Elimu Katika Nyakati za Biblia
“Ni lazima pia myafundishe wana wenu.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 11:19, NW.
1. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anapendezwa na elimu ya watumishi wake?
YEHOVA ndiye Mwelimishaji Mkuu. Hakuwaacha kamwe watumishi wake katika hali ya kukosa maarifa. Sikuzote amekuwa na nia ya kushiriki maarifa pamoja nao. Yeye huwafundisha mapenzi yake na njia zake. Muda wa mileani nyingi zilizopita Mwana wake mzaliwa-pekee alikuwa kando yake, akijifunza daima akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu. (Mithali 8:30, NW) Alipokuwa duniani Yesu alitaarifu hivi: “Kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28) Akimrejezea Mungu kuwa Mwelimishaji Asiye na Kifani, Elihu aliuliza hivi: “Ni nani afundishaye kama yeye?” (Ayubu 36:22) Nabii Isaya alisema juu ya Yehova kuwa ndiye “Mfunzi Mtukufu” wa watu Wake na akatoa unabii huu: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA [Yehova, NW]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi. (Isaya 30:20, NW; 54:13) Bila shaka Yehova atamani viumbe vyake vyenye akili viwe vyenye maarifa na vyenye kuelimishwa vema.
Elimu ya Wazee wa Ukoo
2, 3. (a) Wazee wa ukoo waaminifu walionaje elimu ya watoto wao, na Yehova alimpa Abrahamu agizo gani? (b) Ni kusudi gani tukufu lililochochea lile agizo la kuelimisha wazao wa Abrahamu?
2 Mojawapo haki za msingi za kichwa cha familia katika nyakati za wazee wa ukoo ilikuwa kuwafundisha watoto wake na watu wa nyumba yake. Kwa watumishi wa Mungu elimu ya watoto wao ilikuwa wajibu wa kidini. Yehova alisema hivi kuhusu mtumishi wake Abrahamu: “Nimemjua ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya BWANA [Yehova, NW], wafanye haki na hukumu, ili kwamba BWANA [Yehova, NW] naye akamtimizie Ibrahimu [Abrahamu, NW] ahadi zake.”—Mwanzo 18:19.
3 Taarifa hiyo ya kimungu inaonyesha kwamba Yehova aliona elimu kuwa ya maana kubwa sana. Mungu alitaka Abrahamu, Isaka, na Yakobo waelimishe watu wa nyumba zao katika njia Zake zenye uadilifu na hukumu ili vizazi vya wakati ujao viweze kushika njia ya Yehova. Hivyo, Yehova angetimiza ahadi zake kuhusu mbegu ya Abrahamu na kubarikiwa kwa “mataifa yote ya dunia.”—Mwanzo 18:18; 22:17, 18.
Mfumo wa Kielimu Katika Israeli
4, 5. (a) Ni nini kilichoutofautisha mfumo wa Israeli wa kielimu na ule wa mataifa mengine? (b) Ni tofauti gani nyingine ya maana inayotajwa katika Encyclopaedia Judaica, na bila shaka ni nini kilichochangia tofauti hiyo?
4 Encyclopaedia Judaica hutaarifu hivi: “Biblia ndiyo chanzo hasa cha kupata uelewevu wa utaratibu wa elimu katika Israeli ya kale.” Yehova alimtumia Musa kuwa mwalimu wa kibinadamu wa kwanza wa Israeli. (Kumbukumbu la Torati 1:3, 5; 4:5) Musa alipitisha maneno aliyopewa na Yehova. (Kutoka 24:3) Kwa hiyo, kwa kweli, Mungu hasa ndiye aliyekuwa Mwelimishaji wa Israeli. Hilo lenyewe lilitofautisha mfumo wa kielimu wa Israeli na ule wa mataifa mengine.
5 Kitabu icho hicho cha marejezo hujulisha hivi: “Elimu ya juu zaidi au masomo ya vitabu katika Mesopotamia na Misri ilikuwa rasmi na ilipewa kwa jamii ya waandishi tu, jambo ambalo halionekani lilitukia katika Israeli. Bila shaka tofauti hiyo ilikuwako kwa sababu ya ule mfumo wa kuandika wa kialfabeti ulio sahili zaidi uliotumiwa na Waebrania. . . . Ni lazima umaana wa kuandika kialfabeti katika historia ya elimu usipuuzwe. Hilo lilisababisha mwondoko kutoka tamaduni za waandishi za kimapokeo za Misri, Mesopotamia, na Kanaani ya mileani ya pili. Kujua kusoma na kuandika hakukuwa tena sifa ya kutambulisha na haki ya jamii ya waandishi na makuhani wa kulipwa, waliofahamu sana yale maandishi-kabari na maandishi-michoro yaliyo magumu kuelewa.”
6. Kuna uthibitisho gani wa Kibiblia kwamba tangu mwanzo kabisa wa historia yao, Waisraeli walikuwa watu waliojua kusoma na kuandika?
6 Biblia huandaa uthibitisho wa kwamba Waisraeli walikuwa watu waliojua kusoma na kuandika. Kabla hata ya wao kuingia Bara Lililoahidiwa, waliambiwa waandike sheria za Yehova juu ya miimo ya nyumba zao na juu ya malango yao. (Kumbukumbu la Torati 6:1, 9; 11:20; 27:1-3) Ingawa bila shaka amri hiyo ilikuwa ya kitamathali, kwa hakika isingalikuwa na maana yoyote kwa Mwisraeli wa kawaida ikiwa hakujua jinsi ya kusoma na kuandika. Maandiko kama vile Yoshua 18:9 na Waamuzi 8:14 huonyesha kwamba wengine zaidi ya viongozi kama vile Musa na Yoshua walijua jinsi ya kuandika muda mrefu kabla ya umaliki kusimamishwa katika Israeli.—Kutoka 34:27; Yoshua 24:26.
Njia za Kufundisha
7. (a) Kulingana na Maandiko, ni nani waliowapa watoto Waisraeli elimu yao ya msingi? (b) Ni habari gani inayotolewa na mwanachuo wa Biblia Mfaransa?
7 Katika Israeli, watoto walifundishwa na baba na mama tangu umri wa mapema sana. (Kumbukumbu la Torati 11:18, 19; Mithali 1:8; 31:26) Katika Dictionnaire de la Bible ya Kifaransa, mwanachuo wa Biblia E. Mangenot aliandika hivi: “Mara alipoweza kusema, mtoto alijifunza vifungu vichache vya maneno kutoka kwa Sheria. Mama yake angeurudia-rudia mstari; [mtoto] alipoujua, [mama] angempa mstari mwingine. Baadaye, maandishi ya mistari ambayo tayari wangeweza kukariri kutoka kumbukumbu yangetiwa mikononi mwa watoto. Hivyo, waliingizwa katika hatua ya kwanza ya kusoma, na walipokua wenye umri mkubwa zaidi, wangeweza kuendelea na mafunzo yao ya kidini kwa kusoma na kutafakari juu ya sheria ya Bwana.”
8. (a) Ni njia gani ya kufundisha ya msingi iliyotumiwa katika Israeli, lakini ikiwa na sifa gani ya maana? (b) Ni misaada gani ya kukumbusha iliyotumiwa?
8 Hilo ladokeza kwamba njia ya kufundisha ya msingi iliyotumiwa ilikuwa kujifunza mambo kwa kuyatia moyoni. Mambo waliyojifunza kuhusu sheria za Yehova na kushughulika kwake na watu wake yalipaswa yapenye ndani ya moyo. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Yalipaswa kutafakariwa. (Zaburi 77:11, 12) Ili kuwasaidia vijana na wazee pia wayatie katika kumbukumbu, misaada mbalimbali ya kukumbusha ilitumiwa. Hiyo ilitia ndani herufi ya kialfabeti, kila sentensi katika andiko ikianza na herufi tofauti, kwa kufuata utaratibu wa kialfabeti (kama vile Mithali 31:10-31); mpangilio wa maneno yanayoanza na herufi au sauti ileile; na utumizi wa nambari, kama zile zinazotumiwa katika nusu ya pili ya Mithali sura 30. Kwa kupendeza, Kalenda ya Gezer, kimojawapo vielelezo vya zamani sana cha maandishi ya Kiebrania, hufikiriwa na baadhi ya wanachuo kuwa zoezi la kumbukumbu ya mvulana wa shule.
Taratibu ya Masomo
9. (a) Ni nini iliyokuwa sehemu fulani ya maana ya programu ya masomo kwa watoto Waisraeli? (b) Ensaiklopedia fulani ya Biblia hutaarifu nini juu ya kufundisha kulikofanywa kuhusiana na sikukuu za kila mwaka?
9 Elimu katika Israeli haikuhusisha tu kujifunza kusoma na kuandika. Somo moja la maana ambalo lilifundishwa lilikuwa ni historia. Kujifunza juu ya matendo ya Yehova ya ajabu kwa ajili ya watu wake kulikuwa sehemu ya msingi ya taratibu ya masomo. Kizazi baada ya kizazi kilipaswa kifundishwe habari hizo za hakika za historia. (Kumbukumbu la Torati 4:9, 10; Zaburi 78:1-7) Kuadhimisha sikukuu za kila mwaka kulimwandalia kichwa cha familia nafasi nzuri ya kuwafundisha watoto wake. (Kutoka 13:14; Mambo ya Walawi 23:37-43) Kwa habari hiyo The International Standard Bible Encyclopedia hutaarifu hivi: “Kupitia maagizo ya baba nyumbani na maelezo yake ya umaana wa sikukuu, watoto Waebrania walifundishwa jinsi Mungu alivyokuwa amejidhihirisha Mwenyewe kwao wakati uliopita, jinsi walivyopaswa kuishi wakati huu, na ahadi za Mungu zilikuwa ni nini kwa habari ya wakati ujao wa watu Wake.”
10. Ni mazoezi gani yenye kutumika waliopewa wasichana? wavulana?
10 Elimu kutoka kwa wazazi ilitia ndani mazoezi yenye kutumika. Wasichana walifundishwa stadi za kinyumbani. Sura ya kumalizia ya Mithali huonyesha kwamba stadi hizo zilikuwa nyingi na za aina mbalimbali; zilitia ndani kusokota, kufuma, kupika, kufanya biashara, na usimamizi wa ujumla wa nyumba. Kwa kawaida wavulana walifundisha kazi ya kimwili ya baba yao, iwe katika kilimo au ufundi au stadi fulani. Katika nyakati za baadaye marabi Wayahudi walizoea kusema: “Yeye ambaye hamfundishi mwana wake ustadi ufaao anamlea awe mwivi.”
11. Ni nini kinachoonyesha kusudi hasa la elimu katika Israeli, na hilo lina somo gani kwa wachanga leo?
11 Kina cha kiroho cha njia za kufundishia zilizotumiwa katika Israeli huonekana wazi kotekote katika kitabu cha Mithali. Kitabu hicho huonyesha kwamba kusudi lilikuwa kuwafundisha “wajinga” mambo bora kama vile hekima, nidhamu, uelewevu, mwono-ndani, hukumu, werevu, maarifa, na uwezo wa kufikiri—yote hayo katika “kumcha BWANA [Yehova, NW].” (Mithali 1:1-7; 2:1-14) Hilo lakazia vichocheo vinavyopaswa kumsukuma mmoja wa watumishi wa Mungu leo afanyie maendeleo elimu yake.
Makuhani, Walawi, na Manabii
12. Ni nani zaidi ya wazazi walioshiriki katika kuwaelimisha watu wa Israeli, na ni nini maana ya msingi ya neno la Kiebrania linalotafsiriwa “sheria”?
12 Ingawa elimu ya msingi iliandaliwa na wazazi, kuongezea hiyo Yehova aliwaelimisha watu wake kupitia makuhani, Walawi wasiokuwa makuhani, na manabii. Katika baraka yake ya mwisho juu ya kabila la Lawi, Musa alitaarifu hivi: “Watamfundisha Yakobo hukumu zako, na Israeli torati [sheria, NW] yako.” (Kumbukumbu la Torati 33:8, 10) Jambo la maana ni kwamba, neno “sheria” katika Kiebrania (toh·rahʹ) linatokana na neno la msingi ambalo namna yalo ya kitenzi humaanisha “kuonyesha,” “kufundisha,” “kuagiza.” Encyclopaedia Judaica hutaarifu hivi: “Kwa hiyo maana ya neno [torah] ni ‘fundisho,’ ‘kanuni,’ au ‘agizo.’”
13. Kwa nini sheria ya Israeli ilitofautiana na mifumo ya kisheria ya mataifa mengine?
13 Hilo pia lilitenganisha Israeli na mataifa mengine na hata na mataifa ya ki-siku-hizi. Mataifa ya kisiasa leo yana fungu la sheria ambalo raia kwa ujumla hujua sehemu ndogo tu, watu wanapoihalifu sheria, wanalazimika kulipa mawakili pesa nyingi ili wawatetee. Shule za sheria ni za wastadi. Hata hivyo katika Israeli Sheria ilikuwa njia ya Mungu ya kuwaambia watu wake jinsi alivyowataka wamwabudu na kuishi kulingana na mapenzi yake. Tofauti na mipangilio ya kisheria mingine, hiyo ilitia ndani upendo kwa Mungu na jirani. (Mambo ya Walawi 19:18; Kumbukumbu la Torati 6:5) Sheria ilikuwa tofauti sana na kuwa kitabu cha sheria kisichojali hisia za watu. Iliandaa kanuni, fundisho, na agizo katika njia fulani ya maisha waliyopaswa wajifunze.
14. Ni sababu gani moja iliyomfanya Yehova akatalie mbali ukuhani wa Kilawi? (Malaki 2:7, 8)
14 Walipokuwa waaminifu, makuhani na Walawi walitimiza daraka lao la kulifundisha taifa. Lakini mara nyingi sana, makuhani walipuuza wajibu wao wa kuwaelimisha watu. Ukosefu huo wa kuelimishwa katika Sheria ya Mungu ungekuwa na matokeo yenye misiba kwa makuhani na watu pia. Katika karne ya nane K.W.K., Yehova alitoa unabii hivi: “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako.”—Hosea 4:6.
15. (a) Kuongezea makuhani, Yehova aliwainua nani kuwa walimu katika Israeli, na mwanachuo fulani wa Biblia aliandika nini kuhusu daraka lao wakiwa waelimishaji? (b) Ni nini kilichotukia baadaye kwa Israeli na Yuda kwa sababu walikataa maarifa ya Yehova na njia zake?
15 Pamoja na makuhani, Yehova aliwainua manabii wakawe waelimishaji. Twasoma hivi: “BWANA [Yehova, NW] aliwashuhudia Israeli, na Yuda, kwa kinywa cha kila nabiii, na cha kila mwonaji, akisema, Geukeni, na kuziacha njia zenu mbaya, mkazishike amri zangu na hukumu zangu, sawasawa na ile sheria yote niliyowaamuru baba zenu, nikawapelekea kwa kinywa cha manabii watumishi wangu.” (2 Wafalme 17:13) Kwa habari ya daraka la manabii wakiwa waelimishaji, Roland de Vaux mwanachuo wa Biblia Mfaransa, aliandika hivi: “Manabii pia, walikuwa na utume wa kuwaagiza watu; hiyo ilikuwa sehemu ya kazi yao kadiri ileile kama kutabiri juu ya wakati ujao. Na unabii wenye kupuliziwa roho ulikupa kuhubiri kwao mamlaka ya neno la Mungu. Ni jambo la hakika kwamba chini ya umaliki manabii walikuwa ndio walimu wa kufundisha watu mambo ya kidini na ya kiadili; na, twaweza kuongeza kwamba, walikuwa walimu walio bora kati ya [walimu] wao wote, kama si wenye kutiiwa zaidi sikuzote.” Kwa sababu ya kutopewa elimu ifaayo na makuhani na Walawi pamoja na kukosa kutii manabii wa Yehova, Waisraeli waliziacha njia za Yehova. Samaria lilishambuliwa na Waashuri katika 740 K.W.K., na Yerusalemu na hekalu lalo vikaharibiwa na Wababuloni katika 607 K.W.K.
Elimu Wakati wa Utekwa na Baadaye
16, 17. (a) Ni programu gani ya kielimu iliyolazimishwa juu ya Danieli na wenzake watatu? (b) Ni nini kilichowawezesha wapokee elimu hiyo ya Kibabuloni na bado wabaki waaminifu kwa Yehova?
16 Miaka kumi hivi kabla ya uharibifu wa Yerusalemu, Mfalme Yehoyakini na jamii ya wanawafalme na wakuu walipelekwa mpaka Babuloni na Mfalme Nebukadreza. (2 Wafalme 24:15) Danieli na wakuu wengine wachanga watatu walikuwa miongoni mwao. (Danieli 1:3, 6) Nebukadreza aliamuru hao wanne wapokee mtaala wa mazoezi ya pekee ya muda wa miaka mitatu ili ‘wafundishwe elimu ya Wakaldayo, na lugha yao.’ Na zaidi, waliandaliwa “posho ya chakula cha mfalme, na ya divai aliyokunywa.” (Danieli 1:4, 5) Huo ulikuwa na uwezekano wa kuleta hatari kwa sababu kadhaa. Yaelekea, taratibu hiyo ya masomo haikuwa tu mtaala wa lugha wa muda wa miaka mitatu. Usemi “Wakaldayo” katika kifungu hicho cha maneno wafikiriwa na wengine kuwa wamaanisha, “si Wababuloni wakiwa jamii ya watu, bali ile jamii ya wenye elimu.” (The Soncino Books of the Bible) Katika ufafanuzi wake juu ya Danieli, C. F. Keil hutaarifu hivi: “Danieli na wenzake walitakiwa waelimishwe katika hekima ya makuhani na watu wenye elimu Wakaldayo, iliyofundishwa katika shule za Babuloni.” Posho ya chakula cha kifalme iliwaweka katika hatari ya kuvunja vizuizi vya vyakula vilivyowekwa na Sheria ya Musa. Walikabilianaje?
17 Akiwa msemaji wa wale wakuu wachanga Wayahudi wanne, Danieli alielewesha wazi tangu mwanzoni kwamba hawangekula au kunywa katika kuchafua dhamiri zao. (Danieli 1:8, 11-13) Yehova alibariki msimamo huo thabiti na akaulainisha moyo wa ofisa Mbabuloni aliyekuwa msimamizi. (Danieli 1:9, 14-16) Kwa habari ya masomo yao, matukio ya baadaye katika maisha ya hao Waebrania wachanga wote wanne huthibitisha pasipo shaka kwamba taratibu yao ya masomo ya kulazimishwa ya muda wa miaka mitatu katika utamaduni wa Kibabuloni haikuwafanya wakengeushwe kutoka kwa ushikamano wao wenye kina kwa Yehova na kwa ibada yake safi. (Danieli, sura 3 na 6) Yehova aliwawezesha watoke katika ule uzamisho wa lazima katika usomi wa juu wa Kibabuloni bila kuathiriwa nao. “Basi, kwa habari za hao vijana wanne, Mungu aliwapa maarifa na ujuzi katika elimu na hekima; Danieli naye alikuwa na ufahamu katika maono yote, na ndoto. Na katika kila jambo la hekima na ufahamu alilowauliza mfalme, akawaona kuwa walifaa mara kumi zaidi ya waganga na wachawi waliokuwa katika ufalme wake.”—Danieli 1:17, 20.
18. Ni programu gani ya kielimu iliyofanywa katika Yuda baada ya utekwa wa Kibabuloni?
18 Baada ya utekwa wa Kibabuloni, kazi kubwa ya elimu ilifanywa na Ezra, kuhani ambaye “alikuwa ameuelekeza moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA [Yehova, NW], na kuitenda, na kufundisha maagizo na hukumu katika Israeli.” (Ezra 7:10) Katika hilo alisaidiwa na Walawi waaminifu, waliokuwa ‘wakiwafahamisha watu torati.’ (Nehemia 8:7) Ezra alikuwa mwanachuo wa Biblia na “mnakiliji stadi,” au mwandishi. (Ezra 7:6) Ni katika siku yake kwamba waandishi walipata kuwa na umashuhuri wakiwa jamii.
Shule za Kirabi
19. Ni kikundi gani cha waelimishaji kilichokuwa kimetokea katika Israeli kufikia wakati Yesu alipokuja duniani, na yeye na wanafunzi wake hawakupokea elimu ya Kiyahudi ya juu zaidi kwa sababu zipi za maana?
19 Kufikia wakati Yesu alipotokea duniani, waandishi walikuwa wamekuwa jamii ya walimu wateule wachache, iliyoshikamana zaidi na mapokeo kuliko na mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu. Walipenda kuitwa “Rabi,” neno lililokuwa limekuwa kichwa cha cheo chenye heshima kinachomaanisha “Mkuu (Mwadhamu) Wangu.” (Mathayo 23:6, 7, NW, kielezi-chini) Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, mara nyingi waandishi wanashirikishwa na Mafarisayo, baadhi yao ambao wenyewe walikuwa walimu wa Sheria. (Matendo 5:34) Yesu alishtaki vikundi hivyo viwili juu ya kubatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yao na kufundisha “mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” (Mathayo 15:1, 6, 9) Haishangazi kwamba wala Yesu wala wengi wa wanafunzi wake hawakuelimishwa katika shule za kirabi.—Yohana 7:14, 15; Matendo 4:13; 22:3.
20. Pitio hilo la elimu katika nyakati za Biblia limetuonyesha nini, na ni nini kinachoonyesha kwamba watumishi wa Yehova wanahitaji elimu?
20 Mambo ambayo yamepitiwa kuhusu elimu katika nyakati za Biblia yameonyesha kwamba Yehova ni Mfunzi Mtukufu wa watu wake. Kupitia Musa, Mungu alipanga kitengenezo mfumo wa elimu wenye mafanikio katika Israeli. Lakini baada ya wakati mrefu, mfumo wa Kiyahudi wa elimu ya juu ulisitawi ambao ulifundisha mambo yaliyo kinyume cha Neno la Mungu. Ingawa Yesu hakuhudhuria shule hizo za Kiyahudi, yeye, hata hivyo, alikuwa Mwalimu asiye na kifani. (Mathayo 7:28, 29; 23:8; Yohana 13:13) Yeye pia aliwapa wanafunzi wake utume wa kufundisha, hata umalizio wa mfumo wa mambo. (Mathayo 28:19, 20) Ili kufanya hivyo, wangepaswa kuwa walimu wazuri na kwa hiyo wangehitaji elimu. Kwa hiyo Wakristo wa kweli wanapaswa waoneje elimu leo? Swali hilo litachunguzwa katika makala ifuatayo.
Mtihani wa Kumbukumbu
◻ Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anapendezwa na elimu ya watumishi wake?
◻ Mfumo wa kielimu wa Israeli ulitofautiana na ule wa mataifa mengine kwa habari gani?
◻ Watoto Waisraeli walipokea elimu gani?
◻ Ni njia zipi za kufundisha zilizotumiwa katika Israeli?
◻ Kwa nini Yesu na wanafunzi wake hawakwenda kwenye shule za Kiyahudi ya usomi wa juu?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Elimu ya lazima katika Babuloni haikugeuzia mbali Danieli na wenzake kutoka kwa Yehova