Kusitawisha Urafiki na Mungu
“Kutakuwako wale watakaouona utukufu wa Yehova, fahari ya Mungu wetu. . . . Yeye mwenyewe atakuja na kuwaokoa ninyi watu.”—Isa. 35:2, 4, NW.
1. Kwa sababu gani imetupasa tusitawishe urafiki na Mungu?
URAFIKI na Mungu, au urafiki na ulimwengu—wewe unachagua upi? Ikiwa wapenda uzima, utachagua urafiki na Mungu, kwa sababu yeye ndiye Chanzo cha uzima, lakini taratibu mbovu ya ulimwengu huu ina uadui na Mungu, nayo itapita karibuni. (Yak. 4:4; 1 Yohana 2:15-17) Urafiki na Mungu ni jambo la kusitawisha kwa bidii, hata kama Ibrahimu alivyousitawisha. “Imani [yake] ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na ya kwamba imani ile ilikamilishwa kwa njia ya matendo yale. Maandiko yale yakatimizwa yaliyonena, Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa Mungu.” (Yak. 2:22, 23) Wewe, vile vile, waweza kuwa rafiki ya Yehova.
2. (a) Urafiki wa Mungu utamaanisha nini kwa mwanadamu duniani? (b) Nini itakayokuwa sehemu iliyo tukufu zaidi ya paradiso iliyorudishwa?
2 Je! urafiki na Mungu utamaanisha nini kwa wale wanaouchagua? Kwa wanadamu juu ya dunia hii, utatia ndani kufurahia paradiso iliyorudishwa na ikaenezwa duniani pote. Hata jangwa “litashangilia na kuchanua maua kama waridi.” (Isa. 35:1; Ufu. 21:3, 4) Utajiri wote wa hiyo dunia ya paradiso utakuwa zawadi ya Mungu kwa mwanadamu, itakayofurahiwa bila woga wa migawanyiko, chuki, vita wala pupa ya kibiashara vinavyowahuzunisha wanadamu wenye kuugua leo. (Zab. 115:16; Mik. 4:1-5) Basi, je! hii inamaanisha jamii yenye kufuatia mambo ya kimwili kwa wanadamu? Hata! Kwa maana sehemu iliyo tukufu zaidi ya paradiso iliyorudishwa ni hali yake ya kiroho. Unabii bora mbalimbali wa kurudishwa wa Biblia, kutia na ule uliomo katika Isaya sura za 2, 9, 35, 65 na 66, unao utimizo ulio bora katika maana ya kiroho. Kwa kweli, ni kwa sababu mabaki ya “kundi dogo” ya Wakristo wa kweli walioko duniani leo wamerudishwa kwenye “nchi” yao ya kiroho ya urafiki na Mungu kwamba njia imefunguliwa kwa “kondoo wengine,” vile vile, kusudi waletwe katika paradiso hii ya kiroho, na nyumaye paradiso ya duniani pote.—Isa. 66:8-14; Yohana 10:16.
3. Ni kwa njia gani mwanadamu alivyo mkuu kuliko wanyama?
3 Tofauti na wanyama, wengine wao ambao walitumia muda wao wa maisha katika paradiso ya kwanza ya kidunia, mwanadamu alifanywa aishi katika paradiso ya kiroho vile vile, awe na ujamaa wa karibu na Roho aliye mkuu, Yehova Mungu. Kwa hiyo, Mungu alimpa mwanadamu ufahamu wa ubora wa adili. Inasemwa hivi katika Mwanzo 1:27: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Huu usingeweza kuwa mfano wa kimwili uwezao kuonekana, kwa maana Mungu ni roho. Lakini Mungu alitia katika mwanamume na mwanamke wa kwanza sifa zile zile njema ambazo yeye mwenyewe anazionyesha katika usawa wa ajabu. (1 Yohana 4:11, 12; Flp. 4:8) Kama kiumbe chenye kuwaza mambo ya kiroho, chenye adili, mwanadamu mkamilifu alitengenezwa aitiishe dunia kuwa paradiso ya dunia ikionyesha kwa kila njia sifa za makao ya kiroho ya Yehova.—Isa. 11:6-9.
4, 5. (a) Nini yaliyotokezwa na uasi wa mwanadamu? (b) Ni mpango gani wenye upendo alioufanya Yehova nyuma ya hapo, ukitia ndani toleo gani?
4 Lakini lo! ukaja uasi. Mwanadamu alipoteza urafiki na Mungu. Paradiso yake ya kiroho ikatoweka, na, kwa haki, Yehova akamfukuza atoke katika paradiso ya Kiedeni. Lakini utukufu wa hekima ya Yehova sasa ulipata kuonyeshwa kwa njia ya ajabu. Ingawa macho yake yenye haki yasingeweza kuyatazama makosa na upotovu wa wanadamu wasio watiifu kwa kuyakubali, hata hivyo yeye alifanya mpango kusudi kwamba wale wanaotumia imani katika yeye waweze kuurudia ushirika wa urafiki wake. Namna gani? Kupitia kwa zawadi yenye upendo ya Mwanawe.—Mwa. 3:17-19, 23; Hab. 1:12, 13; Kum. 32:3, 4.
5 Lilikuwa toleo bora kwa upande wa Baba katika kumpeleka Mwana huyu mpendwa duniani—akashutumiwe, akatemewe mate, akateswe na kuuawa chini ya shtaka la kumkufuru Mungu yule yule ambaye alitii kwa uaminifu sana. Kwa upande wa Mwana, lilikuwa toleo gumu kupatwa na mambo haya ya aibu, kukataliwa na kutupwa nje na wale wale ambao kwa ajili yao alikuja kutoa wokovu, akiitoa hata nafsi yake katika mauti. Bila shaka, “hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu.” (Yohana 15:13) Kwa kweli, upendo mwaminifu wa Baba na Mwana vile vile unatoa mfano mzuri kabisa kwetu. Kadiri tunavyokuja kuifahamu sifa yenye kutokeza ya upendo huu, ndivyo itupasavyo kutaka kushiriki katika kundi la Kikristo la kweli, ambamo sifa ya upendo huu inakaa kama “kifungo cha ukamilifu.”—Kol. 3:14.
6. Mtume Yohana alitoa habari gani juu ya upendo?
6 Kama Mkristo aliyekomaa aliyekuwa akiishi katika paradiso ya kiroho ya kundi la karne ya kwanza, mtume Yohana alishukuru sana kwa ajili ya sifa hii ya upendo. Hiyo ndiyo sababu Injili yake na barua zake tatu zinang’aa kwa upendo wenye shukrani kwa hakika. Kama msiri wa Yesu na rafiki ya Mungu, yeye anatoa habari ya maneno ya Yesu mwenyewe juu ya upendo chini ya uongozi wa roho ya Mungu, pamoja na sala yake yenye kuchochea nafsi katika ile siku ya mwisho na wanafunzi wake: “Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua; lakini mimi nalikujua, na hao wamejua ya kuwa ndiwe uliyenituma. Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao.”—Yohana 17:25, 26.
7. Kwa sababu gani unapaswa upendo kusitawishwa, na namna gani?
7 Lo! umoja mzuri namna gani! Upendo huu na urafiki na Mungu na Yesu ni jambo la kusitawishwa kweli kweli. Ndiyo, kusitawishwa, kwa maana maadam tunaishi katika kutokamilika kwa kibinadamu, magugu yataelekea kutia mizizi katika utu wetu. Lazima haya yang’olewe kila mara, kusudi kwamba kusiwe na kizuizi cha kulisha udongo wa mioyo mizuri chakula cha wakati ufaao kutoka Neno la Mungu. Je! kuna njia bora liwezavyo kufanywa hili kuliko kwa kufanya ushirika wenye bidii katika kundi la watu wa Mungu mwenyewe kuwa jambo lililo la muhimu katika maisha zetu? Hivyo, kwa kuwa na Mungu kama Rafiki yetu, twaweza kusema kwa kweli, “Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19; 1 Pet. 4:1-3; Zab. 84:10; 149:1.
UTAWALA WA UFALME WA UPENDO
8. Ni namna gani ya ufalme uliowatawala Wakristo wa kweli sikuzote?
8 Wakati wote tangu siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 C.E., Yesu amekuwa akitumia utawala wa Ufalme juu ya wafuasi wake walio wakf, waliozaliwa kwa roho duniani. Kama inavyosemwa katika Wakolosai 1:13, 14, Yehova “alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi.” Huu ni ufalme hakika unaotawala juu ya Wakristo wa kweli. Hiyo ndiyo sababu Paulo anaandika, mbele tu ya maneno yaliyoko juu, sala yake kwamba “mjazwe maarifa ya mapenzi yake [Mungu] katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu.” (Mist. 9, 10) Kuliko kuwa ufalme wenye kufuatia mambo ya kimwili, ufalme huu unaweka umuhimu mwingi zaidi juu ya mambo bora ya kiroho. “Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika [roho takatifu].”—Rum. 14:17.
9. Ni lini na namna gani unavyoenezwa utawala wa Ufalme?
9 Lakini, utawala wa Ufalme wa Mungu umepaswa kuwa na mengi zaidi kuliko kundi la Kikristo! Katika mwaka wa 1914, kwa utimizo wa ajabu wa unabii wa Biblia, na katikati ya vita ya mataifa ya kilimwengu, “ufalme wa dunia” kwa haki ukawa wa Kristo. Wakati unakaribia kwake “wa kuwaharibu hao waiharibuo nchi.” (Ufu. 11:15-18) Lakini kwanza Yesu, kama mfalme anayetawala, anawakusanya wafuasi wake wa kweli, Wakristo waliotiwa mafuta, naye anarudisha kati yao paradiso ya kiroho kama ile iliyokuwamo kati ya Wakristo wa karne ya kwanza. Ushuhuda wote waonyesha kwamba mkusanyo huu umekuwa ukiendelea tangu mwaka wa 1919. Zaidi ya hayo, urafiki wa Yehova na wa Mwanawe umeenea, zaidi tangu mwaka wa 1935, kutia ndani “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” nao hawa vile vile wanakuja kumhesabia Mungu wokovu na Mwana-Kondoo, Kristo Yesu. Hawa, vile vile, wanayafurahia mapendeleo ya paradiso ya kiroho, wakiwa na tumaini la kupita “dhiki kubwa” karibuni na kushiriki katika kuirudisha paradiso ya duniani pote.—Ufu. 7:9, 10, 13-17; Isa. 26:20, 21; 65:17-25.
10. Katika miaka ya karibuni, wengi wamefanyaje mageuzi katika maisha zao?
10 Paradiso ijayo ya kidunia itaonyesha utukufu wa ile ya kiroho sikuzote. Shukrani ya mambo haya ya kiroho inapoongezeka, wengi wameona haja ya kufanya mageuzi katika maisha zao. Hii imemaanisha kutubu juu ya njia ya maisha ya kwanza isiyofaa, kugeuka, kujiweka wenyewe wakf kwa Mungu kupitia kwa Kristo na kujitoa kwa ubatizo wa maji. (Matendo 17:29-31) Kwa kugeuza maisha zao sasa, wanajitayarisha kuishi katika dunia ya paradiso. Katika miaka mitatu tu iliyopita, watu 477,124 ulimwenguni pote wamekuja kwa njia hiyo kushirikiana na mashahidi wa Yehova na kubatizwa katika maji. Na wangali wanakuja! Kwa kweli, “mataifa mengi” wanajifurahisha wenyewe kuletwa chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo, wakisema, “Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”—Isa. 2:3; Zek. 8:23.
KUKUA KATIKA IMANI
11, 12. Waliobatizwa karibuni wanawezaje kuendelea kukua katika imani?
11 Lo! ni furaha kama nini kuyaona haya mamia ya maelfu ya Wakristo waliobatizwa majuzi, pamoja na wengine wasiohesabika, wakikua katika imani! Kama alivyosema Paulo juu ya kundi lililotengenezwa majuzi katika Thesalonike, ndivyo sisi tunavyosema juu ya hawa waamini wengi wapya: “Imetupasa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kama ilivyo wajibu, kwa kuwa imani yenu inazidi sana, na upendo wa kila mtu kwenu kwa mwenzake umekuwa mwingi.” (2 The. 1:3) Hata katika uchanga wake, kundi hilo liliweza kutoka katika majaribu mengi magumu likiwa salama. Na kwa sababu gani? Kwa sababu ya upendo mwingi ambao wote walikuwa nao kwa mtu na mwenzake, na vile vile kwa sababu ya ‘kuzidi kwao sana katika imani’ kupitia kwa funzo la kawaida na ushirika pamoja. Hivyo, ‘walihesabiwa kuwa wanastahili kuuingia ufalme wa Mungu.’—Mist. 4, 5.
12 Je! wewe unataka ‘kuhesabiwa unayestahili’ mahali fulani katika makao ya ufalme wa Mungu leo? Basi angalia, kama Wathesalonike hao walivyofanya, kwamba imani yako inaendelea ‘kuzidi sana.’ Nyuma ya ubatizo imepaswa tamaa yako kufuata mafundisho ya Biblia iwe yenye nguvu hata zaidi. Unapojifunza Neno la Mungu kwa kuendelea, limepaswa liwe sehemu yako zaidi na zaidi, kusudi kwamba utende juu yake. Yesu alisema: “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.” (Yohana 15:14) Na hiyo inamaanisha kuwa rafiki za Yehova vile vile. Inamaanisha kuondosha njia za kilimwengu na mazoea ambayo yana uadui na Mungu, kupenda haki na kuchukia uovu sawa na alivyofanya Yesu, na sikuzote kuusitawisha utu mpya wa Kikristo.—Zab. 45:7; Efe. 4:23, 24.
13. Nini kilicho muhimu kwa kujenga ubora wa kiroho?
13 Kama Yesu, lazima tuwe waaminifu sana katika kuitegemeza enzi ya Yehova katika neno na katika tendo, tukiona ubora wa pendeleo letu lisilokadirika la kuwa mashahidi wa Yehova wa Kikristo. (Yohana 17:4, 6, 11, 12, 26) Katika huduma yetu ya shambani, twasihi wengine wasome Mnara wa Mlinzi. Twawaambia wanauhitaji, na ni kweli! Ndivyo na sisi! Ni muhimu kwa kujenga ubora wa kiroho, wenye msingi wa Neno la Mungu, kusudi kwamba tuweze kuwa na urafiki na Mungu na Kristo na kuushika. (Yohana 8:31, 32) Paulo alimwonya Timotheo kwa upole: “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.” (1 Tim. 4:15) Imetupasa sisi vile vile tufanye hivyo. Hii inahitaji ushirika wenye bidii katika kundi. Kupitia kwa “wanaume wazee” wake (NW), kundi la Kikristo leo linapendezwa sana katika maendeleo yako na katika kukusaidia wewe usitawishe “furaha ambayo ni ya imani yenu, kusudi kwamba shangwe yenu iweze kuwa nyingi mno katika Kristo Yesu.” Ushirika wa kawaida na funzo unaleta thawabu hiyo.—Flp. 1:25, 26, NW; Zab. 1:1-3; Ebr. 2:1; Yohana 15:7-11.
14. Limepaswa funzo la Mnara wa Mlinzi liwe na matokeo gani juu yetu?
14 Ndiyo, imetupasa tuwe wenye shukrani sana kwa chakula chote kizuri cha kiroho ambacho jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” imekuwa ikitoa kupitia kwa Mnara wa Mlinzi, kwa miaka 94 sasa. (Mt. 24:45-47) Tunapochukua chakula hiki pamoja na wengine penye mikutano ya Kikristo, tunakuja kuwa wenye shukrani sana kwa ajili ya urafiki wa Mungu kutuelekea sisi. Tunakuja kuwa “wenye kuwaka kwa roho,” na lo! namna hii inavyoonyeshwa katika utumishi wetu kwa Mungu! Shauku yetu ile ile kwa ajili ya kweli za ajabu ambazo Yehova anatoa kupitia njia yake inaivuta mioyo ya watu waaminifu. Wanaanza kushangaa ni nini tulicho nacho wasicho nacho. Bila shaka, ni roho ya Mungu inayokuja pamoja na ufahamu wa kweli ya Biblia, nayo imani yetu pamoja na upendo. ‘Vilivyonona’, ‘vilivyo vitamu,’ chakula kizuri kutoka Neno la Mungu tunachokifurahia katika ushirika na wengine, vinajenga ndani yetu furaha hii na shauku ambavyo vina uwezo mkubwa sana wenye kuvuta katika kuipendekeza kweli kwa wengine.—Rum. 12:11, NW; Neh. 8:10; Matendo 4:13.
15. (a) Twaweza kusali kwa ajili ya nini kwa kufaa? (b) Twawezaje kutenda kwa kupatana na sala hizo?
15 Lakini tunapofurahia tumaini hili tukufu, inatupasa “kudumu katika sala” vile vile. (Rum. 12:12, NW; 1 The. 5:17) Kama Sulemani, imetupasa tuombe “hekima na maarifa,” ili tuweze kuuona ubora wa paradiso ya kiroho ya Yehova kabisa. (2 Nya. (Sik.) 1:7-12) Kwa kupatana na sala hizo, na tuweke kando wakati wa kawaida kwa funzo la kipekee na la jamaa, pamoja na kujitayarishia mikutano ya kundi. Kwa kupanga kunakofaa, twaweza kuyafanya mazingira yetu yafae kwa funzo. Yetu yaweza kuwa hali ya sala ya Zaburi 19:14: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee [Yehova], Mwamba wangu, na mwokozi wangu.” Kwa ushirika wenye bidii katika mikutano ya kundi, twaweza kuonyesha kwamba tumeyafanya maneno ya mtunga Zaburi kuwa yetu wenyewe: “Heri . . . waendao katika sheria ya [Yehova]. Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”—Zab. 119:1, 97.
KUSITAWISHA MAISHA ZA KIROHO
16. Ni utimizo gani mbalimbali na mipango ya kitheokrasi zaidi iliyo sababu ya kufurahi?
16 Ufahamu wetu wa kiroho wa wema wa Yehova unaongezeka kwa kadiri tunavyozidi kushiriki katika tengenezo lake. Kupitia kwa njia ya Yehova twapokea elimu inayofahamika zaidi sikuzote juu ya Ufalme na ukamatano wake na kundi la Kikristo lililopo duniani. Kweli, inasisimua kuona unabii mbalimbali wa Biblia ukitimizwa katika matukio ya ulimwengu kufikia kadiri ya kwamba “pembe kumi” za “mnyama” wa Umoja wa Mataifa, zinazofananishwa katika Ufunuo sura ya 17, zimesimama tayari kuitikisa dini ya Kibabeli wakati wo wote. Lakini wenye kusisimua hata zaidi katika utimizo ni unabii mbalimbali unaokamatana ukionyesha kwamba Yehova amepaleta “mahali patakatifu,” kama panavyofananishwa na kundi la Kikristo, “katika hali yake ifaayo” kuwa tayari kuokoka “wakati wa dhiki ambayo haijafanywa kutukia tangu lilipopata kuwako taifa hata wakati huo.” (Dan. 8:14; 12:1, NW) Lo! tunaupokea mpango wa Yehova wa “wanaume wazee” wa kulichunga kundi kwa upendo namna gani! Na vile vile imetupasa tuwe wenye shauku kama nini kuiweka mioyo yetu wenyewe katika hali ifaayo kwa ajili ya kuokoka pamoja na tengenezo la kitheokrasi!—Matendo 20:28; Isa. 60:17; 65:13, 14.
17, 18. (a) Ni mashauri gani yenye hekima Yehova anayowatolea watu wake? (b) Kwa sababu gani hamna kutengana kwa wazazi na watoto katika jamaa za Wakristo wa kweli?
17 Kwa kuitimiza ahadi yake, Yehova anakuja kama Rafiki ‘kuwaokoa ninyi watu.’ Uwezo wake wenye kuokoa unaonekana hata sasa katika ulinzi wenye upendo anaoutoa kwa wote wanaoshiriki katika kundi la Kikristo. Kwa mfano, fikiria mashauri yote yenye hekima ambayo Mnara wa Mlinzi unayatoa kwa ajili ya jamaa. Katika muda mwingi wa mwaka wa 1970 na wa 1971, wazazi walipewa makala zilizokusudiwa kwa njia ya pekee wazisome pamoja na watoto wao wachanga. Karibuni zaidi shauri zuri limetolewa kwa vijana, likionyesha mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kuyajua. Katika kizazi ambapo ulimwengu wa vijana unavurugwa na mchafuko, je! si ajabu kwamba vijana wetu wenyewe wanapokea shauri hilo lifaalo, kwa kuutazamia uzima wa milele?—1 Tim. 4:12; Mit. 3:1-4.
18 Vile vile, kizazi kizee, kufikia kwa wazaa wazazi, kinapokea faraja nzuri sana na msaada kupitia kwa Mnara wa Mlinzi na vitabu vinavyolingana. Ijapokuwa ulimwengu unahuzunikia kutengana kwake kwa wazazi na watoto, hamna kutengana huko katika jamaa zenye msingi imara wa kweli ya Biblia. (Mit. 23:22-25) Vijana wanajua kwamba wao wanaweza kutegemea kupendezwa na uangalizi wenye upendo wa wazazi walio wakf. Wazee wanajua kwamba upendo wa jamaa yao na kupendezwa vitaendelea kuwa nao. Wazazi wanaowaadibisha watoto wao katika haki wana hakika wataheshimiwa na watoto wao, na wakati ule ule wanafurahia urafiki wa wazee wao wenyewe. Hakuna mapengo katika mpango huu wa kitheokrasi wa Yehova.—Kol. 3:15-24; Kum. 31:12.
19. Furaha ya kweli na uradhi vinapatikana wapi leo?
19 Ndiyo, ni katika ushirika wa kundi la Kikristo, na vile vile katika mzingo wa jamaa, kwamba wote wanaweza kusitawisha maisha za kiroho. Hivyo twaweza kupata furaha ile ile kama Daudi, aliyesema: “Nalifurahi waliponiambia, Na twende nyumbani kwa [Yehova].” (Zab. 122:1) Kwa kweli, kuna furaha na uradhi vitakavyopatikana katika ushirika katika jamaa ya duniani pote ya Yehova. Kutoka kwa ushirika huu, pamoja na kumtegemea Yehova kwa sala, inakuja amani ya akili na moyo katika ulimwengu wenye msukosuko. (Zab. 84:4; Flp. 4:6, 7) Kwa kuangalia kila hali ya ushirika, sasa, tunashika mahali petu katika paradiso ya leo ya kiroho, tukiwa na tumaini la urafiki wa milele na Mungu katika paradiso iliyoenezwa itakayokuja.
KUSAIDIA WENGINE WAPATE URAFIKI NA MUNGU
20. Kuna kazi gani ya muhimu ya kufanywa (a) ndani ya kundi? (b) nje ya kundi?
20 Unabii wa Isaya (35:3, 4) waonyesha kwamba watumishi wa Mungu wanayo kazi ya kufanya: “Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu, yafanyeni imara magoti yaliyolegea, waambieni walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope; tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi.” Ndani ya kundi la Mungu lenyewe, waangalizi waaminifu, ‘wanaofaa kuwafundisha wengine,’ wanafanya ziara za kipekee kwa jamaa na kwa walio wagonjwa kwa kimwili na kwa kiroho, na wengine vile vile, nao wanafundisha kwa upendo na uvumilivu katika mikutano ya kundi. (2 Tim. 2:2) Zaidi ya hayo, watu wanaopendezwa karibuni, wanaougua kwa sababu ya machukizo wanayoyaona ndani ya Kristendomu na katika milki yote ya ulimwengu ya dini ya uongo, inawapasa wajengwe kwa kujulishwa kisasi kinachokuja cha Mungu juu ya waovu na tumaini la wokovu. (Eze. 9:4-6; 34:15, 16) Kwa kusudi hili, kazi kubwa ya kufundisha inaendelea duniani mwote leo, ikifika, kwa wastani, katika nyumba 1,269,277 kila juma na mafunzo ya Biblia mnamo mwaka wa 1972.
21. Ni mwaliko gani wa Maandiko unaoenezwa kwa wale walio na kiu ya kweli?
21 Je! wewe mwenyewe unafaidika kutokana na shughuli hii kubwa ya elimu ya Biblia? Ikiwa sivyo, unaalikwa kwa shauku ushiriki katika mikutano penye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika mahali pako—“Haya, kila aonaye kiu, njoni majini, naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; naam, njoni, nunueni divai na maziwa, bila fedha na bila thamani. . . . Nisikilizeni kwa bidii, mle kilicho chema, na kujifurahisha nafsi zenu kwa unono. Tegeni masikio yenu, na kunijia; sikieni, na nafsi zenu zitaishi.”—Isa. 55:1-3; Ufu. 22:17.
22. Nini kitakachotujulisha kama rafiki za Mungu na za Yesu?
22 Yesu mwenyewe alifanya kazi yenye mazao ya kuhubiri alipokuwa duniani. Lakini yeye alisema kwamba mtu atakayetumia imani katika yeye angefanya kazi kubwa hata zaidi. (Yohana 14:12) Leo kazi ya ushuhuda iliyo kubwa zaidi kupita wakati wo wote mwingine ya ulimwenguni pote inaendeshwa ikatimilizwe na wale walio na imani kama ile ya Ibrahimu, rafiki ya Mungu. Vile vile Yesu anawaambia hawa: “Ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu. Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni. Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana.” (Yohana 15:15-17) Kwa upendo huu wenye mfano wa Kristo kwa mtu na mwenzake na uzaaji wa matunda mengi, wao wanajulikana kama wanafunzi wa kisasa wa Yesu.—Yohana 13:34, 35; 15:1-5.
23. Fahari ya Mungu wetu inaangazaje?
23 Lo! namna ulivyo wenye matunda wonyesho unaofanywa juu ya ufalme wa Mungu katika paradiso ya kiroho inayofurahiwa na watu wa Mungu duniani leo! Kwa kweli, fahari ya Yehova inaangaza kupitia kwa watu wake waliojitoa, wanaomtafuta yeye kupitia kwa Kristo, na wanaompata yeye kama Rafiki yao mwenye upendo.—Mt. 7:7, 11; Zab. 103:17, 18.