Kuzoeza Dhamiri Zetu Zitusaidie Zaidi
“Mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo.”—1 Pet. 3:16.
1. Miaka ya karibuni tumejifunza nini juu ya dhamiri?
KATIKA miaka ya karibuni tumepata ufahamu mwingi zaidi juu ya dhamiri inayozoezwa na Biblia na jinsi inavyofanya kazi. Tumepata kufahamu kwamba si nguvu fulani tu ya akili, bali ni maono ya ndani ya adili yanayotetea au kushtaki mawazo na mwenendo wetu. Dhamiri zetu zinaonyesha tumeumbwa kwa mfano wa adili wa Mungu wetu Yehova. (Mwa. 1:26, 27) Dhamiri njema hutokea akili inaposhirikiana na moyo wenye uwezo wa adili.
2. (a) Biblia inasaidiaje kuleta maendeleo ya dhamiri? (b) Kusudi la dhamiri njema ni nini, na inapatikanaje?
2 Kwa kujifunza Neno la Mungu, tunaweza kulisha vizuri mioyo na akili zetu, hasa kwa sababu Biblia ina uwezo wa kututia moyo tuwe na adili bora. Biblia peke yake ndiyo yenye uwezo wa kuchochea mema, kwa sababu inafahamisha mwanadamu utu wa Muumba wake, Yehova, aliyeumba mwanadamu aonyeshe utu wake, Kwa hiyo, kusudi la dhamiri njema ni kuhusiana na Mungu kwa uchangamfu na kwa njia ya kipekee, tukitazamia kupata utakatifu na uzima wa milele. Ndivyo mtume Mkristo Petro alivyotia moyo, akisema: “Kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.” (1 Pet. 1:15, 16; Law. 11:44) Mtu asitawishaye uhusiano huo mtakatifu atathawabishwa amani ya kweli na furaha.
3. Moyo wa mtu unahusianaje na dhamiri yake, na mawazo yake yanaiongozaje?
3 Moyo unahusika sana na nguvu hii bora yenye kufuatisha watu adui, yaani, dhamiri. Kwa hiyo, tunahitaji kile ambacho Biblia inaita“moyo safi.” (Zab. 51:10; 73:1; Mt. 5:8) Huo ni moyo ambao kusudi lake la pekee na tamaa ni kumtumikia Yehova peke yake na kulitakasa jina lake. Mawazo ya moyo yanaongoza sana dhamiri ya mtu ili afanye mema au mabaya. Kwa hiyo, tukichunguza dhamiri zetu na jinsi zinavyofanya kazi huenda pia tukafahamu tamaa na makusudi ya moyo. Tutaona kama tuna moyo mwema au mbaya. Vilevile, tujuapo wajibu wetu wa kufuata mwenendo wa adili, tutaweza kuchunguza kazi za moyo na akili yetu, na kuona sisi tu watu wa namna gani hasa kwa ndani, kama vile Mungu atuonavyo.—1 Sam. 16:7.
4. Kwa sababu gani ni jambo la maana kujua yaliyomo mioyoni mwetu?
4 Lazima tujue yaliyomo mioyoni mwetu ikiwa tunataka kuzoeza vizuri dhamiri zetu. Kufanya hivyo kunaweza kuonyesha wazi mambo mengi kama Yesu Kristo alivyosema “Moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati, wivi, ushuhuda wa uongo, na matukano; hayo ndiyo yamtiayo mtu unajisi.” (Mt. 15:18-20) Si mawazo yanayonajisi yatokayo moyoni tu, bali pia wema utakasao hutoka moyoni. Kwa maana Yesu alisema: “Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.” (Luka 6:45) Ili tufanye maendeleo katika dhamiri zetu lazima tuijue na kuifahamu mioyo yetu.
5. Kuchunguza dhamiri kunaweza kutusaidiaje zaidi?
5 Kuchunguza dhamiri kunaweza kufunua kama tunatumikia Mungu kwa makusudi bora, si kwa kutii tu orodha yenye sheria nyingi. Ndiyo kusema, kutafunua kama tunafuata maadili kwa sababu ya sheria fulani tu, au tunajitahidi tuyafuate kwa sababu twataka kumpendeza Mungu kweli kweli, na kupata kujua zaidi hisani yake kwa kuhusiana naye. (Rum. 12:2) Uchunguzi utatulazimisha tuulize na kujibu ulizo hili: Je! tungekuwa wenye adili hata kama kusingekuwa na amri za Biblia zenye kusema lazima tuwe na adili?
6. Bila shaka chanzo cha adili ni nini, na Yesu Kristo alieleweshaje hilo wazi?
6 Adili ni njia ya Mungu. Bila shaka, ndio mwendo mzuri zaidi kwa sababu unaendeleza amani ya kweli na furaha. Yesu alisema bila shaka chanzo cha adili ni Mungu, aliponena: “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, Waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! nao hawafanyi kama hayo? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:43-48) Kwa hiyo, lazima Yehova, Baba wa kimbinguni, awe ndiye mfano wa kwanza wa dhamiri njema. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”
7. (a) Ni nini kinachoweza kuonyesha vizuri zaidi kama mtu ana dhamiri njema? (b) Kwa sababu gani tuna wajibu wa kufuata mwenendo wa adili juu ya mambo tunayojua kuhusu Mungu?
7 Yesu, aliyekuwa fundi wa kufanya dhamiri iwe nyepesi, alifunua kwamba kupenda Mungu, kunakoonyeshwa katika matendo ya kila siku ya maisha ndiko kunakoweza kuonyesha vizuri zaidi kama mtu ana dhamiri njema. Kazi zote zinazofanywa na wanadamu zapaswa kuwa matendo ya upendo. “Pendo ndilo utimilifu wa sheria.” (Rum. 13:10) Mwenendo wa adili hautokei kwa kulazimishwa. Lazima uwe wa kujitolea, wenye kuongozwa na upendo. Kwa maana “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Na kwa kuwa Wakristo hawako tena chini ya orodha yenye sheria nyingi bali chini ya ‘sheria ya kifalme ya upendo,’ sisi leo tunakuwa na wajibu wa kufuata mwenendo wa adili katika kila jambo tunalojua juu ya Yehova—utu wake, kanuni zake, na makusudi yake. (Yak. 2:8) Upendo wapaswa kutuongoza tutumie ufahamu zaidi tuliopata juu ya vile dhamiri ilivyo na inavyofanya kazi, ili tuweze kusaidia wengine pia, si kuendeleza mafaa yake ndani yetu wenyewe tu. Lazima tuwe na dhamiri nyepesi na yenye mafaa ili tuweze kuongoza maisha zetu kwa usalama katika. nyakati hizi zinazoendelea kuwa na magumu na hatari, ili tuweze kuendelea kumpendeza Yehova.
SABABU MAARIFA PEKE YAKE HAYATOSHI
8. Kwa sababu gani kupata tu maarifa zaidi ya Biblia hakutoshi kufanya dhamiri iwe na maendeleo?
8 Twawezaje basi kufanya maendeleo katika dhamiri zetu? Kujua tu utu wa Yehova, kanuni na makusudi yake hakutoshi. Kupata tu maarifa zaidi ya Biblia hakutafanya utendaji wa dhamiri zetu uwe na maendeleo, ingawa kunaweza kusaidia sana akili na moyo. Mtunga zaburi aliandika hivi: “Sheria ya [Yehova] ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya [Yehova] ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya [Yehova] ni safi, huyatia macho nuru. . . . Tena mtumishi wako huonywa kwazo, katika kuzishika kuna thawabu nyingi.” (Zab. 19:7-11) Hata hivyo, ijapokuwa wema mwingi unatokana na Neno la Mungu, lazima ikumbukwe kwamba dhamiri si utendaji wa akili tu bali ni wonyesho wa vile adili ya mtu ilivyo pande zote. Lazima dhamiri itujulishe sisi tukoje katika maisha halisi; si kutuambia tupaswavyo kuwa tu.
9. Ni nini linaloonyesha kwamba kujipatanisha na utu wa Yehova ndilo jambo kuu zaidi linalotegemewa ili kusitawisha dhamiri njema?
9 Kwa hiyo, Biblia ina sababu ya kutosha kuonyesha kwamba dhamiri njema inahusiana na imani na sifa ya upendo, si na maarifa tu. Katika 1 Timotheo 1:5 twasoma hivi: “Mwisho wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki.” Hivyo twaona kwamba imani, upendo na dhamiri njema zinakwenda pamoja. Kukataa mojawapo ya sifa hizo ni kukataa zile nyingine mbili. Kukataa dhamiri ni kuvunja imani. Vilevile, kusema kwamba upendo hauhitajiwi ni kukataa sifa kuu ya Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo. Hivyo utu wa Mungu, unaofunuliwa katika Neno lake na katika matendo yake na watumishi wake, unaonyeshwa waziwazi kama jambo kuu zaidi ambalo dhamiri njema inategemea ili isitawishwe.
10. Paulo alionyeshaje kwamba upendo ndiyo sifa ya maana zaidi kuliko zote?
10 Kijana Sauli wa Tarso, ambaye baadaye alijulikana kama mtume Paulo, alilazimika kujifunza uhakika huo. Yeye alijua sana sheria ya Musa, na alikuwa amefundishwa katika shule za Kiyahudi na katika njia zao. Lakini baada ya kuwa Mkristo alikata maneno hivi: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi.” (1 Kor. 13:1, 2) Kutokana na maneno hayo ya Paulo ni wazi kwamba kuongeza maarifa tu, au hata kujifunza sheria na kanuni zaidi za Biblia hakuwezi peke yake kuleta maendeleo ya: dhamiri. Huenda maarifa yakamjaa mtu kichwani, lakini yasifike moyoni.
11. Eleza vile maarifa peke yake au matendo ya kijuujuu tu yanavyoweza kukosa kuleta maendeleo ya dhamiri?
11 Hatari kubwa yaweza kutokea. Huenda mtu akafanya matendo ya kujionyesha tu, na kumbe sivyo hali yake ya kiroho ilivyo. Huenda akafanya matendo hayo ya kujionyesha bila kuongozwa na unyofu. Huenda mtu akajionyesha anafuata dini na kumbe ana makusudi yake mwenyewe. Hata matendo yanayoelekea kuwa ya upendo na ya kujikana yaweza kwa vyepesi kuwa matendo ya kujionyesha kijuujuu tu bila kutoka moyoni na bila kuwa na maana katika mwenye kuyafanya. Mtu’ aweza kuanza kuwa na kinaya ya upumbavu, akidhani ana dhamiri njema ya Kikristo kwa sababu anaishi kulingana na kielelezo kilichowekwa cha sheria na kanuni. Maisha, hata ibada, yaweza kuwa desturi tu anayofuata bila shauku, jambo la kusomwa vitabuni tu, kuchunguza-chunguza tu tarehe za matukio. Huenda akadhani si vibaya asipotimiza madaraka makubwa, ati kwa sababu anafanya yale madogo madogo. Yesu alionyesha Mafarisayo uhakika huo, akisema: “Wanafiki! . . . mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na [uaminifu].” (Mt. 23:23) Kufanya mambo hayo madogo madogo kwaweza kutuliza dhamiri inayoruhusu mtu asipende watu. Huenda kufanya kwake mambo madogo mazuri kukampa kisababu cha kutofanya mambo mazito zaidi ya kuhukumu kwa haki na kuelewana na wanadamu wenzake.
12. Ili kumjua Yehova kuwe na mafaa, lazima kufanye nini?
12 Ndiyo sababu maarifa zaidi juu ya Yehova hayapaswi kuleta maendeleo ya akili peke yake. Akili yenye kupashwa habari lazima itende pamoja na moyo wenye kuelekea adili. Lazima ifanye utu wako uelekee zaidi kanuni na makusudi ya Mtu mwingine, yaani, Yehova.
PATANISHA ZAIDI UTU WAKO NA YEHOVA
13. (a) Ili tufanye maendeleo katika dhamiri. kwa sababu gani ni lazima tujifunze Biblia? (b) Maarifa juu ya Biblia yapaswa kutusaidiaje?
13 Mwanadamu duniani awezaje kujipatanisha zaidi na utu wa Yehova ambaye yuko mbinguni? Kwa njia hii: Biblia ni ufunuo kwa wanadamu juu ya vile Mungu mwenyewe alivyo. Inafunua utu wake, kanuni zake na makusudi yake. Kwa hiyo, ili kufanya maendeleo katika dhamiri ni lazima tujifunze Biblia. Maarifa tunayokusanya kwa kujifunza Biblia yamepaswa kutuwekea msingi wa kuwa na uhusiano wa usiri na Mbuni wake, Yehova. Yapaswa kutufahamisha kuwaza kwake, utu wake, kama vile kutembelea rafiki kwa kawaida kunavyotufahamisha naye. Kwa kuwa Mungu ndiye Mtu mwenye hekima na upendo zaidi ya wote katika ulimwengu wote, tunayojifunza kwake yapaswa kuvuta akili na mioyo yetu kwa njia halisi na yenye maana.—Kol. 1:9, 10; Isa. 54:13.
14. Eleza vile maarifa yanayopatikana kwa kujifunza Biblia yanavyoweza kutumiwa yatengeneze dhamiri iwe yenye faida. Toa mifano.
14 Kwa mfano, katika masimulizi ya Mwanzo twasoma juu ya mipango ya Yehova ya upendo kwa wanadamu na kwamba hakuacha kuifanya hata baada ya dhambi kuingia. Hiyo yapaswa kuchochea mioyo yetu tumpende Muumba wetu. (Mwa. 1:29, 30; 8:22) Baadaye, twaona Mungu akionyeshwa kwa mwujiza kuwa mwenye nguvu zote ampapo Ibrahimu mwana. Urafiki wa Ibrahimu na Yehova ulimwaminisha kwamba Mungu angeweza hata kufufua wafu! (Ebr. 11:17-19) Waisraeli wenye kuonewa waliookolewa katika utumwa wa Misri walimwona Yehova kama “mfanya maajabu.” (Kut. 15:11) Yoshua alimwona Yehova kama Mungu mtimiza neno na ahadi Yake, hata akaweza kuwaambia Waisraeli: “Halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu.” (Yos. 23:14) Wakati mtume Petro alipotumwa kwa Kornelio Mtaifa, aliona kwamba “Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Yesu Kristo alisema hivi: “Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako.” (Mt. 11:25, 26) Biblia inafunua utu na fahari ya Yehova kwa uzuri ulioje! Ujumbe wake ulioongozwa na Mungu wapaswa kufikia mioyo yetu, kuamsha na kutengeneza dhamiri zetu.
15. Ni nini kinachohitajiwa ili kukuza ndani ya dhamiri uwezo wa kuona wajibu wetu wa kufuata mwenendo wa adili?
15 Tunapojifunza Maandiko yatupasa tujitahidi kufahamu maana ya haki ya hukumu ya Mungu, upendo na adili yake, na kuzitia ndani sana ya mioyo yetu hata ziwe kawaida yetu kama vile kula na kupumua. Yatupasa tujaribu zaidi tuone wajibu wetu wa kufuata mwenendo wa adili kwa kukuza sana uwezo wa kuona yaliyo haki na yaliyo mabaya. Zaidi ya hilo, yatupasa tufanye dhamiri yetu ione zaidi wajibu wake kwa Mpaji-Sheria na Mwamuzi aliye mkamilifu. (Isa. 33:22) Kwa hiyo tunapojifunza mambo juu ya Mungu, yatupasa tuwe tukijaribu kumwiga kila upande wa maisha.
16. Maarifa juu ya Mungu yanawezaje kutumiwa katika matendo ya kila siku ya maisha?
16 Twajifunza kwamba Mungu husamehe. Lakini je! sisi husamehe? Mungu haonei wala hanyang’anyi. Je! sisi twafanya hivyo? Mungu ni mwenye fadhili kwa wajane, yatima na wageni. Je! sisi tunayo? Mungu ni mwaminifu na mnyofu katika kila jambo. Je! tunajaribu kuwa kama yeye katika maisha yetu ya kila siku? Tunaweza kujaribu. Dhamiri iliyozoezwa haitatosheka bila kukuza utu unaoiga mfano wa Mungu katika mambo yote.
17. (a) Imetupasa tuwe na kusudi la kupata nini kwa kujifunza Biblia? (b) Viongozi wa dini za Kiyahudi walikosaje kuelewa kusudi la Torati yote?
17 Tunapoendelea na funzo letu la Maandiko, yatupasa tukumbuke kupata roho na maana ya kweli, si kuona maandishi tu. Viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza walikuwa na maarifa mengi lakini walikosa maana ya Torati yote. Walikosa kumtambua Yesu, ambaye ndiye alikuwa kweli. (Yohana 14:6) Mara nyingi wao waliona kibanzi katika jicho la ndugu yao lakini hawakuona boriti iliyokuwa ndani ya jicho lao wenyewe! (Mt. 7:1-5) Wakati wanafunzi wa Yesu hawakunawa mikono kabla ya kula, Mafarisayo waliudhika sana. Lakini wao walikuwa vipofu kabisa wasione kwamba walikuwa wakivunja amri za Mungu kwa mapokeo yao. (Mt. 15:1-20) Wakati mwingine waliwaona wanafunzi wa Yesu wenye njaa wakichuma nafaka na kula viini vyake siku ya sabato. Walikasirika sana. Lakini hawakuona ubaya wa kuua, kwa hiyo wakafanya shauri juu ya Yesu “jinsi ya kumwangamiza.” (Mt. 12:1-14) Wanafiki hao hawakujisikia wakiwa na kichomi katika dhamiri zao kwa kumlipa Yuda pesa za hazina ya hekalu ili amsaliti Yesu, lakini alipokwisha kufanya tendo lake baya, walikataa kuzirudisha katika hazina. Kwa wazi sasa waliziona pesa hizo kuwa chafu. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 23:18.) Lakini je! wauaji hao wangeweza kuwa na dhamiri safi?
KUIPATA NIA YA KRISTO
18, 19. (a) Kwa sababu gani jitihada yapaswa kufanywa ili kupata “nia ya Kristo”? (b) Yesu aliwekea wanadamu kanuni gani bora ya adili?
18 Kwa kuwa sikuzote Yesu Kristo alionyesha utu mkamilifu wa Yehova, yatupasa tujitahidi sana tuipate “nia ya Kristo.” (1 Kor. 2:16) Hiyo yamaanisha kwamba, kwa moyo wa kupenda, yatupasa tuwe na maelekeo ya akili ya Kristo yanayohakikisha utu wetu unapatana kila upande na ule wa Yesu. Yesu alionyesha uhusiano mwema uliokuwa kati yake na Baba yake wa kimbinguni aliposema: “Amin, amin, nawaambia, Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile.” (Yohana 5:18-20) Twauona wema wa Mungu katika maisha yote ya Yesu. Ni kama vile Yesu alivyomwambia Filipo: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Sisi Wakristo, tunaagizwa tufuate mfano wa Yesu.—1 Pet. 2:21; tazama pia Zaburi 40:8.
19 Lo! yeye alituwekea mfano mwema namna gani! Petro, aliyetembea pamoja naye, alisema: “Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki.” (1 Pet. 2:22-24) Mfano wa Yesu unaweza kusafisha mtu na kumfaidi. Ufuate sana.
20. (a) Dhamiri yenye maendeleo itatulindaje? (b) Paulo asemaje kwamba dhamiri hiyo inatakiwa kabisa?
20 Tunapozidi kujua maana ya kweli ya Mungu inayofunuliwa katika Yesu mwenyewe kama kichwa cha kundi la Kikristo, maelekeo yote ya akili na mioyo yetu yapaswa kuzidi kuwa na maendeleo. Hiyo itafanya dhamiri zetu zifae zaidi. Tukiwa na dhamiri zenye mafaa ndani yetu tutaweza kuepuka dhamiri mbaya za watu wa ulimwengu, na akili zao zenye giza na mioyo iliyokufa ganzi. Paulo anatukazia jambo hili katika Waefeso 4:17-24, akisema: “Nasema neno hili, tena nashuhudia katika Bwana, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao; ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani.” Lakini angalia anayosema Paulo sasa: “Ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo katika Yesu, mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika [nguvu yenye kuendesha, NW] nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.” Lazima maisha yetu yote yageuzwe na nguvu yenye kuendesha nia zetu, na hiyo inatokana na kupata “nia ya Kristo.”
21. Itampasa Mkristo aendelee kufanya nini ili aige mfano wa Yeye aliyemwumba?
21 Kufahamu kwetu utu wa Yehova, kama ulivyoonyeshwa katika maisha ya Kristo, kutaongezeka tunapojifunza Biblia zaidi sana. Hivyo tutaweza kupatanisha matendo yetu zaidi na zaidi na mfano wa Muumba wetu. Paulo alisihi hivyo, akisema: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.”—Efe. 5:1, 2, NW.
22. Mtume Petro anatutolea shauri gani jema la wakati ufaao?
22 Kama “waigaji wa Mungu,” tutaungana zaidi tukiwa watu wa pekee wa Yehova. Tutaweza kujulikana zaidi kama wachukua nuru katika ulimwengu huu wenye giza. Kwa hiyo, kama vile Petro alivyoonya kwa upole: “Mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema [yaani, ulimwengu wenye tabia chafu] katika Kristo.” (1 Pet. 3:16) Wakiwa na dhamiri safi na nyofu watu wa Yehova wataonekana wakitoa ushuhuda wa Ufalme kwa juhudi huku wakingojea kwa saburi kufunuliwa kwa Bwana Yesu Kristo mwanzoni mwa siku kuu ya Yehova ya kisasi.
—Kutoka The Watchtower, Sept. 1, 1976.