Mkutano wa Utumishi Hutuandalia Vifaa Kwa Ajili ya Kila Kazi Njema
1 Kusudi la Mkutano wa Utumishi ni kutuchochea na kutuandalia vifaa vya kushiriki kikamili zaidi katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (2 Tim. 3:17) Hata hivyo, tusipojitayarisha ifaavyo kwa ajili ya mkutano huo au tukishindwa kutumia yale tunayojifunza, manufaa hayatakuwa mengi.
2 Kujitayarisha kimbele kutakusaidia ushike mafundisho kikamili zaidi. Pitia vichapo vitakavyotumiwa, na uvilete ili uweze kuandamana na msemaji na kuweza kushiriki. Uwe msikilizaji mwangalifu, na uandike kwa ufupi habari za kutumiwa baadaye.
3 Mwangalizi-msimamizi hupitia kwa uangalifu sehemu za mkutano zilizoratibiwa. Wazee na watumishi wa huduma wenye uwezo, walio na sifa za ustahili wanapewa mgawo wa kuzitayarisha. (om-SW uku. 70) Makutaniko yenye wazee na watumishi wa huduma wachache yaweza kuwapa migawo ndugu wengine wenye sifa za ustahili ili wawasaidie. (km-SW 11/76, Sanduku la Swali) Kila msemaji apaswa kujitayarisha kikamili, akishikamana kwa ukaribu na mwelekezo ulioandaliwa, na kuhakikisha kwamba hapiti wakati uliowekwa.
4 Kwa kawaida mkutano huo huanza na matangazo. Ndugu aliyepewa mgawo huo apaswa kuwasiliana na mwangalizi-msimamizi kimbele ili apate kujua ni mambo gani yanayohitaji kutajwa. Huenda mambo hayo yakatia ndani barua kutoka kwa Sosaiti au vikumbusha juu ya mipango ya utumishi au ripoti za kila mwezi. Huenda tukapata kujua kwamba kuna wagonjwa wanaohitaji kutembelewa au huenda tukasikia maelezo zaidi juu ya utendaji mbalimbali wa kutaniko ambao umepangwa kwa wakati ujao. Toa uangalifu zaidi ili uweze kupata habari na kuwa tayari kufanya sehemu yako.
5 Sehemu ya mkutano inapohitaji ushiriki wa wasikilizaji, jitayarishe kwa kusoma habari na maandiko. Fikiria jinsi ambavyo wataka kutumia madokezo na aina ya maelezo uwezayo kutoa ili kutia wengine moyo. Waweza kuonyesha jinsi mafundisho hayo yawezavyo kuwa na thamani yenye kutumika kwa kusimulia ono fupi.
6 Wakati kuna wonyesho jaribu kujiona mwenyewe katika hali sawa na hizo, na ufikirie yale ungesema. Ona hoja zinazotumiwa na njia ya kusababu. Jaribu kukumbuka yale uliyosema ulipokuwa katika hali iliyofanana na hiyo wakati uliopita, na ufikirie jinsi mambo yaliyoonyeshwa yawezavyo kukusaidia upate matokeo mazuri zaidi wakati ujao.
7 Washiriki wa maonyesho na mahoji wapaswa wawe wamejizoeza vema kimbele. Kila mmoja apaswa awe anajua yale atakayosema na yale apaswayo kufanya jukwaani. Kwa kawaida sehemu zisizozoezwa kimbele hazichochei wala kuwatia moyo wasikilizaji. Wengine watakaoshiriki katika wonyesho huja wakiwa tayari kujizoeza kimbele sehemu yao baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi ili waweze kujizoeza wakiwa jukwaani na kuwasiliana na ndugu wanaoshughulikia maikrofoni ili wajue yale yatakayohitajiwa.
8 Nyakati nyingine programu itatia ndani hotuba inayozungumzia uhitaji fulani hususa wa kutaniko au makala ya Mnara wa Mlinzi ya wakati ufaao. Sikiliza kwa ukaribu, zingatia shauri hilo moyoni, na ujaribu kulitumia.
9 Twataka tuwe ‘tayari kwa kila kazi njema.’ (2 Tim. 2:21, NW) Mkutano wa Utumishi ni mojapo maandalizi ambayo Yehova hutoa ili kutusaidia tufanye hivyo. Kuhudhuria kwa uaminifu na jitihada ya moyo mweupe ya kutumia yale tunayojifunza kwa hakika itatusaidia ili tuweze ‘kutimiza kikamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:5, NW.