Kwa Sababu Gani Mashahidi wa Yehova Wanapendezwa Nawe?
PENGINE wewe umetembelewa mara nyingi na mashahidi wa Yehova ukachukua nakala kadha za vitabu vya Watch Tower. Kwa hiyo pengine wakosa kujua sababu ya Mashahidi kuendelea kukutembelea.
Hawapendezwi na pesa zako. Huenda likasikika kuwa jambo geni siku hizi, lakini mashahidi wa Yehova wanakupenda. Wanaamini kwa moyo kwamba maisha yako yamo katika hatari halisi, inayokaribia sana. Wanajitahidi kukuelewesha jambo hilo, kwa sababu wanaamini pia liko jambo jepesi unaloweza kufanya ujilinde mwenyewe na jamaa yako pia.
Pengine unajua kwamba mashahidi wa Yehova hawajaribu kukutumia wajifaidi wenyewe. Ikiwa wao ni jirani zako unajua kwamba wanafanana nawe kwa njia nyingi. Wanafanya kazi wajipatie riziki. Lakini wanatofautiana nawe kwa sababu wanatumia wakati mwingi wakisema na watu juu ya makusudi ya Mungu.
Si kwamba mashahidi wa Yehova wasingefurahia kutumia wakati zaidi wakikaa nyumbani karibu na moto mzuri, wakisoma, au kutazama televisheni, au kuketi kivulini wakiwa na kinywaji cha baridi. Wangeweza kuwa katika bustani au mahali pa kutembelea, ziwani au milimani. Lakini wanatumia saa nyingi wakitembelea watu kama wewe, ambao pengine hawawajui. Kwa sababu gani?
Wanajua, kama ujuavyo, kwamba ulimwengu huu hauna upendo, na kwamba ni watu wachache sana wanaosema maneno ya kirafiki na ya kuchangamsha. Lakini wao wanajua sababu na njia ya kuondoa tatizo hilo. Wanajua kwamba ulimwengu huu utakoma karibuni. Hawajui hivyo kwa sababu wana hekima ya juu zaidi kuliko watu wengine; wanajua kwa sababu wanakisoma kitabu cha pekee ambacho kinatoa maana halisi kinapojibu njia za kutatua matatizo ya leo na kuonyesha yaliyoko mbele.
Kitabu hicho ndicho Biblia. Mashahidi wa Yehova wanaamini kabisa Biblia na wanajua kwamba ndicho chanzo cha pekee kinachotoa tumaini—la serikali njema, la afya, uzima, amani duniani, na la kutokuwa na woga wala kifo. Hakuna hata ahadi moja kati ya hizo inayotoka mahali pengine po pote. Kwa sababu gani usisikilize angaa jambo fulani wanalokuambia Mashahidi?
Watu wengi wanaofahamiana na mashahidi wa Yehova wanasema ni watu wema, wenye utaratibu, wenye watoto ambao kwa kawaida wana adabu. Makusanyiko yao makubwa yameitwa vielelezo vya amani na utaratibu. Maelezo yametolewa, hata katika magazeti, kwamba Mashahidi ni wenye busara wanaposhughulika na watu, ni safi, ni mifano myema mtaani, ingawa (wanaendelea kusema) imani za Mashahidi si za kawaida.
Lakini, fikiri. Je! mambo anayoamini mtu na kuyafuata siyo yanayomfanya awe alivyo? Mashahidi wa Yehova wametoka katika namna zote za maisha, na wengi wao zamani hawakuwa wenye busara katika kushughulika na watu wala hawakuwa wakitafuta amani. Lakini mambo ambayo wamejifunza katika Neno la Mungu yamebadili maisha zao. Mmoja wa mitume wa Kristo alieleza kweli hiyo kwa Wakristo wa kwanza alipoandika hivi:
“Basi vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu: kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu. Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote.”—Kol. 3:5-8.
Hivyo ndivyo mashahidi wa Yehova wamefanya kwa kujifunza Biblia na kujitahidi kutumia waliyojifunza katika maisha zao.
Wakati mashahidi wa Yehova wakuachiapo vitabu, je! wanakuwa wametimiza kusudi lao? Je! wewe unachukua vitabu uwatie moyo au ‘uwasaidie’? Mashahidi wanashukuru kwa fadhili yako. Lakini wao hawatafuti msaada. Mambo yaliyomo katika vitabu ndiyo wanayotaka ufahamu. Wanajua yanaweza kukusaidia wewe uone la kufanya katika nyakati hizi za hatari. Kusudi lao ni kuokoa uhai wako. Ikiwa huoni kwamba taratibu hii ya ulimwengu itapita, wewe na jamaa yako mwapaswa kujua hivyo.
Lakini si hayo tu. Bila ya kuwa na maoni mazuri, bila ya tumaini, usingefaidika. Biblia yatoa habari njema—habari za kwamba nafasi ya taratibu hii ya mambo itachukuliwa na serikali ya Mungu itakayotawala dunia. Badiliko hilo litatuka katika kizazi hiki, wakati ambao mwanadamu amefikia hatua yake ya mwisho. (Mt. 24:34) Sio mashahidi wa Yehova wanaosimamisha serikali hiyo. Mungu ndiye. Wao wanataka kuokoka waishi wakiongozwa nayo, Je! wewe unataka? Wanaotaka hivyo lazima wafuate mwendo tofauti na ule unaofuatwa sasa na watu wengi.
Mashahidi wa Yehova hawataki ujiunge na “dini” tu. Wao si watu wanaofuata dini tu. Wao ni Wakristo wa kweli. Wanakuletea habari ili uweze kuchukua hatua ujilinde mwenyewe, kwa kufuata uamuzi wako mwenyewe, kwa akili.
Utendaji wa namna hiyo si jambo jipya. Si kwamba sasa Mashahidi wamekuwa wenye bidii karne moja tu, bali mashahidi wa Yehova wa zamani pia walikuwa wenye bidii nyakati fulani za hatari. Ni kwa sababu Mungu hutoa onyo la jambo atakalofanya.
Mungu alimtumia Nuhu kutolea ulimwengu uliokuwa kabla ya gharika maonyo mengi sana, kwa miaka 50 au zaidi.—2 Pet. 2:5.
Yesu Kristo na wafuasi wake walisihi Wayahudi wajiokoe wasiharibiwe na kizazi hicho. (Mt. 23:33-39; Matendo 2:40) Kwa sababu gani Yesu alifanya hivyo? Ni kwa sababu aliwapenda wenye mioyo minyofu kati ya watu hao. Wengi walisikia, wakaukimbia Yerusalemu na kuokoka uharibifu wa mji huo ulioletwa na majeshi ya Kirumi. Zaidi ya watu milioni moja walikufa katika eneo hilo dogo sana lililozungukwa na kuta za Yerusalemu, na 97,000 wakapelekwa wakiwa mateka.
Sasa taratibu hii ya mambo ya ulimwengu isiyomcha Mungu inakaribia kuondolewa mbali, katika wakati wa taabu nyingi. Lakini hali za maisha yenye haki zitafuata chini ya Ufalme wa kimbinguni. Wakati wa utawala wa Ufalme huo, Mungu atafufua wafu na kuwawekea mbele yao nafasi ya kuishi milele. Baraka ya Mungu itafanya kuwe na afya kamili na uzima wa milele kwa wanadamu wenye utii.—Ufu. 21:3-5.
Je! wewe unataka kuishi katika dunia ya namna hiyo? Mashahidi wa Yehova wanataka uokoke uifurahie. Wao watakusaidia kwa nguvu zao zote. Watafurahi kutumia wakati wao wenyewe na pesa zao wenyewe wakutembelee na kujifunza nawe Biblia, bila malipo. Chukua hatua sasa ili ‘ushike sana uzima ulio kweli kweli’ wewe mwenyewe na jamaa yako.—1 Tim. 6:19.