiriki katika taifa hilo lililochaguliwa kulikuwa na masharti. Yehova aliweka matakwa ya kiadili na kiroho ya hali ya juu ambayo lazima yangetimizwa. (Gal. 5:19-24) Wale waliojipatanisha na matakwa hayo walijiweka katika mstari wa kuchaguliwa naye. Hata hivyo, wakiisha kuchaguliwa na Mungu, lilikuwa jambo la maana kwamba wabaki wakiwa watiifu kwa sheria zake. Ni wale tu ‘wanaomtii kuwa mtawala’ ndio wangeendelea kupokea roho yake takatifu. (Mdo. 5:32) Wale walioshindwa kumtii walikuwa katika hatari ya kutupwa nje ya kutaniko na kupoteza urithi wao katika Ufalme wa Mungu.—1 Kor. 5:11-13; 6:9, 10.

Lakini wengine wangejuaje kwa hakika kwamba Mungu alikuwa amechagua kutaniko hilo la Wakristo la mapema kuchukua mahali pa Israeli kuwa “kutaniko la Mungu”? (Mdo. 20:28, NW) Watu waliochaguliwa na Mungu walijulikana wazi. Kufuatia kifo cha Yesu, Yeye alitoa vipawa vya kimuujiza kwa washiriki wa kutaniko la Kikristo la mapema ili kuonyesha kwamba wao sasa walikuwa wachaguliwa wa Mungu.—Ebr. 2:3, 4.

Je, ishara zinazopita uwezo wa kibinadamu, au miujiza, ingehitajiwa sikuzote ili kutambulisha wale waliochaguliwa na kuongozwa na Mungu katika nyakati za Biblia? La, hasha. Kazi za kimuujiza hazikuwa tukio la kawaida kotekote katika historia ya Biblia. Watu wengi walioishi katika nyakati za Biblia hawakushuhudia muujiza. Miujiza mingi iliyorekodiwa katika Biblia ilitukia siku za Musa na Yoshua (karne za 16 na 15 K.W.K.), Elija na Elisha (karne za 10 na 9 K.W.K.), na Yesu na mitume wake (karne ya 1 W.K.). Watu wengine waaminifu waliochaguliwa na Mungu kwa makusudi hususa, kama vile Abrahamu na Daudi, waliona au wakapata madhihirisho ya uwezo wa Mungu, lakini hakuna ithibati yoyote kwamba wao wenyewe walifanya miujiza. (Mwa. 18:14; 19:27-29; 21:1-3; linganisha 2 Samweli 6:21; Nehemia 9:7.) Kuhusu vipawa vya kimuujiza vilivyokuwapo katika karne ya kwanza, Biblia ilitabiri kwamba hivyo ‘vingeondolewa mbali.’ (1 Kor. 13:8, NW) Na hilo lilitukia baada ya mtume wa mwisho kati ya wale 12 alipokufa pamoja na wale waliokuwa wamepokea vipawa vya kimuujiza kupitia kwao.—Linganisha Matendo 8:14-20.

Namna Gani Kuhusu Kuchagua kwa Mungu Leo?

Baada ya karne ya kwanza, uasi-imani uliotabiriwa ulisitawi bila kuzuiwa. (Mdo. 20:29, 30; 2 The. 2:7-12) Kwa karne nyingi taa ya Ukristo wa kweli iliwaka kidogo sana. (Linganisha Mathayo 5:14-16.) Na bado, katika kielezi kimoja Yesu alionyesha kwamba kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo,” kungekuwa na tofauti bayana kati ya “ngano,” (Wakristo wa kweli) na “magugu,” (Wakristo wasio wa kweli). Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, ile ngano, au “wachaguliwa wake,” wangekusanywa katika kutaniko la Kikristo la kweli. (Mt. 13:24-30, 36-43, NW) Yesu pia alieleza juu ya washiriki watiwa-mafuta wa kutaniko hilo kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na akaonyesha kwamba katika wakati wa mwisho, wao wangekuwa wakitoa chakula cha kiroho. (Mt. 24:3, 45-47, NW) Mtumwa huyo mwaminifu angeungwa mkono na “umati mkubwa” wa waabudu wa kweli kutoka kwa mataifa yote.—Ufu. 7:9, 10, NW; linganisha Mika 4:1-4.

Waabudu wa kweli wanaoishi katika wakati wa mwisho wangetambuliwaje? Je, sikuzote wangekuwa hawakosei, je, uamuzi wao ungekuwa usioweza kuwa na makosa? Mitume wa Yesu bado walihitaji kusahihishwa. (Luka 22:24-27; Gal. 2:11-14) Kama vile mitume, ni lazima wafuasi wa kweli wa Kristo katika siku yetu wawe wanyenyekevu, wenye nia ya kukubali nidhamu, na inapohitajika, wafanye marekebisho, ili kuleta fikira zao katika upatani wa karibu hata zaidi na zile za Mungu.—1 Pet. 5:5, 6.

Wakati ulimwengu ulipoingia kwenye siku za mwisho katika 1914, ni kikundi kipi kilichothibitika kuwa tengenezo moja la kweli la Kikristo? Jumuiya ya Wakristo ilikuwa na makanisa mengi yaliyodai kumwakilisha Kristo. Lakini swali ni: Ni jipi kati yayo, ikiwa kuna lolote, ambalo lilikuwa likitimiza matakwa ya Kimaandiko?

Hilo kutaniko moja la Kikristo la kweli lingewajibika kuwa tengenezo linaloshikilia Biblia kuwa mamlaka yalo ya kwanza, sio lile linalonukuu mistari hapa na pale lakini linakataa mingine yote wakati hiyo inapokosa kupatana na theolojia yalo ya wakati huo. (Yn. 17:17; 2 Tim. 3:16, 17) Lazima lingekuwa tengenezo ambalo washiriki walo—sio baadhi yao bali wote—kwelikweli wangekuwa si sehemu ya ulimwengu, katika kumwiga Kristo. Kwa hiyo wao wangeweza kujihusishaje katika siasa, kama vile makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamefanya mara kwa mara? (Yn. 15:19; 17:16) Lazima tengenezo la Kikristo la kweli lingetoa ushahidi juu ya jina la kimungu, Yehova, na kufanya kazi ambayo Yesu aliamuru—kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kama lile kutaniko la karne ya kwanza, washiriki walo wote, wala si wachache tu, wangekuwa waeneza-evanjeli wa nafsi yote. (Isa. 43:10-12; Mt. 24:14; 28:19, 20; Kol. 3:23) Waabudu wa kweli wangejulikana pia kwa upendo wao wenye kujidhabihu kwa mmoja na mwenzake, upendo ambao ungepita mipaka ya kikabila na kitaifa na kuwaunganisha katika udugu wa ulimwenguni pote. Lazima upendo huo ungedhihirishwa si katika visa vichache tu bali katika njia ambayo ingewatofautisha kikweli wakiwa tengenezo.—Yn. 13:34, 35.

Kwa wazi, wakati wa mwisho ulipoanza katika 1914, hakuna yoyote ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliyokuwa yakijipatanisha na viwango hivyo vya Biblia vya kutaniko la Kikristo la kweli. Lakini namna gani kuhusu Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo?

Jitihada ya Kutafuta Ile Kweli kwa Mafanikio

Akiwa kijana, C. T. Russell alifikia mkataa kwamba Biblia ilikuwa imefafanuliwa vibaya na Jumuiya ya Wakristo. Aliamini pia kwamba huo ulikuwa wakati ufaao wa Neno la Mungu kuweza kueleweka na kwamba wale ambao wangejifunza Biblia kwa unyoofu na kuitumia maishani mwao wangepata uelewevu.

Kitabu cha masimulizi ya maisha ya Russell, kilichotangazwa muda mfupi baada ya kifo chake, kilieleza: “Yeye hakuwa mwanzilishi wa dini mpya, na hakufanya dai kama hilo kamwe. Alifufua kweli mashuhuri ambazo Yesu na Mitume walifundisha, akawasha nuru ya karne ya ishirini juu yazo. Hakufanya dai lolote la kupata ufunuo wa pekee kutoka kwa Mungu, lakini akasisitiza kwamba huo ulikuwa wakati ufaao wa Mungu kufanya Biblia iweze kueleweka; na kwamba yeye akiwa amejitakasa kikamili kwa Bwana na kwa utumishi Wake, aliruhusiwa kuielewa. Kwa sababu alijitoa mwenyewe kwenye usitawi wa matunda na neema ya Roho Takatifu, ahadi ya Bwana ilitimizwa kwake: ‘Maana mambo hayo yakiwa kwenu na kujaa tele, yawafanya nyinyi kuwa si wavivu wala si watu wasio na matunda, kwa kumjua Bwana wetu Yesu Kristo.’—2 Petro 1:5-8.”—The Watch Tower, Desemba 1, 1916, uku. 356.

Jitihada ya kutafuta uelewevu wa Kimaandiko ya C. T. Russell na washiriki wake ilifanikiwa. Wakiwa wapenda kweli, waliamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa. (2 Tim. 3:16, 17) Walikataa mawazo ya mageuzi ya Darwin na maoni yenye kuangamiza imani ya wahakiki wa Biblia. Wakikubali Maandiko kuwa mamlaka kuu zaidi, walikataa pia mafundisho ya Utatu, kutokufa kwa nafsi, na mateso ya milele kuwa yasiyo ya kimaandiko—mafundisho yenye mashina ya kipagani. Miongoni mwa “kweli mashuhuri” walizokubali zilikuwa kwamba Yehova ni Muumba wa vitu vyote, kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu, aliyetoa uhai wake kuwa fidia kwa ajili ya wengine, na kwamba katika kurudi kwake Yesu angekuwapo bila kuonekana akiwa kiumbe cha roho. (Mt. 20:28; Yn. 3:16; 14:19; Ufu. 4:11) Pia walielewa waziwazi kwamba mwanadamu ni nafsi iwezayo kufa.—Mwa. 2:7; Eze. 18:20.

Si kwamba Wanafunzi wa Biblia walioshirikiana na Russell walifunua kweli hizo zote; nyingi zazo zilikuwa zimeeleweka mapema na watu wanyoofu waliodai kuwa Wakristo, baadhi yao hata wakishikilia masadikisho yao wakati imani hizo hazikupendwa na wengi. Lakini je, watu hao walijipatanisha na matakwa yote ya Kimaandiko kwa ajili ya ibada ya kweli? Kwa kielelezo, je, wao walikuwa kikweli si sehemu ya ulimwengu, kama vile Yesu alivyosema wafuasi wake wa kweli hawangekuwa sehemu yao?

Kuongezea jinsi walivyoiona Biblia, Wanafunzi wa Biblia wa mapema walioshirikiana na Russell walikuwa tofauti katika njia zipi nyinginezo? Kwa hakika katika bidii waliyodhihirisha kwa kushiriki itikadi zao na wengine, wakikazia hususa kupiga mbiu juu ya jina na Ufalme wa Mungu. Ingawa walikuwa wachache, upesi walifikia nchi nyingi wakiwa na habari njema. Je, wao pia walikuwa kwelikweli si sehemu ya ulimwengu, wakiwa wafuasi wa Kristo? Katika mambo fulani, ndiyo. Lakini ufahamu wao juu ya daraka linalohusika na hilo umekua tangu Vita ya Ulimwengu 1, hadi sasa limekuwa jambo lenye kutokeza la Mashahidi wa Yehova. Haipaswi kupuuzwa kwamba wakati vikundi vingine vya kidini vilipokuwa vikisifu Ushirika wa Mataifa na, baadaye, Umoja wa Mataifa, Mashahidi wa Yehova walipiga mbiu ya Ufalme wa Mungu—si tengenezo lolote lililofanyizwa na binadamu—kuwa tumaini pekee la wanadamu.

Lakini je, si baadhi ya imani za Mashahidi wa Yehova zimepata marekebisho kwa kupita kwa miaka mingi? Ikiwa wao walikuwa wamechaguliwa na kuongozwa na Mungu kikweli na hasa ikiwa mafundisho yao yalitegemezwa na mamlaka ya Maandiko, kwa nini mabadiliko hayo yangehitajiwa?

Jinsi Yehova Anavyowaongoza Watu Wake

Wale wanaofanyiza tengenezo la Kikristo la kweli leo hawana mafunuo ya kimalaika au upulizio wa kimungu. Lakini wana Maandiko Matakatifu yaliyopuliziwa, ambayo yana mafunuo ya fikira na mapenzi ya Mungu. Wakiwa tengenezo na watu mmoja-mmoja, ni lazima wakubali Biblia kuwa kweli ya kimungu, waisome kwa uangalifu, na waiache ifanye kazi ndani yao. (1 The. 2:13) Lakini wao hufikiaje uelewevu sahihi wa Neno la Mungu?

Biblia yenyewe husema: “Kufasiri si kazi ya Mungu?” (Mwa. 40:8) Ikiwa katika funzo lao la Maandiko fungu fulani ni gumu kuelewa, ni lazima watafute kupata vifungu vingine vilivyopuliziwa vinavyoeleza juu ya habari hiyo. Hivyo wao huacha Biblia ijifasiri yenyewe, na kutokana na hayo wanajitahidi kuelewa “kiolezo” cha kweli kilichoonyeshwa katika Neno la Mungu. (2 Tim. 1:13, NW) Yehova huongoza au huwaelekeza kwa uelewevu kama huo kupitia roho yake takatifu. Lakini ili kupata mwelekezo wa roho hiyo, ni lazima wasitawishe matunda yayo, si kuihuzunisha au kutenda dhidi yayo, na kuendelea kufuata mielekezo yayo. (Gal. 5:22, 23, 25; Efe. 4:30) Zaidi ya hiyo, kwa kutumia kwa bidii yale wanayojifunza, wao huendelea kujenga imani yao, ikiwa msingi wa kupata uelewevu ulio wazi zaidi na zaidi wa jinsi wanavyopaswa kufanya mapenzi ya Mungu katika ulimwengu ambao wao si sehemu yao.—Luka 17:5; Flp. 1:9, 10.

Sikuzote Yehova ameongoza watu wake wapate uelewevu mzuri zaidi wa mapenzi yake. (Zab. 43:3) Kielezi kifuatacho chaweza kuonyesha jinsi ambavyo amewaongoza: Ikiwa mtu amekuwa katika chumba chenye giza kwa muda mrefu, je, haifai zaidi ikiwa anafunuliwa mwangaza hatua kwa hatua? Yehova amefunulia watu wake nuru ya kweli katika njia hiyohiyo; amewaelimisha kwa kuendelea. (Linganisha Yohana 16:12, 13.) Imekuwa kama vile mithali isemavyo: “Bali njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—Mit. 4:18.

Mishughuliko ya Yehova pamoja na watumishi wake waliochaguliwa katika nyakati za Biblia inathibitisha kwamba uelewevu wa wazi wa mapenzi na makusudi yake mara nyingi huja hatua kwa hatua. Hivyo, Abrahamu hakuelewa kikamili jinsi kusudi la Yehova kuhusu ile “mbegu” lingefanikiwa. (Mwa. 12:1-3, 7; 15:2-4; linganisha Waebrania 11:8, NW.) Danieli hakuelewa tokeo la mwisho la unabii mbalimbali uliorekodiwa. (Dan. 12:8, 9) Yesu alipokuwa duniani, alikiri kwamba hakujua siku wala saa ambayo mfumo wa mambo wa sasa ungekwisha. (Mt. 24:36) Mitume hawakuelewa mwanzoni kwamba Ufalme wa Yesu ungekuwa wa kimbingu, kwamba haungesimamishwa katika karne ya kwanza, na kwamba hata Mataifa wangeurithi.—Luka 19:11; Mdo. 1:6, 7; 10:9-16, 34, 35; 2 Tim. 4:18; Ufu. 5:9, 10.

Hatupaswi kushangaa kwamba katika nyakati za kisasa pia, mara nyingi Yehova ameongoza watu wake wakiwa tengenezo linaloendelea, akiwaelimisha kweli za Biblia hatua kwa hatua. Kweli zenyewe hazibadiliki. Kweli hubaki kuwa kweli. Mapenzi na makusudi ya Yehova, kama yalivyoonyeshwa katika Biblia, hubaki vilevile. (Isa. 46:10) Lakini uelewevu wao wa kweli hizo huzidi kueleweka wazi zaidi “kwa wakati ufaao,” wakati wa Yehova uliowekwa. (Mt. 24:45, NW; linganisha Danieli 12:4, 9.) Nyakati nyingine, kwa sababu ya makosa ya kibinadamu au bidii iliyoongozwa vibaya, huenda maoni yao yakahitaji kurekebishwa.

Kwa kielelezo, katika nyakati mbalimbali katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova, bidii yao na idili kwa ajili ya kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova imeongoza kwenye matazamio yasiyo ya wakati barabara kuhusu ni lini ambapo mwisho wa mfumo huu mwovu wa Shetani ungekoma. (Eze. 38:21-23) Lakini Yehova hajafunua kimbele wakati barabara. (Mdo. 1:7) Kwa hiyo, watu wa Yehova wamelazimika kurekebisha maoni yao katika jambo hilo.

Marekebisho hayo katika maoni hayamaanishi kwamba kusudi la Mungu limebadilika. Wala hayadokezi kwamba mwisho wa mfumo huu uko mbali. Kinyume cha hayo, kutimizwa kwa unabii wa Biblia kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo” wathibitisha ukaribu wa mwisho huo. (Mt. 24:3, NW) Basi, je, uhakika wa kwamba Mashahidi wa Yehova wamekuwa na matazamio yasiyo ya wakati barabara unamaanisha kwamba wao hawaongozwi na Mungu? Sivyo, kama vile ambavyo lile swali la wale wanafunzi kuhusu kukaribia kwa Ufalme katika siku zao halikumaanisha kwamba wao hawakuchaguliwa na kuongozwa na Mungu!—Mdo. 1:6; linganisha Matendo 2:47; 6:7.

Kwa nini Mashahidi wa Yehova wana uhakika sana kwamba wana dini ya kweli? Ni kwa sababu wanaamini na kukubali yale ambayo Biblia husema kuhusu alama zenye kutambulisha waabudu wa kweli. Historia yao ya kisasa, kama ilivyozungumzwa katika sura za mapema za kichapo hiki, yaonyesha kwamba wao hutimiza matakwa hayo, si wakiwa watu mmoja-mmoja tu, bali wakiwa tengenezo: Wao hutetea Biblia kwa uaminifu-mshikamanifu kuwa Neno takatifu la Mungu la kweli (Yn. 17:17); wao hujitenga kabisa na mambo ya ulimwengu (Yak. 1:27; 4:4); wao hutoa ushahidi wa jina la kimungu, Yehova, na hupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu (Mt. 6:9; 24:14; Yn. 17:26); na wao hupendana kikweli.—Yn. 13:34, 35.

Kwa nini upendo ni alama yenye kutokeza ya kutambulisha waabudu wa Mungu wa kweli? Ni upendo wa aina gani unaotambulisha Wakristo wa kweli?

[Maelezo ya Chini]

a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 705]

Wakiisha chaguliwa na Mungu, lilikuwa jambo la maana kwamba wabaki wakiwa watiifu kwa sheria zake

[Blabu katika ukurasa wa 706]

Waabudu wa kweli wanaoishi katika wakati wa mwisho wangetambuliwaje?

[Blabu katika ukurasa wa 707]

“Hakufanya dai lolote la kupata ufunuo wa pekee kutoka kwa Mungu”

[Blabu katika ukurasa wa 708]

Wao huacha Biblia ijifasiri yenyewe

[Blabu katika ukurasa wa 709]

Yehova ameongoza watu wake wakiwa tengenezo linaloendelea, akiwaelimisha kweli za Biblia hatua kwa hatua

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki