SOMO LA 51
Kupima Wakati, Kuwekea Kila Sehemu Wakati Unaofaa
INGAWA tunapaswa kuhangaikia zaidi ufundishaji, pia tunapaswa kufikiria muda wa hotuba zetu. Mikutano yetu imeratibiwa kuanza na kumalizika wakati fulani hususa. Ili mikutano iishe kwa wakati, inatakikana kila mmoja aliye na sehemu katika mkutano afuate wakati.
Maoni ya watu kuhusu maisha katika nyakati za Biblia ni tofauti sana na hali zilizoko sehemu nyingi leo. Wakati ulikuwa unakadiriwa tu kwa maneno kama “karibu saa ya tatu,” au “karibu na saa ya kumi.” (Mt. 20:3-6; Yn. 1:39) Watu hawakujali sana kutunza wakati katika shughuli zao za kawaida. Katika sehemu fulani za ulimwengu leo, kuna maoni kama hayo juu ya wakati.
Lakini, hata ingawa desturi au hali za watu binafsi zinaweza kutufanya tusijali wakati, tunaweza kufaidika tukijifunza kufuata wakati inavyofaa. Ikiwa wasemaji kadhaa wana sehemu katika programu, wanapaswa kufikiria wakati ambao umewekewa kila sehemu. Ile kanuni inayosema “acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango” inaweza kutumiwa kuhusu kupima wakati wa migawo yetu kutanikoni.—1 Kor. 14:40.
Kutunza Wakati. Matayarisho ni muhimu ili kufaulu. Mara nyingi wasemaji wanaoshindwa kutunza wakati hawajitayarishi vizuri. Labda wanajitumaini kupita kiasi. Au labda wanaahirisha matayarisho hadi dakika ya mwisho. Ili utunze wakati, unahitaji kuthamini mgawo wako na uwe tayari kutayarisha vizuri.
Je, una mgawo wa kusoma? Kwanza, pitia Somo la 4 hadi la 7, linalohusu ufasaha, kutua, kutia mkazo, na kukazia mawazo makuu. Kisha tumia ushauri huo unaposoma hotuba yako kwa sauti. Pima wakati wa kuitoa. Je, unahitaji kusoma haraka ili umalize kwa wakati? Ongeza mwendo unaposoma sehemu ambazo si muhimu sana, lakini endelea kutua na kupunguza mwendo unapokazia mawazo makuu. Fanya mazoezi tena na tena. Ufasaha wako unapoboreka, inakuwa rahisi kupima wakati.
Je, utatoa hotuba ukitegemea maandishi? Usiandike mambo mengi mno kana kwamba ni hotuba ya kusoma eti ili usipitishe wakati. Uliposoma Somo la 25, ulijifunza njia bora ya kufanya hivyo. Kumbuka mambo haya matano yanayofuata: (1) Tayarisha habari nzuri, lakini si nyingi mno. (2) Weka akilini mawazo makuu lakini usishike akilini sentensi nzima-nzima. (3) Tia alama kwenye muhtasari wako muda unaopanga kutumia kwenye kila sehemu ya hotuba au muda ambao unapaswa kutumia kabla ya kufikia sehemu fulani-fulani. (4) Unapotayarisha, fikiria mambo madogo-madogo ambayo unaweza kuacha unapoona kwamba unapitisha wakati. (5) Fanya mazoezi ya kutoa hotuba hiyo.
Ni muhimu kufanya mazoezi. Unapofanya mazoezi, tazama wakati unaotumia katika kila sehemu ya hotuba. Pitia hotuba yako tena na tena mpaka hotuba yote itoshee wakati unaotakikana. Usijaribu kutaja habari nyingi mno kwa wakati mfupi. Jipe wakati wa kutosha kwa sababu kutoa hotuba mbele ya wasikilizaji kunaweza kuchukua muda mrefu kuliko wakati unaotumia unapofanya mazoezi peke yako.
Kuwekea Kila Sehemu Wakati wa Kutosha. Kutunza wakati kunahusiana sana na kuwekea kila sehemu ya hotuba wakati unaofaa. Unapaswa kutumia muda mwingi kutoa sehemu kuu ya hotuba kwa sababu sehemu hiyo ina mambo muhimu. Utangulizi unapaswa kuchukua muda unaotosha kutimiza yale malengo matatu ambayo yametajwa katika Somo la 38. Kulingana na Somo la 39, sehemu kuu ya hotuba haipasi kuwa ndefu hivi kwamba unakosa wakati wa kuimalizia vizuri.
Jitihada zako za kutunza wakati zitafanya hotuba yako iwe bora na zitaonyesha kwamba unawaheshimu wasemaji wengine walio kwenye programu na unaheshimu pia kutaniko lote.