Mashahidi wa Yehova Ni Akina Nani?
Wewe unajua nini kuhusu Mashahidi wa Yehova? Watu fulani huwaita Wakristo wenye propaganda, dhehebu jipya la Wakristo, farakano la Kikristo lililotokana na dini ya Kiyahudi, au wazushi ambao hukataa matibabu. Kwa kweli, Mashahidi si watu wa aina hiyo. Kwa nini watu fulani huwaona hivyo? Mara nyingi ni kwa sababu watu hao wameambiwa mambo yasiyo ya kweli.
Kama jina lao linavyoonyesha, Mashahidi wa Yehova wanatoa ushahidi kwa ajili ya Yehova. Yehova ni nani? Yehova ni jina ambalo Mungu Mweza-Yote amejipatia katika Biblia.a Ni jina lake mwenyewe, wala si cheo kama vile Mungu au Bwana. Kwa ujumla, tangu zamani, mtu yeyote ambaye hutoa ushahidi kuhusu utukufu wa Mungu anaweza kuitwa shahidi wa Yehova.—Kutoka 3:13, 15; Isaya 43:10.
Kwa hiyo, Biblia, inapoorodhesha watu wa kale waliokuwa waaminifu kuanzia Abeli, huwaita ‘wingu kubwa la mashahidi.’ (Waebrania 11:4; 12:1) Watu maarufu, kama vile Noa, Abrahamu, Isaka, Yakobo, Yosefu, Musa, na Daudi, wanatajwa kuwa mashahidi wa Mungu—mashahidi wa Yehova. Yesu Kristo anaitwa “shahidi mwaminifu na wa kweli.”—Ufunuo 3:14.
Kwa Nini Mashahidi Wanahitajiwa?
Biblia husema kwamba mwanadamu aliumbwa akiwa mkamilifu na kuwekwa katika paradiso. Muumba alimpa uwezo wa kuishi milele, kuzaa watoto, na kueneza makao yake ya Paradiso ulimwenguni pote. Wakati huo mwanadamu alimjua Mungu wake, na hakukuwa na uhitaji wowote wa mashahidi.—Mwanzo 1:27, 28.
Mungu alimpa mwanadamu uhuru wa kuchagua, lakini wazazi wetu wa kwanza walifanya uamuzi mbaya. Waliamua kujitegemea wenyewe. Kwa hiyo, huku Mungu akiendelea kuwa mkamilifu, mwenye haki, na mtakatifu, wanadamu duniani ni wenye dhambi na si waadilifu. Hata hivyo, Mungu wetu mtakatifu ataruhusu dhambi na uovu ziendelee kwa muda mfupi tu. Biblia huonyesha kwamba tunakaribia mwisho wa kipindi hicho kilichoruhusiwa na Mungu. Ili wanadamu wajue mambo hayo, Mungu amehifadhi Neno Lake—Taurati, Zaburi, na Injili—mpaka leo hii.
Kwa kuwa wanadamu wengi hawamjui Mungu, amewaamuru wanadamu waaminifu watoe ushahidi juu yake. Anawaambia hivi mashahidi hao waaminifu: “Ninyi ni mashahidi wangu.” (Isaya 43:10) Kuhusu kazi wanayotimiza, anasema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
Leo, watu wengi zaidi, kutoka katika jamii, lugha, na mataifa yote, wanalichunguza Neno la Mungu kwa unyoofu. Wameona kwamba desturi nyingi za dini ni za kikafiri na humchukiza Mungu.
Huenda unajua kwamba watu fulani wameitumia dini kwa makusudi ya kibiashara. Wengine wameitumia kuendeleza siasa zao au kutajirika huku wengine wakizidi kuwa maskini. Unafikiri watu hao ambao hufaidika na dini hutendaje wakati ambapo ushahidi wa kweli unatolewa kumhusu Mungu? Bila shaka, watajikuta matatani. Hiyo ni mojawapo ya sababu ambazo huwafanya watu fulani waseme vibaya kuhusu Mashahidi wa Yehova.
Vyovyote vile, Mashahidi wa Yehova hushikamana sana na Biblia. Hawakubuni dini mpya. Wao hufuata tu yaliyoandikwa katika Taurati, Zaburi, na Injili, ambazo ndio msingi wa dini ya kweli. Kwa hiyo, basi, wao huamini nini? Baadhi ya mafundisho yao yameorodheshwa hapa. Soma uone ikiwa ni ya kweli au sivyo.
Mungu Si Utatu
Biblia haifundishi Utatu. Badala yake, hiyo husema kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli na anayeishi milele. “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” (Kumbukumbu la Torati 6:4) Yeye ndiye Muumba—wa milele, mweza-yote, asiye na mwingine anayetoshana naye. Yesu si Mungu Mweza-Yote. Yesu aliishi duniani akiwa mwanadamu mkamilifu na kufa kwa ajili ya wanadamu wasio wakamilifu. Mungu alikubali uhai wa Yesu uwe fidia, na kwa hiyo waaminifu huokolewa kupitia kwake. Hayo ndiyo mapenzi ya Mungu.—Luka 22:42; Waroma 5:12.
Nafsi Inaweza Kufa
Ni nini huwapata watu wanapokufa? Neno la Mungu husema hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Mwanadamu hana nafsi ambayo haifi. Watu ambao hufikiri kwamba wanazungumza na wafu kwa kweli wanawasiliana na roho waovu. Vivyo hivyo, sala zinazotolewa kwa ajili ya wafu hazimfaidi yeyote isipokuwa makasisi ambao hulipwa watoe sala hizo.
Ufufuo
Tumaini halisi la mwanadamu ni ufufuo, kurudi kwa wafu katika dunia iliyofanywa kuwa Paradiso tena. Wale ambao wamemtumikia Mungu watabarikiwa kwa sababu ya uaminifu wao. Wale ambao wamekufa kabla ya kumjua Mungu watapata nafasi ya kufanya hivyo wakati huo. Kwa hiyo, “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Wale tu ambao Mungu atawahukumu kuwa hawastahili ndio ambao hawatafufuliwa.
Hakuna Moto wa Mateso
Mungu mwenye upendo hawezi kuumba mahali ambapo wafu huteseka milele. Kuhusu kuteketezwa na kuteswa kwa wanadamu, Mungu mwenyewe alisema kwamba ni “jambo ambalo sikuamuru wala halikuingia moyoni mwangu.”—Yeremia 7:31.
Majaliwa
Mungu hawaandikii watu mambo yatakayowapata. Hakuna majaliwa ambayo huamua jinsi hali yetu ya wakati ujao itakavyokuwa kabla hatujazaliwa. Tunawajibika kwa yale tunayotenda, kwa maamuzi tunayofanya. “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:12.
Hakuna Vyeo vya Makasisi
Watu wote waliojiweka wakfu kwa Mungu wanatoshana machoni Pake. Waabudu wote wa kweli ni ndugu na dada. Mungu hakuweka makasisi wenye vyeo. Yesu alisema: “Kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, bali yule anayejinyenyekeza atainuliwa.” (Luka 18:14) Mungu atawahukumu vikali wale ambao hutumia dini kujiinua juu ya wengine.—Mathayo 23:4-12.
Hakuna Ibada ya Sanamu
“Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Waabudu wa kweli hawatumii sanamu.
Kutojiingiza Katika Siasa
Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hawaingilii siasa za kitaifa au za mahali wanapokaa. Pia, wao ni watu ambao hutii sheria.—Waroma 13:1, 5-7.
Maadili Bora
Yesu alieleza jinsi ya kuwatambua waabudu wa kweli aliposema hivi: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi.” (Yohana 15:12, 13) Sura nyingine katika Biblia inasema hivi: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Wagalatia 5:22, 23) Wale wanaoonyesha sifa hizo hawasemi uwongo, hawaibi, hawachezi kamari, hawatumii dawa za kulevya, wala kukosa maadili katika ngono. (Waefeso 4:25-28) Wanampenda Mungu, kwa hiyo wanaepuka mambo ambayo Mungu huchukia. Kanuni hizo huongoza maisha ya Mashahidi wa Yehova.
Mwisho Unaokaribia wa Ulimwengu Huu
Ni nini hufanya nyakati zetu ziwe tofauti na nyakati nyingine? Kutimizwa kwa unabii huonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo, ulimwengu huu. (Danieli 2:44) Leo, suala ni, Je, mambo tunayofanya yanampendeza Mungu? Mungu ni mmoja, na lazima kuna dini moja tu ya kweli. Dini hiyo haiwezi kupingana na Taurati, Zaburi, na Injili. Kwa hiyo, lazima tuchunguze Neno hilo.
Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova hufanya. Hata uwe mshiriki wa dini gani, unapaswa kufanya hivyohivyo. Hakuna mtu anayeweza kukuamulia jambo hilo. Kumbuka: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:12.
Hakuna mtu ambaye huzaliwa akiwa Shahidi wa Yehova. Kila Shahidi hufanya uamuzi wa kibinafsi. Baada ya kulichunguza Neno la Mungu kwa unyoofu, mtu hutambua kweli, kisha hujiweka wakfu kwa Mungu wa kweli, ambaye jina lake ni Yehova. Ikiwa ungependa kufanya uchunguzi huo, tafadhali tuma barua kwenye mojawapo ya anwani zilizo hapa chini.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu yote ya Maandiko yametoka katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.
[Maelezo ya chini]
a Katika Uislamu, Biblia ni vile vitabu vinavyoitwa Taurati, Zaburi, na Injili. Angalau aya 64 za Kurani husema kwamba vitabu hivyo ni Neno la Mungu na hukazia uhitaji wa kuvisoma na kutekeleza amri zake. Watu fulani hudai kwamba Taurati, Zaburi, na Injili zimebadilishwa. Hata hivyo, kusema hivyo ni kupuuza maneno ya Kurani na ni kusema kwamba Mungu hawezi kuhifadhi Neno lake.