Watawala wa Dunia kwa Miaka Elfu
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1. Ni kwa muda mrefu namna gani ambavyo wanadamu wamejaribu kujitawala, kwa matokeo gani?
DUNIA imeona watawala wengi wakija na kwenda. Watawala na watawaliwa vile vile wamejaribu kila namna ya serikali ya kibinadamu iwezayo kuwazikana, lakini hakuna yo yote iliyowaletea watu faraja ya kweli na furaha.
2, 3. (a) Ni nani ambaye kwa kweli ametawala, nasi twajuaje yeye ni mbaya? (b) Ni maandiko gani yanayohakikisha hili?
2 Lakini, kwa kweli, kwa kipindi hiki kirefu cha wakati kumekuwako mtawala mmoja juu ya dunia ambaye amezitawala taratibu hizi zote za mambo za ulimwengu. Kwa njia gani? Kwa kuutoa uongozi wake kwa wanadamu wasiokamilika waliozifanyiza taratibu hizo. Twaweza kuona kama mtawala huyu amekuwa mwema au mbaya kwa kuifuata kanuni ya Biblia ya sababu na matokeo: “Wakati ambapo wenye haki ni wenye mamlaka watu hufurahi, lakini wanapiga kite waovu washikapo cheo.”—Mit. 29:2, The New English Bible.
3 Ndiyo, kwa miaka 6,000 watu wamepiga kite kwa maana wametawaliwa kwa njia ya kutoonekana na anayeitwa na Maandiko “mungu wa dunia hii,” na “mkuu wa ulimwengu,” ambaye ndiye adui ya Mungu. (2. Kor. 4:4; Yohana 12:31; 14:30) Biblia yamsema yeye kuwa Shetani Ibilisi. (Ufu. 12:9) Utawala juu ya serikali za dunia ulionyeshwa kuwa wake wakati alipomtolea Yesu Kristo falme zote za ulimwengu kama tuzo kwa tendo la kumwabudu yeye.—Mt. 4:8-10.
4. Kwa sababu gani leo twaweza kujipa moyo?
4 Sasa, watu wanaotaka amani, uzima na uhuru wanaweza kutazamia kitu kilicho bora kuliko hali iliyopo. Wanaweza wakajipa moyo kwa sababu ya kweli ya mithali nyingine ya Biblia: “Waovu wakiongezeka, maasi huongezeka; bali wenye haki watayatazama maanguko yao.” Leo, uovu unaenea pote kwa njia ya kuogofya. Lakini kikomo chake ki karibu.—Mit. 29:16.
5. Je! wakati wa utawala mbovu umekuwa mrefu kupita kadiri?
5 Miaka 6,000 ya historia ya kibinadamu yakaribia mwisho wake, na kwa wanadamu, huo waelekea kuwa muda mrefu sana. Lakini kwa Mtawala wa Ulimwengu Wote, na kwa wakati wa ulimwengu wote, miaka 6,000 ni kama siku chache tu, au saa. Lakini muda huu umewapa watu nafasi ya kutosha wauone ubatili wa jitihada za mwanadamu mwenyewe na haja ya ufalme wa Mungu, ambao ameuandaa na ambao u tayari kuchukua mahali pa utawala wote mwingine wa dunia.—2 Pet. 3:8, 9.
6. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya wale watakaoitawala dunia kwa miaka 1,000, na kwa sababu gani?
6 Kwa muda wa miaka 1,000 ufalme wa Mungu wa Kimasihi utayaondoa matokeo yote mabaya ya utawala wa dunia wa miaka 6,000 wa Shetani. Kristo Yesu ndiye Mfalme, lakini pamoja naye anao wafalme washirika 144,000. Wao ni watawala wa namna gani? Twawezaje kuwa na hakika wao hawataacha upotovu uingie serikalini? (Kwa maana upotovu mdogo kutoka kanuni za haki mwishowe waweza kuenea na kupotosha serikali nzima na watu wake. “Chachu kidogo huchachua donge zima.” [Gal. 5:9]) Watawala hawa wanastahili namna gani vyeo hivyo vya muhimu?
7-10. (a) Viti vya enzi alivyoviona Yohana vilikuwa mahali gani, na ni wangapi waliokuwa huko? (b) Ni siku gani iliyotazamiwa kwa muda mrefu iliyokuwa ikianza hapa?
7 Bila shaka, Yesu Kristo anapendezwa sana na ubora wa wafalme atakaokuwa nao. Wafalme hawa wanatajwa mara nyingi katika njozi aliyompa mtume wake Yohana. Yohana anasema hivi:
8 “Nami niliviona viti vya enzi, na walikuwako wale walioketi juu yake, nao walipewa nguvu ya kuhukumu. Naam, niliziona nafsi za wale waliokatwa kwa shoka kwa ushuhuda walioutoa kwa Yesu na kwa kusema juu ya Mungu, na wale ambao hawakuwa wameabudu wala mnyama wa mwitu wala mfano wake na ambao hawakuwa wameipokea alama juu ya kipaji cha uso wao na juu ya mkono wao. Nao wakawa hai na wakatawala kama wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu. (Mabaki ya wafu hayakuwa hai mpaka miaka elfu ilipomalizika.) Huu ndio ufufuo wa kwanza. Mwenye furaha na mtakatifu ni ye yote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hawa mauti ya pili haina mamlaka, lakini watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala kama wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.”—Ufu. 20:4-6, NW.
9 Viti vya enzi ambavyo Yohana aliviona vilikuwa huko juu mbinguni, siyo duniani, kwa maana kiti cha enzi cha Kristo kiko mbinguni. (Ufu. 3:21) Navyo havikuwa visivyojulikana hesabu yavyo. Hesabu ilikuwa 144,000, ili ilingane na Waisraeli wa kiroho 144,000 waliotiwa muhuri kwa “muhuri ya Mungu aliye hai” na “wamfuatao Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] kila aendako.” (Ufu. 7:1-8; 14:1-5) Hapa Yohana aliuona mwanzo wa siku iliyo tukufu ya hukumu ya kipindi cha miaka 1,000. Siku hii ilizungumzwa kwa Baraza ya Areopago, Athene, zaidi ya karne kumi na tisa zilizopita, kwa maneno haya:
10 “[Mungu] ameiimarisha siku ambayo atafanya ulimwengu uhukumiwe, na kuhukumiwa kwa haki, na mtu wa uchaguzi wake yeye; juu ya hili ametoa uhakikisho kwa wote kwa kumfufua huyo kwa wafu.”—Matendo 17:31, NE (1970).
“WALIOKATWA KWA SHOKA”
11. Kwa sababu gani 144,000 ‘walikatwa kwa shoka’?
11 Twawezaje kuwa na hakika kwamba hawa watawala 144,000 watakuwa waaminifu kwa kutumia haki sawa na Kiongozi wao Mfalme wa Kimasihi Yesu Kristo? Njozi yatuambia kwamba mbele ya ufufuo wao wakawe wafalme, ‘walikatwa kwa shoka.’ Kwa sababu gani? “Kwa ushuhuda walioutoa kwa Yesu na kwa kusema juu ya Mungu.” (Ufu. 20:4, NW) Wao, kama Yesu, waliupata ushindi juu ya ulimwengu kwa kukataa kuuvunja uaminifu wao kwa Mungu. Waliendelea kutoa ushuhuda kwa ajili ya ufalme wa Mungu, kwa ajili ya Yesu kama Mfalme wake na kwa ajili ya Mungu kama Muumba wake, na kwa ajili ya utawala wake unaokuja wa dunia. Ni vifo vyao tu viwezavyo kuukomesha utoaji wao mwaminifu wa ushuhuda.
12. Je! kila mmoja wa waliotiwa mafuta ‘alikatwa kwa shoka’ kwa njia halisi?
12 Andiko halimaanishi kwamba kila mmoja wa 144,000 waliotazamia kuwa wafalme angekatwa kwa shoka la halisi, au kukatwa kichwa. Mtume Yakobo aliuawa kwa upanga kwa amri ya Herode Agrippa wa Kwanza. (Matendo 12:1, 2) Mapokeo yanasema kwamba mtume Paulo alikatwa kichwa huko Rumi, Italia. (2 Tim. 4:6-8) Wengine waliuawa kwa njia mbalimbali, nao wengine wakafa kwa njia “ya kawaida.”
13. Je! ilikuwa lazima hawa waliotazamia kuwa wafalme wafe? Kwa sababu gani?
13 Hata hivyo, iliwapasa wote kuwa waaminifu hata kufa. (Ufu. 2:10) Iliwapasa kufa ili wapate mageuzi ya maumbile kutoka hali ya kibinadamu kuwa “ya kimungu” (yenye mfano wa Mungu, ya kiroho) kwa kufufuliwa, kama alivyopata Kristo. (2 Pet. 1:4, NW) Ilikuwa lazima wafe “kifo kama chake” ili ‘kufikia ufufuo wa mapema kutoka kwa wafu.’ (Flp. 3:10, 11, NW) Kwa hiyo hawafi kwa ajili ya dhambi zao. Kifo chao kwa sababu hiyo chahesabiwa kama “cha dhabihu” pamoja na Kristo. Paulo anaandika hivi: “Kama tulivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika tutaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake.”—Rum. 6:5.
14. N’nini kilichofananishwa na “shoka”?
14 Basi, ni kwa njia gani wawezavyo kusemwa “walikatwa kwa shoka”? Katika Milki ya Kirumi uwezo wa kuua ulifananishwa na shoka lililofungwa katikati ya fito, zilizoitwa fasces. Benito Mussolini aliieneza alama hii mnamo utawala wake wa mtu mmoja tu katika Italia.
15. Basi, ni kwa njia gani ambavyo mataifa ya kisiasa ‘yanawakata’ warithi wa Ufalme?
15 Kwa hiyo, kwa kweli mataifa ya kisiasa yawakata warithi wa Ufalme 144,000 kwa kuwahukumu kama wasiostahili kuishi chini ya mamlaka yake. Yanawahukumia kifo, kana kwamba ilikuwa. Hii ni kwa sababu ulimwengu unawachukia. (Yohana 17:14; Mt. 24:9) Wao ni “wasiotamanika” machoni pa viongozi wa kidini na wa kisiasa wa ulimwengu, sawa na walivyokuwa mitume.—1 Kor. 4:13.
HAWAMWABUDU “MNYAMA WA MWITU”
16. Ni sababu gani nyingine ambayo mataifa yalikuwa nayo kwa ‘kuwakata’ mashahidi hawa?
16 Sisi vile vile twaweza kuwa na uhakika hawa 144,000 kama wafalme wataendelea kuwa waaminifu kwa kuangalia sababu nyingine iliyofanya ‘wakatwe kwa shoka.’ Ni kwa sababu “hawakuwa wameabudu wala mnyama wa mwitu wala mfano wake” wala “hawakuwa wameipokea alama juu ya kipaji cha uso wao na juu ya mkono wao.”—Ufu. 20:4, NW.
17. Je! warithi wa Ufalme walikuwa wamejidukiza katika siasa, au sababu ya ‘kukatwa’ huko ni nini?
17 Hivyo sababu ya ‘kukatwa kwa shoka’ haikuwa utendaji wo wote wa kidini au kuasi serikali kwa ushupavu wala kujidukiza ko kote katika siasa. Ilikuwa kwa sababu hawakuwamo katika mambo ya kisiasa katika misemo yake mbalimbali na matendo duniani mwote. Wao walikuwa upande wa ufalme wa Mungu kama tumaini la pekee la wanadamu. Wala mabaki ya warithi hawa wa Ufalme katika hii karne ya 20 hawakuliabudu tengenezo la Umoja wa Mataifa kwa ajili ya amani ya ulimwengu na usalama.
18. Ni namna gani ambavyo waliotazamia kuwa wafalme hawakuwa na “alama juu ya kipaji cha uso wao na juu ya mkono wao”?
18 ‘Kutoyaabudu’ mataifa ya kisiasa au “mfano” wao, Umoja wa Mataifa, kungemaanisha kutokuondoa tumaini na utii kwa ufalme wa Mungu na kutoviweka katika mawakili hawa walioundwa na mwanadamu. Bali, ndugu hawa wa kiroho wa Kristo wanaendelea kuutangaza Ufalme. Wao hawana “alama juu ya kipaji cha uso wao na juu ya mkono wao.” Yaani, wao hawana alama kama watumwa wa mataifa nao hawajitii kwa bidii katika kuendeleza utendaji wao wa kilimwengu, ulio mbaya mara nyingi. Wao hawakimbilii vyeo vya kisiasa, au kufanya uchaguzi wa wanasiasa. Wanakataa kushiriki katika vita vyake vya damu.
19. Ni wakati gani peke yake mashahidi hawa wa Kikristo wanapokataa kujipatanisha na amri za serikali ya kisiasa?
19 Lakini mashahidi hawa wa Kikristo wa enzi yote ya Mungu hawayapingi mataifa ya kisiasa katika mambo haya hata kidogo. Wao ‘wanamlipa Kaisari ya Kaisari’ kwa kujipatanisha na sheria za maandishi na za kodi na kwa kuzitii sheria zote za nchi zisizopingana na sheria za Mungu kama zilivyotajwa katika Biblia. Ni wakati tu “Kaisari” anapodai kile kilicho cha Mungu, yaani, ibada, au cho chote kinachowaondoa wasiikubali enzi yote ya Yehova, kwamba lazima wakatae, wakichagua ‘kumtii Mungu kama mtawala kuliko wanadamu.’ Hii ndiyo inayowafanya ‘wakatwe kwa shoka’ kwa njia ya mfano na nyakati nyingine kwa njia halisi.—Mt. 22:21; Matendo 5:29, NW.
20. Je! warithi wa Ufalme wanatafuta mateso au ‘kukatwa kwa shoka’?
20 Huku ‘kukatwa kwa shoka’ si jambo linalowapata kwa kupenda kwao. Wao hawajitafutii mateso au kutaka kufia dini. Hata hivyo, wao wanajua mapema kwamba wataichochea chuki ya ulimwengu kwa kutoa ushuhuda juu ya Yesu kama Kristo na Mfalme na kuzungumza juu ya Mungu kama mtawala afaaye wa ulimwengu wote (kutia na dunia yetu). Wao wanajua lazima wazifuate nyayo za Kristo hata kifo cha ukamilifu kwa Mungu, kama chake kilivyokuwa.—1 Pet. 2:21.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.