Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 3/1 kur. 113-114
  • Je! Wewe Una Nia Kupatwa na Magumu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Una Nia Kupatwa na Magumu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUISITAWISHA SIFA
  • KUJIJARIBU MWENYEWE
  • MAMBO YA KUEPUKA
  • Shikamana na Tengenezo la Yehova
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • “Uvumilivu na uwe na Kazi yake Kamilifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • “Acheni Uvumilivu Ukamilishe Kazi Yake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 3/1 kur. 113-114

Je! Wewe Una Nia Kupatwa na Magumu?

NI JAMBO la kupendeza kupata kuthamini fahari ya Mungu, upendo wake, rehema yake na njia yake njema ya kushughulika na watu wake. Vilevile kufahamiana na watu wa Mungu kunachangamsha moyo.

Lakini si vyepesi kufuata Ukristo katika ulimwengu huu. Ukiisha kujua hivyo, ikiwa umeanza kumtumikia Yehova Mungu, unaweza kufaidika kwa kujichunguza ukijiuliza maulizo fulani, kama haya: Mimi huwa na nia gani ninapopatwa na mambo yasiyopendeza? Je! mimi hustahimili kunapokuwa na magumu? Je! nimekata shauri kwamba nitaendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu mateso makali yakitokea? Maoni yangu ni nini juu ya kupingwa, kupatwa na magumu ya uchumi, ugonjwa, kutiwa gerezani au kupatwa na majaribu mengine?

Lazima tuwe waaminifu na kukubali kwamba: Hakuna mtu atakaye kupatwa na magumu. Hakuna mtu anayependa kutaabika. Kuwa na woga kidogo ni jambo la kawaida. Na bila shaka Wakristo hawapaswi kujitafutia matata wala kujitia katika hali ya kuteswa au kuuawa.

Hata hivyo, mateso na magumu mengine yatakuja. Yesu Kristo alitabiri hivyo. Lakini alitabiri pia kwamba, ingawa kungekuwa na magumu, Mungu angewapa watumishi wake mambo mema yenye kuzidi taabu yenyewe, hata ingekuwa nyepesi ikilinganishwa na mambo hayo. Aliwaambia wanafunzi wake hivi:

“Kila mtu aliyeacha nyumba, ‘au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele.”​—Mt. 19:29.

Mtume Paulo, ambaye alipatwa na magumu, alikubali hivyo alipowaandikia Wakristo wenzake hivi:

“Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo na muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”​—2 Kor. 4:17, 18.

Pengine una mali nyingi za kimwili. Je! unazichukua kama vitu vinavyoweza kukusaidia umtumikie Mungu kwa njia bora? Je! ungekuwa na nia ya kuziacha bila kusikitika, suala la ukamilifu likitokea? Tena, mtume Paulo aliandika hivi:

“[Yesu Kristo] ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo.”​—Flp. 3:8; Luka 14:26.

Wakati wa utawala wa Hitler huko Ujeremani, na katika nyakati za karibuni huko Malawi, Wakristo wa kweli walionyesha nia njema hiyo, wakajinyima vitu vyote ili waendelee kushikamana na Mungu.

KUISITAWISHA SIFA

Njia ya kusitawisha uvumilivu ni kumtii Mungu. Je! wewe u mwepesi kadiri gani kuyatii mambo yanayoamriwa na Neno la Mungu? Unapotimiza mapenzi ya Mungu, karibu kila siku unashinda vipingamizi fulani. Hata hivyo, je! wewe unatii kwa moyo wa kupenda? Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia sana katika hali zinazokutaka uwe na uvumilivu usio wa kawaida. Ndugu mzazi mmoja na Yesu, Yakobo, alishauri hivi:

“Yaoneni yote kuwa furaha, ndugu zangu, mnapokutana na majaribu mbalimbali, mkijua mfanyapo hivyo kwamba ubora huu uliojaribiwa [au uhakikisho] wa imani yenu waleta uvumilivu. Lakini acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili mpate kuwa kamili na timamu katika mambo yote, bila ya kupungukiwa katika lo lote.”​—Yak. 1:2-4, NW; Kingdom Interlinear Translation.

Kwa hiyo, ikiwa umeanza kumtii Mungu bila shaka itakupasa kuepuka kushindwa na jaribu lo lote sasa, hata liwe dogo namna gani. Vishawishi vinavyoletwa na tamaa za mwili vinaweza kukaza sana Wakristo, vikitoka ndani yao wenyewe na katika mazingira mabaya pia na mashirika ya ulimwengu huu. Kati ya mambo hayo, mna uasherati, kulewa, kutumia dawa za kulevya na tumbako pia. Mateso pia yanaweza kukaza sana mtu atende dhambi kwa kulegea na kuvunja ukamilifu. Mtume Petro alieleza nia na jitihada ambayo Mkristo apaswa kuwa nayo alipoandika hivi:

“Basi kwa kuwa Kristo aliteswa katika mwili wake, ninyi nanyi jivikeni silaha ya nia ile ile; kwa maana yeye aliyeteswa katika mwili ameachana na dhambi. Tangu sasa msiendelee kuishi katika tamaa za wanadamu, bali katika mapenzi ya Mungu, wakati wenu uliobaki wa kukaa hapa duniani.”​—1 Pet. 4:1, 2.

Kwa hiyo, ikiwa wewe umekubali kufuata njia ya maisha ya Kikristo, ambayo unajua inatia ndani kutaabikia kweli, na labda umekwisha taabikia haki kwa kadiri fulani, huu si wakati wa kurudi nyuma.​—Luka 9:62.

KUJIJARIBU MWENYEWE

Ili kujijaribu uone kama unasitawisha uvumilivu, angalia unafanya nini wakati huu. Je! unaendeleza uaminifu sasa? Je! unajifunza Neno la Mungu kwa kawaida sasa? Je! badala ya kunywa “maziwa” tu ya lile neno, yaani, mafundisho ya msingi, unatwaa pia ‘maarifa sahihi na ufahamu kamili; ili upate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi’?​—Flp. 1:9, 10, NW; Efe. 5:16.

Je! wakati huu unajitokeza usaidie wengine? Au unasitasita kujinyima? (Gal. 6:10) Ikiwa mtu ana nia ya kuingia katika ugumu fulani kwa ajili ya wengine, kwa ajili ya Ukristo wa kweli, anasitawisha sifa ya uvumilivu.​—Yak. 1:27.

Jambo jingine la lazima linakaziwa na ulizo hili, Je! wewe unatambua kwamba nguvu atoazo Mungu ndizo zitakazokuwezesha uvumilie majaribu, si wema wo wote ulio ndani yako? (1 Pet. 4:11) Je! unamtegemea Mungu kwa uhakika ili akupe hekima na uwezo, na je! unatambua kwamba vitu vyote ulivyo navyo vyatoka kwake?​—Flp. 4:13; Yak. 1:5.

MAMBO YA KUEPUKA

Haitupasi kustarehe tukidhani kwamba tumemtii Mungu na tukavumilia mambo kutosha. Wala haitupasi kusitawisha roho ya majisifu, tukijiona kwamba tu “mashujaa” tuvumiliapo jaribu fulani, kwamba tunapaswa kusifiwa zaidi ya wengine, au kwamba tumefanya maendeleo zaidi ya kufikia mradi wa uvumilivu kuliko ndugu zetu. “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” (Mt. 24:13) Ili kuepuka nia mbaya, kumbuka kwamba wengine wa wale waliovumilia mateso miaka mingi katika kambi za Nazi waliangushwa baadaye na utafutaji wa mali za kimwili au uasherati. Kuna sababu moja tu ya kujisifia, na hiyo ndiyo kumjua Yehova.​—Yer. 9:23, 24.

Watu wengine huwa na wasiwasi wakitaja jambo fulani ambalo wanadhani watatendwa mwilini. Hiyo si hekima. Hatujui tutapatwa na magumu gani, mmoja mmoja. Watu wote hawatapatwa na majaribu mamoja. Jambo la maana ni kumtumaini Yehova. “Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”​—1 Kor. 10:13.

Yehova ataka watu wake wawe wenye furaha. Yeye hafurahii kuona watu wake wakitaabika. Lakini yeye hufanya hata wale wanaovumilia magumu wawe wenye furaha kwa sababu wana nafasi sasa ya kuweka kumbukumbu la milele la kuwa wakamilifu kwa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, Yehova Mungu.​—Mt. 5:11, 12.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki