‘Kufanya Kazi Usiku na Mchana’ Kufanya Wanafunzi
“Nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na [nafsi] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa kwetu. . . . Kwa kuwa mchana na usiku tulifanya kazi . . . tukawahubiri hivi Injili ya Mungu.”—1 The. 2:8, 9.
1. (a) Tengenezo la Yehova linafanya kazi kutimiza kusudi gani? (b) Imewapasa watumishi wa Mungu wajishughulishe sasa na jambo gani?
TENGENEZO la Yehova linafanya kazi likiona haraka ya kufanya hivyo. Kuna kazi ya kufanya. Kupatana na sala inayosema jina la Yehova litakaswe, viumbe viaminifu vya kimbinguni ‘havipumziki mchana wala usiku, vikisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Yehova Mungu Mwenyezi.’ (Ufu. 4:8; Mt. 6:9) Vivyo hivyo, katika dunia yote huu “wakati wa mwisho,” watumishi wa Mungu walio wakf, wajapokuwa wenye upungufu wa kibinadamu, wanajishughulisha katika ‘mwendo mutakatifu na utawa, wakitazamia na kutaka sana kuya kwa siku ya Mungu, kwa sababu yake, mbingu zikilungula zitayeyushwa, na viumbe vya asili vitayeyuka kwa moto mukali!’ Ahadi ya Mungu ya “mbingu mpya na inchi mpya” yenye haki itakayofuata “siku” hiyo yenye moto ni nzuri namna gani!—2 Pet. 3:11-13, Swahili Congo Bible; Dan. 12:1-4.
2. Ni nini yanayohusika katika kumtumikia Mungu?
2 Utumishi kwa Mungu si kama kazi ya kimwili yenye kuchosha ya kila siku na ya kawaida tu. Haihusu kufanya kazi zamu ya mchana au ya usiku tu. Ni utumishi unaoongozwa na kutaka sana kujitoa ‘usiku na mchana’ kwa kutii amri za Yesu kuhubiri na kufanya wanafunzi, kwa sababu ya upendo wa Kikristo. (Mt. 24:14; 28:19; Yohana 13:34) Hii haina maana ya kwamba mtu asijali uhitaji wake wa kupumzika na kuburudika, kwa maana baada ya muda fulani hiyo ingemaliza nguvu na afya yake: Lakini imempasa awe mwenye nia na shauku ya kusaidia wengine kwa kiroho katika kila nafasi, iwe ni “mchana” au “usiku.”
3. Paulo na wenzake walilionaje kundi katika Thesalonike?
3 Mtume Paulo na wenzi wake walifanya lilo hilo! Walifanya hivyo kwa sababu ‘waliwatumaini kwa upendo mwingi’ wenye kupendezwa. Walipofanyiza kundi jipya katika Thesalonike, mara moja likapatwa na majaribu na mateso. Lakini kwa sababu ya ukamilifu wao wakiwa chini ya jaribu, Wakristo wapya hawa ‘wakawa wapendwa’ kwa wale waliokuwa wamejifunza nao. Paulo na watumishi wenzake wa Mungu walikuwa wamevutwa kutoa ‘nafsi’ zao wenyewe kwa ajili ya Wathesalonike, si “Injili” peke yake. Walipokuwa na kundi hilo changa, walifanya kazi kwa bidii ‘usiku na mchana’ waangalie mahitaji yao wenyewe na, zaidi ya hilo, wakatumia wakati mwingi wakiwafundisha wanafunzi wapya hao. Kwa njia hii, wao kweli walitoa nafsi zao kabisa katika utumishi wa usiku na mchana kwa Yehova.
4. Imetupasa tuwe na nia gani ya hakika juu ya utumishi wetu leo?
4 Je! kuhangaikia kwetu watu wenye mfano wa kondoo katika eneo letu wenyewe ni kwenye nguvu kadiri hiyo? Tunajua tunayo kazi ya kufanya tuliyogawiwa na Mungu. Lakini walio wengi kati yetu wanafanya kazi za kimwili ili wasiwe mzigo kwa wengine, au tunaangalia jamaa zetu, au tunakwenda shuleni. Nyakati nyingine tunashiriki katika utumishi wa shambani. Lakini tunafikiria kadiri gani watu wanaopendezwa tunaowaona tunapohubiri? Je! kweli ‘tuna upendo mwingi’ kwao? Huenda tukatumia saa nyingi katika utumishi wa shambani, nasi tunafurahia kuachia watu wapole vitabu au magazeti kadiri fulani. Pengine tunafanya ziara za kurudia kadiri fulani. Lakini nyakati nyingine huenda mwezi mmoja au miwili ikamalizika bila ya sisi kurudi kuona wale wenye kupendezwa wanaendeleaje. Je! kweli sisi tunafikiria maisha? Ili wao waweze kuona njia ya uzima, je! ‘tunaona furaha kutoa, si Injili ya Mungu tu, bali na nafsi zetu pia’?
5. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Paulo?
5 Paulo aliweka mfano bora kwa kujitoa kwa ajili ya ndugu zake wapya na wengine wenye kupendezwa. Alipokuwa akiagana kwa mara ya mwisho na wazee wa kundi la Efeso, alisema hivi: “Kwa sababu ya maneno haya angalieni, mukikumbuka ya kama kwa kadiri ya miaka mitatu, usiku na muchana, sikuacha kuonya kila mutu kwa machoni. Nimekwisha kuwaonesha ninyi mufano katika maneno yote, ya kuwa imetupasa kutenda hivi na kusaidia wazaifu, na kukumbuka maneno ya Bwana Yesu, kama alivyosema: Heri ya kutoa inapita heri ya kupokea.” (Matendo 20:31, 35, Swahili Congo Bible) Ikiwa sisi tunapendezwa kweli na “kondoo” kama Paulo, tutatafuta kwa moyo na nafsi njia za kuwasaidia. Tutajaribu kufanya ziara za kurudia kwao baada ya siku chache ikiwezekana, au pengine tuwapigie simu kuamsha kupendezwa kwao. Ibilisi na mawakili wake watajaribu kuharibu kupendezwa huko, kwa hiyo lazima tuwe macho kuwasaidia “kondoo” hao.—Luka 8:11, 12.
KUENDELEA KUWA WENYE SHUGHULI ‘USIKU NA MCHANA’
6, 7. (a) Ni mpanuko (ongezeko) gani unaotokea, na hii inahitaji nini lifanywe? (b) Kwa sababu gani imetupasa tufanye ziara za kwanza na za kurudia katika eneo letu?
6 Tunapoendelea kuzihubiri habari njema tunapata watu wapya wenye kupendezwa. Hivyo kazi inazidi kupanuka. Makundi mapya yanafanyizwa na Biblia zaidi, vitabu zaidi na magazeti zaidi yanaenezwa—jumla ya vitabu 313,229,157 vilichapwa wakati wa mwaka wa utumishi wa 1974. Tena, maandikisho mapya 2,387,904 ya Mnara wa Mlinzi na Awake! yalipatikana. Kuna uhitaji wa haraka kutembelea tena wale wanaopokea vitabu hivi.
7 Huenda wenye nyumba wengine hata wasikubali vitabu. Lakini huenda wakasema mambo ya kuthamini bidii ya mashahidi wa Yehova ya kuwatembelea mara nyingi nyumbani kwao. Wasiwasi wa watu hao juu ya upotovu na uovu unaozidi kuongezeka duniani unafungua njia ya kuwapa msaada zaidi. Watu wenye maelekeo ya haki wanapata kufahamu zaidi na zaidi kwamba jamii yenye choyo na isiyo na huruma ya siku zetu haitoi tumaini lo lote kwa wakati ujao. (Zab. 92:7) Kwa kutembelea watu hao mara nyingi, huenda tukawasadikisha juu ya tumaini lililo hakika. Tukitumainia hilo, “tunatia bidii nyingi na kujitahidi, kwa sababu tumeweka tumaini letu juu ya Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa namna zote za watu, hasa wa waaminifu.”—1 Tim. 4:10, NW.
8. Ni jambo gani linaloweza kutokea kwa kutumia shauri la Mhubiri 11:6?
8 Tukiendelea kuwa wenye kazi nyingi ‘usiku na mchana,’ huenda tukapata itikio zuri tunaposema na wafanya kazi wenzetu, majirani au wanafunzi wenzetu.
Kundi moja lililo katika mji wenye chuo kikuu linasema kwamba majuzi wanafunzi sita wameshirikiana kwa kawaida mikutanoni. Mmoja wa hawa sasa anafurahia utumishi wa upainia wa kawaida huku akihudhuria chuo kikuu. Mwanafunzi mwingine (msichana) aliyepelekewa kweli na Shahidi huyu mpya amerudi katika mji wa nyumbani kwao akafanye utumishi wa upainia, na tena mwingine aliyemfundisha amebatizwa karibuni tu.
Liko shauri zuri katika Mhubiri 11:6: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa, kama ni hii au hii, au kama zote zitafaa sawasawa.” Kwa hiyo kwa kutumia kila nafasi inayopatikana, ‘usiku na mchana,’ kuzungumza na wengine juu ya tumaini tukufu linalopatikana katika “habari njema hizi za ufalme,” tutapata hapa na pale, na mara nyingi mahali pasipotazamiwa, mioyo yenye kuuitikia ujumbe wa Ufalme.
9. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika tutapata baraka ya Yehova?
9 Yehova ‘anaijua mioyo ya watu wote.’ Tukihubiri na kufundisha kwa bidii, ujumbe utatia mizizi katika mioyo minyofu, naye Yehova atazidi “kukuza.” (Matendo 1:24; 1 Kor. 3:6) Huenda tukajibiwa vikali na kukatishwa tamaa tunapoendelea kufanya hivyo, lakini tunaweza kutazamia kwa uhakika utimizo wa maneno ya Sulemani: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.”—Mhu. 11:1.
10. Tunawezaje kufanya kazi tukiwa na kusudi?
10 Kufikiria watu kwa njia ya kweli kumepaswa kuharakishe mashahidi wa Yehova wote warudie watu wenye kupendezwa waliowakuta. Inapokuwa hivyo, wao hawaandiki jina la mtu na basi, kisha wanatia maandishi hayo katika mfuko wa vitabu na kuyasahau. Bali, wao wanataka sana sana kuwapa wapya hawa msaada unaohitajiwa. Kwa hiyo wanafanya kama vile Mithali 3:27 inavyoagiza: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Ndiyo, yatende! Kwa kuwatembelea tena kwa makusudi, upesi inavyowezekana, uendelee kuzungumza juu ya Biblia na mtu mwenye kupendezwa, unaweza ‘kupata udongo uli maji,’ kama tusemavyo, ukiongeza kupendezwa huko kabla wapinzani hawajapata wakati au nafsi ya kuondoa kupendezwa huko.
Mhubiri wa Ufalme alifanya ziara ya kurudia kwa mtu mwenye kupendezwa ilipokwisha saa moja tu baada ya ziara ya kwanza. Baada ya juma moja hivi, ziara za kurudia tatu nyingine zilifanywa ili kujibu maulizo ya Biblia, kisha funzo la Biblia likaanzwa.
11. Uhitaji mkubwa wa watu ni nini, na Mkristo anaweza kusaidia kumaliza uhitaji huo kwa njia gani?
11 Kila mwaka, mamilioni mengi ya vitabu, katika zaidi ya lugha 160, yanaachwa na mashahidi wa Yehova katika nyumba za watu wenye kupendezwa ulimwenguni pote. Lakini watu hawahitaji vitabu tu nyumbani mwao wapate kuachiliwa wapite “dhiki kubwa” inayokuja. Wanahitaji kusaidiwa watie kweli za Biblia katika akili na mioyo yao. (Rum. 10:10-15; 12:1, 2) Imewapasa wapokee “alama” ya utu wa kweli wa Kikristo katika vipaji vya nyuso zao. (Eze. 9:4; Efe. 4:24) Inachukua muda kujifunza kanuni za Biblia na kuvaa huu “utu mpya.” Mtumishi wa Mungu aliye Mkristo anapaswa kuendelea kutoa msaada wa upendo, saburi na huruma, ili walioanza kupendezwa karibuni waweze kujifunza matakwa ya uzima wa milele, na kubadili nia zao wafuate maisha ya Kikristo. Je! wewe una nia ya kuwapa msaada huo? Tukiwa tunakumbuka sikuzote haraka ya nyakati, na kwamba ni shauri la kufa na kupona, na tujitoe kwa ajili yao huku tukisali maadamu wakati upo.—Yohana 9:4; Flp. 1:9-11.
12, 13. (a) Mitume na wengine walifanya marekebisho gani ili washiriki katika kufanya wanafunzi? (b) Tunawezaje kufurahia baraka kama hizo leo?
12 Huenda mtu akasema, “Mimi sina uwezo wa kuongoza funzo la nyumbani la Biblia.” Au, “Sina wakati wa kuongoza funzo kwa mtu kila juma kwa kawaida.” Ni kweli, wengine wetu tu wapya na hatuna ujuzi, au hatuna elimu nyingi. Huenda mkazo wa kujipatia riziki (chakula n.k.) katika jamii hii ya kisasa ukaelekea kumaliza wakati wa mambo mengine. Hata hivyo, je! hatuwezi kufanya kama walivyofanya mitume na wanafunzi wengine wa kwanza? Wengine wao walikuwa wamekuwa na kazi nyingi ya kuvua samaki na shughuli nyingine za kimwili. Lakini walirekebisha (walitengeneza) njia yao ya maisha ili waweze kumfuata Yesu wajifunze kuhubiri na kufundisha. Walitafuta wakati wa kufanya hivyo.—Marko 1:16-20.
13 Mitume hao hawakuwa na elimu wala maarifa mengi ya kilimwengu. Lakini walikuwa na roho ya Mungu, nao waliyakubali mazoezi ambayo Yehova alitoa. Baada ya muda mfupi, kuhubiri na kufundisha kwao kwa bidii kukaleta ongezeko kubwa sana la waamini “kama elfu tano” katika mji wa Yerusalemu. Watawala wenye kupinga walishindwa kulizuia. “Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.”—Matendo 4:4, 13; Yohana 7:46.
14. (a) Mapendezi yetu makubwa leo ni nini, na kwa sababu gani ni jambo la haraka? (b) Kuamini kwetu unabii mbalimbali kumepaswa kutuongoze tufanye nini?
14 Petro, Yohana na wanafunzi wengine walipendezwa na kuokoa maisha. Hayo pia ndiyo mapendezi yetu makuu leo. Ulimwengu uliohukumiwa maangamizi u karibu sana kupatwa na ‘dhiki kubwa’—“wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.” Lakini mabaki ya Israeli wa kiroho wanatazamia kuokoka, na kutakuwa na furaha kuu, pia, wakati ‘mkutano mkubwa kutoka mataifa yote na kabila na jamaa na lugha watakapotoka katika dhiki ile iliyo kuu,’ kwa sababu walionyesha imani katika damu iliyomwagwa ya Mwana-Kondoo, Kristo Yesu, na kwa sababu walifuata ibada ya Yehova “mchana na usiku katika hekalu lake.” (Dan. 12:1; Ufu. 7:9-15) Je! wewe unaamini hili? Basi sababu gani usifanye marekebisho yaliyo ya lazima maishani mwako ili uweze kujitoa kabisa kutembelea watu wenye mioyo minyofu kwa mara ya kwanza na baadaye, na kujifunza nao mpaka wasimame imara katika njia ya wokovu? Haraka ya wakati inataka jitihada hii ifanywe!—Rum. 13:11, 12.
15. Ni kwa njia gani kazi ya kufanya wanafunzi inavyoweza kusitawishwa?
15 Kwa vyo vyote, imetupasa tuwe Wenye kazi nyingi tukisaidia wale wanaopendezwa kweli na Neno la Mungu. Ikiwa kwa sababu fulani hatuwezi kufanya ziara ya kurudia karibuni, imetupasa tumwombe mtangazaji mwingine wa Ufalme asaidie. Wazee na watumishi wa huduma katika kundi watafurahi pia kusaidia kupanga ili watu wote wenye kupendezwa waangaliwe inavyofaa. Mwito unatolewa kwa wote wanaoshiriki katika kazi ya Ufalme, pengine wanaosaidia kwa mara ya kwanza kugawa Kingdom News (trakiti zinazochapwa baada ya kipindi fulani kueneza habari za pekee), wafanye maendeleo kwa kuingia katika pande nyingine za utumishi wa shambani, wakifanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo. Wewe pia unaweza kufanya maendeleo kama mwangalizi kijana Timotheo, kupatana na alivyoomba Paulo: “Ufikili maneno haya, uyitoe kabisa kwa maneno haya, kusudi maendeleo yako yaonekane kwa watu wote. . . . Dumu katika maneno haya; maana kwa kufanya hivi utayiokola mwenyewe nao wanaokusikia.”—1 Tim. 4:15, 16, Swahili Congo Bible.
KUBADILIKA-BADILIKA KULINGANA NA MAHITAJI YA WENYE KUPENDEZWA
16. Vitabu Kweli na Amani na Usalama vinaweza kutumiwaje?
16 Mtumishi wa Mungu aliye Mkristo amepaswa awe mwenye kubadilika-badilika na kuwa mwenye ufahamu katika kuanza na kuongoza mafunzo ya Biblia. Huenda watu walio na habari fulani juu ya Biblia, au ambao wamehusiana na dini za Jumuiya ya Wakristo wakafurahi kujifunza Biblia kwa kusaidiwa na kitabu Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele. Au, ikiwa wanahangaikia sana kupata njia ya kuondolea taabu za ulimwengu au ikiwa wanakasirishwa na mwenendo mbaya wa watu, funzo katika kitabu Amani ya Kweli na Usalama wa Kweli—Kutoka Chanzo Gani? linaweza kufaa. Kabla kila mtu mpya hajabatizwa kama mwanafunzi wa Yesu Kristo, ingeleta mafaa akisoma vitabu vyote viwili vilivyotajwa juu, huku akiangalia Biblia, ili afahamu vizuri mafundisho na kanuni pia za maisha ya Kikristo.—Matendo 17:11.
17. Kazi ya kufundisha inawezaje kubadilishwa ilingane na hali zilizomo duniani mwote?
17 Katika sehemu fulani za dunia, pengine watu hawakusoma sana. Wengine hata hawajui kusoma na kuandika. Lakini wengine kati ya hawa wataonekana kuwa wenye mioyo minyofu na wanaweza kupendelewa kuokoka ‘dhiki kubwa.’ Katika nchi fulani ambako haijapata kuandikwa lugha yo yote katika vitabu, watumishi wa Mungu wametumia picha za ukubwa, namna na rangi mbalimbali kufundisha mafundisho ya maana ya Biblia. Katika nchi nyingi, wapya wanafundishwa na mashahidi wa Yehova kuandika na kusoma, ili waweze kufanya maendeleo katika kujifunza Biblia. Vitabu vinatolewa vya kutumiwa na vipofu. Katika Afrika na katika nchi nyingi za Jumuiya ya Wakristo, kijitabu chenye maneno mepesi kufahamika “Habari Njema Hizi za Ufalme” kimefikia mioyo mingi kikiwa na ujumbe wenye kufahamika waziwazi. Katika nchi fulani za Asia, kijitabu “Tazama! Nayafanya Yote Kuwa Mapya” kimekuwa na matokeo mazuri sana kwa kufundisha wapya wasiojua lo lote juu ya Biblia na hali yake ya msingi. Kwa mfano:
Mwungwana mmoja Mwasia aliyekuwa na cheo kikubwa katika benki alinunua sehemu kubwa ya nchi akafanya mipango ajenge nyumba nzuri. Lakini wakati huu mkewe akaanza kujifunza na mashahidi wa Yehova. Baada ya kuombwa afanye hivyo, yeye pia akaanza kujifunza, akitumia kijitabu “Tazama! Nayafanya Yote Kuwa Mapya.” Walipojifunza mpaka fungu la 4, akaamua kwamba yeye anapendezwa na taratibu mpya ya Yehova. Kuanzia hapo akajifunza Biblia kwa bidii sana. Si kwamba tu aliacha mipango yake ya kujenga nyumba mpya, bali pia aliacha cheo chake katika benki, ili aweze kukaza fikira zaidi juu ya masomo yake ya Biblia. Baada ya miezi miwili ya kujifunza, akawa mtendaji katika utumishi wa shambani. Yeye na mke wake wamehamia nyumba ndogo ili wasiwe na vizuizi wakati watakapostahili karibuni kuingia utumishi wa upainia. Painia anayejifunza nao anasema hivi: “Lo! ni pendeleo zuri kama nini kusaidia watu hawa wenye mfano wa kondoo!”
18. Tunaweza kuwa wenye kubadilika-badilika kwa njia gani tunapojitahidi kufikia mradi wa kuongoza funzo?
18 Viko vitabu vingi vinavyozungumza juu ya Biblia vilivyokusudiwa kuamsha kupendezwa kwa wapya na kutimiza mahitaji yao. Wale wanaojua sayansi au wenye masomo huenda wakasita kujifunza Biblia kwa kuwa inalaumiwa sana. Lakini kuzungumza nao juu ya habari zilizomo katika vitabu Is the Bible Really the Word of God? na Did Man Get Here by Evolution or by Creation? huenda kukawaonyesha kwamba Biblia ndiyo inayotoa masomo bora zaidi na kwamba haikosi kutoa hata habari chache juu ya sayansi. Wengine wanaweza kufikiwa kwa kupendezwa na watoto wao na kuonyesha wazazi namna ya kujifunza kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu pamoja na watoto. Baadaye huenda funzo la kawaida likaanzwa pamoja na jamaa yote. Kwa hiyo imetupasa tuwe wenye kubadilika-badilika tunapotia bidii tukatimize mradi huu wa kuongoza funzo, na pia tunapochagua kitabu cha kusaidia kujifunza Biblia kitakachofaa zaidi.
19. Tunawezaje kubadili mambo tuchukuane na hali zenye magumu?
19 Nyakati nyingine kubadilika-badilika kunahitajiwa katika kupanga wakati na mahali pa kujifunza pia. Kwa mfano, ilimpasa Shahidi aliyekuwa akijifunza na mvuvi wa samaki alipange funzo liwe jioni wakati mvuvi alipokuwa amekwisha rudi kutoka baharini na mashua yake, akabadili wakati wa kujifunza na jamaa yake mwenyewe ili jambo hili liwezekane. Imekuwa lazima wengine wajifunze saa za chakula kazini, pengine wakijifunza mara mbili kila juma kwa ufupi. Mahali pa kujifunzia huenda pakawa ni kiti cha bustani, ndani ya motokaa iliyosimamishwa uwanjani pake, au nyumba ya Shahidi, ikiwa kuna upinzani wa kujifunzia mahali penginepo.
WEWE UTAFANYA NINI KATIKA KAZI HII YA KUFANYA WANAFUNZI?
20. Ili kuwa na matokeo mazuri katika kufanya wanafunzi, ni jambo gani la lazima? Toa mfano.
20 Awezalo kufanya mtu huenda likategemea hali mbalimbali, kama vile madaraka ya jamaa, afya na mambo mengine. Lakini unalotaka wewe ni nini? Je! ni kupanua utendaji wako wa shambani, ili uwe na matokeo mazuri kweli kweli katika kufanya wanafunzi? Basi jitoe, ukiwa na tumaini kamili katika Yehova. Hivi ndivyo mambo yalivyokuwa kwa mtu fulani aliyefanya hivyo:
Kijana wa kike aliyelelewa katika Ukristo wa jina tu aliona kitu fulani kilikuwa kinakosekana. Alivutiwa sana na uzuri wote katika uumbaji, lakini yeye hakuwa akimsifu Muumba. Kutokana na mashahidi wa Yehova akajifunza juu ya tengenezo la Mungu la ajabu la ulimwengu wote na makusudi yake ya Ufalme. Akawa anataka sana sana abatizwe kisha astahili kuwa painia wa kawaida. Kabla ya hapo maisha yake yalikuwa yametayarishwa kumtumikia mumewe na watoto wake tu. Wakiwa wanashirikiana naye kwa umoja, sasa akaweza kurekebisha mambo aendelee kuwatumikia lakini atumikie Yehova kwanza na zaidi kupita wote. Akamaliza magumu yake moja kwa moja kwa kumtegemea Yehova. Mume wake akamruhusu aache kufanya kazi naye kazini pake (mume), na siku ile ile mumewe akashangaa kwa kuwa mapato yake yaliongezwa bila kutazamia yakawa mara mbili ya aliyokuwa akipata. Mwishoni mwa utendaji mwingi wa shambani wakati wa mchana, mkewe akawa anachoka, lakini yeye alitaka mumewe aone kuwa yeye ni mwenye furaha tu. Halafu mumewe akamnunulia gari dogo la kutumia katika utumishi wake wakati ule ule alipokuwa ndio analihitaji sana. Mkewe hakosi mkutano wakati wo wote, naye anasoma Biblia kila siku, akitiwa moyo sana na mifano ya uaminifu ya watumishi wa Yehova wa siku za zamani. Wakati mmoja alisafiri na watoto wake zaidi ya maili elfu moja, akahubiri katika kisiwa cha nyumbani kwao, huko akakuta watu wengi wenye kupendezwa na Biblia hata mapainia wa pekee wakatumwa wakaangalie wenye kupendezwa. Mama huyu wa nyumbani kweli alitimiziwa alilokuwa akitaka maishani.—Zab. 145:16.
21. Ni nani wanaoweza kuona furaha ya kweli katika utumishi wa shambani leo?
21 Kama vile maono haya na mengine ya kweli yanavyoonyesha, kazi ya maana sana ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi haipaswi ifanywe kwa nguvu zetu wenyewe. Lazima tumtegemee Yehova na kuendelea kutafuta uongozi wake. Yeye atatusaidia tusitawishe uwezo wetu mbalimbali. Paulo aliandika hivi kwa Wakristo wa karne ya kwanza: “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, . . . walioitwa.” Sivyo, “bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima.” (1 Kor. 1:26, 27) Ndivyo ilivyo na leo. Si wale wenye masomo ya juu ya kidini walio na matokeo mazuri na furaha katika utumishi wao, bali ni watu wanyenyekevu wanaompenda Mungu na wanadamu wenzao. Kupendezwa kwao kwa kweli na wengine kunang’aa waziwazi, na “elimu ya utukufu wa Mungu” waliyo nayo mioyoni mwao inang’aa pia kwa wengine, kwa uwezo wa Mungu, ili kupendekeza kweli Yake.—2 Kor. 4:6, 7.
22. (a) 1 Wakorintho 15:58 inatoa uhakikisho gani kwa wale wanaofanya bidii? (b) Toa mfano wa mahali penu au wa maono mengine Juu ya furaha itakayopatikana katika utumishi wa usiku na mchana.
22 Hata itikio liwe namna gani, kazi yetu si ya bure. (1 Kor. 15:58) Nyingine za furaha zetu kuu zinaweza kutokana na kufanya wanafunzi. Mama wa nyumbani aliyepingwa na wakwe zake, lakini akaacha kwa uhodari kufanya kazi katika mkahawa wao ili aingie utumishi wa wakati wote wa upainia, anaandika hivi juu ya furaha hii:
Ingawa wazazi walihuzunika, waliweza kuona kwamba jamaa ya mwana wao ilipata kuwa yenye umoja na yenye furaha zaidi, na kwamba binti-mkwe wao alikuwa anafanya kazi kwa bidii nyingi asubuhi hata usiku, badala ya kuwa mvivi. Pia, utendaji wangu ukawa baraka kwa jamaa yetu. Mwaka wa kwanza, mwana wetu mwenye miaka saba akawa mhubiri, alipofika umri wa miaka tisa akabatizwa. Anafurahia utumishi kwa bidii. Kwa muda unaopungua miaka mitano toka nilipoanza utumishi wa upainia, nimesaidia watu kumi na tisa wakabatizwa. Miezi miwili ya kwanza ya mwaka huu wa 1974 wa utumishi, watu watatu ninaojifunza nao wamebatizwa, na leo watu wote wanane ninaojifunza nao wanahudhuria mikutano. Watatu zaidi kati ya hawa wataanza kuhubiri karibuni. Ninapokuta wengine wanaofurahia kujifunza, ninaona kwamba Yehova anajua kondoo zake vema naye anataka wakusanywe, hata ninajawa na furaha kweli kweli. Nyakati nyingine ninakuwa na kazi nyingi sana, na nyakati nyingine ninachoka, lakini ninasoma Isaya 40:25-31 kwa kurudia-rudia. Ninatoa shukrani kwa ajili ya pendeleo langu katika kufanya wanafunzi, nami najiona natosheka kabisa katika maisha. Kama ningaliweza kuanza kuishi upya, ningechagua kazi ii hii na njia ii hii ya maisha.
23. (a) Wale wanaofanya kazi ya kimwili wanaweza kutiwaje moyo na mfano wa Paulo na Sila? (b) Wapya waliofanywa wanafunzi karibuni wanawezaje kuwa “utukufu wetu, na furaha yetu”?
23 Hatuwezi sote kupanua utumishi wetu kwa kadiri ile ile. Na huenda maeneo fulani yakawa yasiyo na itikio yakilinganishwa na mengine. Lakini twaweza sote kufanya kazi kwa moyo na nafsi katika kuhubiri na kufundisha, tukiwa na hakika kwamba Yehova atawaongoza wale walio wake. Wengi wetu wanaweza kuwa kama Paulo na Sila, waliopendezwa kufanya kazi ‘usiku na mchana,’ si katika kazi yao ya kimwili tu, bali pia ‘kutoa Injili ya Mungu pamoja na nafsi zao wenyewe’ kwa wanafunzi wapya wapendwa. Na juu ya hawa tunaweza kusema kama mtume alivyosema: “Maana tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari, ni nini? Je! si ninyi, mbele za Bwana wetu Yesu, wakati wa [kuwapo] kwake? Maana ninyi ndinyi utukufu wetu, na furaha yetu.” (1 The. 2:7-9, 19, 20) Nayo itakuwa furaha yenye kuendelea. Kwa maana baada ya ‘dhiki kubwa’ kupita, itakuwa furaha kuu katika taratibu mpya kuwa na ushirika wenye kupendeza milele wa wale tuliowasaidia wamjua Yehova.