Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jy sura 131 uku. 298-uku. 299 fu. 3
  • Mfalme Asiye na Hatia Ateseka Kwenye Mti

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mfalme Asiye na Hatia Ateseka Kwenye Mti
  • Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Habari Zinazolingana
  • Maumivu Makali Juu ya Mti
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Maumivu Makali Juu ya Mti
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Yesu Alitoa Uhai Wake kwa Ajili Yetu
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
  • Kwa Nini Tumpende Yesu?
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
jy sura 131 uku. 298-uku. 299 fu. 3
Yesu anamwahidi mhalifu aliyetundikwa pamoja naye, “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso”

SURA YA 131

Mfalme Asiye na Hatia Ateseka Kwenye Mti

MATHAYO 27:33-44 MARKO 15:22-32 LUKA 23:32-43 YOHANA 19:17-24

  • YESU ATUNDIKWA KWENYE MTI

  • ISHARA ILIYOBANDIKWA JUU YA KICHWA CHA YESU YALETA DHIHAKA

  • YESU AMPA MHALIFU TUMAINI LA KUISHI KATIKA PARADISO DUNIANI

Yesu anapelekwa katika eneo lisilo mbali sana na jiji, mahali ambapo yeye na wahalifu wawili watauawa. Mahali hapo panaitwa Golgotha, au Mahali pa Fuvu la Kichwa, na panaonekana “kwa mbali.”—Marko 15:40.

Wanaume hao watatu waliohukumiwa wanavuliwa nguo. Kisha wanapewa divai iliyotiwa manemane na nyongo chungu. Inaonekana wanawake kutoka Yerusalemu wameandaa mchanganyiko huo, na Waroma hawawakatazi kuwapa wale wanaouawa kinywaji hicho cha kutuliza maumivu. Hata hivyo, Yesu anapoonja, anakataa kukinywa. Kwa nini? Anataka awe na uwezo kamili wa kufikiri wakati wa jaribu hili kubwa; hataki kupoteza fahamu na anataka kuwa mwaminifu mpaka kifo.

Yesu ananyooshwa kwenye mti. (Marko 15:25) Wanajeshi wanagonga misumari kwenye mikono na miguu yake, wakichoma minofu na misuli, na kumsababishia maumivu makali. Mti unaposimamishwa wima, maumivu yanakuwa makali hata zaidi uzito wa mwili wa Yesu unapopasua majeraha. Lakini Yesu hawashutumu wanajeshi. Anasali hivi: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanachofanya.”—Luka 23:34.

Waroma wana desturi ya kubandika ishara inayoonyesha kosa la mhalifu aliyehukumiwa. Wakati huu, Pilato amebandika ishara iliyoandikwa: “Yesu Mnazareti Mfalme wa Wayahudi.” Imeandikwa kwa Kiebrania, Kilatini, na Kigiriki, basi kila mtu anaweza kusoma. Kwa kufanya hivyo, Pilato anaonyesha kwamba anawadharau Wayahudi waliosisitiza Yesu auawe. Wakuu wa makuhani wakiwa wamekasirika wanapinga: “Usiandike, ‘Mfalme wa Wayahudi,’ andika kwamba alisema, ‘Mimi ni Mfalme wa Wayahudi.’” Hata hivyo, ili wasimsumbue tena, Pilato anajibu: “Yale ambayo nimeandika, nimeandika.”—Yohana 19:19-22.

Wakiwa wamekasirika, makuhani wanarudia ushahidi wa uwongo uliotolewa hapo awali wakati wa kesi mbele ya Sanhedrini. Haishangazi kwamba wapita njia wanatikisa vichwa vyao wakimdhihaki na kumtukana: “Aha! Wewe uliyetaka kuliangusha chini hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe mwenyewe kwa kushuka kutoka kwenye mti wa mateso.” Pia, wakuu wa makuhani na waandishi wanaambiana hivi: “Acheni Kristo, Mfalme wa Israeli, ashuke sasa kutoka kwenye mti wa mateso, ili tuone na kuamini.” (Marko 15:29-32) Hata wahalifu waliohukumiwa walio upande wa Yesu wa kushoto na kulia wanamshutumu, ingawa kwa kweli yeye peke yake ndiye asiye na hatia.

Pia, wanajeshi wanne Waroma wanamdhihaki Yesu. Huenda walikuwa wakinywa divai kali, sasa wanamdhihaki kwa kuiweka mbele ya Yesu, ambaye kwa kweli hawezi kuifikia na kunywa. Kwa dhihaka Waroma wanazungumzia ishara iliyo juu ya kichwa cha Yesu na kusema: “Ikiwa wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi, jiokoe.” (Luka 23:36, 37) Hebu fikiria! Mtu ambaye amethibitika kuwa njia, kweli, na uzima, sasa anatukanwa na kudhihakiwa isivyostahili. Hata hivyo, anakabili mateso hayo yote bila kuwashutumu Wayahudi wanaomtazama, wanajeshi Waroma wanaomdhihaki, au wale wahalifu wawili waliohukumiwa ambao wametundikwa kando yake.

Wanajeshi wanapigia kura vazi la ndani la Yesu

Wale wanajeshi wanne wamechukua mavazi ya nje ya Yesu na kuyagawa vipande vinne. Wanapiga kura ili kugawana vipande hivyo. Hata hivyo, vazi la ndani la Yesu lina ubora sana, “halikuwa na mshono, lilikuwa limefumwa kutoka juu mpaka chini.” Wanajeshi wanaambiana: “Tusilirarue, badala yake tupige kura ili tuamue litakuwa la nani.” Basi wanatimiza andiko linalosema: “Waligawana mavazi yangu, na wakalipigia kura vazi langu.”—Yohana 19:23, 24; Zaburi 22:18.

Baada ya muda, mmoja kati ya wale wahalifu anatambua kwamba kwa kweli Yesu ni mfalme. Anamkemea mwenzake kwa kumwambia: “Je, wewe humwogopi Mungu hata kidogo, kwa kuwa umepata hukumu ileile? Sisi tunastahili kuteseka kwa sababu ya makosa tuliyofanya; lakini mtu huyu hakufanya kosa lolote.” Kisha anamsihi Yesu hivi: “Unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.”—Luka 23:40-42.

Yesu anamjibu hivi: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami,” si katika Ufalme, bali “katika Paradiso.” (Luka 23:43) Ahadi hiyo inatofautiana na ahadi aliyowapa mitume wake, kwamba wataketi pamoja naye kwenye viti vya ufalme katika Ufalme. (Mathayo 19:28; Luka 22:29, 30) Hata hivyo, huenda mhalifu huyo Myahudi amesikia kuhusu Paradiso ya duniani ambayo hapo mwanzoni Yehova aliwapa Adamu, Hawa, na wazao wao iwe makao yao. Sasa mhalifu huyo atakufa akiwa na tumaini hilo.

  • Kwa nini Yesu anakataa kunywa divai anayopewa?

  • Ni ishara gani inayobandikwa juu ya kichwa cha Yesu, na Wayahudi wanatendaje kuihusu?

  • Unabii unatimizwaje kuhusiana na jinsi wanajeshi wanavyogawana mavazi ya Yesu?

  • Yesu anampa tumaini gani mmoja wa wale wahalifu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki