Kupata Kumjua Mungu
“Mmepata kumjua Mungu, au zaidi . . . mmepata kujulikana na Mungu.”—Gal. 4:9, NW.
1. Kuna tofauti kati ya kumjua Mungu na kujua habari zake?
WATU wengi wanajua habari za Mungu. Pengine wanaishi katika mitaa ambamo raia walio wengi wanajidai kuamini kwamba yeye yuko. Lakini je! hii yamaanisha wao wanamjua Mungu kweli kweli? Basi, kuna tofauti kati ya kujua habari za mtawala wa nchi ambako mtu anaishi na kufahamiana naye wewe mwenyewe. Kwa hiyo, pia, ndivyo ilivyo na kumjua Mungu. Watu wanaomjua Mungu kweli kweli wanafurahia uhusiano halisi naye.
2, 3. Kwa sababu gani watu wengine hawaamini Mungu yuko?
2 Bila shaka, watu wengine hawapendezwi hata kidogo na kujua habari zo zote juu ya Mungu. Hata hawaamini kwamba yeye yuko. Kwa sababu gani? Pengine wanashtushwa sana na unafiki unaoendeshwa na wengi wanaojidai wanamwamini. Huenda wakaonyesha matendo ya ukatili sana na umwagaji wa damu wa makusudi ambao wengine wameendesha kwa jina la Mungu na dini. Lakini je! ni jambo la akili kukana kuwako kwa Mungu kwa sababu ya mambo ambayo wanadamu wamefanya? Je! hiyo isingekuwa kama kusema kwamba mtawala wa nchi fulani hayuko kwa sababu watu wanaosingizia kuwa raia zake waaminifu wamemwakilisha vibaya? Je! lingekuwa jambo la akili kuacha masingizio ya watu wengine yazuie kusitawi kwa uhusiano ambao ungeongeza furaha na afya ya mtu yenye kudumu?
3 Na wengine hawataki kabisa wawe na wajibu kwa Mungu. Wao wanataka kuweka kanuni zao wenyewe za kuishilia. Huenda hata wakajitafutia sababu za ubishi wakijaribu kuonyesha kwamba Mungu hayuko. Mara nyingi sababu zao zinakuwa za kujidanganya wenyewe tu, kama vile mwandikaji anayejulikana sana Aldous Huxley alivyokubali wakati mmoja: “Nilikuwa na makusudi ya kutotaka ulimwengu uwe na maana, kwa hiyo nikajifanya niwazie kwamba haukuwa na maana yo yote, nami nikaweza kupata sababu za kutosheleza za kuwazia huku bila shida yo yote.” Lakini kupendelea kwa mtu kuamini kwamba Mungu hayuko ili awe na maisha ‘yenye uhuru’ kwa wazi hakufanyi Mungu atoweke. Yeye anaendelea kuwako, yeye yuko.
4. Ni ushuhuda gani umesadikisha watu walio wengi kwamba bila shaka kuna Mungu?
4 Wakifikiria habari hii, watu walio wengi wanaongozwa kukubali kwamba bila shaka kuna Mungu. Ulimwengu wote wenye kustaajabisha sana, uzuri wake na utaratibu wake, namna zake mbalimbali za mimea na wanyama, mwanadamu mwenyewe—vyote vinaonyesha kuna Mpangaji stadi, Muumba wa uhai na asili ya vitu. Mamilioni ya watu wenye akili ulimwenguni mwote wamepata pia kuthamini sifa fulani za Mungu kwa sababu ya vitu wanavyoweza kuona. Wanakubaliana na mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu: “Sifa [za Mungu] zisizoonekana zinaonekana waziwazi kwa vitu vilivyofanywa.”—Rum. 1:20, NW; Matendo 14:16, 17.
5. (a) Uwezo wa dhamiri unahakikishaje kwamba Mungu yuko? (b) Kuwa kwa mwanadamu na uwezo wa dhamiri kunafunua nini juu ya Mungu?
5 Uwezo wa mwanadamu wa dhamiri ni mfano mmoja wa kweli hii. Biblia inaonyesha kwamba uwezo huu, fahamu hii ya ndani au maono ya yaliyo haki na mabaya, unatoa ushuhuda wa ‘sheria iliyoandikwa moyoni.’ (Rum. 2:14, 15, NW) Kwa wazi wanadamu hawakupata “sheria” hiyo kwa wanyama wakatili, kwa maana kazi zake hazionekani kati yao. Kuwako kwa “sheria” hii ya ndani ndani kunahakikisha kwamba bila shaka kuna mtunga sheria mwenye akili—Mungu. Tena, uwezo huu unafunua hekima ya Muumba na kupendezwa kwake kwingi na upendo wake kwa mwanadamu. Dhamiri ya mwanadamu imesaidia kuzuia matendo yanayohatirisha maisha, afya na usalama wa wanadamu. Kwa kawaida uwezo wa dhamiri unakataza makosa yale yale mamoja nyakati zote na mahali pote. Hata bila ‘orodha ya sheria’ yo yote iliyoandikwa, wanadamu wamejua nyakati zote kwamba mambo kama uuaji, wizi, uzinzi na ngono zilizopotoka ni mabaya. Maarifa haya ya kurithi yameipa jamii ya kibinadamu imara ya kadiri fulani, zaidi kwa mpango wa jamaa. (Mwa. 34:7; 39:9; Ayubu sura 31; 2 Pet. 2:6, 7) Kwa kweli uwezo wa dhamiri ni zawadi ya Mungu mwenye hekima yote na upendo.
NAMNA YA KUPATA KUMJUA MUNGU
6. Kwa sababu gani kujua Mungu ni mtu ni msingi wa Kupata kumjua yeye?
6 Lakini tunawezaje kupata kweli kumjua Mungu asiyeonekana ambaye amejifunua aonekane alivyo kupitia kwa kazi zake za uumbaji? Hatua ya kwanza katika habari hii ni kujua kwamba yeye ni mtu. Mtu anaweza kufahamiana sana au kuwa na uhusiano imara na mtu tu mwingine. (Ebr. 11:6) Mara nyingine wale wanaojidai kuamini kuna Mungu mwenye ukuu wote wanakosa kutambua yeye ni mtu. Mwandikaji wa historia ya maisha ya watu R. W. Clark anadai hivi juu ya mwanasayansi mmoja anayejulikana sana: “Mungu wa Einstein anaonekana kama ulimwengu halisi.” Lakini, basi, je! ulimwengu halisi hauonyeshi utaratibu? Na je! utaratibu si ishara ya akili? Je! akili sikuzote haishirikishwi na utu, na mtu? Kwa hiyo yeye anayeleta utaratibu katika ulimwengu wote, Mungu, bila shaka ni mtu.
7. Uumbaji na kufikiri vinaachana maulizo gani bila kujibiwa?
7 Kufikiri na kuchunguza kunafunua waziwazi si kwamba tu Mungu yuko bali pia kwamba yeye ni mtu kweli kweli, na kwamba anazo sifa za kutamanika. Lakini mengi zaidi kuliko kufikiri kwa kuchunguza ulimwengu wote ulio halisi yanahitajiwa ili mtu apate kumjua Mungu, kufurahia uhusiano naye. Kwa sababu gani? Kwa sababu kufikiri kwetu juu ya vitu tunavyoviona kunaacha bado maulizo mengi juu yake bila kujibiwa. Kwa mfano, huenda kufikiri kukatuambia kwamba kuna Mungu. Lakini je! kutatuambia sababu gani kuna uovu ulimwenguni? Huenda kufikiri kukaonyesha kwamba Mungu mwema asingevumilia uovu milele. Lakini je! kunatuambia wakati ambao tunaweza kutazamia hali hizo ziishe?
8. Mwanadamu anahitaji nini ili amjue Mungu mwenyewe?
8 Kwa hiyo, basi, ni nini kingine kinachohitajiwa? Ufunuo kutoka kwa Mungu mwenyewe. Mithali ya kale inasema hivi: “Pasipo maono [au, ufunuo] watu huacha kujizuia.” (Mit. 29:18) Ndiyo, bila uongozi wa ufunuo wa kimungu, watu wengi wanaelekea kutojizuia katika mwenendo wao, zaidi wanapofikiri wanaweza ‘kuponyoka wasipatikane.’ (Mhu. 8:11) Dhamiri yao isiyokamilika haitoshi kuwazuia. Kwa hiyo Mungu ametoa ufunuo katika Neno lake lililoandikwa, Biblia, upate kutuongoza. Linatufunulia kwamba jina lake ni Yehova na kueleza matendo yake, makusudi, mawazo ya ndani na nia kwa njia ambayo tunaweza kupata kumjua. (Zab. 83:18) Biblia haituachi na shaka juu ya mambo ambayo Mungu anakubali au anayokataa.
9. Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba Biblia imetoka kwa Mungu?
9 Lakini kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba Biblia imetoka kwa Mungu? Kwa sababu ina habari ambazo zisingeweza hata kidogo kutokana na wanadamu. Wanadamu hawawezi kutabiri kwa usahihi kabisa yatakayotukia miezi michache tu tangu leo. Walakini, Biblia inao unabii mwingi ulioandikwa zamani, ambao umetimizwa kwa usahihi au unaoendelea kutimizwa. Ingawa Biblia iliandikwa kwa kipindi cha zaidi ya karne kumi na sita, si kitabu chenye kujawa na filosofia zenye kupingana na kubadilika-badilika, kama ambavyo ingetazamiwa kwa kazi inayotokana na mwanadamu. Upatano wake wa ndani unaonyesha waziwazi ina chanzo cha kimungu. Sheria na kanuni zilizomo ndani ya Biblia hazilinganiki na cho chote ambacho wanadamu wametokeza kiwe kiongozi cha maisha. Sheria zinazosemwa na Biblia zinavuta dhamiri njema na hata zinasaidia kufanya maamuzi yanayofaa, Wakati ule ule Biblia inafunua kanuni bora za Mtunga sheria, Mungu. Na tuangalie namna sehemu moja ya Biblia, Torati iliyopewa kupitia kwa mpatanishi Musa (inayopatikana katika vitabu vya Kutoka, Mambo ya Walawi, Hesabu na Kumbukumbu la Torati) inavyotusaidia tumjue Mungu kama Mtunga sheria mwenye haki na rehema. Tunaweza kufanya hivi kwa kuilinganisha Torati hiyo na jitihada za kibinadamu za kutunga na kufikiliza sheria.
KUJIFUNZA JUU YA REHEMA
10, 11. (a) Wanadamu wamejaribuje kushindana na maovu yanayofanywa kwa jamii ya watu kama vile wizi? (b) Vile torati ya Musa inavyosema juu ya wizi inamfunuaje Mungu kuwa mwenye rehema?
10 Sheria za karibu kila taifa zinakataza maovu yanayofanywa kwa jamii ya watu. Lakini mtu anapoiba—iweje? Mwenye kuiba atendeweje? Kwa kame nyingi wanadamu wamepambana na magumu haya na mara nyingi zaidi wakashindwa kupata matokeo mazuri. Dhamiri isiyokamilika ya kibinadamu haifunui jibu kabisa ikiwa peke yake. Katika Babeli ya kale, Orodha ya Sheria ya Hammurabi ilikuwa kali, yenye kuamuru, kwa mfano, ilisema kwamba mwizi aliyeshikwa akiwa karibu na moto atupwe motoni. Mvunja nyumba usiku alipaswa anyongwe hadharani akielekeana na tundu alilotoboa alipokuwa akivunja aingie nyumbani. Leo wanaume na wanawake wanaoshtakiwa wizi wanawekwa gerezani kwa kawaida ambako mara nyingi wanakuwa wavunja sheria wa kuzoea. Wakati uo huo, inakuwa lazima waibiwa maskini waishi wakiwa na hasara zao.
11 Mungu alifunua visa vya wizi vilipaswa vishughulikiweje katika taifa la kale la Israeli? Kwa njia yenye rehema lakini yenye haki. Tunasoma hivi katika Kutoka 22:1-4, Swahili Congo Bible: “Na kama mutu akiiba ngombe ao kondolo na kumuchinja ao kumwuza, atalipa ngombe watano kwa ngombe mumoya, na kondolo wane kwa kondolo mumoya. . . . Inamupasa yeye kulipa . . . Alichoiba kikionekana hai mukononi mwake akikuwa ngombe, ao punda, ao kondolo; atalipa mara mbili.” Hivyo, mwenye kuiba alipewa adhabu kwa kulazimishwa alipe alichokuwa ameiba, pamoja na adhabu zaidi. Hii ilisaidia kukazia juu yake matokeo yote ya kosa lake. Halafu, tena, alitakiwa atoe dhabihu fulani, akikubali kwa njia hiyo kwamba alikuwa amemtenda Mungu dhambi pia. (Law. 6:2-7) Kwa habari ya mwibiwa, alirudishiwa kitu alichokuwa amepoteza. Adhabu iliyoongezwa juu ya mwizi ilimfaidi mwibiwa, ikimlipa vya kutosha faida ambazo angalipata kwa kutumia mali yake na kumlipa kwa sababu ya magumu yaliyotokezwa na jambo hili.
12. Ilikuwaje ikiwa mwizi alikuwa hawezi kulipa alichoiba?
12 Lakini namna gani ikiwa mwenye kuiba alikuwa maskini na asingeweza kulipa? Alipaswa auzwe afanye kazi kama mtumwa au mtumishi asiyepewa mshahara na kwa njia hiyo amalize kulipa deni yake, (Kut. 22:3) Ni nani anayeweza kukana kwamba mpango huo haukuwa wenye haki na rehema pia? Mwibiwa hakupata hasara ya daima. Mwenye kuiba hakuuawa; uhai wake haukulinganishwa na mali tu aliyokuwa ameiba. Wala hakuvunjwa roho wala hakudhoofishwa kwa kutiwa gerezani. Kipindi chake cha utumwa wa muda kilimpa nafasi ya kurekebisha kosa. Kwa hakika njia hiyo ya hekima na rehema ya kushughulikia jambo hilo ilitoka kwa Mungu.
TORATI YAFUNUA HAKI YA HUKUMU YA MUNGU
13. (a) Ni laumu gani linalotolewa nyakati nyingine juu masimulizi yaliyomo katika Kumbukumbu la Torati 21:18-21? (b) Kwa kweli, hii inaonyeshaje haki ya hukumu ya Mungu?
13 Twajifunza pia kutokana na Torati kwamba rehema ya Mungu ina mipaka. Je! hii maana yake ni kwamba adhabu za Torati zilikuwa za ukatili nyakati nyingine? Namna gani juu ya maneno yanayofuata yaliyomo katika Kumbukumbu la Torati 21:18-21, Swahili Congo Bible?
“Mutu akikuwa na mwana mukaidi na mwenye kuasi asiyetaka kutii sauti ya baba yake, ao sauti ya mama yake, nao wakimwazibu, hawasikilizi: halafu baba yake na mama yake wamukamate na kumuleta kwa wazee wa muji wake, na kwa lango la pahali pake; nao waambie wazee wa muji wake: Huyu mwana wetu ni mukaidi na mwenye kuasi, hataki kutii sauti yetu: ni [mlafi] na mulevi. Na watu wa muji wake wata mutupia mawe afe: hivi utaondola uovu katikati yako; na Israeli wote watasikia na kuogopa.”
Huu, kama wengine wasemavyo, ni mfano wa ukatili mwingi mno kwa watoto? Hata! Kwa kweli, masimulizi haya yanaonyesha wazi-wazi haki ya hukumu ya Mungu alipokuwa akishughulika na waovu wasiorudika waliokataa kuitikia walipotendewa kwa rehema. “Mwana” katika habari hii hakuwa mtoto mdogo bali alikuwa mwenye umri wa kutosha kuwa ‘mlafi na mlevi.’ Zaidi ya hayo, wazazi wake walikuwa wamemwonya mara nyingi, lakini yeye “hawasikilizi.” Na, lililo la maana zaidi, angalia kwamba mwana huyo hakuuawa mpaka alipokwisha kuletwa mbele ya “wazee wa muji wake.” Kanuni hii ya haki inatofautiana kabisa na mambo ambayo yamezoewa katika jamii fulani zenye kusimamiwa na wazee wa ukoo. Akizungumza juu ya makabila fulani ya jangwani katika Mashariki ya Kati, Raphael Patai anasema hivi:
“Kwa kweli, mamlaka kamili ya mzee wa ukoo juu ya uzima na kifo cha washiriki wa jamaa yake ilitia ndani na haki ya kuamua wakati alipozaliwa mtoto kama atamwacha aishi au atamlaani afe. Tunajua kutokana na hati za kihistoria . . . tangu nyakati zilizowatangulia Waislamu mpaka karne ya kumi na tisa kwamba mara nyingi baba aliamua kuua binti mara tu akiisha kuzaliwa au baadaye. Njia ya kawaida ya kuua binti aliyezaliwa karibuni ilikuwa kumzika akiwa hai katika mchanga wa jangwa.”—Family, Love and the Bible, uk. 122.
Kwa hiyo, kati ya makabila mengi, washiriki wa jamaa hawakuwa na nafasi ya kutendewa kwa haki mzee wa ukoo alipoamua kuwatenda vibaya bila kufuata sheria. Walakini, Torati ilimlinda hata mshiriki wa jamaa aliyeshtakiwa, ikimruhusu asikilizwe vizuri katika kesi. Hii inaonyesha wazi Mungu ni mwenye haki ya hukumu ya kweli, si Mwenye ukatili. Torati yake ilisawazisha rehema na haki ya hukumu vizuri sana!
KUPATA KUMJUA MUNGU KUPITIA KWA MWANAWE
14. Maisha ya Yesu yanatusaidiaje kupata kumjua Mungu?
14 Kama vile tunavyoweza kupata kujua na kuthamini kanuni za Mungu za kutamanika kutokana na Torati, ndivyo tuwezavyo kufanya kutokana na sehemu nyingine yote ya Biblia, zaidi kama zilivyofunuliwa kupitia kwa Mwanawe Yesu Kristo. Kwa maelfu mengi sana ya miaka kabla hajaja duniani, Mwana alikaa pamoja na Baba yake mbinguni. (Yohana 17:5; Kol. 1:13-17) Uhusiano wao ulikuwa wa karibu karibu sana nao walipatana sana hata Mwana angeweza kusema hivi: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9; 1:18) Wakati wa huduma yake ya kidunia, Yesu Kristo alikazia kanuni zilizokuwa chini ya torati ya Musa na Maandiko mengine yote ya Kiebrania. Yeye aliishi kulingana na kanuni hizo akafunua roho halisi ya Torati. Kupitia kwake, sifa za Mungu za kutamanika zinaweza kuthaminiwa vizuri zaidi.—Linganisha, kwa mfano, Mathayo 5:21-48; 19:3-9; 23:23.
15, 16. (a) Yesu alimaanisha nini aliposema imempasa mtu ‘amjue’ Baba na Mwana? Toa mfano. (b) Kwa sababu gani kukubali Yesu Kristo ndiye Bwana aliyetufia si yote yanayohusika katika ‘kumjua’ yeye?
15 Kwa hiyo, kupata kumjua Mungu kunamtia ndani yeye na Mwanawe pia. Yesu Kristo alionyesha hili wazi alipokuwa akisema hivi katika sala kwa Baba yake: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) ‘Kujua’ Mungu na Mwanawe hivyo si kuwa na maarifa ya kichwani tu, kuwa na habari ulizojipatia. Maana yake hasa ni kutambua mamlaka ya Mungu na Mwanawe na kuinyenyekea. Kwa mfano, huenda mfanya kazi akawa ana mgawo wa kazi unaojulikana wazi kutoka kwa msimamizi wake. Walakini, kama akipewa mgawo usiopatana na huo kutoka kwa msimamizi mdogo zaidi, huenda akamwambia huyo hivi, Mimi simjui msimamizi mwingine ye yote.’ Kwa kusema hivyo asingekuwa akimaanisha hajui msimamizi yule mdogo yuko wala kwamba hajui yeye ni mtu. Hata hivyo, ‘hajui’ wala hatambui msimamizi mwingine ye yote isipokuwa yule anayefanyia kazi kwamba ndiye mwenye mamlaka juu yake.
16 Vivyo hivyo, huenda mtu akakubali kwamba Yesu Kristo yuko na kwamba ndiye Mwana wa Mungu aliyetoa uhai wake kama dhabihu kwa ajili ya ulimwengu wa wanadamu. Lakini hicho sicho kikomo cha ‘kumjua’ Mwana wa Mungu. Kulingana na maneno ya Yesu mwenyewe, yeye amepewa “mamlaka juu ya wote wenye mwili.” (Yohana 17:2) Kwa hiyo mtu anayemjua Yesu Kristo kweli kweli kuwa mwenye mamlaka hiyo anaonyesha hivi kwa kuzitii amri zake. (Yohana 14:15; 15:10) Ni kama vile mtume Yohana alivyokazia fikira za waamini wenzake: “Na hivi tunayua ya kuwa tumemuyua yeye, ikikuwa tunashika amuri zake. Yeye anayesema: Nimemuyua, wala hashiki amuri zake, ni mwongo, wala kweli si ndani yake.” (1 Yohana 2:3, 4, Swahili Congo Bible) Kwa kuwa amri za Yesu zilitokana na Baba yake hasa, kumjua Mwana au kumtambua kama mtu anayestahili kutiiwa kwamaanisha pia kumjua Baba au kumtambua kama mtu anayestahili kunyenyekewa kabisa.—Yohana 7:16-18; 14:10.
KUJULIKANA NA MUNGU NA KRISTO
17. Habari ya Ibrahimu inaonyeshaje linalomaanishwa na kujulikana na Mungu?
17 Kwa kupata kumjua Mungu kama mtu na kutambua mamlaka yake, sisi pia tunapata kujulikana naye. Ndivyo ilivyokuwa kwa mwanamume mwaminifu Ibrahimu. Yehova Mungu alisema kwamba ‘alimjua’ Ibrahimu, si akimaanisha kwamba yeye alikuwa anajua tu kwamba Ibrahimu yuko bali kwamba alikuwa amefahamiana sana naye. Mwenyezi alikuwa ameona utii wa Ibrahimu na kupendezwa kwake na ibada ya kweli kwa miaka mingi na kwa sababu hiyo akapata kumjua kuwa mwanamume mwenye imani ambaye angefundisha wazao wake kwa usahihi. (Mwa. 18:19; 22:12) Zaidi ya hayo, Mungu alimjua au akamtambua Ibrahimu kuwa mtumishi wake aliyemkubali, rafiki yake.—Yak. 2:23.
18, 19. Ni nini linaloonyesha kwamba kujua tu mambo ya Biblia yalivyo na kumkubali Yesu Kristo ndiye aliyekufa kwa ajili ya dhambi za wanadamu hakutoshi ili mtu atambuliwe kuwa mtumishi anayekubaliwa wa Mungu na Kristo?
18 Kupata kutambuliwa na Mungu kama vile Ibrahimu hakutegemei kujua tu mambo ya Biblia yalivyo. Kuna watu wanaoweza kujibu maulizo juu ya Biblia na nyakati nyingine hata waijue katika lugha ambazo iliandikwa kwazo kwanza. Huenda pia wakamkubali Yesu Kristo kuwa Bwana aliyewafia. Lakini ikiwa hawajihakikishi kuwa watumishi watiifu, Yehova Mungu wala Yesu Kristo hatawatambua watu hao kuwa mali yao. (2 Tim. 2:19; Tito 1:16) Yesu Kristo alitoa onyo hili: “Si kila mutu anayeniambia: Bwana, Bwana, atakayeingia ufalme wa mbinguni; lakini yeye anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wingi wataniambia siku ile: Bwana, Bwana, hatukutabiri kwa jina lako, na kwa jina lako tulitoa pepo wachafu, na kwa jina lako tulifanya matendo mingi ya uwezo? Halafu nitawaambia: Sikuwayua ninyi wakati wo wote; ondokeni kwangu, ninyi munaotenda maovu.”—Mt. 7:21-23, Swahili Congo Bible.
19 Kwa wazi, Yesu Kristo anapaswa afahamiane na watu hawa anaokataa. Ama sivyo asingewasema kuwa ‘watenda maovu.’ Walakini, yeye hawajui wala hawatambui kuwa wenye uhusiano unaokubaliwa naye; hawajui kama wajumbe wake walioamriwa. Kwa hiyo, ni lazima kwetu kuhakikisha kwamba tunajiongoza kwa njia inayopatana na utu wa Mungu, njia zake na matendo yake ili tutambuliwe kama wenye kukubaliwa naye na Mwanawe. (Gal. 4:9) Mambo yakiwa hivyo tu ndipo tunapoweza kutumainia kuokoka uharibifu wa wote wanaodharau amri za Yehova Mungu na Kristo Yesu, wakikataa kuwajua au kutambua mamlaka yao.—2 The. 1:6-9.
20. Ikiwa mtu anajulikana na Mungu, anaweza kuonyesha ushuhuda gani kwamba uhusiano wake ni wa kipekee?
20 Mtu anayejulikana au kutambuliwa na Mungu anafurahia uhusiano wa kipekee na Muumba wake. Katika maisha yake mwenyewe, anaona akiongozwa na kusaidiwa na Mungu. Hali nzito inapotokea maishani, inayohitaji kufanyiwa uamuzi mkubwa, mtu anayemjua Yehova kuwa Mungu mwenye hekima yote, mwenye uwezo wote hatategemea ufahamu wake mwenyewe. (Mit. 3:5, 6) Atamfikia Yehova katika sala, akimwomba msaada na uongozi wake. Kupitia kwa roho yake, Yehova atamkumbusha mtu huyo kanuni zinazofaa kutoka kwa Neno lake na kumsaidia alitumie inavyofaa. (Linganisha Yohana 14:26.) Hata hali au magumu yenye kujaribu yawe ya namna gani, mara nyingi mtu ataona kwamba maneno ya mwanafunzi Yakobo yanayofuata yanamhusu yeye: “Mutu wa kwenu akipungukiwa na akili, alombe Mungu, anayewapa wote kwa ukarimu, pasipo kuhamakia; naye atapewa.”—Yak. 1:5, Swahili Congo Bible.
21. Ni mambo gani yanayotokana na kumjua Mungu na kuendelea kufuata mwendo anaoukubali?
21 Tunapoendelea kutenda kupatana na hekima ya kimungu kama inavyofunuliwa kwetu katika Neno la Mungu ili kujibu sala zetu, matokeo yatakuwa nini? Kupitia kwa roho yake, Yehova Mungu ataendelea kutusaidia tufanye maendeleo katika kusitawisha utu wa kimungu. “Nguvu” au kitu chenye kuendesha ‘kinachoendesha nia zetu’ kitatuvuta tujipatanishe zaidi sikuzote na kanuni za Mungu za haki. (Efe. 4:20-24, NW) Amri za Mungu hazitakuwa maneno matupu tu yaliyochapwa katika kitabu. Bali, zitakuwa sehemu ya nafsi zetu wenyewe, zikiwa zimekazwa akilini mwetu na moyoni mwetu. Tutajua mambo zinayomaanisha na kuthamini ubora wazo ulio mwingi sana kwa sababu tumekwisha ona faida zinazotokana na kuzitii. (Zab. 119:1-16, 74-77, 164-168) Kama mtume Paulo anavyotaja, tutaweza “kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Rum. 12:2, NW.
[Picha katika ukurasa wa 368]
Mwizi aliyeiba ng’ombe dume akamwuza alipaswa alipe kwa ng’ombe dume watano
[Picha katika ukurasa wa 369]
Sheria ya Mungu kwa Israeli ilionyesha kwamba rehema yake ilikuwa na mipaka. Mwana mkaidi aliyekataa kusikiliza sahihisho lenye rehema la wazazi wake aliletwa mbele ya ‘wazee wa mji’ ajaribiwe