“Shoka” na Mwenye Kulitumia
Je! shoka lijisifu [”lijikuze,” NW] juu yake alitumiaye?”—Isa. 10:15
1, 2. (a) Katika historia watu mmoja mmoja au mataifa wametumiwaje kwa kawaida? (b) Tuna mifano gani ya Kutumia wanadamu hivyo kama vyombo?
NI JAMBO la kawaida mtu mmoja kutumiwa na mwingine kama chombo chake cha kufanyia jambo fulani. Inajulikana katika historia ya kibinadamu kwamba hata taifa zima limetumiwa kama chombo cha mtu fulani mwenye mamlaka na mwenye kuheshimiwa kuwa mkuu zaidi kuliko mtawala wa taifa lenye kutumiwa kama chombo.
2 Kwa mfano, tunacho kisa cha Mfalme Daudi wa Yerusalemu. Alimtumia Jemadari Mkuu wake, Yoabu, kama chombo cha kufanya mkuu wa kijeshi Mhiti, Uria, aachwe auawe katika pigano. Uria alikufa bila kujua kwamba Mfalme Daudi alikuwa amemchafua mke wake, Bathsheba. (2 Sam. 11:1 mpaka 12:9; 1 Fal. 15:5) Halafu tuna kisa cha Papa Hadrian (Adrian) wa Nne, aliyekuwa Mwingereza. Mwaka wa 1155 W.K., alitumia Uingereza yenye kutawalwa na Mfalme Henry wa Pili kama chombo chake cha kuanza kutiisha Ireland yote ili viongozi wa kidini wa Ireland watawalwe na Kanisa la Rumi.a
3, 4. (a) Nyakati za kale, ni taifa gani lililotumiwa kama chombo cha vivi hivi tu cha mkononi? (b) Jina la Mwenye kulitumia taifa la Ashuru kama chombo limo katika unabii gani wa Isaya?
3 Nyakati za kale, karne nyingi kabla ya kutiishwa kwa Kanisa la Ireland, taifa hodari na lenye nguvu nyingi za kijeshi lilitumiwa kama chombo na mamlaka nyingine yenye nguvu zaidi. Taifa hilo la kale lilikuwa Ashuru, wakati lilipokuwa mamlaka ya ulimwengu ya siku hizo, mamlaka ya pili ya ulimwengu ya historia ya Biblia. Hata hivyo, ni mamlaka gani yenye nguvu zaidi iliyoweza kutumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama chombo cha vivi hivi tu au cha mkononi? Wanadamu walijulishwa mamlaka hiyo yenye nguvu zaidi kabla Waashuru hawajaishambulia nchi ya Ufalme wa Yuda wakiongozwa na Mfalme Senakeribu mwaka wa 732 K.W.K. Mamlaka iliyozidi Milki ya Ashuru kwa nguvu ilijulishwa kwa maneno yafuatayo:
4 “Je! shoka lijisifu juu yake alitumiaye? je! msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti. Kwa hiyo Bwana, [Yehova] wa majeshi, atawapelekea kukonda watu wake walionona; na badala ya utukufu wake kutawashwa kuteketea kama kuteketea kwa moto. Na mwanga wa Israeli utakuwa ni moto, na Mtakatifu wake atakuwa mwali wa moto; nao utateketeza na kula mbigili zake na miiba yake katika siku moja. Naye atauteketeza utukufu wa msitu wake, na wa shamba lake linalositawi, tangu nafsi hata nyama ya mwili, itakuwa kama vile afapo mtu aliye mgonjwa. Na miti ya msitu wake itakayosalia itakuwa michache, hata mtoto ataweza kuihesabu.”—Isa. 10:15-19.
5, 6. Isaya anasema nini baadaye juu ya uwezo wa Yehova wa kutumia Ashuru kama chombo cha vivi hivi tu?
5 Maneno hayo yaliandikwa na nabii aliyeongozwa na Mungu, Isaya mwana wa Amozi, aliyemaliza kuandika kitabu chake cha unabii chenye kupendeza sana karibu na mwaka wa 732 K.W.K., mwaka ambao ndipo Waashuru walipoishambulia nchi ya Yuda. Hivyo Isaya asema kwamba Mamlaka Kuu yenye kutumia chombo ndiye “Bwana, [Yehova] wa majeshi,” naam, ‘Mwanga wa Israeli na Mtakatifu wake.’ Je! Mtakatifu huyu ana uwezo wa kutumia taifa zima kama chombo cha vivi hivi tu? Ili tupate jibu lililoongozwa na Mungu na tusikie aliyoendelea kusema nabii Isaya juu ya ‘Bwana, Yehova wa majeshi’:
6 “Ni nani aliyeyapima maji kwa konzi ya mkono wake, na kuzikadiri mbingu kwa shubiri, na kuyashika mavumbi ya dunia katika pishi, na kuipima milima kwa uzani, na vilima kama kwa mizani? . . . Tazama, mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani; tazama, yeye huvinyanyua visima kama ni kitu kidogo sana.”—Isa. 40:12-15.
SHOKA LA MFANO
7. Kwa hiyo, yakilinganishwa na Yehova, mataifa yako kama nini, na katika Isaya 10:15, Yeye ajifananisha na nini?
7 Yakilinganishwa na ‘Bwana, Yehova wa majeshi,’ mataifa yote, kutia na Ashuru, ni kama kitone kidogo sana sana cha maji chenye kutoka katika ndoo au kama mavumbi membamba katika mizani. Kwa hiyo yeye anaweza kwa vyepesi sana kutumia taifa lo lote achagualo kama chombo chake cha kutimizia kusudi lake la kimungu. Kwa hiyo, katika Isaya 10:15, yeye ajifananisha na mtumia shoka, mtumia msumeno, mtikisa bakora, mpunga fimbo. Asema kwamba Yeye si “mti.” Naam, yeye si mpini wa shoka, wala yeye si bakora wala fimbo. Yeye ndiye Mungu aliye hai, Mtumiaji mwenye nguvu zote wa vyombo hivyo vya mfano. Basi, shoka la mfano analokatia ni nini?
8. Ni nani hasa “Ashuru” anayetajwa katika Isaya 10;5, 6?
8 Mapema katika sura iyo hiyo ya kumi ya kitabu cha unabii cha Isaya Yehova mwenyewe ajulisha shoka la mfano ni nini. Kwa hiyo, katika Isaya 10:5, 6 twasoma maneno haya ya Yehova: “Ole wake Ashuru! fimbo ya hasira yangu, ambaye gongo lililo mkononi mwake ni ghadhabu yangu! Nitamtuma juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya watu wa ghadhabu yangu, ateke nyara, na kuchukua mateka, na kuwakanyaga kama matope ya njiani.” Kumbe’ chombo cha mfano ambacho Yehova atumia kutimiza kusudi lake alilotaja ni “Ashuru.” Hilo si jina la Mwashuru mmoja, wala si la mfalme wa Ashuru. Lamaanisha taifa zima la Ashuru, Mamlaka ya Ulimwengu ya Pili ya unabii wa Biblia. Hakuna Mwashuru mmoja, hata mfalme mwenyewe, angeweza kuitimiza kazi ambayo Yehova amempa “Ashuru.” Hiyo inaonyeshwa na uhakika wa kwamba, baada ya Yehova kumwita Ashuru “fimbo ya hasira yangu,” ataja “gongo lililo mkononi mwao kwa ajili ya mashtaka yangu!” (Isa. 10:5, NW; angalia mstari wa 24.) Kutokana na hilo ni wazi kwamba iliyomaanishwa ni jamii ya Ashuru, yaani, taifa zima la Ashuru, na hasa majeshi yake.
9. Kutimizwa kwa unabii wa Isaya 10:5, 6 kunatuhusuje leo, naye mtume Paulo aonyeshaje jambo hili?
9 Walakini, unabii huo wa kale juu ya “Ashuru” una maana gani kwetu leo? Ni wa maana sana. Si unabii wa zamani usio na maana. Ni unabii ambao utakapotimizwa siku zetu utatuhusu sote. Lazima utimie kwa kadiri iliyo kubwa na kwa mara ya mwisho katika siku zetu! Si wote uliotimia katika karne ya nane kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Mtume Paulo wa Kikristo aliutaja mstari wa 22 wa sura ile ile ya kumi ya Isaya akautumia kuhusu siku zake katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Kulingana na unabii wa Isaya, ni mabaki machache tu ya Wayahudi walioukubali Ukristo, na kwa sababu hiyo mtume Paulo aliendelea kusema hivi: “Isaya naye atoa sauti yake juu ya Israeli, kusema, Hesabu ya wana wa Israeli, ijapokuwa ni kama mchanga wa bahari, ni mabaki yao tu watakaookolewa. Kwa maana Bwana atalitekeleza neno lake juu ya nchi, akilimaliza na kulikata.”— Rum. 9:27, 28. Tazama pia Warumi 15:4.
10. “Taifa lenye kukufuru” na “watu wa ghadhabu yangu” wanaotajwa na Yehova katika Isaya 10:6 wanahakikishwa kuwa nani?
10 Ni taifa gani la kale ambalo Yehova wa majeshi alishambulia kwa kutumia Ashuru kama “fimbo” na “shoka”? Sisi sote leo tunauliza hivyo kwa sababu taifa hilo la kale liliifananisha Jumuiya ya Wakristo wa sasa! Yehova aliliita taifa hilo la kale “taifa lenye kukufuru” na “watu wa ghadhabu yangu.” (Isa. 10:6) Kwa kusema hivyo Yehova alikuwa akilitaja taifa na watu waliofanyiza Ufalme wa Israeli wa makabila kumi, mji wao mkuu ukiwa Samaria. Taifa hilo lilikuwa limejitenga na ufalme wa Daudi, ambao mji wake mkuu ulikuwa Yerusalemu. Lilijitenga baada ya kufa kwa Mfalme Sulemani mwana wa Daudi. Ushuhuda wa kuonyesha Ufalme wa Israeli wa makabila kumi uliasi imani ukakufuru ni kwamba, “Ashuru” mwenyewe asema kwa dharau juu ya mji mkuu wa Samaria na juu ya “sanamu zake [“miungu yake isiyofaa kitu,” NW].” (Isa. 10:11) Kwa kuwa ufalme huo wa Israeli uliasi ukaacha kumwabudu Yehova kama Mungu, miungu iliyoletwa na wafalme wenye kuasi imani wa taifa hilo isingeweza ‘kufaa kitu.’ Baada ya Israeli kuendelea kumkataa Yehova asiwe Mungu kwa zaidi ya miaka 250, Yeye alikuwa na haki kabisa kuwasema kuwa “watu wa ghadhabu yangu,” ambao angepiga kwa ‘gongo la adhabu yake.’—1 Fal. 12:25 mpaka 13:6; 16:8-33; Isa. 10:5, 6.
11. Ni tengenezo gani la kidini linalofanana leo na Ufalme wa Israeli wa makabila kumi wenye kuasi imani, na kwa sababu gani hatutaki tupatikane sasa tukiwa katika tengenezo hilo?
11 Jumuiya ya Wakristo ya leo inafanana sana na taifa la Israeli lenye kuasi imani la makabila kumi! Si uasi wa Israeli wa kale peke yake juu ya Yehova Mungu uliofananisha kutoka kwa Jumuiya ya Wakristo katika Ukristo wa kweli. Kutoka kwake kulitabiriwa pia na Yesu Kristo na mitume wake. (Mt. 13:24-43; Matendo 20:29-31; 2 The. 2:1-12; 2 Tim. 4:3,4) Kwa hiyo, watu wote wanaoiamini Biblia wanaweza kutazamia kwa hakika kwamba, katika wakati unaofaa Yehova wa majeshi ataitumia “fimbo” ya mfano ya hasira Yake, naam, atalitumia “shoka” la mfano kuwakata ‘watu hawa wa kisasa wa ghadhabu yake.’ Bila shaka hatutaki tupatikane tukiwa kati ya watu hao! Basi, ni vizuri tujifunze kinachofananishwa leo na “fimbo” na “shoka.”
12. (a) Yehova alitumiaje “Ashuru” kama “shoka” juu ya Israeli wa kale? (b) Wakati huo, uhusiano wa Ashuru ulikuwaje na tengenezo la Yehova?
12 Siku za nabii Isaya, Yehova alitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama “fimbo” ya kuukomesha Ufalme wa Israeli wenye kuasi wa makabila kumi. Mwaka huo wenye msiba ulikuwa 740 K.W.K. Kisha Yehova alitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama “shoka” lake kuliangusha taifa la Israeli lenye kuabudu sanamu. Alifanya hivyo kwa kuacha majeshi ya Ashuru yafikie upeo wa mazingiwa yao ya miaka mitatu juu ya mji mkuu wa Samaria kwa kuuteka na kuufanya kama mahali pa kukanyaga-kanyaga matope. (2 Fal. 17:7-23; 18:9-12) Na tuwe waangalifu hapa tuone jambo moja. Jambo gani? Hili: Ingawa Yehova aliitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama chombo chake cha kuleta uharibifu juu ya wenye kuasi ibada Yake, Ashuru haikuwa sehemu ya tengenezo la Yehova. Ilikuwa sehemu ya tengenezo lenye kuonekana la Shetani Ibilisi. Nchi ya Ashuru iliitwa “nchi ya Nimrodi.” Huyo ndiye Nimrodi aliyeuanzisha mji wa Ninawi, ambao ndio ukawa mji mkuu wa Ashuru. Mwanzishaji huyo akawa “Nimrodi, hodari wa kuwinda . . . [kwa kumpinga Yehova, NW].” (Mik. 5:6; Mwa. 10:8-12) Tena, na tuangalie hapa jambo jingine: Ingawa Yehova aliitumia Ashuru kama “fimbo” na “shoka” lake, mamlaka hiyo ya ulimwengu haikuwa sehemu ya tengenezo la Yehova linaloonekana kwa sababu hiyo. Haikufuata ibada Yake!
“SHOKA” LAJARIBU KUJIKUZA JUU YA MWENYE KULITUMIA
13. Nia ya “Ashuru” ilikuwa nini juu ya kutumiwa na Yehova kama chombo?
13 Ashuru ya kale haikutaka kumtumikia Yehova wala haikutaka kuendelea kutimiza kusudi Lake ili kumshuhudia na kumtukuza. Ndiyo sababu aliendelea kusema hivi juu ya “Ashuru”: “Ingawa huenda akawa hataki hivyo, atakuwa na maelekeo ya kufanya hivyo; ingawa huenda moyo wake usitake kufanya hivyo, atapanga, kwa maana kuangamiza kumo moyoni mwake, na kukatilia mbali mataifa yasiyo machache.”—Isa. 10:7, NW.
14. (a) Ingawa “Ashuru” ilitumiwa kama chombo cha vivi hivi tu, ‘ilikuwa na maelekeo’ gani? (b) Kupatana na maelekeo hayo, moyo wake ulikuwa ukifikiria kufanya nini, na kwa sababu gani?
14 “Ashuru” ilijisikia ikitaka kuelekea upande isiotaka kwenda. Wakati huo Yehova alitaka “Ashuru” iwe chombo tu cha kutumiwa na mkono wa kimungu, kutimiza kusudi la kimungu la kuadhibu taifa lenye kupotoka. Lakini, “Ashuru” ilikuwa na maelekeo ya kufanya jambo jingine, jambo lenye kupatana na nia yake ya kutaka makuu. Naam, ilifanya mpango, lakini je! ilifanya hivyo kwa sababu moyo wake uliiongoza iwe kama chombo katika mkono wa Mungu aliyepingwa na mwindaji hodari Nimrodi? Sivyo, moyo wake haukutaka hivyo. Haukuiongoza ikusudie wala kupanga kutenda kupatana na kusudi lenye haki la Yehova. Ilipanga kuangamiza na kukatilia mbali mataifa bila sababu, ikiwa na bidii ya mwindaji mwenye kutaka kuua wanyama kwa mchezo tu. Ilitumaini kupendeza miungu yake ya uongo kwa kufanya hivyo, si kumpendeza Yehova. Ilijiondokea kwa kusudi la kuushinda ulimwengu. Haikutaka kuwa ilivyochaguliwa na Yehova iwe wala haikutaka kuwa ilivyoagizwa, yaani, kuwa wakili wa kuadhibia. Matendo zaidi ya “Ashuru” yalionyesha hivyo.
15. “Ashuru” ilimpa nani sifa ya ushindi wake, nayo maneno yake yaliyoandikwa katika Isaya 10:8-11 yaonyeshaje hilo?
15 Kwa sababu “Ashuru” haikumtambua Mungu Mwenye Nguvu Zote aliyeitumia kama chombo cha vivi hivi tu, haikumpa Yehova sifa bali ilijichukulia sifa yote. Ni vyepesi kwetu kuiona nia hii ya “Ashuru” inapokaribia kuupindua Ufalme wa Israeli wa makabila kumi na kuuteka mji wake mkuu Samaria. Ufalme wa Israeli ni mojawapo la mataifa ambayo “Ashuru” ilikuwa imetilia bidii kuyaangamiza na kuyakatilia mbali: “Maana asema, Je! wakuu wangu si wote wafalme? Je! Kalno si kama Karkemishi? Hamathi si kama Arpadi? Samaria si kama Dameski? Kama vile mkono wangu ulivyofikilia falme za sanamu, ambazo sanamu zao za kuchongwa zilikuwa bora kuliko sanamu za Yerusalemu na za Samaria; je! sitautenda Yerusalemu na sanamu zake vile vile kama nilivyoutenda Samaria na sanamu zake?”—Isa. 10:8-11.
16. Maneno hayo ya “Ashuru” yalimkufuru nani, nayo ilikuwa “Mfalme wa wafalme” yajapokuwako majeshi gani ya kidini?
16 Hayo yalikuwa maneno ya kukufuru namna gani, kwa maana yalisemwa kwa dharau juu ya Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, Yehova! Kwa “Ashuru,” miji ambayo ilifikilia iishinde ilikuwa kama miji iliyokwisha shindwa zamani. Maeneo iliyokuwa imeshinda yalikuwa yametawalwa na wafalme wa maeneo hayo. Sasa ilikuwa imewafanya wafalme hao kuwa watawala-watumwa. Kwa hiyo watawala iliosimamia walikuwa’“wafalme” halisi, na kwa sababu hiyo ingeweza kujisifu kuwa “Mfalme wa wafalme.” “Ashuru” ilijua kwamba miji ambayo iliwashinda wafalme wake ilikuwa na “sanamu” (“miungu,” NW) nyingi, nyingi kuliko zile za Samaria na za Yerusalemu. Hata hivyo, ijapokuwa miungu hiyo na sanamu za kutengenezwa na mwanadamu zilikuwa nyingi sana katika miji hiyo isiyo ya Kiisraeli, “Ashuru” ilikuwa imeishinda miji hiyo ya kipagani. Je! hiyo haikuhakikisha ilikuwa hodari kuliko miungu yote hiyo? “Ashuru” ilijijibu yenyewe ikisema Ndiyo!
17. Kwa hiyo ni kwa sababu gani “Ashuru” iliwaza kwamba Samaria na Yerusalemu ingeshindwa kwa vyepesi?
17 “Miungu” hiyo haikuwa kitu. Kwa hiyo, miji mikuu Samaria na Yerusalemu ilipaswa kushindwa kwa vyepesi, kwa sababu haikuwa na miungu mingi wala sanamu za kuchongwa kama miji ile isiyo ya Kiisraeli iliyokuwa imeshindwa na “Ashuru.” Ndivyo “Ashuru” Mfalme wa wafalme ilivyowaza.
18. “Ashuru” iliweza kuushinda Samaria kwa sababu ya mambo gani?
18 Wakati huo Ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulikuwa taifa lenye kuasi ibada, kafiri! Lilikuwa limeanza kuabudu ndama wa dhahabu, naam, hata kuabudu Mabaali wa kipagani. Mungu wa Samaria hakuwa Yehova. Mji huo ulikuwa na miungu isiyofaa kitu na sanamu za kuchongwa na mwanadamu. Si ajabu basi kwamba “Ashuru” iliuteka Samaria mwaka wa 740 K.W.K. baada ya kuuzingira kwa miaka mitatu! Kwa sababu ya tendo hilo la ujasiri majivuno ya “Ashuru” yaliongezeka, hata jeuri yake ikazidi juu ya ibada ya Yehova katika Yerusalemu. Kwa sababu ya kuushinda Samaria na kuunyang’anya mali zake na kuufanya ‘mahali pa kukanyagwa kama matope ya njiani,’ mshindi wa Ashuru alijipatia utukufu. Alijivunia jeshi lake lililoelekea kutoshindika. Hakujua kwamba alikuwa akitumiwa kama wakili wa kutimizia kusudi fulani katika mkono wa Mungu aliyekuwa ameacha kuabudiwa na Israeli!
19. Kwa hiyo ni ulizo gani linalotokea sasa?
19 Sasa ulizo la kupendeza sana latokea. Ndilo hili: Kwa kuwa Jumuiya ya Wakristo ilifananishwa na Samaria na Ufalme wa Israeli wa makabila kumi, je! katika siku zetu sisi tutaona Jumuiya ya Wakristo wa kisasa ikipatwa na yale yale yaliyowapata Israeli?
AHADI YATOLEWA KWAMBA MPIGA UBWANA ATATOA HESABU
20, 21. Kwa sababu gani ilimpasa Yehova afikirie yaliyosemwa na “Ashuru,” kulingana na Isaya 10:12-14?
20 Twaonaje? Wakati mji ambao juu yake jina la Yehova limewekwa unapotishwa kwa maneno, je! Yeye mwenyewe hapaswi kufikiria jambo hilo? Apaswa! Kwa hiyo, Yehova alikatiza usemi wa kujitukuza wa mkuzaji wa milki ya Ashuru, alipotumia nabii Isaya kusema:
21 “Na itatukia kwamba wakati Yehova atakapomaliza kazi yake yote katika Mlima Sayuni na katika Yerusalemu, mimi nitafanya hesabu ya matunda ya jeuri ya moyo wa mfalme wa Ashuru na ya kujitukuza kwake. Kwa maana amesema, ‘Kwa uwezo wa mkono wangu bila shaka nitachukua hatua, na kwa hekima yangu, kwa maana mimi nina ufahamu; nami nitaitoa mipaka ya mataifa, nami bila shaka nitaviteka vitu vyao walivyoweka, nami nitawashusha wakaaji sawasawa na mtu hodari. Na mkono wangu utazifikilia mali za mataifa, kana kwamba zilikuwa kioto; na sawa na vile mtu hukusanya mayai ambayo yameachwa, mimi mwenyewe nitaikusanya hata dunia yote, wala hakutakuwa na ye yote wa kupigapiga mabawa yake wala wa kufungua kinywa chake wala wa kulia.’”—Isa. 10:12-14, NW.
22. Ili ipate ushindi duniani pote, ingeipasa “Ashuru” iteke nini?
22 Kulingana na usemi huo uliotoka kinywani mwa “Ashuru” ni wazi kwamba Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru isingetosheka hata baada ya kuuteka Samaria. Ingetaka ‘kuikusanya hata dunia yote.’ Yerusalemu na nchi ya Yuda zingekuwa mayai yake mazuri ya kukusanya. Mpiga ubwana wa Ashuru angedhani kwamba ana uwezo, hekima na ufahamu na kushinda duniani pote.
23, 24. (a) Kama “Ashuru ilivyodhani, kukusanya kwake dunia yote kungekuwaje kama kukusanya mayai katika kioto kilichoachwa? (h) Kwa sababu gani Yehova alilazimika kusema juu ya jambo hilo?
23 Kwa “Ashuru” yenye kujitanguliza, jambo hilo lingekuwa jepesi kama kuchukua mayai katika kioto ambacho kimeachwa na ndege mzazi aliyeshtuliwa. Ndege huyo asingepigapiga mabawa yake kuuondoa mkono wenye jeuri ulionyoshwa uchukue mayai. Asingefungua kinywa atete. Hata asingetoa mlio wa kulalamika juu ya kunyang’anywa mali na kuhamishwa na jeshi la Ashuru lenye kushinda. Kwa hiyo “Ashuru” ingetumia ipendavyo maeneo iliyoshinda, ikibadili au kufuta mipaka au kuhamisha wenyeji katika nchi yao, kama vile ilivyohamisha Waisraeli waliookoka katika nchi ya Israeli waliyopewa na Mungu ikawapeleka Ashuru na kuweka mataifa mengine katika nchi iliyoachwa bila watu.
24 Yehova alijua kwamba “Ashuru” ilitamani kuuteka Yerusalemu hasa na nchi ya Yuda. Hiyo ilikuwa ndiyo ngome iliyobaki duniani ya ibada ya Yehova. Kwa haki Yeye alipaswa kusema jambo fulani. Alipaswa kuchukua hatua!
25. Kwa sababu gani Yehova alikuwa na kazi ya kufanya wakati huo juu ya Mlima Sayuni na katika Yerusalemu?
25 Wakati huo wenye hatari katika karne ya nane K.W.K. Yehova, akiwa ndiye ‘Mwanga wa Israeli na Mtakatifu wake,’ alikuwa na kazi ya kufanya katika Mlima Sayuni na katika Yerusalemu, ambao ulikuwa juu ya Mlima Sayuni. (Isa. 10:17) Wakati wa utawala wa Mfalme Ahazi mwenye kuasi imani, nchi ya Yuda na Yerusalemu zilikuwa zimechafuliwa na ibada ya sanamu ya kipagani. Lakini mwanzoni mwa utawala wa mwanawe, Hezekia, roho ya Yehova ilimwongoza mfalme mpya wa Yerusalemu kuondoa nchini ibada ya miungu ya uongo isiyofaa kitu na kurudisha ibada safi ya Yehova juu ya Mlima Sayuni, na katika Yerusalemu, ambapo hekalu la Yehova lilikuwa. Hezekia alianza kutawala miaka mitano kabla “Ashuru” haijaupindua Samaria. Alitawala kwa haki miaka 29, mpaka 716 K.W.K.
26. Sasa Yehova aliona wakati umefika wa kufanya nini, na ni mfalme gani hasa wa Ashuru aliyehusika?
26 Mfalme Hezekia alivunja mapatano ya kisiasa ambayo baba yake, Mfalme Ahazi, alikuwa amefanya na Ashuru. Hiyo ilileta mpambano kati ya “Ashuru” na Yehova, Mungu wa Hezekia. Chini ya hali hizo Yehova aliona wakati ulikuwa umefika wa kumwadhibu mfalme wa Ashuru mwenye kumkaidi Mungu, kwa njia hiyo ‘afanye hesabu ya matunda ya jeuri ya moyo wa mfalme wa Ashuru na ya kujitukuza kwake.’ (Isa. 10:12) Mfalme aliyehusika hapa alikuwa Senakeribu, mwana wa Sargon wa Pili. Jina lake refu linamaanisha “Sin Amezidisha Akina Ndugu,” au, “Sin na Aweke Wengine Mahali pa Ndugu (Waliopotea),” nalo neno “Sin” ndilo jina la mungu-mwezi wa Ashuru.
27. Bila ya kuchafua mipango ya ndani ya nchi ya Ashuru, Yehova angewezaje kuitumia kama “shoka” lake la mfano?
27 Yuko mtu aliye kama Senakeribu leo. Inatupendeza kuangalia jinsi Yehova atakavyoshughulika na kitu cha kisasa kilichofananishwa na “shoka” ambalo atatumia kukata kitu fulani. Tunapoanza kujifunza habari hiyo, na tukumbuke kwamba Yehova aliiruhusu Milki ya Ashuru ya kale iwe na tengenezo lake yenyewe. Yeye hakuchafua mipango ya ndani ya nchi hiyo. Bado iliwezekana kwake kuitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama “shoka” lake. Namna gani? Kwa kuelekeza mapigo ya “shoka” hilo la mfano mahali palipopaswa kupigwa. Kwa njia hiyo Yehova aliangusha alichotaka kiangushwe.b
[Maelezo ya Chini]
a Juu ya jambo hili, M’Clintock and Strong’s Cyclopoedia, Volume IV, ukurasa wa 641, safu ya pili, chini ya “Ireland,” chasema hivi: kipindi cha machafuko ya utawala, ambacho hali ya adili ya mapadre wa Ireland iliharibika sana. Malalamiko ya Rumi wakati huo yalihusu mazoea ya kidini hasa ya Waireland—ndoa ya mapadre, usimamiza wa ubatizo bila ya kutumia mafuta matakatifu, na matumizi ya mpango wao wenyewe wa ibada. Wajumbe wa mapapa mwishowe walifaulu, kutiisha kabisa Kanisa la Ireland chini ya Kanisa la Rumi karibu na katikati ya karne ya kumi na mbili, na inaaminiwa mpaka wakati huo kanisa hilo halikuwa na maungamo ya siri, matoleo ya misa, na mapendeleo, na kuadhimisha Kijio cha Bwana katika aina zote mbili. Mwaka wa 1155 tangazo la papa Hadrian wa Nne lilimruhusu mfalme Henry wa Pili wa Uingereza atiishe Ireland, naye mfalme akamwahidi papa kwamba atayalinda mapendeleo ya papa.”
b Kwa mfano, angalia maneno ya Yesu katika Mathayo 22:7 juu ya mfano wake wa karamu ya arusi ya Mfalme. Majeshi ya upagani ya Kirumi yenye kuongozwa na Jemadari Tito ndiyo yaliyotimiza utabiri wake mwaka wa 70 W.K. juu ya mji wa Yerusalemu usiogeuzwa kuwa wa Kikristo.
[Picha katika ukurasa wa 322]
[Picha katika ukurasa wa 326]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Sin achi ir-i-ba
(Mwezi) (ndugu) (aliongeza)
“Mwezi umezidisha ndugu”
Maandishi ya jina la Senakeribu pamoja na maana yake