Wazo Hilo Laingia Dini za Mashariki
“Sikuzote nilifikiri kwamba kutoweza kufa kwa nafsi ilikuwa kweli yenye kuenea pote ambayo kila mtu alikubali. Kwa hiyo hakika nilishangazwa kusikia kwamba watu fulani wenye akili sana wa Mashariki na Magharibi walijadiliana kwa nguvu juu ya imani hii. Sasa ninajiuliza namna gani wazo la kutoweza kufa lilikuja kuingia katika akili ya Wahindu.”—MWANAFUNZI WA CHUO KIKUU ALIYELELEWA KATIKA IMANI YA WAHINDU.
1. Kwa nini ujuzi juu ya kukua na kuchipuka kwa fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi ya mwanadamu katika dini mbalimbali ni wenye faida kwetu?
NAMNA gani wazo la kwamba mtu anayo nafsi isiyoweza kufa liliingia katika dini ya Wahindu na zile dini nyingine za Mashariki? Ulizo hili ni lenye kupendeza hata kwa wale walio Magharibi ambao huenda hawafahamiani na dini hizi, kwa kuwa imani hiyo hubadili maoni ya kila mtu kuhusu wakati ujao. Kwa sababu fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi ya mwanadamu ni lilelile katika dini nyingi leo, kujua namna wazo hilo lilivyokua bila shaka kunaweza kufanyiza kuwe na mapatano na upashanaji habari bora.
2. Kwa nini India imekuwa chanzo chenye kustahili kuangaliwa cha uvutano wa kidini katika Asia?
2 Ninian Smart, profesa wa mafunzo ya kidini kwenye chuo kikuu cha Lancaster katika Uingereza asema: “Kitovu cha maana zaidi chenye uvutano wa kidini katika Asia kimekuwa ni India. Hili si tu kwa sababu India yenyewe imekuwa chanzo cha imani nyingi—Uhindu, dini ya Buddha, Jaini, Sikh, n.k. bali kwa sababu mojapo wa dini hizi, yaani dini ya Buddha, imekuja kuingiza uvutano wa maana sana katika utamaduni wa karibu Asia ya Magharibi yote.” Tamaduni nyingi zilizovutiwa katika njia hii “bado zaendelea kuitazama India kuwa makao yao ya kiroho,” asema mwanaelimu Mhindu, Nikhilananda. Basi, namna gani fundisho hili la kutoweza kufa kwa nafsi lilingia katika India na sehemu nyingine za Asia?
Fundisho la Kihindu la Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine
3. Kulingana na mwanahistoria mmoja, yawezekana wazo lile la uhamaji wa nafsi liliingizwa na nani katika India?
3 Katika karne ya sita K.W.K., wakati Pythagoras na wafuasi wake katika Ugiriki walipokuwa wakitetea kisio la uhamaji wa nafsi, wanahekima Wahindu waliokuwa wakiishi kando ya kingo za mito India na Ganges katika India walikuwa wakikuza wazo ilihili. Kutokea kwa imani hii katika wakati uleule “katika ulimwengu wa Kigiriki na India hakungeweza kuwa kwa urahisi jambo la bahati tu,” asema mwanahistoria Arnold Toynbee. “Chanzo kilekile kimoja kinachowezekana [cha uvutano],” Toynbee atokeza, “ni jamii ya Waerasia wenye kuhamahama, ambao, katika karne za 8 na 7 K.W.K., walishuka India, Asia ya Kusini-Magharibi, inchi yenye nyika karibu na pwani la Bahari Nyeusi, na Balkani na peninsula za Anatolia.” Kabila za Waerasia wahamaji bila shaka zilichukua pamoja nao mpaka India lile wazo la uhamaji wa nafsi.
4. Kwa nini wazo la uhamaji wa nafsi lilivutia Wahindu wenye hekima?
4 Uhindu ulikuwa umeanza mapema sana katika India, karibu na mwaka wa 1500 K.W.K., Waariani walipofika. Kutoka mwanzoni sana, Uhindu ulishikilia imani ya kwamba nafsi ilikuwa tofauti na mwili na kwamba nafsi huokoka kifo. Kwa hiyo Wahindu walizoea ibada ya mababu na kuandalia chakula nafsi za wafu wao ili wale. Karne nyingi baadaye wakati wazo la uhamaji wa nafsi lilipofika India, lapaswa kuwa lilivuta wanahekima Wahindu waliopambana sana na matatizo yenye kuenea kuhusu uovu na mateso kati ya wanadamu. Kuchanganya fundisho hili na kile walichokiita sheria ya Karma, ile sheria inayosema kwamba kila jambo na sababu yake, wanahekima Wahindu walikuza kisio la fundisho la kuhama kwa nafsi ambalo kupitia kwalo kustahili ao kutostahili katika uhai wa mtu kunathawabishwa au kuadhibiwa katika uhai wa baadaye.
5. Kulingana na Dini ya Kihindu, mradi wa upeo wa nafsi ni nini?
5 Lakini kulikuwa wazo lingine lililovutia fundisho la Kihindu kuhusu nafsi. “Inaonekana kuwa kweli kwamba wakati uleule ambapo kisio la uhamaji wa nafsi na karma liliundwa, au hata mapema zaidi,” yasema Encyclopædia of Religion and Ethics, “wazo lingine . . . lilikuwa likikomaa katika kikundi kidogo cha wenye akili katika India ya Kaskazini—wazo la kifalsafa la Brahman-Ātman [Brahman mkuu zaidi na wa milele, Nafsi ya upeo].” Wazo hili lilichanganywa na kisio la kuzaliwa upya katika mwili mwingine ili kufasiria mradi wa mwisho wa Wahindu—kukombolewa kutoka mzunguko unaojirudia wa uhamaji wa nafsi katika kusudi la kuwa mtu afikiaye mwisho halisi. Imani hii ya Kihindu inafikiwa kwa kufanya jitihada kutokana na mwenendo wa kijamii wenye kukubaliwa na ujuzi wa kipekee wa Kihindu.
6, 7. Ni nini iliyo imani ya Dini ya Kihindu ya kisasa kuhusu uhai baada ya kifo?
6 Hivyo wanaume wenye hekima walifanyiza wazo la uhamaji wa nafsi kuwa fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine kwa kulichanganya na ile sheria ya Karma na wazo la Brahman. Octavio Paz, mwanashairi aliyepata Tuzo la Nobel na balozi Mmeksiko wa kale katika India aandika: “Kadiri Uhindu ulivyotawanyika, ndivyo ilivyokuwa na wazo moja . . . lililo kiini kwa dini ya Kibrahmani, Kibuddha, na dini nyingine za Asia: nafsi kutoka mwili wakati wa kifo na kuingia mwili mwingine kupitia uhai wenye kufaulu.”
7 Fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine ndiyo nguzo ya Uhindu wa siku za leo. Mwanafalsafa Mhindu Nikhilananda asema: “Kupata kutoweza kufa si pendeleo la hesabu ya wachaguliwa wachache pekee, bali ni haki ya urithi ya kila mtu, ni sadikisho la kila Mhindu mwema.”
Mrudio wa Kuzaliwa Upya Katika Dini ya Buddha
8-10. (a) Dini ya Buddha inafasiriaje uhai? (b) Msomi wa Dini ya Buddha alifasiriaje fundisho la kuzaliwa tena?
8 Dini ya Buddha ilianzishwa katika India karibu na mwaka 500 K.W.K. Kulingana na pokeo la Kibuddha, mwana-mfalme Mhindi mwenye jina la Siddhārtha Gautama, aliyekuja kujulikana baadaye kwa jina la Buddha baada ya kupata mnurisho, alianzisha Dini ya Buddha. Kwa kuwa inachipuka kutokana na Uhindu, mafundisho yayo yanafanana katika njia fulani na yale ya Uhindu. Kulingana na Dini ya Buddha, maisha ni kuendelea kwa mzunguko unaojirudia wa kuzaliwa upya na kifo, na kama vile katika Uhindu, hali ya kila mtu katika maisha yake ya sasa inaamuliwa na matendo ya maisha yake yaliyotangulia.
9 Lakini Dini ya Buddha haifasirie uhai katika maneno ya nafsi yenye utu ambayo huokoka kifo. Arnold Toynbee alisema: “[Buddha] aliona katika nafsi ya mwanadamu mifuatano yenye kupita upesi ya hali za kiroho, ambayo huunganishwa pamoja kwa tamaa tu.” Ijapokuwa hivyo, Buddha aliamini kwamba kitu fulani—hali fulani au kani—inaendelea kupita kutoka uhai moja hadi mwingine. Dr. Walpola Rahula, msomi Mbuddha afasiria:
10 “Mtu si kitu ila mchanganyiko wa kani na nishati za kimwili na kiakili. Kile tunachokiita kifo ni kutotenda kwa ujumla kwa mwili wenye nyama. Je! kani na nishati hizo zote hukoma kabisa mwili uachapo kutenda? Dini ya Buddha husema ‘La.’ Kupenda, uchaguzi, tamaa, kiu cha kuishi, kuendelea, kupata kuzaliwa upya tena na tena, ni kani ya ajabu inayosukuma uhai wote, maisha zote, inayosukuma hata ulimwengu mzima. Hiyo ndiyo kani kubwa zaidi, nishati kubwa zaidi kuliko zote katika ulimwengu. Kulingana na Dini ya Buddha, kani hii haikomi mwili unapoacha kutenda, yaani kifo; bali huendelea kujidhihirisha yenyewe katika umbo lingine, ikitokeza maisha mengine yanayoitwa kuzaliwa tena.”
11. Maoni ya Wabuddha ni gani kuhusu uhai baada ya kifo?
11 Maoni ya Wabuddha juu ya uhai baada ya kifo ni haya: Kuishi kwa kudumu milele isipokuwa mtu afikie lengo la mwisho la Nirvana, kukombolewa kutoka mzunguko unaojirudia wa kuzaliwa mara ya pili. Nirvana ni hali isiyo wala ya baraka ya milele wala ya mtu kuwa na nafsi ya upeo. Ni hali tu ya kutokuwako kwa mtu—“mahali pasipo na kifo” kupita kuwako kwa mtu. Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary hufasiria “Nirvana” kuwa “mahali au hali ya kutokumbuka juto, teso, au uhalisi wa nje ya mtu.” Badala ya kutafuta kutoweza kufa, Wabuddha wanatiwa moyo kupita kutoweza kufa na kufikia Nirvana.
12-14. Namna gani vikundi mbalimbali vya dini ya Buddha hufasiria wazo la kutoweza kufa kwa nafsi?
12 Kadiri Dini ya Buddha ilivyosambaa mahali mbalimbali katika Asia, ilibadilisha mafundisho yayo kuyaambatanisha na imani za mahali. Kwa mfano, aina ya Dini ya Kibuddha iitwayo Mahayana ambayo inatawala katika China na Japani yashikilia imani ya mabodhisattva (Mabuddha walionurishwa) wa kimbinguni, au Mabuddha wa wakati ujao. Bodhisattva huahirisha kuingia Nirvana yao na kupata maisha mengi katika kusudi la kutumikia wengine na kuwasaidia wafikie Nirvana. Hivyo mtu aweza kuchagua kuendelea katika mzunguko unaojirudia wa kuzaliwa upya hata baada ya kufikia Nirvana.
13 Badiliko lingine ambalo lilikuwa lenye uvutano wa pekee katika China na Japan ni fundisho la Bara Lenye Utakato la Magharibi, lililoumbwa na Buddha Amitabha, au Amida. Wale wanaoliitia jina la Buddha katika imani wazaliwa tena katika Bara Lenye Utakato, au Paradiso, mahali ambapo hali zafaa zaidi ili kufikia mnurisho wa mwisho. Ni jambo gani lilikomazwa kutokana na fundisho hilo? Profesa Smart, aliyetajwa mapema, afasiria: “Kama ilivyotazamiwa, fahari za paradiso, zilizosimuliwa kwa udhahiri katika maandishi fulani ya Mahayana, zilikuja kuchukua mahali pa nirvana katika mawazo ya watu wengi kama lengo lenye upeo mkubwa.”
14 Dini ya Buddha ya Tibet yaingiza imani nyingine ya mahali. Kwa mfano, kitabu cha wafu cha Tibet chasimulia ajali ya mtu katika hali ya kati kabla ya kuzaliwa tena. Yasemekana kwamba wafu huwekwa kwenye nuru nyangavu ya nafsi ya upeo, na wale wote wasioweza kuvumilia nuru hiyo hawapati ukombozi bali wanazaliwa tena. Bila shaka, Dini ya Buddha katika aina mbalimali yatoa wazo la kutoweza kufa.
Ibada ya Mababu Waliokufa Katika Shinto ya Japan
15-17. (a) Namna gani ibada ya roho za mababu waliokufa ilikomaa katika Dini ya Shinto? (b) Namna gani imani ya kutoweza kufa kwa nafsi ni fundisho la msingi katika Dini ya Shinto?
15 Dini iliyokuwako katika Japan kabla ya kufika kwa Ubuddha katika karne ya Sita W.K. ilikuwa ni dini isiyo na jina, na ilifanyizwa na imani zilizoshirikishwa na adili na desturi za watu. Walakini, pamoja na kuingizwa kwa Ubuddha, uhitaji uliamshwa ili kutofautisha dini ya Kijapani na ile ya kigeni. Ndivyo dini ya “Shinto,” maana yake “njia ya vijimungu,” ilivyotokea.
16 Ni imani gani dini ya Shinto ya asili iliyoshikilia kuhusu maisha baada ya kifo? Ukulima wa mchele kwenye ardhi yenye maji ulipofika, ‘kilimo cha udongo wa majimaji kilitaka jumuiya zilizopangwa vizuri na zenye kuimarika kitengenezo,’ chaeleza Kodansha Encyclopedia of Japan, ‘na sherehe za kilimo—ambazo baadaye zilitimiza fungu la maana sana katika dini ya Shinto—zilisitawishwa.’ Woga wa nafsi zilizoondoka uliongoza watu hawa wa kale kutunga sherehe za ibada za kuzituliza. Hilo likatokeza ibada ya roho za mababu wa kale waliokufa.
17 Kulingana na imani ya dini ya Shinto, nafsi “iliyoondoka” bado ina utu wayo lakini hutiwa uchafu kwa sababu ya kifo. Waliofiwa wanapofanya sherehe za ukumbusho, nafsi inatakaswa kufikia kiwango cha kuondolewa uovu wote, na kutwaa tabia ya amani na ya wema. Baada ya muda, roho hiyo ya babu aliyekufa hupanda ngazi ya kuwa kiabudiwa, au mlinzi. Kwa kuwako pamoja na dini ya Buddha, dini ya Shinto iliingiza mafundisho fulani ya Wabuddha, kutia ndani fundisho la paradiso. Hivyo, tunaona kwamba imani ya kutoweza kufa kwa nafsi ni fundisho la msingi kwa dini ya Shinto.
Kutoweza Kufa kwa Nafsi Katika Dini ya Tao, Ibada ya Roho za Mababu Katika Dini ya Confucius
18. Dini ya Tao inalo wazo gani kuhusu kutoweza kufa kwa nafsi?
18 Dini ya Tao ilianzishwa na Lao-tzu, asemekanaye kuwa aliishi katika karne ya Sita K.W.K. katika China. Kulingana na dini ya Tao, kusudi katika maisha ni kupatanisha utendaji wa mtu na Tao—njia ya maumbile. Wazo la Dini ya Tao kuhusu kutoweza kufa kwa nafsi laweza kujumlishwa kama ifuatavyo: Tao ndiyo kanuni inayoongoza ya ulimwengu wote. Tao hana mwanzo wala mwisho. Kwa kuishi kulingana na Tao, mtu huishiriki na huwa wa milele.
19-21. Kukisia-kisia kwa Wafuasi wa Dini ya Tao kumeongoza kwenye jitihada gani?
19 Katika kujaribu kwao kufanya umoja na maumbile, Wafuasi wa Dini ya Tao kwa muda wakawa wenye kupendezwa hasa na uwezo wa mwili wa kutozeeka na uwezo wa kujiponya. Walikisia-kisia kwamba labda kwa kuishi kwa kupatana na Tao, au njia ya asili, mtu aweza kwa njia fulani kujua siri za asili na apate kingo kutokana na hasara ya kimwili, magonjwa, na hata kifo.
20 Wafuasi wa Dini ya Tao walianza kufanya jaribio la kutafakari, mazoezi ya kupumua, na kula vyakula fulani tu, mambo yaliyofikiriwa yangeweza kuahirisha kuchakaa kwa mwili na kifo. Upesi hadithi za kimapokeo zikaanza kusambaa kuhusu watu wasioweza kufa ambao wangeweza kuruka kwenye mawingu na kutokea na kutoweka wapendapo na ambao waliishi juu ya milima mitakatifu au visiwa vya mbali kwa miaka isiyohesabika, wakila umande au matunda ya kimiujiza. Historia ya China huripoti kwamba katika 219 K.W.K., maliki Ch’in Shih Huang Ti aliongoza msafara wa meli mkiwamo vijana wanaume na wanawake 3,000 wakatafute kisiwa cha kihadisi cha P’eng-lai, kilichokuwa makao ya wasioweza kufa, ili wakalete dawa ya mti-shamba ya hali ya kutoweza kufa. Kwa wazi, hawakurudi na dawa hiyo ya kurefusha maisha.
21 Utafutaji wa uzima wa milele uliongoza Wafuasi wa Dini ya Tao kujaribu mchanganyo wa vidonge vya dawa ya kutoweza kufa kupitia alkemia. Kwa maoni ya Dini ya Tao, uhai watokea wakati zile kani zenye kupingana za yin na yang (kike na kiume) zinapoungana. Kwa hiyo, kwa kuunganisha risasi (aina ya madini ya rangi nyeusi, au yin) na zebaki (mercure yenye kung’aa, au yang), wataalamu hao wa alkemia walikuwa wakiiga utaratibu wa asili, na walifikiri kwamba dawa hiyo ingelitokeza kidonge cha kupatia hali ya kutoweza kufa.
22. Matokeo yalikuwa nini kutokana na uvutano wa Dini ya Buddha juu ya maisha ya kidini ya watu wa China?
22 Kufikia karne ya saba W.K., Dini ya Buddha ilikuwa ikijipenyeza katika maisha ya kidini ya watu wa China. Matokeo yakawa ni muchanganyiko wa sehemu za Dini ya Buddha, uasiliano-roho, na ibada ya mababu waliokufa. Profesa Smart asema: “Dini ya Buddha na Dini ya Tao, zilitolea umbo na msingi wa imani kuhusu uhai baada ya kifo, mafundisho yaliyokuwa ya msingi katika ibada ya kale ya mababu waliokufa katika China.”
23. Msimamo wa Confucius ulikuwa nini kuhusiana na ibada ya mababu waliokufa?
23 Confucius, Mchina mwenye hekima ajulikanaye sana wa karne ya sita K.W.K., ambaye falsafa yake ilikuja kuwa msingi wa Dini ya Confucius, hakutoa maelezo marefu juu ya uhai baada ya kifo. Badala yake, alitilia mkazo ulazima wa wema wa kiadili na tabia zenye kukubalika kijamii. Lakini alikuwa na mwelekeo wenye kufaa kuelekea ibada ya mababu waliokufa na alitia mkazo sana juu ya ufuatiaji wa desturi na sherehe zinazohusiana na roho za mababu wa kale waliokufa.
Dini Zingine za Mashariki
24. Dini ya Jaini yafundisha nini kuhusu nafsi?
24 Dini ya Jaini ilianzishwa katika India katika karne ya sita K.W.K. Mahāvīra, mwanzishi wayo, alifundisha kwamba vitu vyote vyenye uhai vinayo nafsi ya milele na kwamba wokovu wa nafsi kutoka kifungo cha Karma waweza kupatikana tu kupitia kujikana mno na kujitia adabu na kufuatia sana kutofanyia viumbe vyote jeuri. Mpaka leo wafuasi wa Dini ya Jaini hushikilia imani hizi.
25, 26. Imani gani za Dini ya Kihindu zapatikana pia katika Dini ya Sikh?
25 India pia ndipo palipozaliwa Dini ya Sikh, inayofuatwa na watu milioni 19. Dini hii ilianza katika karne ya 16 wakati Guru Nānak alipoamua kuchanganya mafundisho yaliyo bora ya Dini ya Kihindu na Uislamu na kufanya dini yenye muungano. Dini ya Sikh ilichukua imani za Kihindu za nafsi isiyoweza kufa, kuzaliwa upya katika mwili mwingine, na Karma.
26 Bila shaka, imani ya kwamba uhai huendelea baada ya mwili kufa ni sehemu ya maana ya nyingi za dini za Mashariki. Ingawaje, vipi Dini ya Jumuiya ya Wakristo, Dini ya Kiyahudi, na Uislamu?
[Ramani katika ukurasa wa 10]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa.)
ASIA YA KATI
KASHMIR
TIBETI
CHINA
KOREA
JAPAN
Banaras
INDIA
Buddh Gaya
MYANMAR
THAILAND
SRI LANKA
KAMBODIA
JAVA
KARNE YA 3 K.W.K.
KARNE YA 1 K.W.K.
KARNE YA 1 W.K.
KARNE YA 4 W.K.
KARNE YA 6 W.K.
KARNE YA 7 W.K.
Dini ya Buddha ilikuwa na uvutano juu ya dini zote za Asia ya Mashariki
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kuzaliwa upya katika mwili mwingine ndio nguzo ya Uhindu
[Picha katika ukurasa wa 11]
Kwa kuishi kwa kupatana na maumbile, Mfuasi wa dini ya Tao hujaribu kuwa wa milele
[Picha katika ukurasa wa 12]
Confucius alikuwa na maoni yafaayo juu ya ibada ya mababu waliokufa