Sanduku la Swali
◼ Tunaweza kuhakikishaje mikutano ya kutaniko inafuata wakati vizuri?
Wakati hupita haraka sana tunapozungumzia jambo zuri pamoja na rafiki zetu. Kwa sababu hiyo, huenda ikawa vigumu kushughulikia sehemu za mikutano katika wakati uliowekwa. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusipitishe wakati?
Anza kwa wakati. Kutaniko zima linapokutana, huenda ikawa vizuri kuwakaribisha wahudhuriaji kuketi dakika moja au mbili kabla ya wakati ili mkutano uanze kwa wakati uliowekwa kwa njia ya utaratibu. (Mhu. 3:1) Mikutano ya vikundi vidogo, kama vile mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani, haipasi kucheleweshwa ili kuwangojea wale ambao huenda wakaja wakiwa wamechelewa.
Tayarisha vizuri. Njia moja ya kufuata wakati ni kutayarisha mapema. Kumbuka vizuri kabisa kusudi la mgawo. Tambua mambo makuu, na uyakazie. Epuka kukengeushwa na mambo madogo. Toa hotuba yako kwa njia rahisi. Ikiwa mgawo huo una maonyesho au mahojiano, fanya mazoezi mapema. Ikiwezekana, pima wakati wa sehemu yako unapofanya mazoezi kwa sauti.
Ratibu habari zako. Ikiwa mgawo wako ni hotuba au mazungumzo pamoja na wasikilizaji, huenda ukaona inafaa kugawanya habari hizo katika sehemu mbalimbali. Amua wakati utakaotumia katika kila sehemu, na uandike hilo kando ya maandishi yako. Kisha pima wakati wako unapotoa hotuba. Katika mazungumzo pamoja na wasikilizaji, epuka kukubali maelezo mengi sana katika sehemu ya utangulizi hivi kwamba ulazimike kuharakisha mambo mazito yanayofuata baadaye. Viongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi wanapaswa kuruhusu wakati wa kutosha ili kushughulikia sanduku la pitio mwishoni. Wanapaswa pia kujihadhari wasitumie wakati uliowekwa kwa ajili ya wimbo na sala ya kumalizia.
Maliza kwa wakati. Ikiwa mkutano una sehemu kadhaa, kama vile Mkutano wa Utumishi, kila msemaji anapaswa kukumbuka wakati ambao sehemu yake inaanza na kumalizika. Ni nini kinachoweza kufanywa ikiwa mkutano unapitisha wakati? Ndugu mmoja au zaidi wanaweza kupunguza wakati huo kwa kukazia mambo makuu na kuacha mambo mengine madogo-madogo. Uwezo wa kufanya hivyo ni jambo moja linalomtambulisha mwalimu stadi.
Tukiwa wasikilizaji, tunaweza kumsaidia ndugu anayeongoza kwa kutoa maelezo machache na ya moja kwa moja. Kwa hiyo, sisi sote tunaweza kuchangia kuifanya mikutano ‘itendeke kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.