Sababu Gani Uje Mlangoni Kwangu?
“NINA heshima kubwa sana kwenu. Ninapendezwa na unyofu na uhakika wenu. Mnafanya kazi nzuri ya kujaribu kuleta watu kwa Mungu. Lakini sababu gani uje mlangoni kwangu? Mimi tayari nina dini yangu.”
Hayo yaliyo hapo juu ni mfano wa maoni ya wengi wa wenye nyumba ambao Mashahidi wa Yehova hukutana nao katika kazi yao ya kufunza Biblia. Wewe pia, huenda unashangaa sababu gani Mashahidi huendelea kufika mlangoni kwako na katika nyumba za wengine katika mtaa wako ambao wana dini zao wenyewe.
Je! Mashahidi wa Yehova wanajaribu kujipatia faida kwa kuuza vitabu? La, kwa sababu ule mchango mdogo wanaoomba kwa vitabu vyao haulipii kabisa hata gharama ya uchapishaji na ugawaji wa vitabu hivi. Si michango ya fedha bali ujumbe uliomo ndani ya vitabu hivi ndio unaowaongoza wenye kujitoa hawa wasiolipwa waendelee kufika katika nyumba za watu. Sababu gani upendezwe na ujumbe huu?
Kwa sababu unahusiana na kuondolewa kwa vita duniani, ugomvi wa kikabila, uvunjaji wa sheria na jeuri; mwisho wa upungufu wa chakula, upungufu wa nyumba, bei za juu, kodi za juu; hata mwisho wa namna zote za magonjwa na mauti. Je! mambo haya yote hayasumbui watu wa dini zote? Je! wewe hungependa kuona yakimalizika?
Biblia huonyesha ni namna gani na wakati gani Mungu atachukua hatua kumaliza matatizo haya. Maandiko yaeleza waziwazi kwamba sisi sasa tunaishi katika “mwisho wa taratibu [iliyopo] ya mambo” au “mwisho wa kizazi.” (Mt. 24:3, NW; The New English Bible) Bila shaka wewe unataka kujua hili. Si kitu wewe ni wa dini gani.
Lakini, je! mmoja anawezaje kuwa na hakika kwamba kizazi hiki kinachoishi sasa kitapatwa na mgeuko kama huo? Wanafunzi wa Yesu waliuliza ulizo kama hilo: “Ni nini itakayokuwa ishara ya . . . mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW; Marko 13:4; Luka 21:7) Yesu alitia ndani haya katika jibu lake:
“Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na matetemeko makubwa ya nchi, na njaa na tauni mahali mahali.” (Luka 21:10, 11) Lakini, je! vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya nchi na kuambukizana magonjwa hakukuwako katika muda wote wa historia ya wanadamu? Ndiyo, lakini ni tangu mwaka wa 1914 W.K. tu mambo haya yametaabisha wanadamu katika sehemu zote za dunia katika kizazi kimoja. Kwa hiyo, kama alivyosema Yesu, watu wanaoishi sasa wataona taratibu iliyopo ya mambo pamoja na taabu zake zote zikimalizika.—Linganisha Luka 21:29-32.
Hiyo maana yake ni ‘mwisho wa ulimwengu,’ kama vile watu wanavyoufikiria? Je! dunia itaharibiwa pamoja na uhai wote ndani yake? Hata kidogo! Kwa kweli, dunia haitaharibiwa kamwe. ‘Imewekwa imara milele.’ (Zab. 78:69) Basi, ni nini kitakachokwisha? “Kizazi” kilichopo sasa cha uovu. Ndipo kutakapokuwapo na utimizo wa dunia nzima wa ahadi ya Yehova katika Zaburi 37:10: “Asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.” Taratibu mpya kabisa ya mambo itarudi mahali pa hii.
Hiyo taratibu mpya itakuwaje? Mtume aliyeongozwa na Mungu Yohana alieleza nyingine za baraka za taratibu hiyo mpya katika Ufunuo 21:3, 4: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, . . . Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” Nabii Isaya pia husema juu ya mambo ambayo hutupa sisi sababu ya kusadiki kwamba wakati huo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” Pia, vipofu, viziwi, mabubu na vilema wataponywa udhaifu wao. (Isa. 33:24; 35:5, 6) Kutakuwako kujifurahisha kwa kweli uzima katika hali za haki. Je! wewe usingependa kuishi katika hali kama hizi?—2 Pet. 3:13.
Je! kasisi, padre au kiongozi wako wa kidini amepata kukwambia juu ya tumaini hili la ajabu? Viongozi wengi wa kidini hawasemi lo lote juu yake. Kwa kweli, wengi hata hawaamini Biblia. Hii ni sababu kubwa ya Mashahidi wa Yehova kufika katika nyumba za watu wa dini nyingine.
Jitihada za Mashahidi wa Yehova kufikia watu waziwazi na nyumbani mwao zina msingi wa Neno la Mungu. Yesu mwenyewe alienda moja kwa moja kwa watu, na aliwaagiza mitume wake na wanafunzi wengine wafanye hivyo hivyo. (Mt. 10:11-13; Luka 8:1; 10:5) Hasa, kazi ya Mashahidi wa Yehova hufanyiza sehemu nyingine ya ishara Yesu aliyotoa ya kukaribia kwa mwisho wa taratibu hii ya mambo. Yeye alisema: ‘Na habari hizi njema za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.’—Mt. 24:14, NW.
Je! hii kazi ya kuhubiri ‘habari njema za ufalme wa Mungu’ huwa na matokeo? Ndiyo! Mamia ya maelfu ya watu wenye njaa ya kweli wameongezwa imani katika Mungu na katika Biblia kwa kufika kwa Mashahidi wa Yehova nyumbani mwao. Ebu fikiria maono ya mwanamke mmoja kutoka New Caledonia:
“Nilipokuwa katika hali ya wasiwasi na kutaka kujiua, nilipeleka barua nikiomba msaada kwa mtu mmoja niliyeona anaweza kunisaidia—padre wangu. Lakini yeye hakujibu. Lakini, baada ya juma moja mmoja wa Mashahidi wa Yehova akafika kwangu. Nilikubali kuchukua kitabu kimoja cha kunisaidia kujifunza Biblia, na mara tu mwanamke huyo alipoondoka nikasoma kwa hamu kubwa yaliyokuwamo. Baada tu ya siku chache nikaanza kupata faraja ya akili, na hali yenye kuendelea ya uhuru.” Baadaye, mwanamke huyu na mumewe wakawa watumishi wenye furaha wa Mungu, wakileta habari njema kwa wengine zaidi.
Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba watu wengi wana dini zao. Lakini dini za ulimwengu hazisemi lo lote juu ya habari njema za ufalme wa Mungu. Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova waendelea kufika mlangoni kwako. Watakapofanya hivyo tena, sababu gani usiwakaribishe na usikilize ujumbe wao unaotoka katika Biblia?