Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • od sura 12 kur. 123-129
  • Kutegemeza Kazi ya Ufalme Kwenu na Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutegemeza Kazi ya Ufalme Kwenu na Ulimwenguni Pote
  • Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSHUGHULIKIA FAIDA ZA UFALME ULIMWENGUNI POTE
  • KUSHUGHULIKIA MAHITAJI YA KUTANIKO LENU
  • KUSHUGHULIKIA MICHANGO
  • GHARAMA ZA MZUNGUKO
  • KUWATUNZA MASKINI
  • KUGAWA MACHAPISHO
  • Jinsi Kazi za Ufalme Zinavyogharimiwa
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Yote Hayo Hugharimiwaje?
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Fedha za Kuendesha Kazi Yao Zinatokana na Michango ya Kujitolea
    Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote
  • Kundi la Kikristo na Utendaji Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
od sura 12 kur. 123-129

SURA YA 12

Kutegemeza Kazi ya Ufalme Kwenu na Ulimwenguni Pote

MASHAHIDI WA YEHOVA wanatimiza unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho kwa kuhubiri habari njema “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; Mt. 24:14) Ili kufanya hivyo, wametumia wakati na nguvu zao nyingi katika kuwajulisha wengine mambo ya kiroho. Kwa kuwa wanamtegemea Yehova awaandalie mahitaji yao wakiwa wafanyakazi wenzake, wanaendelea kuutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwao. (Mt. 6:25-34; 1 Kor. 3:5-9) Matokeo yanaonyesha wazi kwamba wana kibali na baraka za Yehova.

KUSHUGHULIKIA FAIDA ZA UFALME ULIMWENGUNI POTE

2 Wanapoona jinsi tunavyohubiri habari njema na kutambua kwamba Biblia na machapisho yetu yanayotegemea Biblia hutolewa bila malipo, baadhi ya watu hujiuliza hivi: “Inawezekanaje?” Ni kweli kwamba pesa zinahitajiwa ili kuchapisha Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Pia, pesa zinahitajiwa ili kulipia gharama nyingine za ujenzi na udumishaji wa Betheli kwa ajili ya wahudumu wanaoendesha mashine za kuchapisha, kusimamia kazi ya kuhubiri, na utumishi mwingine wa kueneza habari njema. Isitoshe, waangalizi wa mzunguko, wamishonari, mapainia wa pekee, na wengine ambao wako katika utumishi wa pekee wa wakati wote hupewa pesa kidogo ili kuwasaidia waendelee katika kazi yao. Ni wazi kwamba kuhubiri habari njema kunahitaji pesa nyingi, iwe ni katika eneo letu au ulimwenguni pote. Pesa hizo zote hutoka wapi?

3 Wengi wanaothamini kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuwafundisha watu Biblia hufurahia kutoa michango kwa ajili ya kazi hiyo ya ulimwenguni pote. Hata hivyo, kazi hiyo hutegemezwa na Mashahidi wenyewe, ambao baadhi yao hutuma michango ya hiari katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya kwao. Wanaonyesha roho ya utayari kama ile ya watumishi wa Mungu wa kale waliotegemeza kwa ukarimu ujenzi wa mahali pa kumwabudu Yehova. (Kut. 35:20-29; 1 Nya. 29:9) Michango mingine hutolewa ikiwa wosia, na mingine hutolewa na mtu mmoja-mmoja, makutaniko, na mizunguko. Mara nyingi pesa hizo hutolewa zikiwa michango midogo-midogo. Inapojumlishwa, michango hiyo hutegemeza huduma.

Mashahidi wa Yehova huliona kuwa pendeleo kutumia pesa na mali zao kuendeleza kazi ya kuhubiri

4 Mashahidi wa Yehova huliona kuwa pendeleo kutumia pesa na mali zao kuendeleza kazi ya kuhubiri. Yesu na wanafunzi wake walikuwa na sanduku la pesa ambazo walitumia kulipia gharama. (Yoh. 13:29) Biblia inataja wanawake ambao walitumia mali zao kumhudumia Yesu na wanafunzi wake. (Marko 15:40, 41; Luka 8:3) Mtume Paulo alikubali kwa shukrani msaada uliotolewa kwa upendo na wale waliotaka kuendeleza habari njema na kutegemeza huduma yake. (Flp. 4:14-16; 1 The. 2:9) Mashahidi wa Yehova wanaiga mifano hiyo ya kale ya watu waliotumikia kwa bidii na kutoa kwa ukarimu. Kwa njia hiyo, watu wenye mioyo minyoofu kila mahali wanaweza kupewa “maji ya uzima bure.”—Ufu. 22:17.

KUSHUGHULIKIA MAHITAJI YA KUTANIKO LENU

5 Gharama za kutaniko hulipwa kwa michango ya hiari. Sadaka hazikusanywi; watu hawaambiwi watoe kiasi fulani cha pesa wala hatuchangishi pesa kutoka kwa watu. Masanduku ya michango huwekwa mahali pa mikutano ili mtu anayetaka kushiriki kutoa michango afanye hivyo “kama alivyoazimia moyoni mwake.”—2 Kor. 9:7.

6 Michango hutumiwa hasa kulipia gharama za kuendesha na kudumisha Jumba la Ufalme. Baraza la wazee linaweza kuamua kwamba kiasi fulani cha pesa hizo kinaweza kutumwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ili kuendeleza kazi ya ulimwenguni pote. Kutaniko linapaswa kupitisha azimio la kutuma pesa hizo. Kwa njia hiyo, makutaniko mengi hutoa michango kwa ukawaida kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Ikiwa wote kutanikoni wataelewa kwamba mara kwa mara pesa zinahitajiwa kutanikoni, haitakuwa lazima kutangaza kila wakati kuhusu michango.

KUSHUGHULIKIA MICHANGO

7 Baada ya kila mkutano, ndugu wawili hutoa pesa zilizo katika masanduku ya michango na kuweka rekodi ya pesa hizo. (2 Fal. 12:9, 10; 2 Kor. 8:20) Baraza la wazee litafanya mipango inayofaa ya kuhifadhi pesa hizo hadi zitakapotumwa kwenye ofisi ya tawi au kulipia gharama za kutaniko. Ndugu anayeshughulikia hesabu za kutaniko hutayarisha ripoti ya hesabu ya kila mwezi ambayo husomwa kutanikoni, na mratibu wa baraza la wazee hupanga ukaguzi wa hesabu za kutaniko baada ya kila miezi mitatu.

GHARAMA ZA MZUNGUKO

8 Pesa zinazotumika kugharimia makusanyiko, na vilevile gharama nyingine za mzunguko, hulipwa kwa kutumia michango inayotolewa na Mashahidi walio katika mzunguko huo. Masanduku ya michango huwekwa mahali pa makusanyiko ili michango ya hiari ikusanywe kwa ajili ya mzunguko. Zaidi ya hilo, makutaniko yanaweza kutoa michango wakati mwingine ili kushughulikia gharama zinazohitaji kuendelea kulipwa.

9 Kila mzunguko unapaswa kulipia gharama zozote za lazima zinazojitokeza, na pesa za ziada zinapaswa kutolewa zikiwa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Ikiwa pesa zilizo katika akaunti ya mzunguko hazitoshi kulipia gharama za kusanyiko lililopita au kulipia gharama za kuanzisha kusanyiko linalofuata, kama vile pesa za kukodi mahali pa kusanyiko, mwangalizi wa mzunguko anaweza kuagiza kwamba makutaniko yaandikiwe kuhusu uhitaji wa kutoa michango. Kila baraza la wazee litazungumzia jambo hilo na kuamua mchango ambao kutaniko lao litatuma kwenye hazina ya mzunguko. Kisha azimio litapitishwa kutanikoni.

10 Mambo yanayohusu pesa ambayo yanahitaji kushughulikiwa na wazee wa mzunguko yanapojitokeza, mkutano utafanywa kwenye siku ya kusanyiko la mzunguko. Maamuzi yote isipokuwa yale yanayohusiana na gharama za pekee za makusanyiko yanapaswa kuwa maazimio yaliyoandikwa na kupitishwa na wazee. Maazimio hayo yanapaswa kutaja kiasi hususa cha pesa na kuidhinishwa kila mara pesa za mzunguko  zinapotumiwa.

11 Kila baada ya muda fulani, mipango hufanywa ili kukagua rekodi za pesa za mzunguko.

KUWATUNZA MASKINI

12 Kusudi moja la sanduku la pesa lililotunzwa na Yesu na wanafunzi wake lilikuwa kuwasaidia maskini. (Marko 14:3-5; Yoh. 13:29) Wajibu huo wa Kikristo unaendelea mpaka sasa, kwa kuwa Yesu alisema: “Maskini mnao sikuzote.” (Marko 14:7) Mashahidi wa Yehova hutimizaje wajibu huo leo?

13 Nyakati nyingine, huenda washiriki waaminifu kutanikoni wakahitaji msaada kwa sababu ya uzee, udhaifu, au msiba mkubwa. Watu wa familia, na wengine ambao wanajua jambo hilo wanaweza kuwasaidia. Jambo hilo linapatana na maneno ya mtume Yohana: “Yeyote aliye na mali za ulimwengu huu akimwona ndugu yake akiwa na uhitaji naye akatae kumhurumia, anawezaje kuwa na upendo wa Mungu ndani yake? Watoto wadogo, tunapaswa kupendana, si kwa neno au kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:17, 18; 2 The. 3:6-12) Ibada ya kweli inahusisha kuwatunza waaminifu ambao huenda wanahitaji msaada wa kimwili.—Yak. 1:27; 2:14-17.

14 Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, mtume Paulo alieleza jinsi msaada unavyoweza kutolewa kwa wanaostahili. Unaweza kusoma ushauri wake kwenye 1 Timotheo 5:3-21. Ni jukumu la kila Mkristo kutunza mahitaji ya watu wa nyumbani mwake. Wazee kwa umri au walio dhaifu wanapaswa kusaidiwa na watoto wao, wajukuu wao, au watu wengine wa karibu wa ukoo. Nyakati nyingine, serikali au mashirika ya kijamii hutoa misaada, kwa hiyo watu wa ukoo au wengine wanaweza kumsaidia mwenye uhitaji aombe msaada huo kwa njia inayofaa. Huenda kukatokea hali inayolazimu kutaniko lote lifikirie kuwasaidia kwa njia fulani ndugu na dada wenye uhitaji ambao wamekuwa waaminifu kwa muda mrefu. Ikiwa watu wenye uhitaji hawana washiriki wa familia au watu wengine wa ukoo wanaoweza kuwasaidia, na serikali au mashirika ya kijamii hayatoi msaada wa kutosha, baraza la wazee linaweza kutoa mapendekezo yanayofaa ili kuwasaidia kwa njia fulani. Wakristo huona kuwa ni pendeleo kuwasaidia wenye uhitaji kwa mali zao.

15 Huenda ndugu na dada wengi wakawa na uhitaji kwa sababu ya mateso, vita, matetemeko ya nchi, mafuriko, njaa, au misiba mingine ambayo ni ya kawaida katika siku hizi za hatari. (Mt. 24:7-9) Katika pindi hizo, huenda makutaniko yasiweze kuwasaidia, kwa hiyo Baraza Linaloongoza hupanga ili ndugu wa maeneo mengine wawasaidie. Wakristo wa Asia Ndogo walifanya vivyo hivyo walipowapa chakula ndugu wa Yudea kulipokuwa na njaa. (1 Kor. 16:1-4; 2 Kor. 9:1-5) Tunapoiga mfano wao, tunawathibitishia ndugu zetu kwamba tunawapenda na kuonyesha kwamba sisi ni wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.—Yoh. 13:35.

KUGAWA MACHAPISHO

16 Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia husaidia sana kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa kawaida baraza la wazee humpa mtumishi wa huduma mgawo wa kutunza machapisho ya kutaniko. Ndugu waliopewa migawo hiyo huchukua majukumu yao kwa uzito. Wanaweka rekodi nzuri ya machapisho ili kutosheleza mahitaji ya kutaniko.

17 Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tunatambua kwamba wakati wetu, akili na nguvu, vipaji, mali zetu, hata uhai wetu wenyewe ni zawadi kutoka kwa Mungu na tunapaswa kuzitumia katika utumishi wake. (Luka 17:10; 1 Kor. 4:7) Tunapotumia vizuri kila kitu tulicho nacho, tunaonyesha kwamba tunampenda sana Yehova. Tunatamani sana kumheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye thamani, tukijua kwamba anapendezwa na zawadi yoyote tunayomtolea ili kuonyesha kwamba tumejitoa kwake kwa nafsi yote. (Met. 3:9; Marko 14:3-9; Luka 21:1-4; Kol. 3:23, 24) Yesu alisema: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mt. 10:8) Tunapojitoa wenyewe na kila kitu tulicho nacho katika utumishi wa Yehova, tunapata shangwe kubwa sana.—Mdo. 20:35.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki