Kutayarishwa Kusema Maneno Yapendezayo ya Kweli
1, 2. (a) Nyuma ya ufufuo wake, ni amri gani Yesu aliyowapa wanafunzi wake alipokutana nao Galilaya? (b) Kwa sababu gani walikuwa na sababu ya kushangaa, lakini Yesu alitoa uhakikisho gani?
WAKATI Yesu alipofufuliwa kwa wafu na nyuma ya hapo akawatokea wanafunzi wake kumi na mmoja katika mlima fulani Galilaya, kama alivyokuwa ameahidi, ilionyesha yeye alikuwa mnenaji wa kweli wa Yehova. Angekuwa na maneno gani ya kutia moyo na maagizo? Yeye aliwatangazia: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Mamlaka hii duniani ingetia ndani kitu fulani alichokipenda sana, kuendelea kwa utendaji wa kuhubiri aliokuwa ameuanzisha. Aliendelea kuwaagiza wanafunzi: “Kwa hivo nendeni mkafanye watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kuyashika mambo yote niliyowaamuru ninyi. Na, tazama! mimi ni pamoja nanyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.”—Mt. 28:16-20, NW; Yohana 2:19-21.
2 Lo! ni amri inayoshangaza namna gani! Wazia kuambia kikundi kidogo cha wanafunzi kumi na mmoja waende wakawahubiri watu wa mataifa yote, wakiwafundisha na kuwabatiza! Kama mfano tu: leo zipo lugha 149 kila mojawapo ikizungumzwa na watu milioni moja au zaidi, lugha 16 kila mojawapo ikizungumzwa na watu milioni 50 au zaidi. Lo! ingekuwa kazi kama nini kwa kikundi hiki kidogo kujifunza tu lugha hizo nyingi au kuyafundisha mamilioni yaliyoishi wakati huo njia ya uzima ipasavyo! Lazima wawe walishangazwa na nguvu za maagizo haya. Kweli, Yesu alisema angekuwa pamoja nao, lakini je! kazi hiyo kubwa sana ingetimilizwaje?
3. Kumiminwa kwa roho takatifu katika Pentekoste kulisaidiaje katika maenezi ya kweli?
3 Ni siku kumi kamili nyuma ya kupaa kwa Yesu kuelekea mbinguni walipokuwa pamoja karibu wanafunzi 120 katika Yerusalemu wakati wa sikukuu ya Pentekoste. Kwa ghafula, wakasikia mvumo kama ule wa upepo wenye nguvu uendao kasi nazo ndimi kana kwamba za moto zikaonekana juu ya kichwa cha kila mmoja wao. Maana yake ikawa wazi kwa kuwa walijawa na roho takatifu ya Mungu nao wakaanza kusema katika lugha mbalimbali. Wakati uo huo karibu watu 3,000 walipata kuukubali ujumbe kwa moyo nao wakabatizwa. Tendo hili halikuonyesha kwamba roho ya Yehova na uongozi vilikuwa pamoja na kikundi hiki kidogo cha Wakristo waaminifu tu; lakini vile vile mlango ulifunguliwa ili ujumbe ambao Yesu alikuwa amekuwa akiutangaza uenezwe kwa kasi kwa Wayahudi waaminifu waliotawanyika katika mataifa mengi.—Matendo 2:1-4, 41.
4. Kitu gani kilichoanza Kornelio alipoongolewa?
4 Lakini, ujumbe usingekuwa wa watu wa ukoo wa Kiyahudi peke yao. Yesu alikuwa amewaambia wafuasi wake ‘kufanya wanafunzi wa watu wa mataifa yote.’ Hivyo, karibu miaka mitatu na miezi minne nyuma ya hapo, roho takatifu ilimwongoza Petro akubali ukaribishaji uliotolewa kwake na akida wa kikosi wa Italia Kornelio. Kuongolewa kwa Mtaifa huyu na jamaa zake na wasiri wake kulionyesha mwanzo wa jitihada kubwa kuueneza ujumbe wa Ufalme kati ya watu wa mataifa yote. Nyumaye, Paulo na wenzi wake walisonga mbele na safari zao za kuhubiri katika Asia Ndogo yote, Ugiriki, Italia na pengine kufika Spania. (Matendo 10:1-35; 11:18; Rum. 15:24) Wanafunzi wa kwanza waliona waziwazi uzito na umuhimu wa kazi yao ya kueneza injili. Kama vile Paulo na Barnaba walivyotangaza: “Ndivyo tulivyoamriwa na [Yehova], Nimekuweka uwe nuru ya Mataifa, upate kuwa wokovu hata mwisho wa dunia.”—Matendo 13:47; 1 Kor. 9:16.
5, 6. Ni mifano gani yenye kutia moyo itupasayo kuangalia hata ingawa huenda tusijisikie kwamba tunastahili sana kuihubiri kweli kwa wengine?
5 Je! wewe unayashiriki maoni hayo? Je! unafahamu kwamba Yesu yupo pamoja na wafuasi wake katika wakati wetu, akitumia mamlaka mbinguni na duniani hata mnamo mwisho wa hii taratibu ya mambo, ambamo sasa twaishi? Hii yamaanisha kwamba Wakristo wangali wana mgawo wa kuendeleza kazi ya kufanya wanafunzi! Huenda ukakataa kwamba wewe si msemaji wala mwalimu, kwamba usingeweza kuyafanya yaliyofanywa na mitume. Lakini je! wao walijisikiaje juu ya jambo hili? Kumbuka kwamba walisemekana kuwa “watu wasio na elimu, wasio na maarifa.” Lakini walijifunza kusema kwa uhodari hivi kwamba hata watawala na wazee wa Wayahudi “wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.”—Matendo 4:13.
6 Hata wanenaji wenye kutokeza na watumishi wa Yehova tangu nyakati zilizopita kama vile Musa na Yeremia walijisikia kutofaa kuzitimiliza amri za Yehova. Yehova alipomwamuru Musa akaseme na Farao, yeye alikataa kwamba hakuwa “mwepesi wa kusema,” kwa maana alikuwa na ‘ulimi mzito.’ (Kut. 4:10) Lakini, nyumaye Musa aliweza kuhutubia mamia ya maelfu kwa uongozi wa Yehova alipokuwa akiwaelekeza watu wa Israeli kwenye Nchi ya Ahadi. Vivyo hivyo, Yeremia alisema: “Aa, Bwana [Yehova]! tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Hali Yehova alijibu: “Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru.”—Yer. 1:6, 7.
7. Ni jambo la maana kufikiria ulizo gani, na kitu gani kinachoonyesha kwamba tegemezo la Jehova linatosha?
7 Hata tukijisikia hatuna elimu kama vile mitume, au wenye ulimi mzito kama Musa, au wachanga mno kama Yeremia, kwa kweli ulizo ni, Je! sisi tunayo tamaa ya kushiriki katika utumishi wa Yehova? Ikiwa ndivyo, basi twaweza kuwa na uhakika wa kwamba Yehova atatoa mazoezi, nguvu na tegemezo kusudi tuweze kushiriki katika kazi ya kufundisha na kufanya wanafunzi ambayo Yesu aliamuru lazima ifanywe na ambayo ingali ikifanywa katika huu wakati wa mwisho kwa kadiri isiyo na kifani sasa. Vijana na wazee, zaidi ya milioni moja na mia sita elfu wenye nguvu, wanashiriki sasa katika utendaji huu wa huduma katika nchi 208 na vikundi vya visiwa vya ulimwengu. Lakini mwisho wa kazi hii unakaribia kwa kasi nao wafanya kazi zaidi wanahitajiwa. Je! wewe utashiriki? (Mt. 9:37; 10:23) Ikiwa ungependa kuuongeza uwezo wako kama msemaji na mwalimu wa habari njema, utafurahia kuangalia namna Yehova anavyotoa njia.—2 Kor. 3:5.
MAZOEZI YA NYUMBANI
8. Je! ni msaada gani wa Maandiko wa kuzoezea vijana kumsifu Yehova?
8 Mazoezi kwa ajili ya utumishi wa Yehova yanaanzia nyumbani, kuanzia hata utotoni. (2 Tim. 3:14, 15) Yesu aliwakumbusha wakuu wa makuhani na waandishi: “Hamkupata kusoma, Kwa vinywa vya watoto wachanga na wanyonyao umekamilisha sifa?” (Mt. 21:15, 16) Hii inahitaji msaada mwingi na kutiwa moyo na wazazi. Lazima Yesu awe alipata mazoezi ya ajabu ya nyumbani, yakimfahamisha na Maandiko na imani katika hayo, hivi kwamba wakati alipokuwa mwenye umri wa miaka kumi na miwili tu hata waalimu hekaluni walistaajabishwa na ufahamu wake na majibu. (Luka 2:47) Vivyo hivyo leo jamaa za Kikristo zinatiwa moyo kujifunza na kusoma pamoja wakitazamia kuwafundisha watoto wao katika njia za Yehova.
9. Kwa sababu gani usomaji wa Biblia ni wa maana?
9 Neno la Yehova lina uongozi wa maisha, na kwa hiyo ni vema kuliona kama la maana katika mazungumzo yetu ya jamaa. Kwa kuwa Yehova mwenyewe aliongoza kuandikwa kwa mawazo lililo nayo, linatupa maoni yake juu ya kazi za bure na zifaazo na kutoa uongozi mzuri katika usemi wenye kujenga na wenye maana. Wengi wa mashahidi wa Yehova wanafurahia usomaji wa Biblia wa kawaida wa jamaa pamoja. Wanaona kwamba hauendelezi tu uwezo wao wa kusoma na kusema, lakini, hata la maana zaidi, unaitia imani yao nguvu na ufahamu wa makusudi ya Yehova nao unawasaidia watoto wao waanze kuenenda inavyofaa katika maisha, wakiwa na tamaa ya kuishiriki kweli na wengine.
10. Ni uwezo gani upaswao kukuzwa, na kwa njia gani?
10 Lakini kusoma tu hakutoshi. Imetupasa tupendezwe na kushiriki katika kazi ya kueneza injili chini ya uongozi wa Yesu, na ni muhimu kuyakumbuka tunayoyasoma kusudi tuweze kuyapitisha kwa wengine. Hii inachukua fikira nyingi na kurudia-rudia. Je! unasema na wengine juu ya mambo unayoyasoma? Kwa sababu gani usiifanye kuwa kawaida kuzungumza na jamaa yako mambo ya Maandiko na yenye kujenga unayoyaona? Watu walio wengi ni wenye shughuli nyingi siku hizi, na si wote wanaopata wakati mwingi wa kusoma kama wengine, kwa hiyo, nafasi inapopatikana, inafundisha na kufaidi tukiyashiriki tunayojifunza. Je! umeweza kuchagua habari fulani kwa ajili ya mazungumzo ya kawaida ya jamaa wakati ya chakula? Huenda ikachukua jitihada fulani kwa upande wa wazazi kuwatia wote moyo katika jamaa washiriki, lakini ni jambo la ajabu namna gani kuwaona watoto wako wakikuza uwezo wa kusema vizuri, zaidi juu ya mambo ya Maandiko na mengineyo yaliyo ya muhimu katika maisha.—Kut. 12:26, 27; Mit. 4:1, 4.
11. Vyanzo vingine vizuri kwa mazungumzo ya Maandiko ni gani?
11 Chanzo kizuri cha habari kwa mazungumzo ya jamaa chaweza kupatikana katika mikutano ya kila juma ya mashahidi wa Yehova. Jaribuni kuyarudia yaliyotolewa. Au mwaweza kufurahia kuzizungumza makala mbalimbali zilizomo katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Awake! Nyuma ya kusoma makala fulani, ieleze jamaa yako mambo mbalimbali uliyoyaona yenye kupendeza. Vile vile jamaa nyingi zinafanya mazoea ya kuzungumza andiko na maelezo ya siku kama yanavyopatikana katika Yearbook of Jehovah’s Witnesses. Lakini usiyaache mazungumzo yaelekee upande mmoja kwa wazazi. Watie watoto wako moyo watoe maelezo juu ya habari ambayo huenda mnasoma, au juu ya andiko la siku. Au ujaribu kuwagawia jambo fulani lenye kuwapendeza zaidi wawezalo kurudia kuliangalia pamoja na jamaa kusudi wafaidike kutokana na maono na kujisikia hata wao wanashiriki.
12. Ndugu mzee aliwezeshwaje kusema kwa uhuru juu ya habari za Biblia?
12 Mazoezi yanatokeza maendeleo. Hii ilikuwa kweli kwa habari ya shahidi wa Yehova mzee aliyetumia miaka mingi akitembelea makundi kama mwangalizi wa mzunguko kuyajenga kwa kiroho. Kwa muda wa miaka mingi aliukuza uwezo wa kutoa maelezo akifikiri sana juu ya mambo mengi mbalimbali ya Maandiko. Haukuwa ugumu kwake kujibu ulizo la Biblia kwa urefu sana na kwa maelezo mengi yenye kupendeza wakati wo wote, lakini ilikuwa ni kwa sababu alikuwa ameweka wakati katika funzo la faragha kisha kuyarudia aliyokuwa amejifunza, akifanya hivyo mara kwa mara katika mazungumzo ya faragha, juu ya mafunzo ya Biblia na vile vile katika hotuba za watu wote.
13. Twaweza kuisaidia jamaa yetu ‘kufundishwa na Yehova’ kwa njia gani, na hii itawafaidije wote?
13 Je! wewe waweza kufanya lile lile? Namna gani juu ya watoto wako? Je! wanaweza kueleza kwa maneno machache zaidi yale wanayoyaamini juu ya habari mbalimbali za Biblia? Watu walio wengi wanayafurahia mambo wanayoyafanya vema, kwa hiyo kwa msaada wako na kwa kukuza mazungumzo ya jamaa yenye kujenga, jamaa yako yote yaweza kufanya maendeleo katika uwezo wa kufikiri na kusema. Uwezo huo, nao, huenda ukatufaa kusaidia wengine katika njia ielekeayo kwenye uzima wa milele. (Mit. 15:2) Jaribu kuifanya kawaida ya kuzungumza juu ya kweli za Maandiko na jamaa yako kila siku, hivyo ukiiongeza imani yao katika Yehova na upendo wao kwa makusudi yake. Kisha nao vile vile watatamani kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi chini ya uongozi wa Yesu. Kwa njia hii itakuwa kweli juu ya watoto wako kama ilivyo juu ya wale ambao Yehova anawakubali kama “watoto”: “Watoto wako wote watafundishwa na [Yehova]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.”—Isa. 54:13.
MAFUNDISHO YA KUNDI
14. (a) Nini kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? (b) Nani wawezao kufaidika, na wapi?
14 Mbali na kutia moyo juu ya mazoezi hayo mazuri ya jamaa, makundi ya mashahidi wa Yehova yanatoa mafundisho ya kila juma yakiwa na kusudi la kufundisha kwa ajili ya utumishi wa huduma. Paulo alimtia Timotheo moyo awe “mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli,” na moyo unaofanana na huo wanapewa vijana leo. (2 Tim. 2:15) Mpango wa kutokeza ambao Yehova ameufanya kupitia kwa tengenezo lake awasaidie wote wenye kupendezwa wawe wanaoistahili sana huduma ya “habari njema” ndiyo Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Taratibu hii ya kila juma ya mafundisho imetayarishwa na Watch Tower Society katika makundi zaidi ya 28,000 ya mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Watu wote wanaotaka wazoezwe na Yehova kwa ajili ya huduma ya shambani watafaidika kutokana na mpango huu wenye mafundisho, shukrani kwa mazoezi yanayoendelea kutolewa nao.—Mit. 4:18.
15. (a) Ubora wa mpango wa shule unaonyeshwaje? (b) Imekuwa na matokeo gani?
15 Zijapokuwa hazipatikani tarakimu rasmi za hesabu iliyoandikishwa ulimwenguni pote, hudhurio la wastani penye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika United States siku hizi inapita 100 kwa mia ya wale wanaoshiriki katika huduma ya shambani. Hii ingeonyesha kwamba sasa wako watu zaidi ya milioni moja na mia sita elfu katika sehemu zote za ulimwengu wanaopokea mazoezi katika kusema juu ya habari za Biblia ili kuwatayarisha kwa ajili ya utumishi wa huduma. Je! kuna taratibu nyingine yo yote ya shule inayohudhuriwa na wengi hivyo kwa ajili ya mazoezi katika huduma ya Kikristo? Je! kuna shule nyingine yo yote iliyowatokeza wasemaji wa hadhara wengi hivyo ulimwenguni pote au waalimu wengi hivyo wenye matokeo wa Neno la Mungu? Mnamo mwaka mmoja tu wa karibuni, hotuba za Biblia 1,190,748 zilitolewa na watu waliozoezwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Tunayo sababu nzuri kuwa wenye shukrani kwa pendeleo linalotolewa kwa wote wanaoshirikiana na makundi ya mashahidi wa Yehova kuwa na sehemu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.
16. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inatoa faida gani tatu?
16 Ikiwa wewe hufahamiani na taratibu hii ya mazoezi ya huduma, wakaribishwa uhudhurie penye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la mahali pako kusudi uufurahie mpango wake wenye mafundisho bila ya malipo. Si lazima uwe mmoja wa mashahidi wa Yehova ili ufanye hivyo. Hata wale wasioandikishwa katika shule wanaweza kufaidika kwa njia tatu. Namna gani hivyo? Kwanza, kuna mpango wa kila juma wa kusoma Biblia, pamoja na habari ya ziada kwa funzo la nyumbani inayopatikana kwa wahudhuriaji wote. Halafu, kuna shule yenyewe pamoja na mpango wake wa kila juma wa hotuba tano za Biblia zinazotayarishwa na watu waliandikishwa katika shule hii, vijana na wazee vile vile, wanaume na wanawake. Hotuba hizi zinafuatana na mashauri yenye msaada kwa maendeleo yanayotolewa na mhudumu aliyegawiwa kuiongoza taratibu hii. Mwishoni, kama wajuavyo wale walioandikishwa katika shule, kuna nafasi nyingi za kutumia habari iliyogawiwa za kuijenga imani ya watu wengine.
17. Je! habari kutoka Shule ya Huduma yaweza kutumiwa katika utumishi wa shambani? Eleza.
17 Shahidi mmoja katika Japan alitayarisha hotuba juu ya habari “Watu wa Mungu Waagizwa Watoke katika Babeli.” (Ufu. 18:4) Mwanamke huyu aliamua ingekuwa vema kurudia kuiangalia habari na mtu aliyemfahamu aliyekuwa mshiriki wa kanisa aone ataitikiaje. Kwa hiyo akafanya ziara ya pekee naye akafanya mazoezi kwa ajili ya mtu huyu. Kama matokeo, mwanamke huyo akapendezwa sana na ujumbe wa Biblia naye akakubali kuwa na funzo la nyumbani la Biblia.
18. Nini kinachokaziwa katika taratibu ya shule, na lengo likiwa nini?
18 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inaikazia Biblia kama chanzo chetu cha maagizo ya kimungu. Inakazia fikira kusaidia watu wote wanaopendezwa wawe wenye matokeo katika kufundisha jamaa zao wenyewe Neno la Mungu na vile vile wengine. (Ebr. 5:12) Inatilia mkazo uhakika wa kwamba haitupasi tuitegemee hekima yetu wenyewe katika kufundisha wengine, bali, Neno la Mungu, linalosimuliwa vema kama “neno la uzima.”—Flp. 2:16.
19. (a) Ni namna gani yenye matokeo ya kufundishia aliyoiweka Yesu? (b) Kwa sababu gani hakupaswi kukosa elimu ya kidunia kumzuie mtu asiyashiriki mazoezi haya?
19 Namna ya kufundisha inayoshauriwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni sawa na aliyoitumia Yesu—tegemeo lake juu ya Neno la Mungu lenye kuamuru, wepesi ambao kwao alizungumza, na matumizi yake ya mifano. Uhakika wa kwamba wepesi ni ufunguo wa kufundisha kwenye matokeo unawatia wengi moyo. Kama Paulo alivyoeleza, sio walioelimishwa sana wala wale “wenye hekima ya mwilini” aliowaita Mungu, “si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima . . . Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu.” (1 Kor. 1:26-31) Kwa hiyo kukosa elimu ya kidunia hakupaswi kumzuie mtu asijiandikishe katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ama asiishiriki kweli na wengine.
20. Kitu gani kilichokuwa cha muhimu kwa Sulemani ili kutumia maneno yapendezayo katika kuwafundisha wengine kweli?
20 Kuwa mwenye matokeo katika huduma kunachukua jitihada kwa kila mtu. Hata juu ya Mfalme Sulemani iliandikwa: “Kwa sababu huyo Mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa; naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.” Wale walioandikishwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi wana tamaa ya namna ile ile ya kufundisha wote wanaoitafuta kweli Neno la Yehova. Wanafahamu kwamba hii inachukua uchunguzi mwingi sana na funzo la Maandiko kusudi wayapate maneno yapendezayo yatakayoufanya ujumbe wao wenye kupendeza na wenye kuwafundisha wasikiaji wao vile vile. Kama Sulemani alivyochunguza, maneno hayo yaliyochaguliwa vizuri yanaweza kuwa yenye nguvu kama mchokoo katika kuwaongoza watu katika njia ya uzima.—Mhu. 12:9-11.
21. Imetupasa tuzungumze namna gani na jamaa zetu, lakini imetupasa tuepuke kitu gani?
21 Ikiwa mapendezi yetu, kama ya Sulemani, ni kutafuta na kutumia maneno manyofu yapendezayo ya kweli, basi yamepaswa yageuze namna tunavyosema kila siku. Yamepaswa yageuze mazungumzo yetu na jamaa yetu na rafiki zetu, kazini na katika huduma ya shambani, kwa sababu haiwapasi Wakristo kuwa na kanuni mbili za usemi. Akina baba wanaambiwa wasiwe ‘wanawachokoza watoto wao.’ Wake wanaambiwa wawe na ‘ustahifu’ kwa waume zao, watoto ‘kuheshimu baba yao na mama.’ (Efe. 4:31–5:4, 33; 6:2-4; Tito 2:7, 8) Kwa sababu gani wo wote wazungumze kwa njia inayohuzunisha jamaa, ama kupendezwa na kueneza porojo, ama kufurahia kusema maneno yenye kutia uchungu? Kama vile Yesu alivyoeleza: “Vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi. Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati, wivi, ushuhuda wa uongo, na matukano; hayo ndiyo yamtiayo mtu unajisi.”—Mt. 15:18-20.
22. Moyo wetu waweza kuvutwa kwa njia gani tuseme mambo yenye kujenga?
22 Tofauti yake yenyewe ni kweli vile vile. Tukiweka mioyoni mwetu habari yenye kujenga, yenye kuitia imani nguvu inayotolewa kama ‘chakula cha kiroho katika majira yafaayo’ na jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” basi mambo ambayo moyo wetu utatuvuta kuyasema yatakuwa maneno ya uzima yanayoendeleza kuponya, amani, furaha na kicho kwa Muumba wetu. Je! hii ndiyo hali ya moyoni ambayo ninyi wazazi mnajenga ndani ya watoto wenu? Je! ndiyo hali unayotia nguvu ndani yako kwa mpango wa kawaida wa kusoma Biblia na funzo? Ikiwa ndivyo, wewe unafuata mwendo utakaojenga ndani yako ufahamu mzuri wa makusudi ya ajabu ya Yehova na utakaokuwezesha kushiriki katika ‘kulijenga kundi’ na katika kuongezea maisha yenye furaha ya jamaa vile vile.—1 Kor. 14:12; Zab. 19:14.
23. Ni katika kazi gani ambayo ingali inaendelea imetupasa tutamani kushiriki, na kwa njia gani?
23 Ikiwa ni tamaa yako kuweza kusema maneno yanayopendeza ya kweli kama alivyofanya Sulemani, Yehova atakusaidia kufanya hivyo. Onyesha hivyo kwa namna unavyosema kwa jamaa yako mwenyewe, na kwa kutoa shukrani kwa ajili ya mambo ambayo Yehova ametoa. (Efe. 5:20) Elekeza mioyo na akili za jamaa yako na rafiki kwenye Muumba unaposema, “si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na [roho].” (1 Kor. 2:13) Kwa kufanya hivyo wewe na jamaa yako mtavutwa kushiriki katika kazi iliyo kuu ya kueneza injili iliyotabiriwa na mnenaji wa Yehova wa kweli, Yesu, kazi ambayo sasa inatimilizwa ulimwenguni pote. Kwa kadiri isiyoonekana wakati mwingine wo wote mbele Yehova anawatayarisha watu wake wakafanye watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi. Wewe vile vile waweza kushiriki katika kazi hii ya unabii kwa kuukubali ukaribishaji wa mtunga zaburi: “Kila mwenye pumzi na amsifu [Yehova]. Haleluya.”—Zab. 150:6.
—Kutoka The Watchtower, Sept. 1, 1973.
[Picha katika ukurasa wa 113]
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inawatayarisha watu wote wenye kupendezwa kufundisha jamaa zao wenyewe Neno la Mungu na vile vile wengine
Kuna watu zaidi ya 1,600,000 wanaohudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, vijana na wazee vile vile, wanaume na wanawake