Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 7/15 kur. 321-334
  • Kukombolewa Kujako na “Shoka” Lenye Kupinga Dini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukombolewa Kujako na “Shoka” Lenye Kupinga Dini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • CHOMBO CHA KISASA CHENYE KUPINGA DINI
  • WALIOFANANISHWA NA SENAKERIBU NA HEZEKIA
  • JARIBIO LA “SHOKA” LENYE KUPINGA DINI
  • KUKOMBOLEWA NA VITA KATIKA HAR-MAGEDONI
  • “Shoka” na Mwenye Kulitumia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Msiogope Ashuru
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Malaika wa Yehova Alimlinda Hezekia
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • No Help From This World
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 7/15 kur. 321-334

Kukombolewa Kujako na “Shoka” Lenye Kupinga Dini

1. Ni jambo gani la hakika juu la dini litaonyeshwa kwa watu wengi, na kwa njia gani?

JAMBO moja lililo gumu kwa watu wengi leo kufahamu ni kwamba kunaweza kuwa na kuna dini moja tu ya kweli. Kwa sababu gani wanapinga uhakika huo? Ni kwa sababu hiyo ingemaanisha dini nyingine zote ni za uongo, na hiyo ingetia ndani dini yao wenyewe. Kwa hiyo, wanapaswa kuonyeshwa ukweli kwa nguvu. Jambo hilo litafanywa karibuni, kwa maana dini zote za uongo zitafutiliwa mbali wakati huo katikati ya dhiki ya ulimwengu iliyo kubwa kupita zote, na ni ile dini moja tu ya kweli itakayookoka. Itakombolewa katika uharibifu wa dini ulio mkubwa zaidi katika historia yote ya kibinadamu.

2. Sasa lazima Yehova afanye nini ndio aondoe vita vyote vya kidini?

2 Biblia Takatifu inaonyesha ni nani Wa Pekee anayepaswa kuabudiwa na wanadamu wote? Ni Mungu Aliye Juu Zaidi na Mwenye Nguvu Zote, aitwaye Yehova. (Tazama Kutoka 6:3; Zaburi 83:18; Isaya 12:2 na 26:4 katika Union Version.) Kwa vile Mungu aliye hai na wa kweli ni mmoja, kwaweza kuwako dini moja tu inayofaa, dini safi isiyo na taka ambayo Yeye ameieleza wazi katika Biblia Takatifu. (Tazama Yakobo 1:27.) Wanadamu walikuwa na dini moja safi hapo mwanzoni. Sasa wakati umefika wa Mungu Mwenye Nguvu Zote kuunganisha wanadamu wote katika ibada moja Yake iliyo sawa na kuondoa vita vyote vya kidini kwa njia hiyo.​—⁠Sef. 3:8, 9; Efe. 1:9, 10; 4:4-6.

3. Ni kwa njia gani wakati wa utawala wa Mfalme Hezekia ndio uliokuwa wa hatari kwa Ufalme wa Israeli na Ufalme wa Yuda pia?

3 Uharibifu wa dini yote ya uongo ulionyeshwa mapema katika karne ya nane kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Wakati huo Milki ya Ashuru, mji wake mkuu ukiwa Ninawi, ndiyo iliyokuwa mamlaka ya ulimwengu. Milki hiyo ilipoendelea kupanuka, Ufalme wa Israeli wa makabila kumi, wenye mji mkuu Samaria, uliharibiwa nao Ufalme wa Yuda ulio jirani wa makabila mawili, wenye mji mkuu Yerusalemu, ukashambuliwa vikali sana. Wakati wa hatari kwa falme hizo mbili ulifika wakati wa utawala wa Mfalme Hezekia wa Yerusalemu, aliyeanza kutawala mwaka wa 745 K.W.K. Miaka mitano baadaye, au katika mwaka wa 740 K.W.K., Ufalme wa Israeli wa makabila kumi uliangushwa na Waashuru wajeuri. Ilionekana kwamba Ufalme wa Yuda ulio jirani ndio ungefuata kuangushwa, tena karibuni sana! Lakini, miaka minane ilipita, Hezekia akawa bado amekalia kiti cha enzi Yerusalemu. Pia, Senakeribu, mwana wa Sargon wa Pili, alikuwa amepata kuwa mfalme wa Milki ya Ashuru yenye kupanuka.

4. Kwa sababu gani kushindwa kwa mataifa, kutia na taifa la Israeli, kulikuwa shughuli ya kupinga dini ya Milki ya Ashuru​—⁠kwa njia isiyo ya moja kwa moja?

4 Nasaba ya wafalme wa Ashuru iliyohusika kushinda ulimwengu ilifunua wazi uongo wa miungu ya falme na mataifa yaliyoshindwa, kwa maana iliionyesha kuwa si miungu, kuwa ni “miungu isiyofaa kitu.” (Isa. 10:10, 11, NW; 2 Fal. 18:33-35; Isa. 36:18-20 na 37:12, 13) Kushushwa kwa miungu ya mataifa ya kilimwengu kulifikia upeo Samaria ulipopinduliwa pamoja na miungu ya uongo iliyokuwa imechaguliwa badala ya Yehova, Mungu wa babu zao Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Miungu yote hiyo ilishindwa kuokoa kila mmoja taifa lake kutokana na mkono hodari wa Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kwa sababu, kama alivyosema Mfalme Hezekia katika sala kwa Yehova, “hawakuwa miungu, bali kazi ya mikono ya wanadamu.” (Isa. 37:18-20) Kwa kushinda sana hao ‘wasiokuwa miungu’ wa mataifa, Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru ilikuwa na shughuli kubwa sana ya kupinga dini​—⁠kwa njia isiyo ya moja kwa moja.

CHOMBO CHA KISASA CHENYE KUPINGA DINI

5. Ingawa shughuli ya kupinga dini ya Ashuru ilifanyika zamani za kale, kwa sababu gani inahusu siku zetu.

5 Yehova Mungu alikuwa akisaidia shughuli hiyo ya kupinga dini, hasa wakati Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru ilipoupiga Ufalme wa Israeli wenye kuasi imani, ingawa mamlaka hiyo haikujua ilikuwa ikisaidiwa. Yehova alikuwa akiitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama “shoka” na “fimbo” yake ya mfano. (Isa. 10:5, 15) Hilo lilikuwa jambo la zamani za kale, lakini kilichofananishwa kwa unabii lazima kitokee. Lazima kitokee karibuni, katika kizazi chetu. Chombo, “shoka” au “fimbo” ya mfano ambayo Yehova atatumia kuvunja-vunja dini yote ya uongo ni nini? Kama zamani za kale, chombo hicho si sehemu ya tengenezo la Yehova linaloonekana, wala hakimwabudu Yeye kama Mungu mmoja aliye hai na wa kweli. Kitabu cha mwisho cha Biblia chaeleza chombo hicho ni nani. Ufunuo, sura ya kumi na saba, wakionyesha kuwa “mnyama” mwekundu sana mwenye vichwa saba na pembe kumi, aliyepandwa na kahaba wa kidini wa mataifa yote, Babeli Mkuu. Kulingana na Ufunuo 17:7-12, “mnyama” huyo ni Mamlaka ya Ulimwengu ya Nane, tengenezo la mataifa yote la amani na usalama wa ulimwengu, Umoja wa Mataifa.

6. Ni nani anayefananishwa na mwenye kumpanda “mnyama,” na kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo pia inaharibiwa mpandaji anapoharibiwa?

6 Kama inavyoonyeshwa na Ufunuo, “mnyama” huyo atamharibu mwenye kumpanda, “mwanamke” huyo wa mfano ambaye amefanya uasherati kwa njia ya mfano na watawala wote wa kisiasa wa ulimwengu. “Mwanamke” huyo hafananishi kingine ila milki ya ulimwengu ya dini ya uongo ya Kibabeli. Milki hiyo ya kidini yatia ndani Jumuiya ya Wakristo, ambayo ndio mfano wa kisasa wa mwasi dini wa kale, yaani, Ufalme wa Israeli uliokuwa na mji mkuu Samaria. Mpaka leo hii Jumuiya ya Wakristo imekataa kutii amri ya Mungu ya kujitenga na milki ya ulimwengu ya dini ya uongo ya Kibabeli: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.” (Ufu. 18:4, 5) Kwa hiyo, uharibifu utakaompata Babeli Mkuu kwa ujumla utaipata Jumuiya ya Wakristo, sawa na vile uharibifu ulivyoupata Ufalme wa Israeli wenye kuasi imani pamoja na mji wake mkuu wa Samaria.

7, 8. (a) Mtume Yohana anatuonyeshaje kwa ufupi uharibifu wa milki ya ulimwengu ya dini ya uongo? (b) Mbingu zitampa nani utukufu kwa sababu ya uharibifu huo, lakini ni nini kitabaki duniani baada ya kuanza kwa “dhiki kubwa”?

7 Sisi leo twaonyeshwa kidogo jambo litakalofanywa kwa milki ya ulimwengu ya dini ya uongo na “mnyama” mwenye pembe kumi, wakati malaika wa Mungu anapomwambia mtume Yohana hivi: “Na zile pembe kumi ulizoziona ni wafalme kumi, ambao hawajapokea ufalme bado, lakini wapokea mamlaka kama wafalme muda wa saa moja pamoja na yule mnyama [ambaye sasa ni Umoja wa Mataifa]. . . . Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.”​—⁠Ufu. 17:12-16.

8 Yehova atamtumia “mnyama” huyo aliye Umoja wa Mataifa kama “shoka” lake la mfano amharibu Babeli Mkuu, naam, aiharibu Jumuiya ya Wakristo yenye unafiki, tengenezo la kisasa linalolingana na Ufalme wa Israeli wa makabila kumi na mji wake mkuu Samaria,a ingawa Umoja wa Mataifa hautajua unatumiwa na Yehova. Ndiyo sababu sifa ya uharibifu wa Babeli Mkuu wote inapewa kwa Yehova. Kelele itatoka mbinguni kwa nguvu kusema: “Wokovu na utukufu na nguvu zina Bwana Mungu wetu; kwa kuwa hukumu zake ni za kweli na za haki; maana amemhukumu yule kahaba mkuu aliyeiharibu nchi kwa uasherati wake, na kuipatiliza damu ya watumwa wake mkononi mwake.” (Ufu. 19:1, 2) Yehova atakapofikiliza hukumu juu ya kahaba wa kidini wa mataifa yote, Babeli Mkuu, ndipo “dhiki kubwa” iliyotabiriwa itakapoanza, dhiki isiyo na kifani katika historia ya kibinadamu. (Mt. 24:21, 22) “Dhiki” hii haitakwisha baada ya Jumuiya ya Wakristo na sehemu nyingine yote ya Babeli Mkuu kuharibiwa. Bado atakuwako “mnyama” yule mwekundu sana, mwenye vichwa saba na pembe kumi, ambaye ndiye “shoka” la mfano atakalotumia Yehova Mungu kuangusha sehemu zote za milki ya ulimwengu ya dini ya uongo ya Kibabeli.

9. Kwa sababu gani inafaa kuuliza kama Umoja wa Mataifa utakuwa sehemu ya tengenezo la Yehova kwa sababu ya kazi yake ya kufikiliza hukumu, nasi twaweza kupata jibu kwa nani?

9 Hapa, kama katika habari ya Ashuru ya kale, twauliza ulizo hili: Umoja wa Mataifa, ambao ndio “mnyama” huyo, utakuwa sehemu ya tengenezo la Yehova linaloonekana kwa sababu Yeye atautumia kama “shoka” lake? Inafaa tuulize ulizo hilo. Kwa sababu gani? Kwa sababu, huko nyuma katika Desemba wa 1918, ushirika uliotangulia Umoja wa Mataifa, yaani, Ushirika wa Mataifa ulishangiliwa kama “wonyesho wa kisiasa wa ufalme wa Mungu duniani.” Ulishangiliwa na nani? Na Baraza ya Mwungano wa Makanisa ya Kristo katika Amerika (Federal Council of the Churches of Christ in America). Kushindwa kwa Ushirika wa Mataifa kuzuia Vita ya Ulimwengu ya Pili kulifanya kuwe na uhitaji wa kufuatwa kwake na tengenezo la kisasa la ulimwengu, Umoja wa Mataifa. (Ufu. 17:8) Papa wa Rumi ameutangaza kuwa “tumaini la pekee la ulimwengu.” Basi, je! sisi tuseme kwamba Umoja wa Mataifa ni sehemu ya tengenezo linaloonekana la kidunia la Yehova Mungu? Ili tupate jibu, na tuulize nusu ya mataifa yale 144 yaliyo wanachama wa Shirika hilo na yasiyojidai kuwa ya Kikristo. Kwa kadiri wajuavyo, wao hawataki kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova.

10. Baada ya kutumiwa na Yehova kama “shoka,” nia ya tengenezo la “mnyama” itakuwa nini juu Yake, kama inavyoonyeshwa na Ufunuo 17:13, 14?

10 Baada ya Umoja wa Mataifa, ambao ni “mnyama,” kutumiwa na Yehova kama “shoka” lake la kuangushia Babeli Mkuu, tengenezo hilo lililo “mnyama” litakuwa na nia gani juu ya Mwenye kulitumia “shoka”? Je! litakuwa au halitakuwa na nia ya kumpendelea Yehova Mungu na Kristo wake? Ili tupate jibu mapema twauendea unabii wa Biblia. Unabii unaonyesha kwa wazi jinsi mataifa ya kilimwengu yanavyounga mkono kwa umoja tengenezo la mataifa yote la amani na usalama wa ulimwengu. Kwa njia hiyo wanakuwa kikosi chenye umoja wapambane na ufalme wa kimbinguni wa Mwana wa Yehova aliyetiwa mafuta, Yesu Kristo, “Mwana-kondoo wa Mungu.” Ufunuo 17:13, 14 wasema hivi juu ya “mnyama” na “pembe kumi” zake: “Hawa wana shauri moja, nao wampa yule mnyama nguvu zao na mamlaka yao. Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme; na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.”​—⁠Tazama pia Ufunuo 19:19-21; Yohana 1:29.

11. Kwa sababu gani nia hiyo inalingana na ile iliyofuatwa na Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru ilipokwisha kuupindua Samaria?

11 Sasa tumepata jibu la ulizo letu. Humo tumeonyeshwa kwa unabii nia inayofuatwa na “shoka” la mfano atakalotumia Yehova Mungu wakati wa kufikiliza hukumu juu ya Babeli Mkuu. “Shoka” litamgeukia Mtumiaji wake wa kimbinguni na kujaribu kujikuza juu Yake! Kwa kuungana wapigane na Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme aliyetiwa mafuta na Yehova, mataifa yatakuwa yakipigana kwa mpango na Yehova Mungu mwenyewe. Kwa sababu gani? Ili waendelee kuwa na enzi zao za kitaifa duniani. Hiyo italingana kabisa na hatua iliyochukuliwa na “Ashuru” katika karne ya nane kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, “Mwana-kondoo wa Mungu”! Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru ilifuata nia ya kujikuza kwa jeuri baada ya kupindua Samaria na kuhamisha waasi imani wa Kiisraeli waliookoka kuwapeleka kwenye maeneo ya Ashuru.

12. “Shoka” la Ashuru lilitendaje siku za Mfalme Senakeribu, naye kwanza aliutisha Yerusalemu kwa kadiri gani?

12 Zamani hizo “shoka” la mfano lilijipatia utukufu na sifa yote ya kushinda kisha likamgeukia Mwenye kulitumia. Mwendo huo ulifikia upeo wa majivuno na jeuri siku za mtawala Senakeribu wa Ashuru. Kwa kutumia jeshi lake hodari aliishambulia nchi ya Ufalme wa Yuda wa makabila mawili. (2 Fal. 18:9-25) Njia alizopitia akishambulia zimeandikwa vizuri katika Isaya 10:28-32, na hapo panasimulia vile jeshi la Senakeribu lilivyoogofya watu mahali pote lilipokuwa likisonga mbele kwenda hapa na pale bila kupingwa, likiuelekea Yerusalemu juu ya Mlima Sayuni. Bila shaka wakaaji wa mji huo walitusha mioyo jeshi la Ashuru lilipoendelea kusonga likaupita Yerusalemu kwa kuutisha kidogo tu.

13, 14. Senakeribu alijidai kuwa na agizo gani, kusudi la kutoa dai hilo kwa wakaaji wa Yerusalemu lilikuwa nini?

13 Hata hivyo, lengo kubwa la Senakeribu lilikuwa kuuharibu mji mtakatifu ambamo Mfalme Hezekia alikalia ‘kiti cha enzi cha Yehova.’ (1 Nya. 29:23) Kwa hiyo, ili kuwaogofya wakaaji wa Yerusalemu ndiyo wamwasi Mfalme Hezekia kumpa Senakeribu mji huo, wajumbe wenye kufuatana na jeshi kubwa sana la Ashuru walisimama mbele ya kuta za Yerusalemu. Mkuu Mwashuru mwenye kusema Kiebrania alisema waziwazi kwamba Senakeribu alikuwa amepata agizo kutoka kwa Yehova na kwamba ndiye wakili wa Yehova wa kutiisha Yerusalemu. Ili Wayahudi waliokuwa juu ya kuta za Yerusalemu wapate kusikia, mnenaji wa Senakeribu alisema hivi kwa kujitanguliza:

14 “Je! nimepanda mimi, ili kupigana na mahali hapa na kupaangamiza, bila shauri la [Yehova]? [Yehova] ndiye aliyeniambia, Panda upigane na nchi hii na kuiangamiza.”-​—2 Fal. 18:9-25.

15. Kulingana na Isaya 10:15, Senakeribu alikuwa akijitanguliza afanye nini kwa kutisha kuushambulia na kuuharibu Yerusalemu?

15 Kwa hiyo, Yehova alikuwa na sababu kamili za kulifunua kusudi la mfalme wa Ashuru lenye kumkaidi Yeye kwa kumwuliza: “Je! shoka lijisifu juu yake alitumiaye? je! msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti.” (Isa. 10:15) Ndiyo kusema, “shoka” la mfano, Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru sasa itamtumia Yehova Mungu kama chombo chake, yeye ambaye si sanamu ya mti iliyochongwa iabudiwe? Jibu ni Hapana! Lakini mfalme wa Ashuru alikuwa akijitanguliza afanye hivyo kwa kutisha kwamba ataushambulia na kuuharibu Yerusalemu na hekalu lake.

16. Ili kuhakikishia watu Wake kwamba Ashuru isingefaulu, Yehova alisema atafanya nini, kulingana na Isaya 10:16-19?

16 Ili kuwahakikishia watu wake kwamba Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru isingefaulu kujikuza juu ya Yehova, ambaye ndiye Mwenye kulitumia shoka la mfano, Yeye aliendelea kusema hivi: “Kwa hiyo Bwana, [Yehova] wa majeshi, atawapelekea kukonda watu wake walionona [watu wanene na wenye maungo wa Ashuru]; na badala ya utukufu [au, wingi] wake kutawashwa kuteketea kama kuteketea kwa moto. Na mwanga wa Israeli utakuwa ni moto, na Mtakatifu wake atakuwa mwali wa moto; nao utateketeza. na kula mbigili [“magugu,” NW] zake na miiba yake katika siku moja. Naye atauteketeza utukufu wa msitu wake, na wa shamba lake linalositawi, tangu nafsi hata nyama ya mwili, itakuwa kama vile afapo mtu aliye mgonjwa. Na miti ya msitu wake itakayosalia itakuwa michache, hata mtoto ataweza kuihesabu.”-​—⁠Isa. 10:16-19.

17. Ni maulizo gani yanayohusu wakati huo na wakati ujao yanayotokezwa na matumizi ya Yehova ya usemi wa mfano?

17 Yehova wa majeshi alikuwa ndiye ‘Mwanga wa Israeli’ na ‘Mtakatifu wake.’ Kwa hiyo ni jinsi gani angeteketeza vikosi vya nchi kavu vya Senakeribu kama magugu mengi sana na miiba mingi na kukomesha wakuu wa kijeshi wa Ashuru kama miti iliyonyoka ya mwituni au ya bustani? Ni jinsi gani Yehova angepunguza wakuu walio mfano wa miti wa jeshi la Senakaribu hata hesabu ya wenye kubaki iwe ndogo sana kiasi cha kuwezesha mtoto kuiandika kwa kuhesabu vidole vyake kumi?b Pia, ni jinsi gani ulinganifu wa kisasa wa mambo hayo yote utatimizwa na Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote hivi karibuni? Hayo ni maulizo ya kupendeza, nayo yastahili kufikiriwa sasa.

WALIOFANANISHWA NA SENAKERIBU NA HEZEKIA

18, 19. Senakeribu na Hezekia wanatambulishwa bado kuwa walifananisha nani, kama ilivyoelezwa katika matoleo ya zamani ya The Watchtower?

18 Kwa kuwa unabii huo wa karne ya nane K.W.K. una utimizo wa kisasa, Mfalme Senakeribu alifananisha nani naye Mfalme Hezekia alifananisha nani? Bado wanatambulishwa kama walivyotambulishwa katika makala iliyokuwa na kichwa “Enzi Kuu ya Yehova ya Ulimwengu Wote Yashuhudiwa,” iliyochapwa katika The Watchtower la Aprili 1,1945. Katika fungu lake la kwanza, ukurasa wa 102, makala hiyo ilisema hivi: “Kristo Yesu ndiye Hezekia Mkuu; yaani, yeye ndiye Mfalme mwenye kutawala aliyefananishwa na Hezekia lakini aliye mkubwa zaidi kuliko Hezekia. Mpinzani wa Mfalme Hezekia, Senakeribu, alimfananisha Shetani Ibilisi, ambaye aliabudiwa na kutumikiwa na Senakeribu kwa faida ya utawala wa ulimwengu wa Shetani.” Maelezo hayo yalipatana na toleo la zamani kidogo la The Watchtower la Septemba 1, 1942. Katika makala yake “Hakuna Kurudi kwa Dini,” katika kurasa 270, 271, fungu la nne kutoka mwisho lilisema hivi juu ya kuondolewa kwa Shebna na kuwekwa kwa Eliakimu awe wakili wa kifalme wa Mfalme Hezekia:

19 “Badiliko la uwakili lililofanywa na Mfalme Hezekia lilikuwa la kujitayarisha kwa hatari iliyokuwa inakuja ambayo ingetokea wakati Senakeribu angeushambulia Yerusalemu. Senakeribu amfananisha Ibilisi pamoja na tengenezo lake wanaposhambulia watu wa Yehova wa agano baada ya kuja kwa Bwana hekaluni wakati ashushapo wasioaminika na kuwapa upendeleo watumishi waaminifu.”​—⁠Tazama Isaya 22:15-25.

20. Basi, wakaaji wa Yerusalemu wenye kutawalwa na Mfalme Hezekia wanafananaisha nani?

20 Ni nani basi waliofananishwa na wakaaji wa Yerusalemu wakati wajumbe wa kijeshi wa Senakeribu waliposimama mbele ya kuta za Yerusalemu wakajaribu kumshushia heshima Mfalme Hezekia na kujaribu kufanya wakaaji wa mji wakubali wameshindwa bila kuzingirwa? Kwa kuwa jambo hilo lilitokea karibu miaka minane baada ya majeshi ya Ashuru kuharibu Ufalme wa Israeli wa makabila kumi yenye kuasi imani, raia waaminifu wa Mfalme Hezekia waliokuwa wakikaa Yerusalemu walifananisha waabudu wa Kikristo wa Yehova ambao wametoka katika Babeli Mkuu wa kisasa, kutia na mfano wa kisasa wa Israeli wenye kuasi imani. Wao wamesimama upande wa ufalme wa Kimasihi wa Yehova wakiwa chini ya Hezekia Mkuu, Yesu Kristo.​—⁠Ufu. 18:4,

21. Ni kipindi gani cha utimizo wa unabii kinachoonyeshwa hapa, wakati Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanapokuwa hai bado?

21 Hiyo yaonyesha unabii huo utatimizwa katika wakati uliowekwa barabara. Huo ni wakati “dhiki kubwa” itakapokuwa imeanza. Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, kutia na Jumuiya ya Wakristo, itakuwa imekwisha haribiwa kupitia kwa “shoka” la mfano la Yehova. Kwa kuwa mashahidi wa Yehova wa Kikristo wameitii amri ya kimungu wakatoka katika Babeli Mkuu (kutia na mfano wa kisasa wa Ufalme wa Israeli wa makabila kumi yenye kuasi imani), wao hawashiriki dhambi za Babeli Mkuu na kwa hiyo hawatapatwa na yo yote ya “mapigo” yake wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja.

JARIBIO LA “SHOKA” LENYE KUPINGA DINI

22. Wakati huo mataifa yataanza kupigania nani, naye Yehova atauliza ulizo gani la karne ya nane K.W.K kwa mara nyingine?

22 Hapa imetupasa tukumbuke kwamba Joka, Shetani Ibilisi, ndiye aliyempa “mnyama” wa mfano “nguvu” na “kiti cha enzi” na “uwezo mwingi,” naye “mnyama” huyo ametengenezewa “sanamu” ya kisiasa tangu mwaka wa 1919 W.K. Kwa hiyo wakati wa kutishwa kwa Yerusalemu na Senakeribu unafananisha wakati mataifa yanayofanyiza “sanamu” ya mnyama yatakapoanza kupigana na “Mwana-Kondoo wa Mungu,” Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme, wakimpigania Shetani Ibilisi. (Ufu. 17:14; 19:19-21) Huko kutakuwa ndiko kupambazuka kwa “siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” juu ya hali ya ulimwengu iitwayo Har–​Magedoni. (Ufu. 16:14-16) Hiyo yaonyesha nini? Yaonyesha kwamba matukio ya ulimwengu yamefikia kiasi cha kumfanya Yehova aulize tena ulizo lililoulizwa mara ya kwanza karne ya nane K.W.K.: “Je! shoka lijisifu juu yake alitumiaye? je! msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti.”​—⁠Isa. 10:15.

23. Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wa Kikristo hawashirikiani na mfano wa kisasa wa “Ashuru” kumshambulia Babeli Mkuu, na kwa sababu gani hata Watch Tower Bible and Tract Society haishirikiani nao?

23 Wakati huo Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote atalitupa chini “shoka” la mfano kama kitu kisichomfaa Yeye tena. Sasa atakuwa na sababu zaidi ya kuliharibu. (Isa. 10:16-19) Halikuwa sehemu ya tengenezo Lake, wala “shoka” hilo la mfano halitakuwa sehemu ya tengenezo lake la kitheokrasi kwa sababu amelitumia kwa muda. Kwa sababu hiyo kubwa Mashahidi wa Yehova wa Kikristo hawatashirikiana kamwe na majeshi yenye jeuri ya “Ashuru” wa kisasa kuharibu milki ya ulimwengu ya dini ya uongo wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja. Wala shirika la kidini ambalo limeshirikiana na Mashahidi wa Yehova kwa muda mrefu, yaani, Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, halitafanya hivyo. Sosaiti hiyo haitafanya hivyo, ingawa tangu ilipoandikishwa kisheria Desemba wa 1884 imekuwa ikifunua wazi Babeli Mkuu na kuonyesha kwamba ataharibiwa na Mungu.

24. (a) Yehova ametumiaje Watch Tower Bible and Tract Society of Pennslyvania kama chombo chake kwa tofauti na ile anayotumia “Ashuru” wa sasa kama “Shoka” (b) Je! Sosaiti imepata kuiga “Ashuru” wa kale kwa kujikuza, au itafanya hivyo wakati wa “dhiki kubwa”?

24 Yehova ametumia Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, kama chombo chake kwa njia tofauti kabisa na jinsi atumiavyo “shoka” la Ashuru wa kisasa. Yehova ameitumia sosaiti hiyo kama chombo chake kufunua wazi uongo wa dini ya Babeli Mkuu, kutia na Jumuiya ya Wakristo, kwa kutumia Maandiko. Yehova ameitumia Sosaiti hiyo kuonya mataifa yote (hasa watu wenye kujidai kuwa Wakristo) watoke katika milki hiyo ya ulimwengu ya dini ya uongo kabla hajaihukumu. Mamia ya mamilioni ya nakala za vitabu vya Watch Tower Society vimepelekwa katika ulimwengu mzima katika lugha zaidi ya 160. Katika kazi zake zote na kwa zaidi ya miaka 90 chombo hicho kilichomo mkononi mwa Yehova hakijajaribu kamwe kuiga “Ashuru” wa kale wala ‘kujikuza juu’ ya Mwenye kukitumia, Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu.c (Isa. 10:15) “Dhiki kubwa” itakapoanza Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania na Matawi yake yaliyoko duniani pote itakataa kujiunga na Umoja wa Mataifa ambao ni “mnyama” kushambulia dini ya Babeli Mkuu kwa njia yenye jeuri.

25. (a) Kukataa kujiunga na shoka, kwa kulikuza, yaani, “Ashuru” ya kisasa kutaleta nini? (b) Wakuu wa kisiasa wenye kupinga dini wataweza kuvunja nini, nao hawataweza kuvunja nini?

25 Sosaiti hiyo ikiuokoka uharibifu wenye jeuri wa Babeli Mkuu (kutia na Jumuiya ya Wakristo), itakataa kabisa kujiunga na “shoka” la Ashuru wa kisasa katika kujikuza au kujitukuza juu ya Mwenye kulitumia. Bila shaka “shoka” la Ashuru wa leo litachukua hatua kali juu ya Sosaiti hiyo na Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanaowakilishwa na kutumikiwa na Sosaiti hiyo, kwa sababu ya kukataa kujiunga nalo. Umoja wa Mataifa ambao ni “mnyama” utapigana na “Mwana-Kondoo,” Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme kwa njia hiyo ya kuchukua hatua juu ya watangazaji wa mataifa yote wa ufalme wa Yehova kupitia kwa Kristo. (Ufu. 17:14) Hiyo itakuwa ndiyo njia ya kujikuza kwa “shoka,” yaani, Ashuru ya kisasa, juu ya Yeye aliyelitumia. Wakuu wa kisiasa wenye kupinga dini wa dunia wataweza kuvunja mashirika ya kidini yaliyoandikishwa kwa sheria ya nchi ya zamani, lakini hawataweza kamwe kuvunja udugu unaopatikana ulimwenguni pote, “ushirika mzima wa ndugu,” au Mashahidi wa Yehova wa Kikristo, wasioandikwa kama dini na sheria ya kilimwengu.​—1 Pet. 2:17; 5:9, NW.

KUKOMBOLEWA NA VITA KATIKA HAR-MAGEDONI

26, 27. (a) Huenda Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wakaweza kusikia maneno gani wakati huo yanayofanana na yale ya “Ashuru” wa kale? (h) Wakati huo wafuasi wa enzi kuu ya Yehova watakumbuka maneno gani yaliyoandikwa katika Isaya 10:24-26?

26 Kwa kuwa sisi Mashahidi wa Kikristo wa Yehova tunafananishwa na wakaaji wa Yerusalemu wenye kutawalwa na Mfalme Hezekia, na tuyakumbuke maneno yenye jeuri ya wajumbe wa Ashuru huko nyuma mbele ya kuta za Yerusalemu mwaka wa 732 K.W.K.: “Ni miungu gani iliyookoa nchi yao na mkono wangu, hata [Yehova] auokoe Yerusalemu na mkono wangu?” (2 Fal. 18:35) Unabii huo utakapotimizwa mwishoni mwa “dhiki kubwa” inayokaribia sana, je! mabaki waaminifu wa Waisraeli wa kiroho na “mkutano mkubwa” wa wenzi wao waaminifu wa kidunia watasikia maneno yanayofanana na hayo? Badala ya kukubali kushindwa wakati huo wa hatari na Senakeribu wa kisasa, Shetani Ibilisi, na mawakili wake wa kidunia wenye kujitanguliza, sisi wafuasi wa enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote tutayakumbuka maneno yenye kutia moyo yaliyosemwa kwa Yerusalemu juu ya Mlima Sayuni:

27 “Enyi watu wangu mkaao katika Sayuni, msiogope Ashuru, ingawa akupiga kwa fimbo, na kuliinua gongo lake juu yako, kwa namna ya Kimisri. Maana bado kitambo kidogo tu ghadhabu [ya kimungu] itakoma, na hasira yangu itageukia kuwaangamiza. Na [Yehova] wa majeshi ataamsha mjeledi juu yake, kama vile alivyopiga Midiani karibu na jabali la Orebu; na fimbo yake itakuwa juu ya bahari, naye ataiinua kwa namna ya Kimisri.”​—⁠Isa. 10:24-26; Amu. 7:12 mpaka 8:21; Kut. 14:1-31.

28. Mfalme Hezekia alifanya nini alipotatizwa mwaka wa 732 K.W.K., naye Senakeribu alipashwa habari atazamie nini?

28 Wakati Mashahidi wa Yehova watakapotatizwa kabisa “dhiki kubwa” ya ulimwengu ifikiapo upeo, jambo gani litazamiwe? Huko nyuma katika mwaka wa 732 K.W.K., Senakeribu alimfanyia Yehova mzaha wa kupita kiasi, kana kwamba Yeye alikuwa sawa na miungu ya uongo ya mataifa yenye kuabudu sanamu. (2 Fal. 19:10-13) Wakati huo Mfalme Hezekia alisali kwa Yehova juu ya jambo hilo hekaluni katika Yerusalemu. Yehova alimwondolea Hezekia mashaka kupitia kwa nabii Isaya na vilevile akapeleka ujumbe wa kumkaidi Senakeribu aliyekuwa Libna wakati huo, maili kadha kutoka Yerusalemu. (2 Fal. 19:8, 14-34) Kwa njia hiyo Senakeribu mwenye makufuru alijulishwa atazamie kushindwa kwa njia yenye msiba na Mungu aliyekuwa amekaidi (amedharau). Ndipo Yehova alipochukua hatua ya kujishuhudia kuwa Mungu halisi!

29, 30. (a) Pengine Senakeribu alionaje alipokemewa hivyo na Yehova kupitia kwa Isaya? (b) Ikawaje basi?

29 Baada ya kupashwa habari hizo za Yehova zenye kumwaibisha zilizopitishwa kwa nabii Isaya, Senakeribu alilalaje? Inaelekea kwamba Senakeribu alikata maneno kumwonyesha Mungu huyu, Yehova, chamtema-kuni kesho yake, baada ya kukanywa kwa ukali hivyo! Senakeribu alitaka kuhakikisha amefanya hivyo akiwa na jeshi lake la askari karibu 200,000! Lakini lazima kwanza alale kidogo! Kwa ghafula kukawa na kimya ya ajabu. Askari Waashuru waliendelea kulala fofofo wakiwa wametapakaa kama magugu na miiba katika eneo hilo. Usingizi wao haukuwa wa kawaida! Ikawaje?

30 “Ikawa usiku uo huo malaika wa [Yehova] alitoka, akakiingia kituo cha Waashuru, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu. Na watu walipoondoka asubuhi na mapema, kumbe! hao walikuwa maiti wote pia. Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda zake, akarudi akakaa Ninawi. Ikawa, alipokuwa akiabudu nyumbani mwa Nisroki, mungu wake, Adrameleki na Shareza [wanawe] wakampiga kwa upanga; [wakakimbia].”​—2 Fal. 19:35-37.

31. Kwa kutimiza mfano huo wa kale, “shoka,” yaani, Ashuru ya kisasa, litashindwaje kujikuza juu ya Mwenye kulitumia?

31 Kumbe! lile “shoka,” yaani, Ashuru, lilishindwa kujikuza juu ya Mwenye kulitumia! Ndivyo itakavyokuwa wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja wakati mfano wa kisasa wa Senakeribu na jeshi lake atakapojaribu kujikuza juu ya Mungu yule yule kwa kutisha kufutilia mbali mashahidi Wake watoke duniani. The Watchtower la Aprili 1, 1945, kurasa 108, 109, laeleza jambo litakalofuata:

. . . Wakati huo mashahidi wa Yehova, wakiwa ndani ya tengenezo lake la Kitheokrasi, watakuwa wamezingirwa nao wataelekea kutishwa na uharibifu na majeshi yenye kulemeza ya aliyefananishwa na Mwashuru, Shetani Ibilisi. Lakini msiwe na wasiwasi juu ya wakati ujao wa aina hiyo: Yehova atapiga vita kwa ajili ya mabaki yake na wenzi wao. Atalitenda “tendo la ajabu” lake penye Har–​Magedoni, kama alivyofanya maelfu ya miaka iliyopita katika nchi ya Yuda, ‘kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya Mfalme wake mpendwa.’ Bila shaka Yehova Mungu ataondoka akapigane na kuleta uharibifu juu ya tengenezo la ulimwengu la mpinzani mwovu kwa kumtumia Mwana yule yule wa Mungu, yaani, Kristo Yesu aliye Mfalme, ambaye ndiye malaika aliyetumiwa kuua askari 185,000 wa Senakeribu na kumrudisha huyo akauawe vibaya sana. Kama Senakeribu, Shetani Ibilisi ataliona tengenezo lake linaloonekana duniani likiuawa kabisa. Kisha ataliona tengenezo lake lisiloonekana la mashetani likiharibiwa kabisa, na mwishowe yeye mwenyewe atafutiliwa mbali kwa nguvu nyingi. Hakuna uwezo wa kishetani utakaoweza kumwokoa.

32. Kwa sababu gani hatutakuwa na haja ya kuwa na wasiwasi mapema wala wakati Yehova atakapoanza kulipunga “shoka” la mfano?

32 Kwa hiyo, siku moja iliyo karibu, sisi Mashahidi waaminifu wa Yehova tutaliona “shoka” lenye kupinga dini likipungwa katika mkono hodari wa Mungu wetu kupiga Babeli Mkuu. Litaiharibu milki hiyo ya ulimwengu ya dini ya uongo kwa njia ya kuogofya sana! Je! wakati huo tuwe na wasiwasi chombo cha ulimwengu cha kisiasa kitakaposhambulia dini na kumchukia “kahaba” mkuu wa mataifa yote aliyekuwa akifanya uasherati nacho? Hapana! Ulimwengu hutuchukia, lakini Yehova Mungu na Yesu Kristo hawafanyi hivyo. Naye Yehova atakapoanza kulizungusha-zungusha “shoka” lenye kupinga dini, hatakuwa akilielekeza kwetu sisi mashahidi wake waaminifu. Tutakuwa na pendeleo kubwa la kuona Babeli Mkuu ikikatwa na kuangushwa na kuteketezwa kwa uharibifu wenye moto! Twajua kwamba, baada ya uharibifu huo, “shoka” lenye kupinga dini litajaribu kujikuza juu ya Mwenye kulitumia, Yehova. Hilo litakuwa tisho kubwa la kutaka kutuondolea mbali. Lakini haitatupasa kuogopa wanadamu wanaomchukia Mungu wetu. Acheni tumwogope Yehova wakati huo!

33. Yehova atatuma malaika gani akafikilize hukumu kali sana, na matokeo yatakuwa nini kwetu sisi mashahidi na kwa Yehova?

33 Wakati huo wa kuogofya mataifa yatakuwa yamefika penye Har–​Magedoni kwa kujikaza kabisa, penye uwanja wa pigano la kukata maneno kabisa kati ya wanadamu na Mungu. (Ufu. 16:14-16) Wakati utakuwa umefika wa kuletwa kwa hukumu ya Yehova iliyo kali kuliko zote. Italetwa juu ya “shoka” hilo lenye kupinga dini, ambalo wakati huo litatupiliwa mbali na Yehova. “Shoka” hilo lenye kupinga dini halitaweza kamwe kujiinua litukate-kate vipande vipande. Yehova wa majeshi atamtuma Malaika wake aliye mkuu zaidi ya wote, Yesu Kristo, akayaangushe majeshi yote yenye kushambulia ya Senakeribu Mkuu, Shetani Ibilisi, naye atayalaza fofofo yasiamke tena! Huko kutakuwa kukombolewa kwetu wa namna gani na “shoka” lenye kupinga dini katika upeo wa “dhiki kubwa”! Lakini, kwa maana zaidi, ‘Bwana Yehova wa majeshi’ atashuhudiwaje kupitia kwa wakili wake aliye mwaminifu sikuzote, Yesu Kristo, Hezekia Mkuu!

34. Itakuwaje kwa dini ya kweli na kwetu sisi tunaoifuata sasa?

34 Basi, jipeni moyo enyi Mashahidi wa Yehova wenye bidii! Dini ya kweli, namna ya ibada tunayofuata na yenye kupatana na Maandiko haitafutiliwa mbali kamwe itoke usoni pa dunia. Sisi tutalindwa tupite mwisho mbaya sana wa taratibu nzima ya mambo iliyo mbovu na kuingizwa katika taratibu mpya ya mambo ya Yehova, isiyoweza kuharibika. Humo ibada yake safi itasitawi milele ikiwa chini ya Hezekia Mkuu, Mfalme Yesu Kristo.​—⁠Kutoka The Watchtower, Jan. 15, 1976.

[Maelezo ya Chini]

a Linganisha msiba wa Samaria kama unavyoelezwa katika Ezekieli 23:1-10.

b Tofauti na hilo, angalia yanayosemwa katika 2 Wafalme 18:3, 24.

c Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania iliandikwa kisheria Desemba 13. 1884, chini ya sheria za wilaya ya Pennsylvania. Kwa sasa imepewa ruhusa kwa sheria iwe na washiriki kufika 500, lakini wakati wa kuandikwa kwa gazeti hili (la Kiingereza) ina washiriki 397 tu. Sosaiti hii ina baraza ya wasimamizi saba, wa kusimamia mambo ya Sosaiti. Kulingana na mkataba wa Sosaiti katika kila mkutano wa mwaka washiriki wa Baraza ya Wasimamizi wanachaguliwa na washiriki wote wa Sosaiti wanaohusika. Baada ya uchaguzi huo wa kila mwaka Baraza ya Wasimamizi huchagua maafisa wao wenyewe, kama vile msimamizi (president) wa Sosaiti, n.k. Kulingana na masharti ya Mkataba Sosaiti hutenda kama “chombo cha usimamizi” cha Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wote walioko duniani pote. Sosaiti hutunza maafisi ya Matawi 96 duniani pote.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki