Je! Watu Wanashiriki Lawama Pamoja na Watawala?
MATAIFA wakigongana na Mungu kutakuwako uharibifu mkubwa usioweza kuzuiwa. Lakini je! ikiwa ni viongozi wa dini na wa kisiasa wanaoongoza katika kumpinga Mungu, kwa sababu gani imewapasa watu kuumia?
Vema, je! twaweza kuwalaumu watawala peke yao? Hapana. Kwamba serikali ni mfano wa watu inayowatala hata wakubwa wanakubali. “Kila nchi ina serikali inayoistahili,” ndivyo alivyoeleza maoni haya Joseph de Maistre, mjumbe wa serikali ya Kifaransa aliyeishi wakati wa karne ya kumi na tisa. Na William Penn, waziri wa serikali ya Uingereza, alisema: “Serikali zinawategemea watu, kuliko watu kuzitegemea Serikali. Watu na wawe wema, na serikali haiwezi kuwa mbaya. Ikiwa ngonjwa wataiponya, lakini watu wakiwa wabaya, acha serikali iendelee kuwa nzuri, nao watu watajaribu kuipotosha na kuiharibu.” Biblia inakubaliana na jambo hili kwa kadiri ambavyo serikali za wanadamu ndizo zinazotajwa.
Hata katika Israeli, ambapo Sheria ya Mungu ndiyo ilikuwa ‘katiba’ ya taifa, watawala pamoja na watu wote walipatikana na hatia na wakaumia. Sababu yenyewe ilikuwa, kama Yehova alivyosema: “Manabii wanatabiri uongo, na makuhani wanatawala kwa msaada wa hao; na watu wangu wanapenda mambo yawe hivyo.”
Katika Kristendomu, wanaojidai kuwa watu wa Mungu, taifa lake takatifu, hali ile ile ndiyo iliyoko. Kwa hiyo maneno ya Mungu kwa Israeli yanatumika kwa mkazo ule ule sasa: “Je! nisiwapatilize kwa mambo hayo? . . . je! nisijilipize kisasi juu ya taifa la namna hii?”—Yer. 5:29-31.
Katika upande wa dini, je! watu hawakuwasikiliza wanadamu kuliko Mungu? Wanayo Biblia na wanaweza kuisoma, hata hivyo wameendelea kuwa watu wa makanisa na kuyategemeza makanisa ambamo mafundisho ya uongo juu ya Mungu na kukana kwa Neno lake vimefundishwa, ambamo watu wasio waaminifu na wafisadi wameachwa tu bila kukanywa, na ambamo fundisho la kumkana Mungu la mageuzi limekubaliwa. Je! jambo hili laweza kumpendeza Mungu?
SERIKALI ZA ULIMWENGU HAZIWEZI KUONDOA MABAYA YA DUNIA
Watu wakubwa wamekubali kwamba serikali haziwezi kuyaondoa mabaya mengi yanayoupata ulimwengu: uvunjaji wa sheria, matumizi mabaya ya dawa yanayoongezeka, magonjwa ya kisonono na kaswende, uchafu na maogofyo mengine makubwa zaidi kwa wanadamu. Sababu gani hawawezi? Kwa sababu ili kuondoa haya ni lazima watu wenyewe washirikiane kabisa, ni lazima wazoee upendo wa kweli. Lakini hivi sivyo ilivyo.
Serikali haiwezi kuwafundisha watu haki. Choyo kimezidi sana kwamba hakuna mpango wa elimu unaopangwa na mawakili wa kilimwengu utakaokiondoa. Mipango inayoanzishwa, kama ya usitawi, ya kurudisha sifa njema, na mengine, mwisho inaharibika kwa sababu ya upendeleo, choyo na rushwa. (Mhu. 1:15) Kwa hiyo watu wenyewe wanashiriki sehemu kubwa katika lawama.
Hali hizi zote zinazowapata watu kwa kimwili na kati ya wao kwa wao zinaonyesha namna ilivyo hali mbaya ya kiroho. Biblia inafananisha roho ‘inayovutwa’ na watu wa ulimwengu kwa hewa ya anga letu. Roho hii au nguvu inayotawala, nia au maelekeo ya ulimwengu, ni roho ya uasi. (Efe. 2:2) Inaenea na kutusonga kutoka kila upande, kama ifanyavyo hewa. Katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo hasira ya Mungu inaonyeshwa ‘ikimiminwa juu ya anga’ kama ‘pigo.’ Bila shaka roho inayosukuma ulimwengu kwa jumla ni roho ‘ngonjwa’ na ugonjwa wake unajionyesha wazi wenyewe kwa mapigo yale yale ya uharibifu katika utendaji wote wa jamii ya kisasa,—Ufu. 15:1; 16:17.
TARATIBU YOTE YA MAMBO LAZIMA IONDOKE
Mungu kwa kuwatazama wanadamu kutoka kwenye cheo Chake cha juu, anaona jambo hili na anajua kwamba si kikundi kimoja au sehemu moja peke yake ya kulaumiwa. Bali, taratibu yote ya mambo kama ilivyo leo imewafungia watu katika njia ya maisha ambayo ni vigumu mtu kuepuka kuifuata. Ni taratibu ambayo lazima iondolewe. Haiwezi kugeuzwa iende upande mwingine, kama vile gari la moshi lisivyoweza kuondoka relini na kupitia mashambani. Yesu Kristo alionyesha kwamba taratibu hii ya mambo ya ulimwengu huu ingefikia “mwisho” chini ya hali tuzionazo duniani leo.
Wengine wanaona njia ya pekee ya kuokoka ni kufuatana na taratibu hii ya mambo na kanuni zake za udanganyifu. Lakini kuachilia mbali huku kwa kanuni kunamweka mtu katika kushiriki lawama ya uovu wake, na uharibifu. Lakini si lazima mtu ajione kulazimishwa kwenda pamoja na taratibu. Mungu anamlaumu kila mtu mmoja mmoja kwa matendo yake mwenyewe. Kwa hiyo anatoa njia ya kutokea kwa wale ambao kweli wanataka kufuata mwendo mnyofu wa maisha, ulio safi. (Sef. 2:3; 1 Kor. 10:13) Yeye ni Mungu mwenye upendo mwingi sana. Fadhili zake za upendo ndiyo habari tutakayokuja kuangalia wakati mwingine.