Wafanya Kazi Wenzi Katika Mavuno
“Ndipo [Yesu] alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake.”—Mt. 9:37, 38.
1. Upinzani mkali kwa kazi yetu unaweza kuonwa kwa njia gani?
SIKUZOTE kazi ya kuvuna haifanywi katika hali rahisi au zinazofaa, bali kwa uvumilivu. Mahali kwingine upinzani mkali unatokea, lakini maana ni kwamba kazi ya kukusanya yaendelea. Yanayoonwa yanaonyesha kwamba mara nyingi wasiopendezwa na Mashahidi wa Yehova wanaanza kuchunguza upya hali hiyo kwa sababu ya upinzani. Mwishoni mwa ripoti iliyo katika 1978 Yearbook, nchi 18 ambazo katika hizo upinzani ni mkali sana, zimepangwa pamoja. Na katika nchi hizo 18 walikuwako watu 9,673 waliobatizwa mwaka tu uliopita!
2. Ni upinzani gani mkali uliokuwako katika siku za Nehemia, na ulipambanwaje nao?
2 Si jambo jipya kwa watumishi wa Yehova kufanya kazi, na kufanya kwa bidii katika upinzani mkali. Sasa iko kama ilivyokuwa siku za Nehemia, walipokuwa na kazi ya kujenga ukuta wa Yerusalemu nao jirani wakaongeza upinzani hata kufanya fitina ya kuufanyia mji vita. Nehemia anatoa taarifa hivi: “Watu wale walioujenga ukuta, na wale waliochukua mizigo, walijitweka wenyewe, kila mtu alifanya kazi kwa mkono mmoja, na kwa mkono wake wa pili alishika silaha yake; nao wajenzi, kila mtu alikuwa na upanga wake, umefungwa ubavuni mwake, ndivyo alivyojenga. Na yeye aliyepiga baragumu alikuwa karibu na mimi.”—Neh. 4:17, 18.
3. (a) Ilikuwaje wakati huo kwamba watu walikuwa na “moyo wa kufanya kazi”? (b) Ni katika njia gani zinazolingana ambazo katika hizo unabii wa Isaya unatutia moyo leo?
3 Katika sura iyo hiyo, katika mstari wa 6, inasema kwamba “watu walikuwa na moyo wa kufanya kazi.” Je! twaijua siri ya hali hiyo nzuri ya moyo? Inatajwa katika Nehemia 8:10: “Kwa kuwa furaha ya [Yehova] ni nguvu zenu.” Je! sivyo ilivyo na sisi leo? Je! hatukumbushwi maneno ambayo Yehova alisema kupitia kwa nabii wake Isaya, yakionyesha tofauti kati ya watumishi wa kweli na watumishi wa uongo hivi: “Tazama, watumishi wangu watafurahi, bali ninyi mtatahayarika; tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo, bali ninyi mtalia kwa huzuni ya moyo; mtapiga kelele kwa sababu ya uchungu wa roho zenu”? Ndipo Yehova alipoendelea kusema: “Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya . . . Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.”—Isa. 65:13-18.
KUFANYA KAZI KWA FURAHA KWA NENO LA MUNGU
4. Ni mipango gani ambayo Yehova ametufanyia ili tuwe wafanya kazi wenye furaha?
4 Bila shaka tuna kila sababu ya kuwa wafanya kazi wenye furaha. Tuna baraka ya Yehova. Tuna roho ya Yehova, nayo “furaha” ni sehemu ya tunda la roho hiyo. (Gal. 5:22) Tunao vilevile “upanga wa [r]oho, ambao ni neno la Mungu.” (Efe. 6:17) Lo! ni furaha namna gani kuutumia huo katika kuhubiri “habari njema” kwa wengine! Mambo haya ya kweli yaliyoonwa yanaonyesha hivyo.
5-7. Katika yaliyoonwa yanayohusu kitabu Kweli, baraka ya Yehova inaonekana katika njia gani?
5 ‘Tulipokuwa tukifanya kazi katika utumishi wa shambani nyumba kwa nyumba siku moja, mimi na mwenzangu tulikutana na mwanamke kijana aliyeonyesha kupendezwa na mahubiri yetu ya Maandiko, akakubali kuchukua kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Alikuwa na maulizo fulani, na katika kujibu tulivuta fikira zake kwenye Biblia. Alisikiliza kwa makini sana yale yanayosemwa na Biblia juu ya maulizo yake. Kwa kuwa yeye na mumewe walikuwa wanakaribia kwenda safarini, tulifanya mipango turudi wakirudi. Lakini tulipokuwa tukitoka katika nyumba hiyo, mumewe akafika akiendesha gari lake. Nilisita-sita kidogo, kisha nikaamua kwamba ingekuwa vizuri nizungumze naye sasa na huenda kufanya hivyo kukaondoa matatizo (magumu) yo yote baadaye. Tulimweleza kifupi kusudi letu la kuwatembelea, tukataja kwamba mkewe alikuwa amekubali kitabu cha kusaidia kujifunza Biblia na kwamba tungependa kurudi wakati mwingine baadaye tuzungumze zaidi juu ya Biblia. Jibu lake lilikuwa jema sana, akasema kwamba yeye na mkewe hawakujua sana Biblia, na kwamba wangependa kujua!
6 ‘Mume wangu nami tuliporudi Jumamosi ya kwanza katika Juni, tulipokewa kwa uchangamfu na tukafurahia mazungumzo mazuri sana ya Biblia. Juma lililofuata, tulijifunza kwamba wote wawili walikuwa wamesoma kitabu Kweli wakakimaliza na walikuwa na ukurasa mzima wa karatasi waliokuwa wamejaza maulizo. Juma lililofuata walianza kuhudhuria hotuba ya watu wote na funzo la Mnara wa Mlinzi. Wakati mfupi baada ya hapo walianza kuhudhuria funzo la kitabu, na katika mwezi uliofuata walijiandikisha katika Shule ya Kitheokrasi. Walakini, hata kabla ya kuhudhuria mikutano yote, walikuwa wameanza kufanya mabadiliko ya ghafula katika maisha yao, wakiacha mazoea ya kuvuta tumbako na kuacha kushirikiana na rafiki zao walimwengu. Walifunza kitoto chao cha miaka miwili kukaa kimya mikutanoni na katika mwezi wa kwanza baada ya kuanza kuhudhuria mikutano yote, walikuwa wakifurahia utumishi wa shambani pamoja na sisi. Kama miezi mitatu hivi baada ya hapo walibatizwa na wanaendelea kupata mapendeleo zaidi na zaidi kundini.
7 ‘Kupata kuitikia kwa haraka kutoka kwa mtu fulani na kuona kupendezwa huko kukipoa tena ni jambo ambalo sisi sote tumepata kuona, kwa hiyo bila shaka wazo hilo liliingia akilini mwangu mwanzoni. Walakini, baada ya ziara hiyo ya pili, ambayo katika hiyo tamaa hiyo nyingi sana ya kumtumikia Mungu ilionyeshwa, mume wangu nami tuliamua kwamba bila shaka malaika wanaongoza kazi ya Yehova chini ya uangalizi wa Yesu. Walipoulizwa sababu ya kuitikia mahubiri yetu ya “habari njema” mara moja, walijibu: “Ilikuwa Biblia.” Walipoiona katika Biblia, walijua ni kweli; hivyo, uamuzi wao ulikuwa—Kwa sababu gani tungoje? walitaka kushiriki, nao hawakupoteza wakati. Yesu alikuwa amesema kweli: “Nawajua kondoo wangu nao kondoo wangu wanijua mimi.”’
KUJULISHA KICHWA CHA BIBLIA
8, 9. Biblia inawezaje kutumiwa vizuri, wakati tunapotoa ushuhuda?
8 ‘Wakati mimi na Shahidi mwingine tulipokuwa tukifanya kazi ya shambani nyumba kwa nyumba, mama mmoja alitukaribisha ndani, tukaanza kuzungumza naye juu ya habari njema, na kumwomba achukue Biblia yake. Kwa kuwa alitaja kwamba alikuwa ameisoma Biblia mara nyingi na kwenda kanisani, tulimwuliza atuambie kama alikuwa amejifunza na kujua kichwa cha Biblia. Tulisoma naye Isaya 9:6, Danieli 2:44, Mathayo 6:10, na mengineyo. Kisha tukamwuliza kama sasa anakijua kichwa cha Biblia, naye alijibu akasema, ‘Ndiyo, ni Ufalme!’ Ndipo tuliposoma maandiko yanayoeleza faida za utawala huo wa Ufalme duniani. Inaonekana tulikaa muda wa zaidi ya saa moja. Tulipomkaribisha kwenye hotuba ya Jumapili, alisema kwamba akiisha kuamua kuja, angeweza kuja peke yake.
9 ‘Lo! ajabu! singeweza kusadiki alipohudhuria mkutano asubuhi, naye alikuwa ametembea maili tatu [kilometres 5] kutoka nyumbani kwake kufika kwenye Jumba la Ufalme. Alingojea kipindi chote cha mkutano kisha akataka mazungumzo mengine. Tulipanga kujifunza naye katika kitabu Good News. Lakini jambo lenye kupendeza juu ya mwanamke huyu ni kwamba amekuwa mpinzani wa kweli mpaka sasa. Sana sana, yule dada aliyekuwa pamoja nami, tulipokuwa tukikaribia mlango wake, alikuwa akifikiria jinsi mwanamke huyu alivyokuwa mpinzani wa ujumbe. Kwa hiyo, watu wanabadilika!’
KWA MSAADA WA ROHO YA MUNGU
10. Maandiko yanaonyeshaje ukuu wa Yehova? (Isa. 46:9-11)
10 Roho ya Yehova inatenda kwa nguvu sana. Akijitaja yeye mwenyewe kama Muumba wa vitu vyote tuonavyo tunapoinua macho yetu juu, anasema: “Kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.” Mtume Paulo anasema vilevile juu ya tendo hilo moja kuu la uweza wa Yehova, “nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu [kutoka kutokuwapo], akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho, juu sana kuliko . . . [vingine vyote], [wala si katika taratibu hii ya mambo tu, bali katika ile ijayo pia].”—Isa. 40:26; Efe. 1:19-21.
11. Kupatana na hilo, Ufunuo 11:7-12 unaelezaje tukio la ajabu lisilotazamiwa lililotimizwa katika siku hizi zetu?
11 Mpaka wakati wetu huu, mnamo mwanzo wa kiangazi cha mwaka 1918, yule “mnyama” wa kisiasa, anayetajwa katika Ufunuo 11:7, aliua mabaki waliotiwa mafuta, waliofananishwa na ‘mashahidi wawili,’ akikomesha kazi yao ya kutoa ushuhuda, na washiriki wa baraza inayoongoza wakapelekwa gerezani wafungwe miaka ishirini. Walionekana machoni pa adui zao kama mizoga isiyozikwa. Halafu nini? Kama ilivyokwisha kutajwa, jambo la ghafula lilitukia. Baada ya “siku tatu u nusu” fupi na za mfano, masika ya mwaka 1919, “roho ya uhai itokayo kwa Mungu [roho ile ile ya uhai iliyomfufua Kristo kutoka kwa wafu] ikawaingia [mashahidi hao wawili], wakasimama juu ya miguu yao . . . Wakasikia sauti kuu kutoka mbinguni ikiwaambia. Pandeni hata huku. Wakapanda mbinguni,” wakarudishwa kwenye kibali ya Mungu na kuwa na uhai mpya wa kiroho na utendaji machoni pa wote.—Ufu. 11:7-12.
12. Ni kitu gani kinachoweza kutumainiwa na watumishi wa Yehova sikuzote na kinafanya kazi namna gani?
12 Roho takatifu au nguvu ya utendaji kutoka kwa Mungu imekuwa pamoja na watu wa Yehova waliojiweka wakf kweli kweli nyakati zote. Yesu alisema juu ya nia ya Baba yake ya “kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao.” (Luka 11:13) Kama alivyosema Yesu: “Ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu.” (Yohana 16:24) Shirikiana na roho hiyo takatifu na uitumaini. Kama Paulo alivyoandika: “Naweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:13) Tena kumbuka sababu yake katika Warumi 8:11, NW: “Ikiwa, sasa, ile roho yake yeye aliyemfufua Yesu kutoka kwa wafu yakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu kutoka kwa wafu ataifanya pia miili yenu inayokufa iwe hai kupitia kwa roho yake inayokaa ndani yenu.” Lo! tunavyopewa uhakikisho bora!
13. Licha ya wale walio na tumaini la kimbinguni, nani wengine wanaoweza kushiriki katika mipango ya Yehova? (Isa. 61:5-7)
13 Ijapokuwa ni kweli kwamba baadhi ya maandiko haya yanahusu (yanapasa) wale walio na tumaini la mbinguni, Waisraeli wa kiroho, vilevile Neno la Mungu lasema juu ya “mkubwa” wa wengine, likiwataja kama “wageni” wakilinganishwa nao, linawakaribisha wao vilevile wawe wafanya kazi wenye furaha. “Na wageni, walioandamana na [Yehova] ili wamhudumu, na kulipenda jina la [Yehova], kuwa watumishi wake [na kumfanyia kazi]. . . Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala . . . kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.”—Isa. 56:6, 7.
WAFANYA KAZI WENZI PAMOJA NA MUNGU NA KRISTO
14. Je! tuna sababu ya kujiona kana kwamba tunafanya kazi peke yetu?
14 Namna inavyofurahisha kujua kwamba hatufanyi kazi peke yetu! Kama Yesu alivyosema kwa ukaribishaji sana: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu [maneno ya pembeni NW: “Ingieni chini ya nira yangu pamoja nami”], mjifunze kwangu, kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mt. 11:28-30.
15. Waangalizi kati ya watu wa Mungu wanapaswa kuweka mfano mzuri katika njia gani?
15 Imetupasa sote tuwe na roho ii hii—tufanye kazi pamoja na Yehova na Mwanawe. Wazee wanauona mfano uliowekwa na Kristo Yesu nao imewapasa waweke mfano wa kufanya kazi pamoja na wengine, sana sana katika utumishi wa nyumba kwa nyumba. Lo! inapendeza kama nini wakati roho hiyo inapoonyeshwa! Paulo aliwasihi Wafilipi, akisema: “Ijalizeni furaha yangu, ili [nyote] mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja . . . Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenzake kuwa bora kuliko nafsi yake”—mpole, mnyenyekevu,-—Flp. 2:2, 3.
16, 17. Ni kutiwa moyo gani tunakoweza kupata tunapofanya kazi katika joto la mchana?
16 Lo! namna wanavyobarikiwa watumishi wa Mungu wanapotumikia kwa roho ile ile ya kujinyima kama aliyoionyesha Yesu! Bila shaka, wao wanakuwa wafanya kazi wenye furaha, kama mifano inayotajwa hapo chini inavyoonyesha:
WAKATI WA JOTO LA MCHANA
17 ‘Mke wangu na Mashahidi [akina dada] wachache walikuwa wakihubiri shambani wakati wa joto. Kulibaki nyumba moja tu ya kutembelea, naye mke wangu aliichukua. Alimfikia msichana mlangoni akazungumza naye juu ya hali zilizopo ulimwenguni na kumwuliza msichana huyo kama anajua kuna ye yote anayeweza kutatua matatizo [kumaliza magumu] ya ulimwengu. Msichana huyu alijibu kwamba aliona ajabu ya kuulizwa ulizo hilo na mke wangu, kwani ndilo jambo ambalo yeye na mama yake wamekuwa wakizungumza kitambo kidogo tu. Pale pale mke wangu alianza funzo, na kwa vile tulivyokuwa wageni, alimpa dada mwingine funzo hilo. Hivi majuzi tumepata habari ya kwamba msichana huyu pamoja na watu wengine wanne ambao alifikia, wamekwisha kuweka maisha zao wakf kwa Yehova kwa sababu ya kuwatembelea wakati wa joto [la mchana], nayo ilikuwa ndiyo nyumba ya mwisho.’
FURAHA YA KUFANYA UPAINIA
18-22. Watumishi wa wakati wote wanajifurahisha mambo gani yenye faida, na ni sifa gani sana sana zinazohitajiwa? (Flp. 3:16)
18 ‘Nilitaka kuwaandikieni juu ya furaha ninayopata katika utumishi wangu wa shambani. Imekuwa furaha kweli kweli kufanya upainia, sana sana miezi michache iliyopita. Mimi naona [mabadiliko ya matakwa ya saa] ni baraka kuu kutoka kwa Yehova. . . . Rafiki wengi wanapanga mambo yao ili tufanye utumishi pamoja. Mimi mwenyewe sihangaikii wakati wangu. Sasa nafurahia kufikiria ziara zangu za kurudia na mafunzo ya Biblia.
19 ‘Yehova amenipa baraka nyingine ya kuwa na funzo la Biblia lenye maendeleo. Ningetaka nishiriki pamoja nanyi mambo haya niliyoona. Asabuhi moja Jumamosi, mwezi wa Julai, nilikuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba. Nilikaribishwa nyumbani, na tulipokuwa tukizungumza juu ya Biblia, Carol, jirani, akaja. Alipoona kwamba sisi tulikuwa Mashahidi wa Yehova, alitaka mara hiyo ajue tulivyoamini, kwa kuwa, kama alivyosema, alikuwa akitafuta dini ya kweli lakini hakuwa ameiona. Nilipojua kwamba alikuwa akisema kwa unyofu wa moyo, nilifanya mpango wa kumfikia na kumwonyesha jinsi ya kujifunza Biblia yake.
20 ‘Kulikuwa kumepita mwezi mmoja na kitu kabla sijamwona tena; wakati huu nilimkuta akiwa katika duka la vyakula. Nilijitolea nimpeleke nyumbani kwake na kumwuliza kama bado alikuwa akitaka kujifunza Biblia, na kama ndivyo, ningemkuta nyumbani kwake wakati gani? Juma chache baadaye nilimkuta nyumbani kwake, tukajifunza kwa muda wa saa mbili, alikuwa ana maulizo mengi. Baada ya kujifunza safari nyingine chache, dada aliyekuwa pamoja nami alimkaribisha aje kwenye Jumba la Ufalme, na tangu Oktoba 10 hajakosa mkutano hata mmoja. . . . Anaona uhitaji wa kuwa na uhusiano wa karibu sana na Yehova na kuwa mmoja wa watu wake. Anasema kwamba kweli imemfanya yeye na watoto wake wawe karibu zaidi. Imemfanya awe mtulivu na mwenye furaha zaidi. Anasema kwamba anajua hii ndiyo kweli kwa sababu kila tunalosema linathibitishwa na Biblia.
21 ‘Namshukuru Yehova kwa kuniruhusu niwe na pendeleo hili la kujifunza na mtu na kumwona akiendelea katika kweli. Naweza kuona faida ya kuwa na funzo la Biblia. Jambo hili limenifanya niazimie hata zaidi kuendelea kufanya upainia ili niwe na nafasi zaidi ya kushiriki kuwatafuta wale wanaoona kiu ya kweli.’
FURAHA YA KUANZA FUNZO JIPYA LA BIBLIA
22 ‘Nilibatizwa Agosti mwaka 1960. Kwa jumla huu utakuwa mwaka wangu wa tano wa kufanya upainia wa kawaida, nami nimependelewa kusaidia watu zaidi ya hamsini [50] waijue kweli. Kawaida yangu ninakuwa na wastani ya mafunzo ya Biblia sita, lakini mwezi huu nitaripoti mafunzo manane. Nimeona kwamba njia bora ya kuanza mafunzo ni kwa kufanya utumishi wa mlango kwa mlango. Ukiisha kuona wanaopendezwa kwanza, unarudia na kuanza funzo.’
MAVUNO NI LAZIMA YAENDELEE!
23. Maneno ya mwisho ya Yesu katika Mathayo 28:20 ni onyo na kitia-moyo namna gani?
23 Je! bado kuna watu wanaotakiwa kukusanywa wakati huu wa mavuno? Ripoti zinazotoka shambani ulimwenguni pote zaonyesha kwamba wako. Tutafanyaje? Je! tutazidi kufanya kazi pamoja na Kristo Yesu, chini ya nira yake? Tunahakikishwa kwamba angekuwa nasi mpaka mwisho wa taratibu ya mambo. Basi, na tuendelee kufanya kazi mpaka mavuno yakusanywe kabisa, tukifanya kazi sote pamoja na Kristo, tukifanya kazi sote pamoja kwa furaha. Hii ni kazi ambayo Yehova ameagiza watu wake wafanye leo.
24, 25. (a) Ni katika njia gani sisi tunazo sababu za kufurahi kuliko Paulo? (b) Sisi tuna sababu gani kuu inayotutia moyo tushiriki katika kazi ya Yehova?
24 Paulo alifurahi kwa sababu alipewa “habari njema za Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11, NW) Bila shaka tuna sababu hata zaidi ya kufurahi kwa kuwa tumepewa “habari njema” za Ufalme uliosimamishwa ‘zinazopaswa kuhubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote’ kabla mwisho haujakuja. (Mt. 24:14) Ikiwa kuzaliwa kwa Yesu ilikuwa sababu iliyomfanya malaika atangaze “habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote,” bila shaka kutawazwa kwake kama Mfalme wa mbinguni ni sababu kuu zaidi ya kufurahi, wakati ‘ufalme wa dunia ulipokwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.’ (Luka 2:10; Ufu. 11:15) Kutangazwa huku kwa “habari njema” ni kazi ambayo Yehova ameagiza watu wake wafanye leo. Kuunga mkono ufalme huo kwa uthabiti na kufanya kazi kwa ushikamanifu kwa ajili ya faida zake kutaufurahisha hata moyo wa Yehova. “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.”—Mit. 27:11.
25 Lo! namna tulivyo na pendeleo la ajabu! Namna linavyotutia moyo tushiriki pamoja na Yesu Kristo kufanya kazi ya Yehova kwa furaha!
—Kutoka The Watchtower June 1, 1978.