Mahali pa Kwenda Ili Kupata Majibu
“Kisio la kuteswa milele halipatani na imani katika upendo wa Mungu kuelekea vitu vilivyoumbwa. . . . Kuamini katika adhabu ya milele ya nafsi kwa sababu ya makosa ya miaka michache, bila kuipatia hiyo nafasi ya kujikosoa, ni kwenda kinyume cha kanuni zenye akili nzuri.”—NIKHILANANDA, MWANAFALSAFA MHINDU.
1, 2. Tufikiriapo imani mbalimbali kuhusu uhai baada ya kifo, ni maulizo gani hutokea?
KAMA mwanafalsafa huyu Mhindu, watu wengi leo husumbuliwa na fundisho la mateso ya milele. Wengine, wakionyesha dalili ileile, wanayo magumu ya kusikia mawazo kama yale ya kufikia Nirvana ao kufanya umoja na Tao.
2 Lakini, kwa sababu ya wazo la kwamba nafsi ni isiyoweza kufa, dini za Mashariki na Magharibi zimesitawisha mfululizo wenye kubadilika-badilika unaotia wasiwasi wa imani kuhusu uhai baada ya kufa. Je! inawezekana kujua kweli kuhusu jambo linalotufikia tunapokufa? Je! kweli nafsi ni isiyoweza kufa? Tunaweza kwenda wapi ili kupata jibu?
Sayansi na Falsafa
3. Je! sayansi au njia za kisayansi za uchunguzi zatoa majibu kwa maulizo yanayohusu uhai baada ya kufa?
3 Je! sayansi au njia za kisayansi za uchunguzi zatoa majibu kwa maulizo yanayohusiana na uhai baada ya kifo? Kwa msingi wa habari za karibuni kuhusu mkaribio-kifo au hisi za ‘nje ya mwili,’ watafiti fulani wamejaribu kusimulia kuhusu uhai baada ya kifo. Akirudilia upya baadhi ya madai yao katika hotuba yake “Kifo Kama Vile Kiingilio katika Nuru?,” mteolojia Mkatoliki Hans Küng alimalizia: “Hisi za aina hii hazionyeshi kitu chochote kuhusu uwezekano wa uhai baada ya kifo: hapa ni jambo la dakika tano za mwisho kabla ya kifo na si la uhai wa milele baada ya kifo.” Akaongeza: “Swala la uwezekano wa uhai baada ya kifo ni lenye umaana mkubwa kwa ajili ya uhai kabla ya kifo. Hilo lataka jibu ambalo laweza kutafutwa mahali pengine ikiwa haliwezi kutolewa na wataalamu wa kiganga.”
4. Je! falsafa yaweza kutusaidia kupata majibu kutoka katika uwezekano mwingi unaotolewa na dini mbalimbali kuhusu uhai wa baadaye?
4 Vipi kuhusu falsafa? Je! yaweza kutusaidia kupata majibu kutoka katika uwezekano mwingi unaotolewa na dini mbalimbali kuhusu uhai wa baadaye? Uvumbuzi wa kifalsafa hutia ndani “utendaji wa kukisiakisia,” asema Bertrand Russell, mwanafalsafa Muingereza wa karne ya 20. Kulingana na The World Book Encyclopedia, falsafa ni “aina ya utafiti—njia ya mchanganuo, upekuzi, fasirio, kisiokisio.” Kuhusu kichwa cha habari cha uhai baada ya kifo, makisiokisio ya kifalsafa yamebadilika kutoka kuita kutoweza kufa kuwa wazo tamanifu tu mpaka kutangaza hilo kuwa haki ya kuzaliwa ya kila mwanadamu.
Chanzo Pekee cha Majibu
5. Ni kipi kilicho kitabu cha zamani zaidi kilichopata kuandikwa?
5 Hata hivyo, kuna kitabu ambacho ndani yake mnapatikana majibu ya kweli kwa maulizo ya maana kuhusu uhai na kifo. Hicho ndicho kitabu cha zamani zaidi kilichopata kuandikwa, sehemu zacho zikiwa zimeandikwa yapata miaka 3,500 iliyopita. Sehemu ya kwanza ya kitabu hiki iliandikwa karne chache kabla ya kutungwa kwa mashairi ya mapema zaidi ya Uhindu, yaani Veda, na karibu miaka elfu moja kabla ya Buddha, Mahāvīra, na Confucius kuishi duniani. Kitabu hiki kilikamilishwa katika 98 W.K., zaidi ya miaka 500 kabla ya Muḥammad kuanzisha Uislamu. Chanzo hiki cha pekee cha hekima ya juu ni Biblia.a
6. Kwa nini twaweza kutazamia Biblia itueleze nafsi ni nini?
6 Katika Biblia mna historia ya zamani iliyo sahihi zaidi sana kuliko kitabu kingine chochote kilichopo. Historia iliyorekodiwa katika Biblia yarudi nyuma mpaka kwenye mwanzo wa familia ya kibinadamu na inafasiria namna tulivyokuja kuwa hapa duniani. Hiyo huturudisha nyuma hadi kwenye wakati wa kabla wanadamu kuumbwa. Bila shaka kitabu kama hicho kinaweza kutupatia ufahamu wa kujua namna mtu alivyofanywa na nini iliyo nafsi.
7, 8. Kwa nini twaweza kuiendea Biblia kwa matumaini ili kupata majibu ya kweli na yenye kutosheleza kuhusu kile kinachotufikia tunapokufa?
7 Zaidi ya hilo, Biblia ni kitabu cha unabii ambao umekuwa na utimizo usiodanganyika. Kwa mfano, ilitabiri moja kwa moja kuinuka na kuanguka kwa milki za Umedi na Uajemi, na Ugiriki. Maneno haya yalikuwa sahihi sana kiasi cha kwamba wapekuzi wamejaribu, lakini bila kufanikiwa, kuthibitisha kwamba yaliandikwa baada ya mambo hayo kutukia. (Danieli 8:1-7, 20-22) Unabii mwingine mbalimbali ulioandikwa katika Biblia unaendelea kutimizwa moja kwa moja katika wakati wetu.b—Mathayo, sura 24; Marko, sura 13; Luka, sura 21; 2 Timotheo 3:1-5, 13.
8 Hakuna mwanadamu, hata awe mwenye akili kama nini, angeweza kutabiri kwa usahihi hivyo matukio ya wakati ujao. Mwenye uweza wote na Muumbaji mwenye hekima yote peke yake aweza kufanya hivyo. (2 Timotheo 3:16, 17; 2 Petro 1:20, 21) Hakika, Biblia ni kitabu kutoka kwa Mungu. Bila shaka, kitabu kama hicho kinaweza kututolea majibu ya kweli na yenye kutosheleza kuhusu jambo linalotufikia tunapokufa. Kwanza, acheni tuone kile inachosema kuhusu nafsi.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama broshua Kitabu Kwa Ajili ya Watu Wote, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Tazama Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kitabu cha zamani zaidi kilichopata kuandikwa
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kitabu kinachotoa majibu yenye kutumainika na yenye kutosheleza