Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ed kur. 4-9
  • Jinsi Mashahidi wa Yehova Huona Elimu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Mashahidi wa Yehova Huona Elimu
  • Mashahidi wa Yehova na Elimu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Namna Gani Elimu ya Ziada?
  • Taratibu ya Masomo
  • Elimu—Itumie Kumsifu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Elimu Katika Nyakati za Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Elimu?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
  • Je, Biblia Inapinga Elimu?
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova na Elimu
ed kur. 4-9
Picha katika ukurasa wa 4

Jinsi Mashahidi wa Yehova Huona Elimu

Kama vile wazazi wote, Mashahidi wa Yehova wanahangaikia wakati ujao wa watoto wao. Kwa hiyo wao huiona elimu kuwa ya maana sana. “Elimu yapaswa kusaidia watu wawe washiriki wa jamii wenye mafaa. Yapaswa pia kuwasaidia wasitawishe ufahamu wa urithi wao wa kitamaduni na kuishi maisha yenye kuridhisha zaidi.”

KAMA vile nukuu hili kutoka katika The World Book Encyclopedia lidokezavyo, mojapo makusudi makuu ya elimu ni kuzoeza watoto kwa ajili ya maisha ya kila siku, ambalo latia ndani kuwawezesha kutunza mahitaji ya familia siku moja. Mashahidi wa Yehova huamini kwamba hili ni daraka takatifu. Biblia yenyewe husema hivi: “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Timotheo 5:8) Miaka inayotumiwa shuleni hutayarisha watoto kwa ajili ya madaraka watakayopata maishani. Kwa hiyo, Mashahidi huhisi kwamba elimu yapasa kuchukuliwa kwa uzito sana.

“Elimu yapaswa kusaidia watu wawe washiriki wa jamii wenye mafaa. Yapaswa pia kuwasaidia wasitawishe ufahamu wa urithi wao wa kitamaduni na kuishi maisha yenye kuridhisha zaidi.” —The World Book Encyclopedia

Mashahidi hujitahidi kuishi kulingana na amri hii ya Biblia: “Lolote mfanyalo, mlifanye kwa moyo wenu wote, kana kwamba mwamfanyia Bwana na si wanadamu.” (Wakolosai 3:23, Today’s English Version) Kanuni hiyo yatumika kuhusu sehemu zote za maisha ya kila siku, kutia ndani shule. Hivyo Mashahidi hutia moyo vijana wao wasome kwa bidii na kuchukua kwa uzito kazi wanazogawiwa shuleni.

“Lolote mfanyalo, mlifanye kwa moyo wenu wote, kana kwamba mwamfanyia Bwana.”—Wakolosai 3:23, Today’s English Version

Biblia hufundisha pia kutii sheria za nchi ambako mtu aishi. Kwa hiyo elimu inapokuwa ya lazima hadi umri fulani, Mashahidi wa Yehova hutii sheria hiyo.—Warumi 13:1-7.

Picha katika ukurasa wa 6-7

Starehe ifaayo, muziki, mambo ya kujifurahisha, mazoezi ya kimwili, na kuzuru maktaba na nyumba za kuhifadhi mambo ya kale yote ni sehemu ya maana katika elimu yenye usawaziko

Bila kupunguza umaana wa mazoezi kwa ajili ya maisha ya kila siku, Biblia huonyesha kwamba hili si lengo pekee wala lengo kuu la elimu. Elimu yenye mafanikio yapasa pia ikuze ndani ya watoto shangwe ya kuishi, na kuwasaidia wachukue mahali pao katika jamii wakiwa watu mmoja-mmoja wenye usawaziko mzuri. Hivyo, Mashahidi wa Yehova huhisi kwamba chaguo la utendaji wa ziada baada ya masomo ya darasani ni la maana sana. Wao huamini kwamba starehe ifaayo, muziki, mambo ya kujifurahisha, mazoezi ya kimwili, kuzuru maktaba na nyumba za kuhifadhi mambo ya kale, na kadhalika, ni sehemu ya maana katika elimu yenye usawaziko. Kwa kuongezea, wao hufundisha watoto wao wastahi watu wenye umri mkubwa na kutafuta fursa za kuwasaidia.

Namna Gani Elimu ya Ziada?

Kwa sababu ya tekinolojia mpya, fursa za kupata kazi zinabadilika daima. Likiwa tokeo, vijana wengi watalazimika kufanya kazi katika sehemu au katika ufundi mbalimbali ambao hawajapata mazoezi hususa juu yao. Hali ikiwa ni hivyo, tabia zao za kufanya kazi na mazoezi yao ya kibinafsi, na hasa uwezo wao wa kubadilikana na hali, utakuwa wenye thamani zaidi kwao. Kwa hiyo, kama ilivyoelezwa na Montaigne, aliyekuwa mwandikaji-insha wa nyakati za Mfufuo wa Harakati, ni bora zaidi kwa wanafunzi kuwa watu wazima wenye ‘vichwa vilivyofundishwa jinsi ya kutumia ujuzi kuliko kuwa wenye vichwa vilivyojaa ujuzi.’

Ukosefu wa kazi za kuajiriwa, unaoathiri nchi zenye utajiri na pia zilizo maskini, mara nyingi hutisha vijana ambao hawana mazoezi ya kutosha. Kwa hiyo, ikiwa fursa za kupata kazi zahitaji mtu awe na mazoezi yanayozidi yale ya msingi yanayotakiwa na sheria, ni daraka la wazazi kuongoza watoto wao katika kufanya uamuzi juu ya elimu ya ziada, wakipima manufaa zinazoweza kupatikana na pia dhabihu ambazo masomo hayo ya ziada yaweza kuhusisha.

Hata hivyo, yaelekea utakubali kwamba mafanikio maishani hutia ndani mengi zaidi ya ufanisi wa kimwili tu. Katika nyakati za karibuni wanaume na wanawake waliotumia maisha zao zote katika kazi-maisha zao walipoteza kusudi lao la kuishi walipopoteza kazi zao. Wazazi fulani wamedhabihu maisha yao ya familia na wakati ambao wangaliweza kutumia pamoja na watoto wao, wakikosa fursa ya kuwasaidia wafikie hali ya kuwa watu wazima, kwa sababu walitumia wakati wote kazini.

Kwa wazi, elimu yenye usawaziko yapasa izingatie kwamba mengi zaidi kuliko ufanisi wa kimwili yanahitajiwa ili kutufurahisha kikweli. Yesu Kristo alisema hivi: “Imeandikwa: ‘Mwanadamu haishi kwa mkate pekee, bali kwa kila neno litokalo kinywani mwa Mungu.’” (Mathayo 4:4, New International Version) Wakiwa Wakristo, Mashahidi wa Yehova huthamini umaana wa kusitawisha sifa za kiadili na za kiroho na pia kujitayarisha ili kutunza mahitaji yao ya kimwili.

Elimu Katika Nyakati za Biblia

BIBLIA hufundisha kwamba elimu ni yenye umaana sana. Hiyo humwonyesha Mungu kuwa “Mfunzi Mtukufu” wa watu wake, na katika kurasa zayo zote huwaalika watumishi wake waongeze ujuzi wao kumhusu yeye.—Isaya 30:20, New World Translation.

Picha katika ukurasa wa 8-9

Katika nyakati za Biblia, ni jamii fulani tu zenye kupendelewa zilizojua kusoma na kuandika, kama vile waandishi katika Mesopotamia na Misri. Tofauti kabisa na hilo, kila mtu katika Israeli la kale alitiwa moyo kujifunza kusoma na kuandika. “Bila shaka tofauti hiyo ilikuwako kwa sababu ya ule mfumo wa kialfabeti wa kuandika ulio sahili zaidi uliotumiwa na Waebrania. . . . Ni lazima umaana wa kuandika kialfabeti katika historia ya elimu usipuuzwe. Kulisababisha mwondoko kutoka tamaduni za waandishi za kimapokeo za Misri, Mesopotamia, na Kanaani ya mileani ya pili. Kujua kusoma na kuandika hakukuwa tena sifa yenye kutambulisha na ya pekee ya jamii ya waandishi na makuhani wa kitaalamu, wenye ujuzi wa yale maandishi-kabari na maandishi-michoro yaliyo magumu kuelewa.”—Encyclopaedia Judaica.

Njia za Kufundisha

Picha katika ukurasa wa 9

Katika Israeli la kale, watoto walifundishwa na baba na mama kutoka umri wa mapema sana. (Kumbukumbu la Torati 11:18, 19; Mithali 1:8; 31:26) Katika Dictionnaire de la Bible, msomi wa Biblia E. Mangenot aliandika hivi: “Mara tu alipoweza kusema, mtoto alijifunza vifungu vichache vya maneno kutoka Sheria. Mama yake angeurudia-rudia mstari; [mtoto] alipoujua; [mama] angempa mstari mwingine. Baadaye, maandishi ya mistari ambayo tayari wangeweza kukariri kutoka kumbukumbu yangetiwa mikononi mwa watoto. Hivyo, waliingizwa katika hatua ya kwanza ya kusoma, na walipokua wakawa wenye umri zaidi, wangeweza kuendelea na mafunzo yao ya kidini kwa kusoma na kutafakari juu ya sheria ya Bwana.”

Ili kusaidia vijana kwa wazee wakumbuke, misaada mbalimbali ya kukumbusha ilitumiwa. Hiyo ilitia ndani herufi ya kialfabeti (mistari yenye kufuatana katika shairi ikianza na herufi tofauti kwa kufuata utaratibu wa kialfabeti), mpangilio wa maneno yanayoanza na herufi au sauti ileile, na utumizi wa nambari. Kwa kupendeza, Kalenda ya Gezer (katika Jumba la Hifadhi la Akiolojia la Istanbul), ambayo ni kimojapo vielelezo vya zamani sana vya maandishi ya Kiebrania, hufikiriwa na baadhi ya wasomi kuwa zoezi la kumbukumbu la mvulana wa shule.

Taratibu ya Masomo

Elimu kutoka kwa wazazi katika nyakati za Biblia ilitia ndani mazoezi kwa vitendo. Wasichana walifundishwa stadi za kinyumbani. Sura ya kumalizia ya kitabu cha Mithali yaonyesha kwamba stadi hizo zilikuwa nyingi na za aina mbalimbali; zilitia ndani kushughulika na ununuzi wa mali na shamba na kufanya biashara ndogo-ndogo, na pia kusokota, kufuma, kupika, kufanya biashara na usimamizi wa ujumla wa nyumba. Kwa kawaida wavulana walifundishwa kazi za kimwili za baba yao, iwe ni katika kilimo au ufundi au stadi fulani. Kati ya wanadini Wayahudi, usemi ufuatao ulikuwa wa kawaida: “Yeye asiyemfundisha mwana wake ustadi ufaao anamlea awe mwivi.”

Ndivyo, elimu katika nyakati za Biblia ilivyostahiwa sana.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki