Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 7/15 kur. 315-319
  • ‘Udhambi Unaozidi’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Udhambi Unaozidi’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TAMAA YA UKUU NDIO MWANZO WA UKENGEUFU
  • TOFAUTI YA MAPADRE NA WATU WA KAWAIDA
  • UPINZANI WA WAZI KWA MUNGU
  • ‘NDOA’ YA KANISA NA SERIKALI
  • Kutambulisha “Mtu wa Kuasi [Sheria]”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Uasi Juu ya Mungu Unafunuka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kifo cha Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Je, Kunapaswa Kuwa na Tofauti Kati ya Makasisi na Waumini?
    Amkeni!—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 7/15 kur. 315-319

‘Udhambi Unaozidi’

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1. Dhambi ni nini, kutokana na maoni ya Mungu, na dhambi ni hatari kadiri gani?

DHAMBI ni mbaya kadiri gani? Matokeo ya hata dhambi “ndogo” huenda yakawa na mfiko wa umbali gani? Maneno ya Yesu alipokuwa akishauri wanafunzi wake juu ya uaminifu yanafungamana na ulizo hili. Alisema: “Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Kutokuwa mwaminifu kwa Mungu ni dhambi, na, kulingana na mtume Yohana, “Kila atendaye [“azoeaye,” NW] dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi.” (1 Yohana 3:4) Kama vile kwa mtu mmoja, pia kwa kikundi au jamii ya watu, kubwa au ndogo, kupotoka kidogo kutoka kwa kanuni za haki, kunaweza kuleta uasi mkubwa na taabu isiyohesabika, kukiachiliwa.​—Rum. 7:13.

2. Wakristo wa kwanza walipata maonyo gani juu ya kuja kwa “mtu wa kuasi”?

2 Mfano wenye nguvu wa matokeo mabaya sana wa jambo ambalo kwanza pengine lilionwa kuwa jambo dogo unapatikana katika usitawi wa “mtu wa kuasi.” Biblia inaueleza kupitia kwa maandiko ya mtume Paulo katika 2 Wathesalonike sura ya 2. Mitume Paulo na Petro walionya makundi mapema juu ya kuja kwa “mtu” huyu kwamba “katika ninyi wenyewe [wazee katika kundi la Kikristo] watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao,” kwamba ‘wangeleta madhehebu zenye kuharibu’ na kwamba wengi ‘wangefuata matendo yao ya mwenendo mpotovu.’​—Matendo 20:30; 2 Pet. 2:1-3.

TAMAA YA UKUU NDIO MWANZO WA UKENGEUFU

3, 4. Yesu alionyaje wanafunzi wake juu ya kusitawisha roho ya viongozi wa kidini wa Kiyahudi?

3 Huenda mtu akasema, ‘Hali kama hiyo ingewezaje kuanza katika kundi la Mungu mwenyewe?’ Basi, halikuwa jambo lililotokea usiku mmoja. Lilisitawi kwa njia ya werevu sana. Yesu alikuwa ameweka mfano unaofaa, naye alikuwa ameonya wanafunzi wake waziwazi juu ya roho ya viongozi wa kidini wa Wayahudi, akisema hivi:

4 “Matendo yao yote huyatenda ili kutazamwa na watu; . . . hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi, na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi [Mwalimu]. Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu. Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote akayejidhili, atakwezwa.”​—Mt. 23:5-12.

5. Wazee fulani katika kundi la kwanza la Kikristo walianzaje usitawi mbaya sana wa “mtu wa kuasi” kwa “mambo madogo madogo”?

5 Yako maonyo mengine ya upole kama hilo katika Maandiko ya Kikristo. Lakini wanaume wengine wenye vyeo vya madaraka katika kundi la kwanza kwa wazi walianza kujichukulia faida ndogo ndogo. Walijiona kuwa wa maana kidogo katika cheo walichokuwa nacho. Waliona kwamba kiliwastahilisha heshima zaidi kuliko aliyostahili mshiriki “wa kawaida” wa kundi. Walijipa mapendeleo ya pekee, nao walitazamia vitu vya kimwili kutoka kwa ndugu zao. Kwa njia hiyo wangeweza kutegemewa kama watu ambao “wamo.” Hayo ndiyo yote waliyotaka, kwanza. Lakini kidogo kidogo wao na warithi wa vyeo vyao wakawa wenye kudai, wenye uhodari zaidi, wenye kuonyesha mamlaka kwa kutumia nguvu zaidi. Walidanganya kundi wakalipotoa watosheleze tamaa zao na ‘kuwadanganya kwa maneno yaliyotungwa.’ Mtume Paulo anaeleza wanaume fulani kati yao walivyokuwa katika 2 Wakorintho 11:19, 20.​—2 Pet. 2:3.

6, 7. (a) Wazee hawa inaelekea walidhani nini juu ya waliyokuwa wanafanya? (b) Tunawezaje kuchunguza usitawi wa “mtu wa kuasi”?

6 Inawezekana hapo mwanzoni wanaume hawa hawakuwaza kutaka kwao mapendeleo machache tu kungeelekeza kwenye nini mwishowe​—jambo lenye kuogofya na la kuchukiza sana ambalo lingetokezwa baadaye na kusitawisha kwao tamaa “ndogo” ya kichoyo. Wao walidhani kwamba kupotoka kwao, ikiwa kulikuwapo, kulikuwa kudogo. Lakini na tuchunguze historia ya maelekeo haya tuone matokeo ambayo wanaume awa hawa wakawa wa kulaumiwa kwa sababu yake.

7 Kutokana na masimulizi ya Biblia ya kuonekana kwanza kwa ukengeufu wa “mtu wa kuasi” tunaweza kuchunguza usitawi wake katika maandishi ya historia.

TOFAUTI YA MAPADRE NA WATU WA KAWAIDA

8. Mpango ulikuwa nini katika kundi la Kikristo siku za mitume?

8 Yesu Kristo hakuwa amewapa wanafunzi wake maagizo wagawanyike katika jamii za mapadre na watu wa kawaida. Wote walikuwa wanalingana wakiwa washiriki wa jamaa ya kiroho, wote wakiwa ndugu za Yesu Kristo waliozaliwa kwa roho, waliotiwa mafuta wawe jamii ya makuhani, wenye matumaini ya kuwa wafalme na makuhani wa kimbinguni pamoja na Kristo. Mtume Petro aliwaita “ukuhani wa kifalme.” (1 Pet. 2:5, 9, NW) Ingawa wengine walikuwa na madaraka kama “wachungaji,” wote walikuwa makuhani kwa maana ya kiroho na wote walishiriki kazi ya kutoa dhabihu za kiroho. (1 Pet. 5:1-4) Hakukuwa na wazo la mgawanyiko wa ‘jamii ya mapadre na ya watu wa kawaida.’ Walakini, angalia inayosema historia:

9. Usitawi wa “mtu wa kuasi” unaonyeshwa katika historia?

9 “Ushindani wa Kiyahudi wa mapadre na watu wa kawaida ulikuwa haujulikani kwanza kati ya Wakristo; na ilikuwa ‘wakati tu watu walipoondoka katika maoni ya Kiyahudi’ wazo la ukuhani wa Kikristo wa waamini wote lilipoachia nafasi kabisa lile la ukuhani wa pekee au mapadre. . . . Ndivyo Tatuliano, hata (De Baptismo, c. 17, kabla hajawa Mkaa mlimani): ‘Watu wa kawaida wana haki pia ya kutoa sakramenti na kufundisha mtaani. Neno la Mungu na sakramenti zilitolewa kwa wote kwa neema ya Mungu, na kwa hiyo zinaweza kutolewa na Wakristo wote kama vyombo vya neema ya kimungu. Lakini ulizo hapa halihusiani na yanayoruhusiwa kwa watu wote tu, bali pia yenye faida chini ya hali zilizopo. Hapa tunaweza kutumia maneno ya Mt. Paulo, “Mambo yote ni halali kwa wanadamu, lakini mambo yote hayana faida.” Tukiutazama utaratibu ulio wa lazima kuendelezwa katika Kanisa, watu wa kawaida basi wamepaswa watumie haki yao kutoa sakramenti wakati na hali tu zinapotaka iwe hivyo.’ Kutoka wakati wa Cyprian, . . . baba ya utawala wa serikali ya mapadre, tofauti kati ya mapadre na watu wa kawaida ilionekana wazi, na karibuni sana ikakubaliwa ulimwenguni mwote. Kwa kweli, kuanzia karne ya tatu na kuendelea, neno clerus (kle’ros, ordo’) karibu lilitumiwa kwa wahudumu peke yao kuwatofautisha na watu wa kawaida. Utawala wa serikali ya mapadre wa Kirumi ulipositawishwa, mapadre hawakupata kuwa tofauti na watu wengine tu (ambao wanaweza kuwa na kanuni zote na mafundisho ya mitume), bali pia kutambuliwa kama ukuhani wa pekee, na njia ya maana ya mazungumzo kati ya mwanadamu na Mungu.”​—M’Clintock and Strong’s Cyclopædia, Volume II, ukurasa 386.

10, 11. (a) “Utawala wa serikali ya mapadre,” ambao ni tofauti na wazo la udugu wa Kikristo, ulianzaje? (b) “Mtu wa kuasi” ni nani, na tunaonaje kwamba si mtu mmoja?

10 Thascius Caecilius Cyprian aliyetajwa juu alikuwa askofu wa kanisa katika Carthage, Afrika. Alizaliwa wapata mwaka wa 200 C.E. akafa mwaka wa 258 C.E. Alikuwa padre, anayeitwa hapa “baba ya utawala wa serikali ya mapadre,” mojawapo ya jamii ya mapadre iliyokuwako si zaidi ya karne moja baada ya kufa kwa mitume wa Kristo na washirika wao wa karibu. Kuanzia wakati huo na kuendelea, kupita nyakati kusipokuwa na elimu au mwangaza wa uvumbuzi wa vitu (mwaka 476 C.E. mpaka karibu 1000 C.E.), kuingia katika wakati wa Matengenezo ya kanisa na mwanzo wa Makanisa ya Kiprotestanti, na hata siku hizi, tofauti hii kati ya mapadre na watu wa kawaida imekuwako katika Jumuiya ya Wakristo.

11 Hawa wanaoitwa mapadre ‘wa Kikristo’ ndio wamejionyesha kuwa “mtu wa kuasi . . . mwana wa uharibifu,” katika habari ya ukengeufu au uasi wa 2 Wathesalonike 2:3. Ni wazi kwamba kwa matumizi ya usemi huu Biblia Takatifu inamaanisha “mtu” mwenye watu wengi ndani, anayeendelea kuwako kwa kipindi kirefu na ambaye mwundo wake na jamii ya watu wake inabadilika kadiri wakati unavyopita.

UPINZANI WA WAZI KWA MUNGU

12. Uasi wa “mtu wa Kuasi” unafanywa juu ya nani, naye anafika wapi katika mwendo wake?

12 Kwa kuwa uasi huu (kama ilivyozungumzwa katika toleo letu lililotangulia) u juu ya Yehova Mungu, haishangazi kwamba “mtu” huyu mwenye watu wengi ndani yake anajaribu kujifanya mungu, kama alivyofanya Shetani Ibilisi mwasi mkuu, ambaye Biblia inamwita “mungu wa taratibu hii ya mambo.” (2 Kor. 4:4, NW) Mtume Paulo alisema hivi kwa unabii juu ya “mtu wa kuasi”: “Yule mpingamizi, ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa; hata yeye mwenyewe kuketi hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye [“ni mungu,” NW] ndiye Mungu.”​—2 The. 2:4.

13, 14. Ni dai gani la mapadre linaloonyesha nia ya jamii nzima yao?

13 “Mtu wa kuasi” ni jamii yenye watu wengi. Walakini, tunaweza kuelekeza kwenye dai linalotolewa juu ya mmoja wa mapadre hawa linaloonyesha nia ya jamii yote. Juu ya papa wa Kanisa Katoliki la Kirumi, kamusia ya kidini ya Ferraris inasema hivi:

14 “Papa ni mwenye fahari na ukuu sana hata yeye si mwanadamu tu bali, twaweza kusema, Mungu, na Mjumbe wa Mungu. . . . Kwa hiyo papa anavikwa taji yenye vyeo vitatu, kama mfalme wa mbingu, wa dunia na wa “hell.” . . . Sivyo, ubora na uwezo wa papa si kwamba tu unapita mambo ya kimbinguni, ya kidunia na ya “inferno” (motoni), bali pia yeye yu juu ya malaika, naye ndiye mkuu wao . . . Hata kama ingewezekana malaika wapotoke katika imani, au wakubali nia zinazotofautiana nayo, wangeweza kuhukumiwa na kufukuzwa na papa. . . . Yeye ni mwenye fahari kuu sana na uwezo hata yumo katika baraza ile ile ya hukumu pamoja na Kristo . . . Hata lo lote lile analofanya papa linaelekea kuwa limetoka katika kinywa cha Mungu. . . . Twaweza kusema, papa ni Mungu duniani, mkuu wa pekee wa waaminifu wa Kristo, mfalme mkuu zaidi wa wafalme wote, mwenye uwezo mwingi; ambaye kwake usimamizi wa ufalme wa kidunia na wa kimbinguni unakabidhiwa. . . . Papa ni mwenye mamlaka kuu na uwezo mkuu sana hata anaweza kurekebisha, kutangaza na kutafsiri sheria ya kimungu. . . . Nyakati nyingine papa anaweza kufuta sheria ya kimungu kwa kupunguza, kueleza,” n.k.

15. Ingawa huenda mapadre wa Kiprotestanti wakakosa kukubaliana na madai yanayofanyiwa papa, je! wao kweli wana nia tofauti?

15 Uwezo na nguvu hizi anazohesabiwa papa zimeungwa mkono na mapadre wa Katoliki, na, ingawa wengi wa mapadre wa Kiprotestanti huenda wakakataa, wao pia wanajikweza kama “Reverend,” “Right Reverend” na “Father” na kutumia vyeo vingine vinavyowaweka juu ya watu wa kawaida, wapate kutegemewa, kuheshimiwa na kupewa vitu vya kimwili, mara nyingi vitu vyenye mapambo mengi​—kwa njia inayofanana na roho ya dai la papa.​—Ayubu 32:21, 22.

16. Zaidi ya kujikweza, “mtu wa kuasi” amejionyeshaje kuwa ‘mpingamizi wa Mungu’?

16 “Mtu wa kuasi” amejionyesha kuwa mpinzani wa Mungu si kwa kujikweza huku, bali pia kwa kujifanya “rafiki” ya ulimwengu. (Yak. 4:4) “Mtu” huyu mwenye watu wengi anampinga Mungu pia anapojaribu kufanya Neno la Mungu aliloliongoza mwenyewe liwe halifai kitu, akiliita “hadithi,” “kuukuu,” “lisilotegemeka,” “lenye kujawa na makosa” na hata kusema “Mungu amekufa.”

‘NDOA’ YA KANISA NA SERIKALI

17, 18. Uhusiano kati ya Kanisa na Serikali umekuwa wa karibu kadiri gani, na ni nini linalosemwa juu ya jambo hili katika The Encyclopedia Americana?

17 Katika nchi nyingi kumekuwa na hata sasa kuna umoja wa Kanisa na Serikali. Katika ‘ndoa’ hizo Kanisa limejaribu kutoa amri. Mapadre wameongoza kuwaza kwa watu kwa kadiri kubwa, nao watawala wa kisiasa, wakijua hili, wamewapa mapadre mamlaka, heshima kuu, ulinzi na mapendeleo, pesa, na vitu kama hivyo. Kwa habari ya “Kanisa na Serikali,” The Encyclopedia Americana, Volume 6, kurasa 657, 658, kinasema hivi:

18 “Kati ya mashirika mawili haya, katika nyakati za kisasa, hakujapata kuwa na upatano kamili. Shindano hili, ambalo limefululizwa muda mrefu sana, litaelekea kuendelea sikuzote usipotokea msukosuko wa kustaajabisha. Limekuwa kali. Limehusu faida nyingi likatokeza mazungumzo makubwa. Limechochea maasi ya namna zote likafanya vitabu vichapwe vya matusi yasiyolinganika nje ya ugomvi wa kisiasa. Halikuwa shindano la kisiasa tu. . . . Chini ya Konstantino Kanisa liliingia katika uwanja wa utendaji wa ulimwengu wote kama msaidizi katika kazi ya kustaarabisha watu. Likitambuliwa kama mtawala wa kiroho, kidogo kidogo lilijipatia makao ya mahali pake na jina kama mtawala wa dunia hii. Likawa mamlaka ya ulimwengu. Kufaulu huku ndiko kulikokuwa mwanzo wa misiba mingi yote ya Kanisa. . . . Kutoka kwa Konstantino mpaka kwa Charlemagne mamlaka ya raia ilijiingiliza katika serikali yake, huku ikitambua Kanisa kisheria. Kutoka kwa Charlemagne mpaka kipindi cha karibu na kile cha Matengenezo ya kanisa, Kanisa na serikali zilikuwa zimeungana sana na watu wote walikubali utii wa raia kwa mamlaka ya kiroho.”

19. Hali hiyo imekuwa afadhali au imebadilika katika karne hii ya 20?

19 Katika karne hii ya 20, hali hiyo imeendelea kuwapo. Vita zimepigwa juu ya maulizo ya kidini na Vita za Ulimwengu zilizo kuu zaidi, za damu na zenye kuharibu zaidi zimepigwa, mataifa ya Jumuiya ya Wakristo yakaongoza yakiwa na silaha zenye kuua zaidi.

20. (a) Je! wazee wote wa kwanza walifuata njia ya uchoyo iliyositawishwa na “mtu wa kuasi”? (b) Dhambi ya wazee hao wa kwanza iliyopotoka kutoka amri na mfano wa Kristo ilikuwa mbaya kadiri gani?

20 Fikiria maumivu ya moyo, msiba, machinjo, kusingiziwa kwa jina la Mungu na kwa jina la Ukristo, ambayo yametokana na mwanzo wa tamaa ya ukuu na faida ya kipekee! Wengi walibaki waaminifu kati ya wale wazee wa kwanza waliowekwa walichunge kundi la Mungu. Wao walifuata kanuni iliyosemwa na Yesu, aliyesema hivi: “Mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote.” (Marko 10:44) Lakini wachoyo kati yao walisababisha uasi wa kidini ulioletea mamilioni msiba. Kama wangalifuata amri ya wazi na nyepesi na mfano wa Kristo, jambo hilo baya sana lisingalitokea.

21, 22. Kutokana na historia hii ya usitawi wa “mtu wa kuasi,” tunaweza kujifunza somo gani juu ya kufanya dhambi ‘kidogo tu’?

21 Sisi kama watu mmoja mmoja tunaweza kujifunza mengi kutokana na hili. Mungu anaposema jambo ni baya, ni baya kweli kweli. Tunapopuza onyo lake juu ya namna yo yote ya dhambi, tusidhani kamwe tunafanya ‘jambo dogo tu.’ Hatupatani na mpango wa Mungu wa ulimwengu wote na tunajitia katika mwanzo wa jambo linaloweza kuumiza sana watu wengi. Kanuni ya Biblia ni hii: “Chachu kidogo hulichachusha donge zima.” (1 Kor. 5:6) Tusipotubu upesi, tuache dhambi hiyo na kufanya yote tunayoweza kurekebisha jambo hili, tunaweza kuwa wenye laumu kwa matukio mabaya sana.

22 Kwa mfano, angalia aliyoandika Yakobo ndugu mama-mzazi mmoja na Yesu Kristo juu ya ulimi wenye kusemasema yasiyofaa: “Ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum.” (Yak. 3:6) Ukitumiwa vibaya, ulimi unaweza kuchafua maisha yetu na maisha za wengine wengi. Yakobo alionyesha pia kwamba dhambi inaweza kuwa na mwanzo wenye hila sana. Alisema: “Kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”​—Yak. 1:14, 15.

23. Kwa kuwa sote tunafanya dhambi, hata hivyo tunawezaje kuepuka matokeo yake yote yaliyo mabaya sana?

23 Ni kweli, kila mtu anafanya dhambi nyakati nyingine. Lakini, shukrani kwa Yehova Mungu kwa kutoa msaada, kupitia kwa fadhili zake zisizostahilika, ili tuweze kuepuka kuendelea kufuata mwendo wa dhambi, pamoja na matokeo yake mabaya sana. Tunaweza kuuepuka mwendo wenye msiba wa “mtu wa kuasi.” Tunaweza kufanya hivi kwa kuamini dhabihu yenye kupatanisha ya Mwanawe Yesu Kristo. (Rum. 7:21-25; 8:1, 2) Ni kwa kutambua ‘udhambi unaozidi’ na kumwendea Yehova tu tusamehewe juu ya msingi wa dhabihu ya Kristo tunapofanya dhambi, tunavyoweza kupata msaada wa Yehova tuepuke matokeo yote ya tendo letu lenye makosa.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

[Maelezo ya Chini]

a Prompta bibliotheca canonica, juridicao-moralis, theologica partim ascetica, polemica, rubricistica, historica, lliyotayarishwa katika Bologna, jimbo la Emilia-Romagna, Italia, mwaka wa 1746 na Lucio Ferraris, Vol. VI, kur. 31-35; kulingana na nakala katika Chuo cha Columbia, mji wa New York.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki