Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jy sura 54 uku. 132-uku. 133 fu. 1
  • Yesu​—“Mkate wa Uzima”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yesu​—“Mkate wa Uzima”
  • Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Habari Zinazolingana
  • “Mkate wa Kweli Kutoka Mbinguni”
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Yesu “Mkate wa Kweli Kutoka Mbinguni”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je, Umeonja Mkate wa Uzima?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • “Mkate wa Uzima” Upo kwa Watu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
jy sura 54 uku. 132-uku. 133 fu. 1
Wanaume wanakusanya mana; wanawake wanasaga mana, na kutengeneza mikate ya mviringo, kisha wanaipika

SURA YA 54

Yesu​—“Mkate wa Uzima”

YOHANA 6:25-48

  • YESU NDIYE “MKATE KUTOKA MBINGUNI”

Akiwa upande wa mashariki wa Bahari ya Galilaya, Yesu alilisha kimuujiza maelfu ya watu kisha akatoroka walipotaka kumfanya awe mfalme. Usiku huo alitembea juu ya bahari yenye dhoruba na akamwokoa Petro, ambaye pia alitembea juu ya maji lakini akaanza kuzama alipokosa imani. Yesu pia aliutuliza upepo, labda ili kuwaokoa wanafunzi wake wasizame baharini.

Sasa Yesu amerudi upande wa magharibi wa bahari hiyo, katika eneo la Kapernaumu. Wale aliowalisha kimuujiza wanampata na kumuuliza: “Ulifika hapa wakati gani?” Yesu anawakemea na kusema kwamba wanamtafuta kwa sababu wanatumaini kulishwa tena. Anawahimiza hivi: “Msifanye kazi kwa ajili ya chakula kinachoharibika, bali kwa ajili ya chakula kinachodumu kwa ajili ya uzima wa milele.” Basi wanauliza: “Tufanye nini ili tutimize kazi za Mungu?”—Yohana 6:25-28.

Huenda wanafikiria matakwa yaliyoandikwa katika Sheria, lakini Yesu anataja kazi yenye thamani ya juu zaidi: “Hii ndiyo kazi ya Mungu, kwamba mmwamini yule aliyemtuma.” Hata hivyo, watu hawamwamini Yesu, licha ya mambo yote aliyofanya. Wanamwomba afanye ishara ili wamwamini. Wanamuuliza: “Unafanya kazi gani? Mababu zetu walikula mana nyikani, kama ilivyoandikwa: ‘Aliwapa mkate kutoka mbinguni ili wale.’”—Yohana 6:29-31; Zaburi 78:24.

Kuhusu ombi lao la kutaka ishara, Yesu anawaelekeza kwenye Chanzo cha kweli cha miujiza: “Ninawaambia, Musa hakuwapa mkate kutoka mbinguni, lakini Baba yangu anawapa mkate wa kweli kutoka mbinguni. Kwa maana mkate wa Mungu ni yule anayeshuka kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.” Wakiwa hawajaelewa anachomaanisha, wanamsihi: “Bwana, tupe mkate huo sikuzote.” (Yohana 6:32-34) Hata hivyo, Yesu anamaanisha “mkate” gani?

Anaelezea hivi: “Mimi ndio mkate wa uzima. Yeyote anayekuja kwangu hatapata njaa kamwe, na yeyote anayeniamini hatapata kiu kamwe. Lakini kama nilivyowaambia, mmeniona na bado hamwamini. . . . Sikushuka kutoka mbinguni kufanya mapenzi yangu, bali mapenzi ya yule aliyenituma. Haya ndiyo mapenzi ya yule aliyenituma, kwamba nisipoteze yeyote kati ya wote alionipa, bali niwafufue katika siku ya mwisho. Kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Baba yangu, kwamba kila mtu anayemtambua Mwana na kumwamini awe na uzima wa milele.”—Yohana 6:35-40.

Watu wanakasirishwa na jambo hilo, nao Wayahudi wanaanza kulalamika kumhusu. Anawezaje kusema kwamba yeye ndiye “mkate ulioshuka kutoka mbinguni”? (Yohana 6:41) Kwa maoni yao, yeye ni mwana wa wazazi wa kibinadamu kutoka jiji la Galilaya huko Nazareti. Watu wanauliza: “Je, huyu si Yesu mwana wa Yosefu, ambaye baba yake na mama yake tunawajua?”—Yohana 6:42.

Yesu anawaambia: “Acheni kunung’unika miongoni mwenu. Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba aliyenituma amvute, nami nitamfufua siku ya mwisho. Imeandikwa katika Manabii: ‘Wote watafundishwa na Yehova.’ Kila mtu ambaye amemsikiliza Baba na kujifunza huja kwangu. Hakuna mwanadamu yeyote ambaye amemwona Baba, ila yule aliyetoka kwa Mungu; huyo amemwona Baba. Kwa kweli ninawaambia, yeyote anayeamini ana uzima wa milele.”—Yohana 6:43-47; Isaya 54:13.

Hapo awali alipozungumza na Nikodemo, Yesu alitaja uzima wa milele na akauhusianisha na imani katika Mwana wa binadamu, akisema: “Kila mtu anayemwamini [Mwana mzaliwa pekee wa Mungu] asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:15, 16) Lakini sasa anazungumza na watu wengi zaidi, akiwaambia kwamba anatimiza jukumu fulani ili wapate uzima wa milele, ambao hauwezi kupatikana kupitia mana wala mkate unaopatikana huko Galilaya. Basi uzima wa milele unaweza kupatikanaje? Yesu anarudia maneno yake: “Mimi ndio mkate wa uzima.”—Yohana 6:48.

Mazungumzo hayo kuhusu mkate kutoka mbinguni yanaendelea, nayo yanafikia kilele Yesu anapofundisha katika sinagogi huko Kapernaumu.

  • Kwa kutegemea matukio ya hivi karibuni, kwa nini ombi la kumtaka Yesu afanye ishara halifai?

  • Wayahudi wanaitikiaje Yesu anaposema kwamba yeye ndiye “mkate [wa kweli] kutoka mbinguni”?

  • Kwa nini mkate ambao Yesu anazungumzia ni bora kuliko mana au mkate wa kawaida?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki