Je! Wewe Waweza Kuwa na Uhusiano wa Karibu Sana na Mungu?
“Siri ya [Yehova] iko kwao wamchao, naye atawajulisha agano lake.”—Zab. 25:14.
1. Mungu ana uhusiano gani na watu wote?
MUNGU, akiwa Muumba, ana uhusiano fulani na watu wote. Mtume Paulo alikiambia hivi kikundi cha wanafilosofia katika Athene: “Ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Walakini wale wanaoendelea kuwa waovu hawawezi kuwa wasiri wake. (Mit. 3:32) Hata hivyo, yeye anaruhusu waendelee kupata watoto, wafurahie mambo mazuri ya dunia, na kuwa na nafasi ya kutubu, ikiwa wana nia ya kufanya hivyo.—Matendo 14:16, 17.
2. Ni jambo gani linalohitajiwa. ili kupata kibali ya Mungu, na je takwa hili laweza kutimizwa na wanadamu?
2 Walakini, uhusiano wa karibu zaidi ya kuwa kiumbe tu wa Mungu ni wa lazima ili kupata kibali yake na kuwa rafiki na mshiriki wake wa karibu. Kuwa na upatano naye na makusudi yake ni jambo la lazima ikiwa mtu atakuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. Jambo lililo la ajabu ni kwamba kila mtu aweza kupata uhusiano huu ikiwa kweli anautamani baada ya kufunguliwa nafasi, kwa kuwa mtume Paulo aliwaambia wale Waathene kwamba vilevile Mungu ametoa nafasi ili watu “wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.
3. Wote wanaomkaribia Mungu lazima wakubali kizuizi gani kinachotenganisha Mungu na wanadamu?
3 Ni jambo gani linalopasa kumtafuta Mungu? Naye Mungu anachukua hatua gani kumwelekea yule anayemtafuta kwa unyofu? Kizuizi chetu katika kumkaribia Mungu ni dhambi ya kibinadamu. Dhambi zetu zaweza kuzuia mawasiliano (kupashana habari) kama vile wingu kubwa jeusi. (Linganisha Maombolezo 3:44.) Zaweza kutuzuia hata tusitake kumsihi Mungu; zaweza kutufanya tujisikie wachafu na wasiostahili kumkaribia. Hata hivyo, tusipokubali kwamba sisi ni wenye dhambi, tukifanya kila siku mambo ambayo hata dhamiri zetu zinalaumu, hatumo katika hali ya kumkaribia Mungu, naye Mungu hatasikia sala za wale wasiokubali uhakika huu unaowahusu wanadamu. wote ulimwenguni pote.—1 Pet. 3:12.
MAUTI NA UFUFUO WA KRISTO NDIO MSINGI
4. Mungu alichukua hatua gani ya kwanza ya kuondoa kizuizi cha kupashana habari na kuwa na uhusiano wa karibu naye.
4 Kwa kweli, Mungu mwenyewe amechukua hatua ya kwanza ya kutuwezesha kuwa na uhusiano pamoja naye kwa kufanya mpango wa kuondoa kizuizi hiki cha kuwa na mawasiliano na uhusiano wa karibu naye. Mpango huu ni mpango gani? Mtume Paulo anajibu hivi: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Rum. 5:8) Kristo alikuwa mtu mkamilifu, asiye na dhambi alipokuwa duniani, walakini yeye mwenyewe alichukua adhabu ya wenye dhambi kama kwamba ndiye aliyekuwa mwenye dhambi. Ajapokuwa bila kosa, alipatwa na adhabu kamili kwa ajili ya dhambi za wanadamu. Mtume Petro anatuambia hivi: “Yeye alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti . . . Na kwa kupigwa kwake mliponywa.” (1 Pet. 2:24) Jambo hili lilikusudiwa na Mungu karne nyingi mbele, kama alivyotabiri nabii Isaya: “Alijeruhiwa kwa makosa yetu, alichubuliwa kwa maovu yetu.” (Isa. 53:5) Tendo la Yesu Kristo la kuwa badala ya wanadamu lilisawazisha madai yote ya haki ya hukumu kwa ajili ya dhambi zilizofanywa, likaweka msingi wa kuondoa laana kwa wote wanaokubali dhambi zao wenyewe na kuonyesha imani katika mpango wa Mungu.—Rum. 8:1.
5. Sababu gani ufufuo wa Yesu ulikuwa wa maana kwetu pia, wala si mauti peke yake?
5 Na zaidi ya hayo, uhakika wa kwamba Kristo hakuendelea kuwa mfu, bali alifufuliwa na sasa yu hai, unathibitisha msaada wake unaoweza kupatikana kila wakati, hivi kwamba mtu anaweza kufurahia uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Maandiko yanatuhakikishia: “Alitolewa [ateseke na kufa] kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili tupate kuhesabiwa haki.” (Rum. 4:25) Alionekana mbele za Mungu ili amtolee thamani ya dhabihu yake. Leo yeye ndiye Yesu aliyetukuzwa aliyeonwa na Yohana katika njozi akiwa katikati ya vinara vya taa saba vya dhahabu, vikiwakilisha kundi la Kikristo, pamoja na nyota saba, au baraza ya waangalizi watiwa mafuta, zikiwa katika mkono wake wa kuume. (Ufu. 1:12-16) Kwa habari yake akiwa Kuhani Mkuu wetu aliye hai, imeandikwa hivi: “Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.”—Ebr. 7:25.
6, 7. Inakuwaje kwamba Kristo “aliifia dhambi” walakini sasa “amwishia Mungu”?
6 Kwa hiyo, mtu amwaminiye Kristo aweza kuishi si kama mtu aliyekufa kiroho kwa sababu ya dhambi zake, ambaye mawasiliano yake na Mungu yamezuiwa, bali kama mtu aliye hai, akimtumikia Mungu, katika njia inayofaa, yenye kujenga, akiwa na juhudi katika kutii amri za Mungu, na kuwajenga wengine. Juu ya hili, mtume awaambia “watakatifu” katika Rumi hivi: “Tukijua ya kuwa Kristo akiisha kufufuka katika wafu hafi tena, wala mauti haimtawali tena. Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; lakini kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu. Vivyo hivyo ninyi nanyi jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi, na walio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu.”—Rum. 1:7; 6:9-11.
7 Hapa mtume anaonyesha kwamba Kristo alikuja duniani hasa kwa kusudi la kushughulika na kitu hicho kichafu, chenye kuchukiza—dhambi—kitu kinachochukiwa na wote wawili Mungu na Kristo. (Ebr. 1:9) Ijapokuwa sikuzote Kristo alifurahia kufanya mapenzi ya Babaye, dhambi ni adui, na, katika kuimaliza dhambi, Yesu alilazimika kupatwa na mambo mengi sana yasiyopendeza. Kabla tu ya kufa kwake, alisema hivi: “Imekwisha.” (Yohana 19:30) Kwa hiyo aliteseka na kufa kwa habari ya dhambi—ili kuimaliza dhambi. Walakini sasa “amwishia Mungu.” Yeye ametukuzwa mbinguni, milele, akishirikiana na Mungu, kwa kuwa dhabihu yake haihitaji kurudiwa tena. Hili likiisha kutimizwa angeweza kuingia kwenye kazi yenye kujenga, kuwaleta watu tena katika uhusiano wa karibu sana na Mungu, na kutimiza mapenzi ya Mungu kwa wote wanaotaka uzima.—Ebr. 7:25; 8:1; 9:28.
MUNGU AWAVUTA WATU KWA KRISTO
8, 9. Mungu anawavutaje watu kwa Kristo?
8 Yehova Mungu aliwaonyesha wanadamu upendo mwingi sana pamoja na fadhili zake zisizostahilika kwa kufanya mpango huu. Na hata zaidi ya hilo, Mungu anatenda kupatana na kusudi lake. Mungu ndiye anayewavuta watu wenye mioyo minyofu kwa Kristo. Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka.” Yeye alisema kwa habari ya mitume wake kwamba walipewa kwake kutoka kwa Baba.—Yohana 6:37, 39, 44.
9 Mungu anawavutaje? Bila shaka hili halifanywi bila kupenda kwa mtu, kwa kupendelea, au kwa kumlazimisha mtu. Nia ya mwanadamu mwenye shingo ngumu, mwenye dhambi, kwa asili haielekei kumtii Mungu. Walakini Mungu aweza kuleta mabadiliko katika nia ya mtu. Yeye anajua yaliyomo ndani sana moyoni mwa mtu. Hivyo aweza si kumwezesha mtu kusikia habari za Kristo pamoja na njia ya wokovu tu, bali pia kumwezesha mtu afahamu mpango huo. Yeye aweza kufumbua macho ya vipofu. Mungu huwavuta wanaume na wanawake wamwamini Kristo katika wakati wa taratibu hii ya mambo, ijapokuwa hawangefanya hivyo kwa uwezo wao wenyewe, kwa kutia katika mioyo yao maarifa ya uzuri wa Kristo, pamoja na faida ya kuunganishwa pamoja naye.
10. Kule kuvuta watu kwa Mungu kunakuwa na matokeo gani kwa watu wenye mioyo minyofu?
10 Ndipo, kwa upande wa mtu mwenyewe, anatamani kumfuata Kristo na kuungana pamoja naye kutoka kwa moyo, kama vile watu, wanapoona kweli kweli wema wa mtu na kuukubali, wanatamani kumkaribia na kuwa rafiki yake. Mfano wa tendo la Mungu la kuvuta mioyo ya watu unaonekana katika watu wa Israeli wa kale katika siku za Daudi mwana wa Yese. Mungu alimwahidi Daudi ufalme. Ulipofika wakati wa kumpa Daudi ufalme, alivuta mioyo ya watu kwa Daudi, watumikie kwa nia chini yake. (2 Sam. 2:4; 3:36; 5:1-3) Hivyo Mungu huvuta mioyo ya watu kwa Kristo.
LAZIMA NIA YA MTU BI NAFSI IONYESHWE
11. Nia ya mtu mwenyewe inakamatanaje na kule kumjia Kristo, nayo nia ya wale wasiofahamu inabadilishwaje?
11 Haina maana kwamba nia ya mtu binafsi haihusiki katika jambo hili. Ijapokuwa huenda mwanzoni mtu asiwe na nia yenye kutenda ya kumjua Kristo, nia hiyo yaweza kubadilika ajifunzapo—‘macho ya moyo wake’ yafumbuliwapo. (Efe. 1:18) Yesu alitumia maneno ya unabii wa Isaya juu ya wale wanaokuwa watoto wa mwanamke wa kimbinguni wa Yehova, Sayuni, katika wakati wa taratibu hii ya mambo, akisema: “Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na [Yehova]. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu.” (Yohana 6:45; Isa. 54:1, 13) Mtu huyu, kwa kuona na kwa kufahamu, anabadili nia yake. Ikiwa hataki kufanya hivyo, hashurutishwi kufanya badiliko hilo. Kufahamu kunaleta imani, nayo imani ya mtu huyo inamwongoza Mungu na Mwanawe wamkubali, kama vile Yesu alivyowaambia wafuasi wake baadaye: “Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake. . . . Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake.”—Yohana 14:21-23.
12. Kisha, Kristo naye anamletaje mtu karibu zaidi na Mungu?
12 Kwa kuwa sikuzote Baba amekuwa asiyeonekana kwa wanadamu, yeye anajidhihirisha kwa wanadamu kupitia kwa Kristo, kwa kuwa Yesu, alipokuwa duniani, alidhihirisha sifa bora za utu wa Mungu, hivi kwamba aliweza kusema: “Aliyeniona mimi amemwona Baba [pia].” (Yohana 14:9) Wakimjia Kristo, wale wanaoamini wanakuja kumjua Baba sana kama vile Kristo anavyofunua mioyoni mwao kina na wema wa sifa za Mungu.
13. Lazima mtu ajioneje, ili aweze kumkaribia Mungu katika njia anayoikubali Mungu?
13 Hivyo, kwa upande wa mtu bi nafsi, ni hatua gani zinazotakiwa zichukuliwe ili aweze kumkaribia na kuwa msiri wa Mungu? Lazima mtu awe na hali ya uhitaji, ajione kwamba si kila kitu kinachoridhisha maishani mwake. Lazima ajione kuwa mtu asiyekamilika, asiyetosheka, akikubali kwamba yeye ni mwenye dhambi, na kukubali ubatili wa hali yake. Ikiwa mtu ye yote haoni kabisa hali yake ya uhitaji, kufikiria Sheria iliyotolewa Israeli na Mungu kupitia kwa Musa kutamhakikisha kabisa kwamba yeye ni mwenye dhambi. Kusudi la sheria hiyo lilikuwa kuonyesha kwamba hakuna mtu mwenye haki na vilevile kuwaongoza watu wenye mioyo minyofu, wanaochunguza waone uhitaji wa mkombozi.—Gal. 3:19, 24.
14. Ni hatua gani zaidi zinazohitajiwa kuchukuliwa na mtu anayetaka kuwa na uhusiano pamoja na Mungu?
14 Kwa kuona uhitaji huu, mtu mwenye moyo mnyofu ataangalia kwa unyofu na kwa bidii katika Biblia na kujifunza njia ya Mungu kupitia kwa Kristo. Anapokuja kujua kwamba yeye hana uhusiano wo wote na Mungu, yeye vilevile anahakikishwa juu ya ubaya halisi wa dhambi na vile imemtenda. Anaona kwamba kwa kweli yeye ni adui ya Mungu. (Rum. 5:10) Na kwa kupatana na hilo, yeye anatubu na kuomba msamaha. Wakati wote lazima akubali kwamba si kwa sababu ya ufahamu au wema wake mkuu, bali Mungu ndiye anayemvuta. Mtu huyo ameona kwamba anaweza kupata msamaha huo kwa msingi wa dhabihu ya Kristo yenye kufunika dhambi. Akiisha jua na kuthamini kusudi la Mungu, yeye anaonyesha tamaa yake na uamuzi wa kuwa mtumishi aliye wakf kabisa wa Mungu, naye anaonyesha imani na uamuzi huu mbele ya wengine kwa kuomba abatizwe katika maji.
UHUSIANO MPYA PAMOJA NA MUNGU
15. “Dhamiri njema” anayoomba mtu anayebatizwa ni nini?
15 Kwa ubatizo huu, mtu huyo anamwomba Mungu dhamiri njema. (1 Pet. 3:21) “Dhamiri njema” inamaanisha kwamba yeye halemewi katika dhamiri yake na kujiona kuwa mwenye hatia kwa sababu ya dhambi zake za zamani. Zaidi ya hayo, inamaanisha kwamba, yeye ana uhusiano mpya pamoja na Mungu na Kristo wakiwa rafiki zake. (Yohana 15:14, 15) Sababu yake ni kwamba imani yake katika dhabihu ya Kristo inamwezesha kusamehewa dhambi zake za zamani na vilevile zaidi ya hilo.
16. Sasa mtu huyo anakuwa na msimamo gani mwema pamoja na Mungu, naye anawezaje kuuendeleza?
16 Kutumia mfano: Msamaha kutoka kwa mamlaka ya kilimwengu wafuta matendo ya uhalifu ya mhalifu. Walakini mhalifu huyo anarudia pale pale tu alipoanza. Yeye hana faraja au uhakikisho kwamba hataulizwa makosa ambayo huenda akafanya katika wakati ujao. Walakini yeye anayemwamini Kristo anakubaliwa na Mungu kama rafiki, ambaye Mungu huendelea kumtendea kama msiri wake, sasa na katika wakati ujao, mpaka mwishowe mtu huyo akamilishwe. (1 Pet 5:10) Maadam yeye anaendeleza imani na uaminifu uo huo, anaweza kuomba asamehewe dhambi anazofanya siku kwa siku na kuhifadhi uhusiano huo wa karibu sana. Bila shaka haimpasi ‘kukubali fadhili zisizostahilika za Mungu na kukosa kusudi lake.’ (2 Kor, 6:1, NW) Yeye hana haki ya kufikiri kwamba anaweza kuchezea uhusiano huo wa karibu na Mungu na kuendelea kuwa na msimamo mzuri kwake.
KUKABIDHIWA MIKONONI MWA KRISTO
17. Mungu avutapo mtu kwa Kristo, Kristo anamfanyiaje mtu huyo?
17 Mungu anapomvuta mtu kwa Yesu Kristo, hali yake inakuwaje? Yesu alikubali kwamba watu wote ni mali ya Baba na ya kwamba wale wanaovutwa na Yehova wanapewa Yesu, wanatolewa kwake awaangalie na kupata ukuzi wa Kikristo. (Yohana 17:9, 10) Mungu alikuwa ameahidi hivi kuhusu Kristo kupitia kwa nabii Isaya: “Ataona mazao ya taabu yake, na kuridhika.” (Isa. 53:11) Kwa hiyo Yesu Kristo alimtazamia Mungu atokeze mazao katika kazi na dhabihu yake. Vilevile Yesu alisema kwamba Mungu alikuwa amempa mamlaka juu ya wote wenye mwili. (Yohana 17:2) Kwa kutumia mamlaka hii yeye anaweza kuwalinda wote wanaovutwa kwake na Mungu, akiwalinda na wapinzani waovu na wakatili wanaopinga kweli. Kwa habari ya wote aliopewa, Yesu alisema hivi: “Nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu.” (Yohana 10:28, 29) Kwa hiyo, haiwapasi Wakristo kuogopa mateso yo yote, magonjwa, dhiki, upinzani, au kitu kinginecho, hata mauti.—Rum. 8:38, 39.
18. Matokeo ya mwisho kwa mtu anayemfuata Kristo kwa uaminifu yanakuwa matokeo gani?
18 Wakiwa chini ya Yesu Kristo Mchungaji Mwema, wale wanaomfuata kwa uaminifu wanahakikishiwa uzima wa milele. Yesu alisema hivi: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
19, 20. Hivyo, basi, ni nini thamani ya kuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu?
19 Uzima wa milele! Ajapokufa mtu, tumaini lake halififii. Kwa kuwa Yesu alionyesha hali ya kudumu na isiyovunjika ya uhusiano mwema wa Mwana pamoja na wale wanaoletwa kwake na Baba wakiwa washiriki wa “kundi dogo” la kondoo wake aliposema: “Wote alionipa Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe.”—Luka 12:31, 32; Yohana 6:37.
20 Hivyo, wakiwa chini ya uangalizi wa Mchungaji Mwema wale wanaokuja kwake waweza kutazamia msaada na uongozi katika kila sehemu ya maisha zao, wakiwa na tumaini la uzima wa milele mbele yao. Hivyo, basi, ni jambo gani linaloweza kuwa bora zaidi kuliko kupata uhusiano mwema pamoja na Mungu na Mwanawe? Lakini, katika mambo ya maisha ya kila siku, uhusiano huo unakuwaje halisi—uhusiano mchangamfu, wa karibu, na ulio salama?