SOMO LA 17
Kutumia Kikuza-sauti
NDUGU na dada zetu Wakristo hujitahidi sana na kutumia muda mwingi kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Ili mikutano iwafaidi, ni lazima waweze kusikia wasemaji vizuri.
Katika Israeli la kale, hakukuwa na vifaa vya kukuza sauti. Musa alipozungumza na taifa la Israeli katika Nyanda za Moabu kabla ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, mamilioni ya watu waliwezaje kumsikia? Labda Musa alipitisha habari akitumia watu waliokuwa wakirudia maneno yake, ambao walikuwa wamewekwa mahali fulani-fulani panapofaa katika kambi. (Kum. 1:1; 31:1) Baada ya Waisraeli kuanza kuteka eneo la magharibi la Yordani, Yoshua alikusanya taifa hilo mbele ya Mlima Gerizimu na Mlima Ebali, na inaonekana Walawi walikuwa katika bonde lililotenganisha milima hiyo. Wakiwa pale, watu wote walisikia na kuitikia baraka za Mungu na laana zake walizotangaziwa. (Yos. 8:33-35) Inawezekana watu walitumiwa pindi hii pia kupashana habari, ingawa inaonekana sauti pia iliweza kusambaa kwa urahisi katika eneo hilo.
Miaka 1,500 hivi baadaye wakati ‘umati mkubwa sana ulipokusanyika’ kando ya Bahari ya Galilaya kumsikiliza Yesu, yeye alipanda mashua, akasonga kidogo baharini, akaketi na kuanza kuzungumza na umati. (Mk. 4:1, 2) Kwa nini Yesu alizungumza kutoka mashuani? Inaonekana alifanya hivyo kwa sababu sauti ya mtu husambaa sana juu ya maji matulivu.
Kufikia mwanzoni mwa karne ya 20, idadi ya wale ambao wangeweza kusikia mambo yanayosemwa ilitegemea kiasi cha sauti ya msemaji na jinsi alivyosikika vizuri. Lakini katika miaka ya 1920, watumishi wa Yehova waliweza kuanza kutumia vifaa vya kukuza sauti katika makusanyiko.
Vifaa vya Kukuza Sauti. Vifaa hivyo vinaweza kukuza sana sauti ya msemaji na bado vidumishe vizuri ubora na hali ya sauti yake. Msemaji hahitaji kukaza sauti yake kupita kiasi. Wasikilizaji hawahitaji kukaza sana masikio ili kusikia yanayosemwa. Badala yake wanaweza kusikiliza kwa makini.
Jitihada nyingi hufanywa ili kuhakikisha kuna vifaa vizuri vya kukuza sauti katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Na zaidi, Majumba mengi ya Ufalme hutumia vifaa vinavyokuza sauti za wale wanaotoa hotuba, wanaoongoza mikutano, au wanaosoma jukwaani. Na makutaniko mengine yana vikuza-sauti ambavyo hutumiwa na wahudhuriaji wanapotoa maelezo wakati wa mikutano. Kama kutaniko lina kikuza-sauti, jifunze kukitumia vizuri.
Miongozo Fulani ya Msingi. Ili ukitumie vizuri kikuza-sauti, kumbuka mambo yafuatayo: (1) Kwa ujumla kikuza-sauti kinapaswa kuwa sentimeta 10 hadi 15 hivi kutoka mdomo wako. Kikuza-sauti kikiwa karibu sana na mdomo wako, sauti yako itabadilika. Kikiwa mbali sana na mdomo wako, sauti yako haitakuwa wazi. (2) Kikuza-sauti kiwe mbele yako wala si upande. Zungumza tu wakati uso wako umeelekea kikuza-sauti, lakini si wakati umeelekeza uso kulia au kushoto. (3) Ongea kwa sauti ya juu kidogo na kwa mkazo zaidi kuliko unavyozungumza kwa kawaida. Lakini usipige kelele. Vifaa vya kukuza sauti vitainua sauti yako kwa urahisi na hata wale walio mbali watasikia. (4) Ukihitaji kusafisha koo au ukishikwa na kikohozi au chafya, hakikisha umegeuza kichwa kutoka kwenye kikuza-sauti.
Unapotoa Hotuba. Unaposimama utoe hotuba, kwa kawaida kuna ndugu ambaye hurekebisha kikuza-sauti. Anapokirekebisha, simama kwa njia ya kawaida ukitazama wasikilizaji. Weka maandishi yako kwenye kinara cha msemaji, lakini hakikisha kwamba kikuza-sauti hakikuzuii kutazama maandishi yako.
Unapoanza kuzungumza, sikiliza jinsi sauti yako inavyosikika. Je, unaongea kwa sauti ya juu sana, au maneno fulani yanatokeza sauti ya “pu”? Unaweza kusonga nyuma kwa sentimeta 2.5 au 5. Unapotazama kifupi maandishi yako, kumbuka kwamba unapaswa kuzungumza na kusoma wakati tu uso wako umeelekea kikuza-sauti au ukiwa juu kidogo ya kikuza-sauti, lakini uso wako usiwe kamwe chini ya kikuza-sauti.
Unaposoma Jukwaani. Ni vizuri kuinua Biblia au kichapo kingine ili uso wako uelekee wasikilizaji. Huenda ukahitaji kushika kile unachosoma kwa upande fulani kidogo kwa sababu labda kikuza-sauti kitakuwa mbele yako. Yaani, kichwa chako kielekee kidogo upande mwingine wa kikuza-sauti. Ndipo unaposoma, sauti yako iingie moja kwa moja kwenye kikuza-sauti.
Ndugu wengi wanaosoma kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi husoma wakiwa wamesimama, wakitumia kikuza-sauti kilicho kwenye kinara. Hiyo inawawezesha kupumua vizuri na kusoma kwa hisia zaidi. Kumbuka kwamba kusoma mafungu ni sehemu muhimu ya mkutano. Faida ambazo wasikilizaji hupata hutegemea sana usomaji.
Unapotoa Maelezo Mkutanoni. Ikiwa kutaniko lenu linatumia vikuza-sauti wakati wa kutoa maelezo, kumbuka kwamba bado unapaswa kuzungumza kwa njia ya wazi na kwa kiasi kinachofaa cha sauti. Unapotoa maelezo, jaribu kushika mkononi kichapo cha funzo au Biblia. Hiyo itakuwezesha kuona habari hiyo vizuri huku ukiongea kwenye kikuza-sauti.
Katika makutaniko mengine kuna ndugu ambao wana migawo ya kuwapelekea vikuza-sauti wale wanaoitwa kutoa maelezo. Ikiwa ndivyo ilivyo kwenu, endelea kuinua mkono ikiwa umeitwa ili ndugu anayewapokeza kikuza-sauti aone mahali ulipo na kukufikia haraka. Ikiwa mnatumia kikuza-sauti kinachoshikiliwa mkononi, uwe tayari kukichukua. Usianze kuongea kabla ya kikuza-sauti kuwa mahali panapofaa. Ukimaliza kutoa maelezo, mrudishie huyo ndugu kikuza-sauti haraka.
Mnapofanya Onyesho. Tunahitaji kufikiria kimbele jinsi tutakavyotumia kikuza-sauti tunapofanya onyesho. Kikuza-sauti kikiwa kimeshikiliwa na kinara, mikono yako itakuwa huru kufungua Biblia na maandishi. Mkitumia kikuza-sauti mnachoshikilia kwa mkono, mnaweza kuwa huru zaidi kusonga, lakini mtahitaji kupanga ili mwenzako akishike. Mkifanya hivyo mikono yako itakuwa huru kufungua Biblia. Mnahitaji kufanya mazoezi na mwenzako ili ajue jinsi ya kushika kikuza-sauti vizuri. Pia kumbuka kwamba unapokuwa jukwaani usiwageuzie wasikilizaji mgongo, hasa unapoongea.
Katika maonyesho ya Mikutano ya Utumishi, huenda ikawa kuna washiriki kadhaa, na huenda watatembea-tembea pale jukwaani. Kwa hiyo, wanaweza kuhitaji vikuza-sauti kadhaa. Vikuza-sauti hivyo viwekwe mapema mahali panapofaa au wale watakaofanya onyesho wapewe wanapoenda jukwaani. Ni vizuri kufikiria mapema kuweka kikuza-sauti mahali panapofaa na kwa wakati unaofaa. Kufanya mazoezi kabla ya kutoa onyesho kunatokeza nafasi ya kufundisha wale ambao watafanya onyesho jinsi ya kutumia kikuza-sauti vizuri. Ikiwa haiwezekani kufanya mazoezi jukwaani, huenda ikafaa washike kitu kinachotoshana na kikuza-sauti ili kujifunza kukitumia vizuri. Baada ya onyesho, wanapaswa kurudisha vikuza-sauti kwa utaratibu, wakijihadhari wasijikwae kwa kamba za vikuza-sauti wanapoondoka jukwaani.
Kutumia vikuza-sauti vizuri kunahusiana moja kwa moja na mojawapo ya malengo makuu ya mikutano yetu, yaani, kila mmoja kufaidika na mazungumzo yetu ya Neno la Mungu. (Ebr. 10:24, 25) Kwa kujifunza kutumia vikuza-sauti vizuri, sisi mmoja-mmoja tunaweza kutimiza kusudi hilo muhimu.