Maisha na Huduma ya Yesu
Maumivu Makali Juu ya Mti
PAMOJA na Yesu wanyang’anyi wawili wanaongozwa nje wakauawe. Si mbali na jiji, andamano linasimama mahali panapoitwa Golgotha, au Fuvu la Kichwa.
Wafungwa hao wanavuliwa mavazi yao. Halafu wanapewa divai iliyotiwa manemane ambayo ni dawa ya kulevya. Inaonekana imetayarishwa na wanawake wa Yerusalemu, na Waroma huwa hawawanyimi wenye kutundikwa mchanganyo huu wa kinywaji chenye kufisha ganzi maumivu. Hata hivyo, Yesu anapokionja, anakataa kunywa. Kwa nini? Kwa wazi anataka kudhibiti nguvu zake zote za kufikiri wakati wa jaribu hili la imani yake lililo kubwa kupita yote.
Sasa Yesu amenyooshwa juu ya mti huku mikono yake ikiwa imewekwa juu ya kichwa chake. Ndipo askari wanapotwanga misumari mikubwa ndani ya mikono yake na ndani ya miguu yake. Yeye anajigeuza-geuza kwa maumivu wakati misumari inapochoma mnofu na nyuzi za mwili. Mti unaposimamishwa wima, maumivu yanazidi kweli kweli, kwa maana uzito wa mwili wake unapasua sehemu za majeraha yenye misumari. Hata hivyo, badala ya kutisha, Yesu anasali hivi kwa ajili ya askari hao Waroma: “Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo.”
Pilato amefanya ishara ibandikwe juu ya mti huo ambayo inasema hivi: “YESU MNAZARETI, MFALME WA WAYAHUDI.” Inaonekana, yeye anaandika hivi si kwa sababu tu anaheshimu Yesu bali pia kwa sababu anachukizwa sana na makuhani Wayahudi kwa kuwa wamemkamua mpaka akalazimika kuhukumu Yesu kifo. Ili wote waweze kusoma ishara hiyo, Pilato anaagiza iandikwe katika lugha tatu—katika Kiebrania, katika Kilatini rasmi, na katika Kigiriki cha kawaida.
Wakuu wa makuhani, kutia na Kayafa na Anasi, wanafadhaika. Tangazo hili la uhakika linaharibu saa yao yenye shangwe ya ushindi. Kwa hiyo wanapinga hivi: “Usiandike, Mfalme wa Wayahudi; bali ya kwamba yule alisema, Mimi ni mfalme wa Wayahudi.” Akiudhika kwa kuwa ametumika kama chombo cha kutimizia nia ya makuhani hao, Pilato anajibu kwa madharau ya kuazimia: “Niliyoandika nimeyaandika.”
Makuhani, pamoja na umati mkubwa, sasa wanakusanyika mahali pa uuaji, na makuhani wajaribu kukanusha ushuhuda wa ile ishara. Wanarudia ule ushuhuda wa bandia uliotolewa mapema kidogo kwenye majaribu ya Sanhedrini. Kwa hiyo, haishangazi kwamba wapita njia wanaanza kusema kwa matusi, wakitikisa vichwa vyao kwa mzaha na kusema: “Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani [kutoka kwenye mti wa mateso, NW]”!
“Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe”! nao wakuu wa makuhani na marafiki zao wa kidini wanaingilia kama kwamba ni kwa sauti moja. “Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani [kutoka kwenye mti wa mateso, NW], nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”
Kwa kunaswa katika roho hiyo, askari wajiunga katika kufanyia Yesu mzaha. Wanamtolea divai kali kwa mzaha, yaonekana ikiwa imepita kidogo tu mbele ya midomo yake iliyokauka. “Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi,” wanadhihaki vikali, “ujiokoe mwenyewe.” Hata wale wanyang’anyi—mmoja akiwa ametundikwa kwenye kulia kwa Yesu, na yule mwingine kwenye kushoto kwake—wanamdhihaki. Fikiria hilo! Binadamu mkubwa zaidi aliyepata kuishi, ndiyo, yule aliyeshiriki pamoja na Yehova Mungu katika kuumba vitu vyote, anapatwa na fedheha yote hii akiwa ameazimia!
Askari wanachukua mavazi ya Yesu ya nje na kuyagawanya sehemu nne. Wanatupa kura kuona yatakuwa ya nani. Hata hivyo, lile vazi la ndani halina mshono wa kuliunga, kwa kuwa ni la ubora mwingi. Hivyo basi askari hao wasemezana hivi: “Tusiipasue, lakini tuipigie kura, iwe ya nani.” Hivyo, bila kujua, wanatimiza andiko linalosema hivi: “Waligawanya nguo zangu, na vazi langu wakalipigia kura.”
Baada ya muda, mmoja wa wanyang’anyi anakuja kuthamini kwamba kwa kweli ni lazima iwe Yesu ni mfalme. Kwa hiyo, akikemea mwandamani wake, anasema hivi: “Wewe humwogopi hata Mungu, nawe u katika hukumu iyo hiyo? Nayo ni haki kwetu sisi, kwa kuwa tunapokea malipo tuliyostahili kwa matendo yetu; bali huyu hakutenda lo lote lisilofaa.” Halafu anaongea na Yesu, akiomba hivi: “Nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.”
Yesu anajibu, “Kweli kweli mimi nakuambia wewe leo, Wewe utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (New World Translation) Ahadi hii itatimizwa wakati Yesu atakapotawala mbinguni na kufufua mtenda maovu huyu mwenye kutubu kwenye uhai duniani katika Paradiso ambayo waokokaji wa Har–Magedoni na waandamani wao watakuwa na pendeleo la kuisitawisha. Mathayo 27:33-44; Marko 15:22-32; Luka 23:27, 32-43; Yohana 19:17-24.
◆ Kwa nini Yesu anakataa kunywa divai iliyotiwa manemane ambayo ni dawa ya kulevya?
◆ Yaonekana ni kwa nini ile ishara imebandikwa juu ya mti wa Yesu, ni nayo inaanzisha msemezano gani kati ya Pilato na wakuu wa makuhani?
◆ Yesu anadhihakiwa zaidi namna gani juu ya mti wa mateso, na kwa wazi ni nini kinachoongoza jambo hilo?
◆ Unabii unatimizwaje katika linalofanywa na mavazi ya Yesu?
◆ Mmoja wa wanyang’anyi anafanya badiliko gani, na Yesu atatimizaje ombi lake?