Wakristo Walioteswa—“Tamasha kwa Dunia”
“Nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu.”—1 Kor. 4:9.
1, 2. Watu wengi wanaogopa nini? Wanaweza kupata faraja gani?
WAZO la kutaabika kama Yesu na mitume walivyotaabika linaogofya watu wengi. Kweli, wanajua kwamba faida nyingi za ajabu zapatikana kwa wale walio na maoni ya kiroho yaliyokuzwa juu ya maisha. Lakini hawadhani kwamba wao wenyewe wataweza kuyashinda mashambulio makali wanayoona siku moja yataipata imani yao.
2 Je! huo ndio woga wako? Ikiwa ndivyo, fikiria: Haikufariji kujifunza katika makala iliyotangulia kwamba waweza kuwa mtu wa kiroho? Ndiyo, ‘mtu wa kawaida’ kama wewe—mwuzaji, mpasua mbao au mke anayefanya kazi ya nyumba—anaweza kweli kuwa na “nia ya Kristo.” Vile vile utaona inatia moyo kujifunza kwamba wewe pia waweza kuvumilia kwa kufanikiwa chini ya jaribu lo lote liwezalo kukujia kutoka upande wo wote wa huu ulimwengu wa kimwili.
3. Yesu alisema imewapasa wafuasi wake watazamie nini?
3 Imempasa Mkristo atazamie kuchukiwa na ulimwengu. Yesu alieleza: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Aliyoyasema yaliwapata mitume. Nayo yatawapata na Wakristo wa kweli leo, watu wa kiroho kweli kweli. Lakini huenda ikaulizwa, sababu gani mitume, watu wa kiroho, walipatwa na “udhia” (mateso)?
4. Kwa sababu gani watu wa kiroho kati ya Wakristo wa karne ya kwanza walipatwa na mateso?
4 Katika sala Yesu alisema hivi kwa Yehova, Baba yake: “Ulimwengu umewachukia [wafuasi wa nyayo zake]; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, . . . Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni. . . . ulimwengu haukukujua; . . . hao wamejua ya kuwa ndiwe uliyenituma.”—Yohana 17:14, 17, 18, 25.
5. Eleza namna ambavyo ulimwengu wa kimwili uliwachukia Wakristo hao wa kwanza.
5 Mitume, watu wa kiroho waliozoezwa na Yesu, walikuwa “si wa ulimwengu.” Ndiyo sababu uliwachukia. Tofauti iliyokuwa kati ya watu hao wa kiroho na ulimwengu wa kimwili ikawa dhahiri kwa viumbe vyote. Baada ya Yesu kuondoka duniani mitume walijitoa bila kuchoka kulitimiza agizo lao kuhubiri na kufundisha “hata mwisho wa nchi.” (Mt. 28:16-20; Matendo 1:6-8) Ulikuwako upinzani mkali kwa kazi yao tangu mwanzoni. Upinzani wa kwanza ulitoka kwa wananchi wenzao. (Matendo 5:40; 12:1-5) Kazi ilipotoka nje ya Uyahudi na Samaria, yalikuwako mapambano na wafuasi wa miungu ya Mataifa walioogopa kwamba vyombo vyao vya ibada ‘vingehesabiwa si kitu.’—Matendo 19:23-41; 14:1-7.
“TAMASHA KWA DUNIA”—KWA NJIA GANI?
6, 7. Paulo ana maana gani katika 1 Wakorintho 4:9 anaposema kwamba mitume walikuwa “tamasha kwa dunia”?
6 Mtume Paulo anaonyesha vizuri taabu zilizowapata Wakristo katika 1 Wakorintho 4:9.
“Nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu.”
7 Hapa Paulo hakuwa akiwazungumza mitume kama tamasha katika mambo ya kawaida tu ya maisha na kusema kwamba wakati watu wale wengine walipowaona wakiishi maisha za uaminifu, zenye kujenga, waliusadiki unyofu wa njia ya maisha ya Kikristo. Sivyo, yeye anazungumza taabu iliyowapata mitume, kana kwamba waliwekwa wazi katika uwanja wa michezo kwa kushutumiwa mbele ya wahudhuriaji wengi. Theological Dictionary of the New Testament chasema “tamasha” wanayoionyesha mitume katika Biblia ‘si yenye fahari kulingana na kanuni za kibinadamu, bali yenye kusikitisha na ya kudharauliwa.’
8, 9. (a) Tafsiri za Tatuliano na James Moffatt zatusaidiaje kuona kwamba wakati Paulo anaposema mitume walikuwa “tamasha” alikuwa akizungumza juu ya taabu iliyowapata? (b) Je! Paulo alipata kuwa katika uwanja halisi wa michezo wakati wo wote?
8 Tafsiri ya karne ya tatu ya 1 Wakorintho 4:9 ya Tatuliano yatusaidia kuiona picha hii dhahiri ya Wakristo wenye kutaabika wakati inapowasema kama “watu waliowekwa wapigane na wanyama-mwitu.” (On Modesty, sura ya 14) Kama isemwavyo katika Biblia ya mwanafunzi James Moffat iliyotafsiriwa kwa halisi, wao walikuwa “kama watu waliohukumiwa wapige vita na wanyama katika uwanja wa michezo!” Kwa hiyo mtu aweza kuwazia maandamano ya ushindi ya nyakati za Warumi. Huko nyuma kinakuja kikundi chenye uaminifu cha mitume na Wakristo wengine wakielekezwa kwenye uwanja wa michezo kama wahalifu waliodharauliwa ambapo watazamaji watafurahia kutaabika kwao na kifo chao.
9 Bila shaka, inaelekea kama mtume Paulo, kama vile Wakristo wengine wa kwanza, alipambana hasa na wanyama-mwitu katika uwanja wa michezo, tukiamua kulingana na anavyosema katika 1 Wakorintho 15:32: “Ikiwa, kwa jinsi ya kibinadamu, nalipigana na hayawani wakali kule Efeso . . . ” Ni kweli kwamba Paulo alikuwa amekwisha pambana na watu “wa kinyama” katika “mahali pa michezo” pa mfano katika Efeso. (Matendo 19:29-41) Lakini angalia kwamba katika 2 Wakorintho 1:8-10 anaitaja “dhiki ile iliyotupata katika Asia [ambapo Efeso ulikuwa]” na ambapo, mtume Paulo anaendelea kusema, ‘tulijiona tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu . . . Mungu alituokoa.’ Hii inaelekea kudokeza kwamba wakati mmoja Paulo alipambana na wanyama-mwitu wa kweli katika uwanja wa michezo wa Efeso.
10. Zitaje taabu ambazo Paulo anasema ziliwapata wafuasi wa Kristo.
10 Walakini, katika 1 Wakorintho 4:9 Paulo anatoa mfano. Anasema kwamba “malaika na wanadamu,” wahudhuriaji wengi, waliitazama aibu, upinzani na mateso ambayo yalimpata yeye na wenzi wake walipokuwa wakiiendesha huduma yao. Anaendelea kuieleza taabu iliyowapata:
“Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi [wengine katika Korintho] ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima. Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao; kisha twataabika tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili; tukisingiziwa twasihi; tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote hata sasa.”—1 Kor. 4:10-13. Linganisha Waebrania 10:32-34.
11. Ni nani aliyewaacha mitume wafanywe tamasha hiyo?
11 Kujapokuwa kutaabika ambako mitume walikuvumilia, watu wenye kuwaza mambo ya kiroho huko nyuma wangalijua kwamba Mungu aliwategemeza mitume. Kama Paulo alivyosema, watu hao wangejua kwamba “Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe.” (1 Kor. 4:9) Ndiyo, Mungu aliwaacha mitume waonekane kuwa wadogo kulingana na kanuni za ulimwengu.
12, 13. (a) Kwa hiyo, ni akina nani leo wanaoweza kutazamia kutaabika? (b) Ni ulizo gani linalotokea?
12 Leo mashahidi wa Yehova wanataabika namna ile ile wanapoiendesha huduma yao ya ulimwenguni pote. Hii haina maana ya kwamba Mungu amewakataa. Kwa kweli, katika makala iliyotangulia ilionyeshwa wazi kwamba mtu analihitaji kundi la kisasa la mashahidi wa Yehova leo aweze kuwa mtu wa kiroho. Kweli haipatikani kwa wale wanaopendwa sana na ulimwengu. Mtume Paulo anatukumbusha hivi: “Wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.”—2 Tim. 3:12.
13 Lakini ulizo latokea: Je! leo watu wengi wanaosema ni “Wakristo” wasio mashahidi wa Yehova hawapatwi pia na mateso? Ni kweli, wengi wanaojidai kuwa “Wakristo” wanataabika leo. Hata wapagani na wasioamini kuwako kwa Mungu wanateswa. Lakini kwa sababu gani wanataabika? Watu wa kiroho kweli kweli wanayaamini na kuyatetea mambo yale yale ambayo Yesu na mitume wake waliyatetea, kwa hiyo wanapatwa na upinzani kwa sababu zile zile.
JE! KRISTENDOMU NI “TAMASHA KWA DUNIA” YA KISASA?
14. Je! makanisa ya Kristendomu yanataabika? Kwa sababu gani?
14 Je! lo lote la makanisa ya Kristendomu linauwakilisha Ukristo wa kweli? Je! watu wake ni wa kiroho na je! kwa sababu hiyo wanapatwa na chuki na mateso kwa sababu ile ile kama Wakristo wa karne ya kwanza? Makanisa mengi ya Kristendomu leo yanaudhika. Yanapoteza washiriki na fedha. Maongozi yake yanafifia. Lakini si kwa sababu wanataabika kwa ajili ya haki kama mitume. (Linganisha 1 Petro 2:19-21.) Twajuaje? Angalia hili:
15. Makanisa yanalinganaje na mitume kwa habari ya kuamini unyofu au ubaya wa kuua?
15 Mitume waliamini kwamba ni vibaya kuua, hata kuchukia. (1 Yohana 4:20, 21; Ufu. 21:8) Je! makanisa ya Kristendomu hayakuachilia mauaji ya jumla ya ulimwengu katika uwanja wa vita, kuyaunga mkono na kutia moyo juu yake? Kitabu Black Jack Pershing cha Richard O’Connor chatusaidia kulijibu ulizo hili. Kinasema hivi juu ya kuingia kwa Amerika katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza:
“Hakuna watu waliofanya haraka zaidi kutaka Amerika iende vitani kuliko wahudumu wa Mungu. The New York Federation of Churches iliitangaza tarehe ya Machi 11 kuwa ‘Jumapili ya Vita.’ Kutoka pwani hata pwani, mapadre wenye kutaka vita walikana kwamba Kristo hakuwa mpatanishi, kwamba vita haikuwa mbaya, kwamba kuua Wajeremani hakukuwa uvunjaji wa zile Amri. Mweneza Injili Billy Sunday, akihutubia makutano katika Times Square, alikuwa akidhihirisha mawazo yao zaidi tu alipopiga kelele, ‘Kama hell ingeweza kupinduliwa, ungeona nyuma yake pameandikwa, “Imetengenezwa katika Ujeremani”!”
Katika nchi ambako makanisa au viongozi wa Kristendomu wamewekewa vizuizi, kwa kawaida ni kwa sababu ya kujitia kwao kwa muda mrefu katika siasa. Hivyo twasoma hivi katika New York Times la Oktoba 21, 1973: “Wakuu wa kijeshi wa Chile leo wameagiza mapadre watatu wa kigeni wafukuzwe. Mapadre hao—Waspania wawili na Mfaransa mmoja—walikuwa wamekuwamo katika ‘utendaji wa kupita kadiri,’ kulingana na habari rasmi.”—Ukurasa wa 9.
16, 17. Je! makanisa ya Kristendomu yanaamini na kutenda kama mitume (a) katika adili (b) katika shauri la kusema uongo?
16 Mitume walichukizwa sana na uzinzi, uasherati na ufiraji nao waliwaondoa wale walioendesha mazoea hayo machoni pao. Paulo alisema waziwazi: “Mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.” (1 Kor. 5:11-13; 6:9-11) Lakini ni wakati gani uliokuwa mara yako ya mwisho kusikia mtu akifukuzwa katika kanisa lako—au kanisa lo lote la Kristendomu—kwa sababu ya mazoea hayo?
17 Waongo hawakuruhusiwa katika kundi la kwanza la mitume. (Matendo 5:1-11) Lakini je! ni viongozi wangapi na wafanya biashara unaowatumaini kama wasiosema uongo? Na hali, je! wao, sana sana, si washiriki wa kanisa—pengine lako mwenyewe?
18. Hivyo, kwa sababu gani twaweza kusema kwamba Kristendomu si “tamasha kwa dunia”?
18 Majibu ya maulizo haya ya wazi. Matengenezo mengi yanayoachilia mazoea hayo, bila ya kujali kujidai kwao kwa kinafiki kuwa “ya Kikristo,” si “tamasha kwa dunia.” Bali, yanapatana na ulimwengu. Kristendomu imejionyesha kuwa “rafiki wa dunia,” na kwa hiyo “adui wa Mungu” pia. Mungu anawaita hao “wazinzi.”—Yak. 4:4.
19. Ni jambo gani ambalo lingali mbele ya Kristendomu?
19 Hivyo, maumivu yanayoyapata makanisa ya Kristendomu hayayapati kwa sababu ya kufuata nyayo za Yesu wala za mitume. Yanavuna yaliyoyapanda; yanastahiliwa. Kutaabika kwayo sasa ni mwanzo tu wa yanayotazamiwa kuijilia milki nzima ya ulimwengu ya dini ya uongo, inayosimuliwa katika kitabu cha Ufunuo kama kahaba aliyepambwa sana aliyeketi juu ya mnyama. Kama vile kahaba huyo, dini ya uongo inajaribu kuyaongoza mataifa ya kinyama. Lakini “mnyama” aliyetajwa humo katika Ufunuo anamgeukia na kumwangamiza. Wakati wa kukoma kwa dini yote ya uongo wakaribia sana. Wale walio sehemu yake sasa si watu wa kiroho wanaotaabika kwa ajili ya haki. Wao wana sababu ya halali kupatwa na wasiwasi, hata kuogopa.—Ufu. 16:12-21; 17:15-18; sura ya 18; linganisha Ezekieli sura ya 24; Mathayo 13:42.
MASHAHIDI WA YEHOVA—“TAMASHA KWA DUNIA” YA KISASA KATIKA MATESO
20-22. Mashahidi wa Yehova wanataabikaje?
20 Kwa upande mwingine, mashahidi wa Yehova wametaabika sana katika nyakati za kisasa. Walichukiwa sana katika Ujeremani ya Kinazi. Barua iliyochapwa kwa ajili ya Commission for Ecumenical Affairs of the Archdiocese of Hartford, Connecticut, inaukubali ukweli huu, ikisema: “Wayahudi wa Ujeremani . . . hawakuteswa peke yao katika kambi za mateso za Hitler. Mashahidi wote [wa Yehova] wajulikanao nchini mwao walifungwa pia. Ndipo walipoambiwa wangeachwa huru kama tu wangeinama na kujikana. . . . Kunyongwa, kupigwa risasi wala kuteswa kikatili kwa mwili au akili kusingeweza kuwageuza. Hasira ya mapolisi wa SS ilikuwa nyingi sana kwa sababu mashahidi wasingeweza kujikomesha.”
21 Siku hizi Mashahidi wanatendewaje wakiwa chini ya serikali? Twasoma hivi katika kitabu Aspects of Religion in the Soviet Union 1911-1961: “Mashahidi wa Yehova wanapigwa marufuku katika ulimwengu wote.” Katika mataifa mengine, pia, Mashahidi wamekuwa tamasha. Kwa mfano, je! ulijua kwamba katika Uturuki ni “uvunjaji wa sheria” kwa mashahidi wa Yehova kumwabudu Mungu? Wanafanyiwa mashtaka ya uongo kabisa. Mashahidi mmoja mmoja katika Uturuki wanafainiwa sehemu kubwa ya mapato yao ya mwaka.
22 Katika Bara ya Afrika, mashahidi wa Yehova wamekuwa ndio watu wa kuchukiwa zaidi katika Malawi kwa miaka kadha. Wanaume wengi wamepigwa, ndiyo, wengine wameuawa. Wamepoteza kazi na kuona wake zao wakinajisiwa. Maelfu wamefukuzwa kama ng’ombe si nyumbani kwao tu, lakini nchini mwao hasa.
23, 24. (a) Je! Mashahidi wanataabika kwa sababu wamejishughulisha na siasa za mataifa au kwa sababu ni wafisadi? (b) Basi kwa sababu gani wanataabika?
23 Lakini kwa sababu gani wametaabika hivi? Je! ni kwa sababu wamejaribu kuyaongoza mambo ya kisiasa ya mataifa mbalimbali ambamo wanakaa? Sivyo! Je! wameziacha kanuni bora ambazo Yesu na mitume wake walitetea? Angalia vile mtu wa nje, mtazamaji asiyependelea, anavyosema juu ya mwenendo wa Mashahidi. Bryan Wilson wa Oxford University anasema hivi juu ya kutaabika kwao katika Afrika:
“Hata hivyo, kupiga marufuku . . . huenda kukaleta hasara nyingi zaidi kuliko inavyoelekea kuwa. Mashahidi wamefanikiwa zaidi sana katika kuwafanya wafuasi wao waendeleze kanuni bora za ugumu wa adili na kujiadibisha. Wanafundisha ubora wa bidii, ukawaida, kiasi na kujiheshimu. Uhusiano wa jamaa wa washiriki wao ni bora kama isivyo kawaida katika Afrika Mashariki. Njia zao za kufundisha ni zenye matokeo mazuri sana katika mashauri ya adili na ya elimu pia . . . Wanasiasa wa Kiafrika kwa kawaida wanalaumu ukabila. Pengine Mashahidi ndio wenye kufanikiwa zaidi kuliko kikundi kingine katika mwendo ambao wanaondoa ukabila kati ya washiriki wao.”—New Society, Julai 12, 1973, ukurasa 75.
Kwa wazi, mashahidi wa Yehova si hatari kwa sheria na utengemano. Wao ni Wakristo wa kweli. Wanafikia hali za maisha ambazo kila taifa lililoelimishwa linazitaka kati ya raia zake.
24 Mashahidi wa Yehova wanaliwakilisha kabisa kundi la kweli la Kikristo. Hii yahakikishwa na namna wanavyojaribu kwa uangalifu kuyatumia Maandiko katika maisha zao wenyewe. Kundi lao la kisasa linalingana na lile lililosimamiwa na mitume na manabii katika karne ya kwanza. (Efe. 2:20-22) Watu wake wanafundisha kweli zile zile. Mashahidi wa Yehova ni “tamasha kwa dunia” ya kisasa katika kutaabika kwa ajili ya mambo yale yale ambayo Yesu na mitume wake walitaabikia. Na kama tengenezo, wao wanajua kwamba wataendelea kupatwa na dhiki hata mwisho wa hii taratibu mbovu ya mambo.—2 The. 1:6-10.
JE! WEWE UTAINGIA KATIKA UWANJA WA MICHEZO WA KISASA?
25. Ni ulizo gani linalomkabili kila mtu?
25 Lakini kuna ulizo kwa kila mtu: “Je! mimi mwenyewe nina nia ya kuukubali upinzani ule ule na kuwa sehemu ya “tamasha kwa dunia” ya kisasa inayoonyeshwa na watu wa kiroho wa kisasa?” Ikiwa unataka, unaweza kulithamini shauri ambalo Paulo alimpa Timotheo: “Usiuonee haya ushuhuda juu ya Bwana wetu, wala juu yangu mfungwa kwa ajili yake, bali ushiriki sehemu yako katika kupatwa na uovu kwa ajili ya habari njema kulingana na uwezo wa Mungu.”—2 Tim. 1:8, NW.
26. Awezaje mtu kuvumilia taabu kama mtu wa kiroho kweli kweli?
26 Huenda ukauliza, awezaje mtu kuvumilia taabu hiyo? Kuna njia moja tu ambavyo mtu aweza kuendelea kuwa imara kama Mkristo ‘anapopatwa na uovu’: Lazima awe mtu wa kiroho, awe na maoni ya Mungu juu ya mambo. Atajua kwamba anataabika kwa ajili ya kweli. (Mt. 5:11) Lakini ikiwa kuwaza kwa kimwili kunayageuza maisha yake na anayo maoni ya kilimwengu, hata mtu anayejidai kuijua njia ya kweli huenda akaeleza mambo kulingana na akili za kibinadamu na kuridhiana. Hii ingeweza kuelekeza kwenye uharibifu wake wa milele. Kwa hiyo, kukiwa kungali kuna utulivu wa kadiri katika sehemu kubwa ya ulimwengu, sasa ndio wakati wa kujitahidi kusitawisha “nia ya Kristo” na kuiacha iongoze katika kila upande wa maisha ya mtu. Jitahidi ujifanye namna ya mtu ambaye Mungu angemkubali wakati wo wote.
27. Ni maelekeo gani ambayo imempasa mtu wa kiroho ayaepuke? Badala yake, maoni yake yamepaswa yawe nini?
27 Si jambo la hekima kuendelea kuwa na woga mwingi juu ya majaribu ya wakati ujao. Wala si jambo la busara kujiumiza na mawazo yanayohusu mambo ambayo huenda adui watawafanyia watu wa Mungu siku moja. Badala yake, Mkristo atauonyesha uaminifu wake kwa Mungu kila siku. Upinzani waliouvumilia mitume haukuwa mateso makali ya papo hapo tu. Kumbuka, Paulo alisema hivi katika 1 Wakorintho 4:10-13 (kulingana na The New American Bible): “Sisi ndio walio dhaifu . . . wanatufanyia mzaha . . . twaona njaa na kiu, hatuvikwi vya kutosha, twatendewa vivi hivi . . . hatuna makao . . . twatukanwa . . . twachongewa.”
28. Ni kwa njia gani zaidi ambavyo Wakristo wa kweli leo wanataabika zaidi ya kuteswa vikali na adui?
28 Leo Wakristo wa kweli lazima wavumilie kutendewa namna ile ile. Sikuzote si “adui” wanaotenda hivyo, bali huenda wakawa ni wale tunaowapenda, washiriki wa jamaa yetu wenyewe (1 Pet. 2:18-3:6), au watu tuliokua nao. Huenda wakati fulani Mkristo akaonewa katika kazi yake kwa sababu ya kanuni zake bora. Au huenda akaona inamlazimu kuacha cheo kikubwa chenye mshahara mkubwa kwa sababu hakipatani na dhamiri yake iliyozoezwa na Maandiko; kwa hiyo huenda akapasishwa mikazo mingi na kufanyiwa mzaha. Au huenda Mkristo kijana akadhihakiwa na wanadarasa wenzake kwa sababu anatetea anayojua kuwa haki kama mwanamume wa Kikristo. Ikiwa Wakristo wanaweza kupambana na matendo hayo yote leo—nao wanafanya hivyo kila siku—sababu gani wauogope mno wakati ujao? Mtu wa kiroho anajua kwamba anaweza kuvumilia lo lote analoruhusu Mungu. Kama vile mitume na Yesu mwenyewe, mtu wa kiroho anafanya lengo lake liwe kuwa mtu mwenye uhodari mwingi na furaha.—Yohana 16:33; Rum. 12:12; Kol. 1:24; 1 Pet. 1:6, 7; 3:14; 4:12-16.
29. Ni matumaini gani yaliyoko mbele ya kila mtu aliye wa kiroho kweli kweli?
29 Kwa wazi, kuwa mtu wa kiroho si shauri la unafiki tu. Lazima kuonyeshwe katika kila jambo analofanya mtu. Endelea kuzidisha uaminifu wako kwa Yehova. Ukifanya hivyo utaweza kupambana na matatizo yo yote na mateso yaliyoko mbele. Kwa kuvumilia mateso utaendelea kuwa sehemu ya “tamasha kwa dunia” hata mwisho wa hii taratibu nzima ya mambo. Ndiyo, kama mtu wa kiroho utaliokoka shambulio kali la Gogu juu ya “wakaao katikati ya dunia,” na kuishi katika taratibu mpya ya mambo iliyo nzuri ajabu.—1 Kor. 4:9; Eze. 38:12; Ufu. 21:1-4.
—Kutoka The Watchtower, April 1, 1974.
[Picha katika ukurasa wa 445]
Wakristo wa kweli ni “tamasha kwa dunia” kama vyombo vya mateso yake