Muumba Wako Anakupenda Sana Wewe
“Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
1. Upendo wa Mungu kwa wanadamu umekuwa mkubwa kadiri gani, na kwa hiyo ni jambo gani lingekuwa gumu kwetu kuwazia?
MUNGU Aliye Juu Zaidi amekwishaonyesha upendo wake mwingi sana kwa wanadamu. Ingawa alimpenda sana Mwana wake mzaliwa pekee, Yehova Mungu alipanga mambo ili afe kwa ajili yetu ili tuweze kupatanishwa Naye na mwishowe tujifurahishe uzima wa milele katika ukamilifu. (Yohana 3:16; Rum. 5:6-8) Kwa sababu hiyo, je! tunaweza kufikiri kwamba Mungu anaweza kuwaona wanadamu kama tu jumla ya watu “wasio na nyuso,” au kwamba anaweza kuchagua kikundi fulani cha watu ambao angeonyesha kibali chake na kutowajali wengine?
2. Yehova anawaonaje watu mmoja mmoja?
2 Hilo lisingeweza kutukia hata kidogo! Kila mtu anajulikana kwa Mungu kama mtu aliye pekee. Yeye “hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.” (1 Tim. 2:4) Alipoona Mungu anakubali watu wa ‘Mataifa waingie katika kundi la Kikristo, mtume Petro alipaza sauti hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu [mtu mmoja mmoja] amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”!—Matendo 10:35
3. Ni kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo kila mtu mmoja mmoja atafikiriwa?
3 Yesu Kristo alitumwa na Mungu ajitoe mwenyewe awe “ukombozi kwa ajili ya wote.” (1 Tim. 2:6) Yeye ‘aliionja mauti kwa ajili ya kila mtu,’ akiinunua jamii nzima. (Ebr. 2:9) Basi, je! lingekuwa jambo la busara kwa Mwana wa Mungu kuwa na moyo wa kutofikiria watu, akisema hivi: ‘Nilimpa kila mtu damu yangu, lakini mtu huyu mmoja ana faida gani? Kama akipoteza uhai wake au hapana, yote ni mmoja kwangu’? Hata kidogo! Kila mtu atakayepewa faida za ukombozi chini ya ufalme wake, ataangaliwa apate nafasi ya uzima.
4. Tunajifunza nini kutokana na Biblia juu ya kuendelea kwa upendo wa Mungu?
4 Kwa hiyo Yehova ana nia na yuko tayari sikuzote kumpa mtu ye yote anayemwanamini msaada wake na kumwonyesha upendo wake. Na upendo wake mwingi ambao anaendelea kuonyesha wapita sana upendo tunaoweza kuwaonyesha wengine. Ebu ukumbuke upendo ambao Mungu alionyesha Ibrahimu, Isaka na Yakobo, waliokuwa wanadamu wasiokamilika lakini waliomtumikia kwa moyo wote. Karne zilizofuata, upendo huo wa Yehova ulikuwa wenye nguvu kama zamani. Musa aliliambia taifa la Israeli hivi: “[Yehova] aliwafurahia baba zako, na kuwapenda.” (Kum. 10:15) Kwa sababu ya upendo huu, alivumilia ukaidi wa taifa hilo karne nyingi.—Mal. 3:6.
5. Yehova anataka kuonyesha upendo wake kwa wachache tu waliochaguliwa?
5 Upendo wa Yehova ni mkubwa na wenye kuendelea kwa wale wanaomtumikia leo. Yeye anatazamia nafasi ya ‘kumfurahia’ ye yote anayemwomba kwa moyo mweupe na kweli. Biblia yasema hivi: “Kwa maana macho ya [Yehova] hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” (2 Nya. 16:9) “Masikio yake husikia maombi yao.”—1 Pet. 3:12.
6. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yehova hatafuti makosa?
6 Yehova anawahurumia sana wanadamu anapoitazama dunia na kuona taabu nyingi ambazo watu wanapata. Yeye anatamani kumsaidia kila mmoja wao. Ijapokuwa haachilii makosa, yeye si mtu wa kutafuta-tafuta makosa ya watu, bali anatafuta mambo mema wanayofanya. Mtunga zaburi alisema: “[Yehova], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Badala yake, anapotutazama Yehova anakumbuka ya kuwa sote “tu mavumbi.”—Zab. 130:3; 103:14.
7, 8. (a) Yesu alionyeshaje kwamba kwa kweli yeye alitaka kusaidia watu? (b) Huruma za Mungu na Kristo kwa wanadamu zinapaswa zitusukume tufanye nini?
7 Alipokuwa duniani, Mwana wa Mungu alitamani sana kuutumia uwezo wake asaidie watu. Mwenye ukoma alipomwambia: “Ukitaka, waweza kunitakasa,” Yesu “akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika,” kisha akamponya.—Marko 1:40, 41.
8 Watu waliokuja kutaka msaada kwake, Yesu aliwaponya kwa huruma. Vilevile wakati huu, Yehova Mungu na Mwanawe wanamhurumia ye yote ambaye ameacha mambo ya maisha ya kila siku ili asikilize habari njema za kusudi la Mungu. Je! unasoma Neno la Mungu sasa hivi upate kuchunguza kikweli na kupata kumjua Yeye? Ikiwa ndivyo, huu ni ushuhuda unaoonyesha kwamba anapendezwa nawe. Jambo hili lawezaje kusemwa hivyo kwa hakika?
9. Yehova anamfanyiaje mtu anayechunguza Neno Lake kwa unyofu wa moyo?
9 Usemi huu ni wa kweli kwa sababu Mungu anaona uzuri fulani katika moyo wa mtu ye yote anayelichunguza Neno lake kwa unyofu wa moyo. Kwa sababu hiyo, anazifungua akili za mtu huyo ili apate ufahamu. Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka.” (Yohana 6:44) Bila msaada wa roho ya Mungu, huwezi kuyafahamu makusudi ya Mungu. Ikiwa unajifunza kusudi la Mungu, unaweza kuwa na hakika ya kwamba anakusaidia.
MFANO WA KUTHAMINI KWA MUNGU
10. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yehova anathamini watumishi wake?
10 Kwa kuitikia jitihada yako ya kupata ufahamu, Mungu anakuonyesha sifa nyingine njema. Sifa hiyo ni kuthamini. Bila shaka una sifa hiyo na unathamini mambo mengi ambayo wengine wanakutendea, labda unasema, Asante, au unaonyesha hiyo katika njia nyingine. Lakini kule kuthamini kwa wanadamu si kwingi sana kama Mungu anavyothamini wale wanaomwonyesha imani yao na wanaoliheshimu Neno lake. Yeye anawafurahia. Yesu hata alisema juu ya furaha mbinguni juu ya mwenye dhambi mmoja anayetubu au anayeacha mambo mabaya ili ampendeze Mungu. (Luka 15:10) Kwani, Yesu alisema kwamba mtu anayempa kikombe tu cha maji baridi mmoja ambaye anatambua kuwa mtumishi wa Mungu hangekosa hata kidogo zawadi yake. (Mt. 10:42) Siku zote thawabu (zawadi) ya Yehova yapita ubora wa ibada au utumishi ambao mtu anamtolea. Yehova anamtazama na kuthamini kila mtu anayeheshimu na kuhurumia watu wake. Kwa hiyo, moyo wake na msaada wake unamwelekea mtu huyo.
11. Marko 14:3-9 inaonyeshaje kwamba hata Yesu alikuwa akithamini?
11 Mwanamke alipoingia nyumbani ambamo Yesu alikuwa akila chakula, akamimina mafuta mazuri kichwani pake, Yesu alithamini sana hata akasema: “Amin, nawaambia, Kila ihubiriwapo Injili katika ulimwengu wote, na hili alilotenda huyu litatajwa kwa kumbukumbu lake.” Maneno yake yamekuwa ya kweli, kwa sababu tendo jema la mwanamke huyo limeandikwa katika Maandiko, mamilioni ya watu wakasoma, ijapokuwa ni tendo dogo.—Marko 14:3-9.
12. Roho ya kuthamini ya Baba na Mwana inapaswa iwe na matokeo gani kwetu?
12 Sisi nasi imetupasa tuthamini fadhili za Mungu kwa kutusaidia tujue kusudi lake na kwa kutupa nafasi ya kupata uzima wa milele. Imempasa mtu awe na shukrani kwa vile Mungu ameona yafaa amruhusu awe kama wale watu ambao Paulo aliandikia katika mji fulani katika Asia Ndogo. Wayahudi wa huko waliojidai kumtumikia Mungu waliipinga kweli. Lakini maandishi yasema hivi: “Mataifa waliposikia hayo [nafasi ya kukubaliwa na Mungu] wakafurahi, wakalitukuza neno la Bwana, nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele wakaamini.” (Matendo 13:48) Watu hao walithamini fadhili za Mungu. Kuthamini kwao kuliwasaidia wawe watu ambao Mungu anafurahia kukubali.
MSIKIAJI WA SALA
13. Sala zetu kwa Mungu zinapaswa kupitishwa kupitia kwa nani, na kwa sababu gani hatupaswi kuogopa kwamba hatasikiliza?
13 Basi, twajua kwamba Mungu ametupelekea kusudi lake. Je! sisi nasi hatuwezi kumpelekea Mungu mawazo yetu ya ndani na tamaa za mioyo yetu? Twaweza. Na hilo ni kupitia kwa sala. Usiogope kwamba Mungu hatakusikiliza. Jambo linalotakiwa tu ni kuwa na moyo mnyofu na kukiri u mwenye dhambi, anayehitaji msaada. Mtu anayemwomba ataonyeshwa la kufanya. Mtu huyo atajua kwamba sala zinazotolewa kwa Mungu zapaswa zitolewe kupitia kwa Yesu Kristo, Kuhani Mkuu aliyewekwa na Mungu. Mtume aliandika hivi: “Kwa maana sisi tunaye kuhani mkuu, si yeye asiyeweza kusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi, lakini bila dhambi. Kwa hiyo, na tukikaribie kiti cha enzi cha fadhili zisizostahilika tukiwa na uhuru wa kusema, tupate kupokea rehema na kuona fadhili zisizostahilika za kutusaidia wakati unaofaa.”—Ebr. 4:15, 16, NW.
14-16. Ni jambo gani tunaloweza kuomba kwa kufaa, na kwa sababu gani?
14 Ni mambo gani ya kuzungumza katika sala? Lo lote litakalopasa uhusiano (ushirikiano) wa mtu na Mungu; lo lote litakalompasa mtu kiroho. Mtume Yohana alisema hivi: “Tukiomba sawasawa na mapenzi yake, atusikia.”—1 Yohana 5:14.
15 Kuomba “sawasawa na mapenzi yake” kungemaanisha hatungeomba mambo yanayoendeleza faida za kichoyo, kama mali, cheo cha kuzidi wenzetu, kulipa kisasi, anasa za kichoyo na mambo kama hayo. Lakini, kwa mfano, huenda mtu asiyeoa au asiyeolewa anayetamani sana kufunga ndoa akamwomba Mungu amsaidie aone mwenzi wa ndoa anayefaa. Huenda wale waliofunga ndoa wakaomba wawe na watoto, au Wapate hekima ya kulea watoto. Tunayo mifano kama Hana, aliyemwomba Mungu ampe mtoto, na wazazi wa Samsoni, walioomba wapewe shauri juu ya kulea mtoto wao wa kiume. (1 Sam. 1:10-17; Amu. 13:8-14) Vilevile, twaweza kuomba ndoa yetu iwe na upatano, tukimwomba azibariki jitihada zetu za kufanikisha ndoa yetu. Hata twaweza kuomba tuhamie mahali pengine au kuona kazi nyingine, kwa sababu huenda jamaa ikapungukiwa mapato na hali yao ya kiroho idhoofike kwa sababu hiyo.
16 Ijapokuwa haya ni mambo ya kipekee, bila shaka yanapasa maisha yetu nayo yanataka mageuzo ambayo katika hayo twahitaji hekima ya Mungu. Mungu anapendezwa na afurahia kutusikia tukimtolea sala hizo. Lo lote tunaloomba, jambo la kwanza lapaswa liwe kuwa na tamaa ya kutaka kufanya mapenzi ya Mungu. Bila shaka, kila mtu ana hali zake mwenyewe, zilizo tofauti na za wengine, na hizi zitaamua mambo ya kuzungumza katika sala zake.
17. Ni uhakika gani unaotolewa na Zaburi 32:8 juu ya Mungu kujibu sala zetu?
17 Lile jibu litakalotoka kwa Mungu laweza hakika kutazamiwa kuja kwa namna ya uongozi wenye hekima utakaohusu hali ya mtu mwenyewe. Mungu anaahidi hivi: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.”—Zab. 32:8.
18. Kutenda kupatana na sala zetu kunaweza kutia ndani jambo gani?
18 Bila shaka, mtu akiisha kuomba, imempasa aendelee kufanya kama alivyosema katika sala yake. Kwanza, imempasa atafute shauri juu ya kutatua tatizo (kumaliza magumu) kutokana na Biblia. Kama mtunga zaburi alivyosema: “Nimeita kwa moyo wangu wote; Ee [Yehova], uitike; nitazishika amri zako.” (Zab. 119:145) Akitangulia kuyajua matatizo (magumu) yetu, Mungu aliona yafaa kuandikisha shauri juu ya matatizo (magumu) yote ya wanadamu katika Neno lake lililoongozwa. Vilevile, mtu anaweza kuomba wengine wamsaidie kuona Biblia inavyosema juu ya tatizo (gumu), hata kuwaambia wamwombee. Imempasa aendelee kuomba mpaka afahamu vizuri mwendo wa hekima ambao atafuata. Ikiwa hafanyi hivyo, hatakuwa akimwonyesha Mungu kwamba anayo imani au ya kwamba anatamani sana akujibiwa na Mungu. Hiyo ndiyo iliyokuwa maana ya mfano wa Yesu juu ya mjane aliyezidi kumwomba hakimu amsaidie kabla hajakubali kufanya hivyo mwishowe. —Luka 18:1-8; Yak. 1:5-8.
19. Huenda tukapata kumjua Mungu vizuri zaidi kwa njia gani?
19 Mtu anayeomba na kutenda akiwa na imani na Mungu, anaweza kuhakikishwa kwamba ataongozwa aufuate mwendo wenye faida zaidi. Kweli atamjua Mungu, anayeahidi hivi: “Siri ya [Yehova] iko kwao wamchao.” (Zab. 25:14) Mungu atashirikiana naye, naye atafahamu kwamba ‘anatembea na Mungu,’ akisaidiwa, kuongozwa na kupendwa na Mungu. Kule kumcha (kumwogopa) Mungu kunakotajwa katika Zaburi si kuogopa kusikofaa, bali ni kule kwa kumheshimu Mungu inavyofaa. Iwapo wampenda Mungu utataka umpelekee matatizo (magumu) yako, nawe hutaogopa ukidhani utajibiwa vikali au kukataliwa. Kwa habari ya hofu hiyo yenye kizuizi, mtume Yohana aliandika hivi: “Pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu.”—1 Yohana 4:18.
20. Kwa sababu gani hatupaswi kuogopa kumjua Mungu tukiwa na tatizo (taabu) lo lote?
20 Usiogope hata kidogo wala kusita kumpelekea Yehova mambo yo yote yaliyo ya siri zaidi, kutia na dhambi zako. Yeye hataona matatizo (magumu) yako kuwa ya upuzi wala hatakucheka kama wanadamu wanavyoweza kufanya. Anawapa “wote kwa ukarimu, wala hakemei.” “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”—Yak. 1:5; 1 Yohana 1:9.
MPAJI WA ZAWADI
21. Yehova anataka tuoneje juu ya yeye kuwa mtoaji wa zawadi, na hii inapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?
21 Zaidi ya hayo, inafaa kabisa, na si uchoyo, kumtazamia Mungu atupe thawabu (zawadi) kwa sababu ya kuwa waaminifu kwake, si kusikia sala zetu tu. Yehova ataka tuitazamie zawadi ya uzima kama kitu anachofurahia kutoa, akijua twauthamini tena tutautumia katika njia inayofaa. Yehova ataka tujue kwamba yeye ni Mungu mwenye fadhili anayewapa zawadi wale wanaompenda. Yeye si kama watu wengi wa ulimwengu wasiothamini wala kuwaangalia wale wanaotenda kwa upendo au kwa uaminifu. Na kamungu Kasikothamini uaminifu, na hakawapi hata kidogo watumishi wake zawadi, hakangestahili kuabudiwa. Lakini Yehova Mungu ni mwaminifu, ni mwenye huruma na wema, naye anawabarikia sana rafiki zake. Anawaahidi hivi, wale wanaomwamini: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”—Ebr. 13:5.
22. (a) Ni zawadi gani tunazolifurahisha hata sasa kutokana na kumtumikia Mungu? (b) Ni baraka gani ambazo bado ni za wakati ujao?
22 Kwa hiyo, kuna zawadi kubwa sasa inayotokana na kuwa msiri wa Mungu, kuongea naye na kutembea naye. Tena kuna zawadi iliyo kubwa zaidi kuitazamia, zawadi ya mambo kupita yale tuwezayo kufahamu. Kwanza, kuendelea na uaminifu wetu kwa Mungu kunatupa maisha bora sasa, yenye kusudi, na uhuru mwingi usio na matatizo (magumu) na masumbufu yanayoupata ulimwengu huu. (Efe. 3:20) Halafu, kuna tumaini la kuwa sehemu ya “msingi” wa “nchi mpya.” Itakuwa furaha kama nini, kuwa wa kwanza kufanya dunia kuwa paradiso, au kufufuliwa mapema, na kuishiriki kazi hiyo! Lo! itapendeza kama nini kuwapo ili kuwakaribisha wengine watakaofufuliwa na kuwafundisha, kuwasaidia na kuwazoeza! Mbele yetu kuna wakati ujao wenye furaha nyingi —kuna kusudi jema ya kuishi mbele yetu!
23. Ni kwa sababu gani ni jambo la maana watu wasikawie kuchukua msimamo wao katika upande wa Mungu, na hii inatia ndani nini?
23 Lakini usiipoteze nafasi bora uliyo nayo sasa ya kumtumikia Mungu. Kwa maana hii ndiyo nafasi ya mwisho ambayo watu watakuwa nayo ili wamwunge Mungu mkono katika suala la (sababu ya) utawala wa ulimwengu wote katikati ya ulimwengu wa watu wasiojua mipango ya Mungu. Zaidi ya hayo, hii ndiyo nafasi ya mwisho ya kuwatangazia watu hawa habari njema katika hali za upinzani. Lo! njia bora gani ya kuonyesha Mungu ushikamanifu wako! Kufanya hivi kunaleta zawadi iliyo kubwa kupita zote. Sasa ndiyo nafasi yako ya kufanya kazi kama mshiriki wa “jamaa ya Mungu, ambayo ndilo kundi la Mungu aliye hai, nguzo na tegemezo la kweli” kwa kushiriki na kutangazia wengine habari njema za Ufalme. —1 Tim. 3:15. NW.—Kutoka The Watchtower, Feb. 1, 1978
[Picha katika ukurasa wa 11]
Kutafuta uongozi wa Yehova kwa kusali pamoja kwaweza kusaidia watu wawili waliooana waendeleze upatano wao katika ndoa.