Maagizo kwa Ndugu Walio na Migawo Katika Mkutano wa Utumishi
Kuanzia toleo hili la Huduma Yetu ya Ufalme, maneno katika ratiba ya Mkutano wa Utumishi yamerahisishwa. Maagizo na vikumbusho vifuatavyo vitatoa habari na maelezo ya karibuni zaidi kuhusu mambo yaliyozungumziwa katika makala, “Jinsi ya Kutayarisha Mkutano wa Utumishi,” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Mei 2009.
◼ Hotuba: Hii ni hotuba inayotegemea habari zilizoonyeshwa bila kuwashirikisha wasikilizaji. Msemaji anapaswa kukazia mambo ambayo yatanufaisha kutaniko.
◼ Maswali na Majibu: Kama Funzo la Mnara wa Mlinzi, sehemu hii ina utangulizi na umalizio mfupi sana. Maswali yataulizwa katika mafungu yote. Kiongozi anapaswa kuepuka kutoa maelezo mengi. Maandiko yanayokazia mambo makuu yanaweza kusomwa kadiri muda unavyoruhusu. Mafungu hayapaswi kusomwa isipokuwa iwe imeagizwa.
◼ Mazungumzo: Hii ni hotuba ambayo inatia ndani maelezo ya wasikilizaji. Si hotuba tu, na wala si maswali na majibu pekee.
◼ Maonyesho na Mahojiano: Maagizo yanaposema onyesha, inamaanisha kwamba ndugu aliye na sehemu hiyo ana daraka la kupanga onyesho; si lazima yeye binafsi ashiriki onyesho. Watu atakaochagua kufanya onyesho wanapaswa kuwa wenye kustahili na walio mfano mzuri. Ikiwezekana, wanapaswa kujulishwa mapema. Haifai kuwatumia wahubiri wapya wasio na uzoefu kuonyesha jinsi kazi ya kuhubiri inavyofanywa eti kwa sababu tu ndugu anataka kuwapa fursa ya kuwa jukwaani, ingawa wengine wao wanaweza kutumiwa kama wenye nyumba. Wahubiri wanaotoa onyesho wasiwaonyeshe wasikilizaji mgongo. Wanaohojiwa wanapaswa kutoa maelezo yao wakiwa jukwaani kuliko wakiwa wameketi. Wahubiri walio na maonyesho na watakaohojiwa wanapaswa kufanya mazoezi mapema. Ikiwa ndugu aliye na mgawo anaona kwamba mkutano utapitisha wakati na analazimika kufupisha sehemu yake, ataepuka kuondolea mbali maonyesho na mahojiano. Watumishi wa huduma watashauriana na mratibu wa baraza la wazee kabla ya kuchagua wahubiri atakaowatumia katika maonyesho au mahojiano.
Ikiwa sehemu fulani ina maagizo ya pekee, maagizo hayo yanapaswa kufuatwa kwa uangalifu. Ndugu wanapotimiza migawo yao ya Mkutano wa Utumishi kupatana na maagizo yaliyo juu, wanachangia kufanya Mikutano ya Utumishi ‘itendeke kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.